Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Shangwe Yako Katika Utumishi wa Yehova

Dumisha Shangwe Yako Katika Utumishi wa Yehova

Dumisha Shangwe Yako Katika Utumishi wa Yehova

“Sikuzote shangilieni katika Bwana. Mara moja tena hakika nitasema, Shangilieni!”—WAFILIPI 4:4.

1, 2. Ndugu mmoja na familia yake waliwezaje kudumisha shangwe yao licha ya kupoteza kila kitu?

JAMES, Mkristo mwenye umri wa miaka 70 anayeishi Sierra Leone, alikuwa amefanya kazi kwa bidii katika maisha yake yote. Wazia shangwe aliyopata wakati ambapo hatimaye alikusanya pesa za kutosha kununua nyumba ya kiasi yenye vyumba vinne! Hata hivyo, muda mfupi baada ya James na familia yake kuhamia nyumba hiyo, vita vya wenyewe kwa wenyewe vilizuka nchini humo na nyumba yao ikateketezwa kabisa. Walipoteza nyumba yao, lakini hawakupoteza shangwe yao. Kwa nini?

2 James na familia yake hawakufikiria hasara waliyopata, bali walifikiria mambo ambayo wangepata baadaye. James aeleza hivi: “Hata wakati wa vitisho, tulifanya mikutano, tukasoma Biblia, tukasali pamoja, na kushiriki na wengine vitu vichache tulivyokuwa navyo. Tuliweza kudumisha shangwe yetu kwa sababu tulitafakari juu ya uhusiano wetu mzuri pamoja na Yehova.” Kwa kufikiria mambo mazuri waliyofurahia, jambo kuu zaidi likiwa ni uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova, Wakristo hao waaminifu waliweza ‘kuendelea kushangilia.’ (2 Wakorintho 13:11) Bila shaka, haikuwa rahisi kuvumilia hali zao zenye taabu. Lakini hawakuacha kushangilia katika Yehova.

3. Wakristo fulani wa mapema walidumishaje shangwe yao?

3 Wakristo wa mapema walikabili majaribu kama yale yaliyompata James na familia yake. Hata hivyo, mtume Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania maneno haya: “Kwa shangwe mkakubali kwa uvumilivu kuporwa mali zenu.” Kisha Paulo akaeleza kilichosababisha shangwe yao: “Mkijua nyinyi wenyewe mna miliki bora na yenye kudumu.” (Waebrania 10:34) Naam, Wakristo hao wa karne ya kwanza walikuwa na tumaini lenye nguvu. Walitazamia kwa hamu kupokea kitu wasichoweza kuporwa, kitu kisichoweza kunyauka, ambacho ni “taji la uhai” katika Ufalme wa kimbingu wa Mungu. (Ufunuo 2:10) Leo, tumaini letu la Kikristo—liwe ni la kimbingu au la kidunia—laweza kutusaidia kudumisha shangwe hata wakati wa taabu.

Shangilieni Katika Tumaini”

4, 5. (a) Kwa nini shauri la Paulo “shangilieni katika tumaini” lilikuwa la wakati ufaao kwa Waroma? (b) Ni nini kinachoweza kumfanya Mkristo apoteze tumaini lake?

4 Mtume Paulo aliwatia moyo waamini wenzake katika Roma ‘washangilie katika tumaini’ la uhai udumuo milele. (Waroma 12:12) Shauri hilo kwa Waroma lilitolewa kwa wakati ufaao. Muda unaopungua mwongo mmoja baada ya Paulo kuwaandikia, walinyanyaswa vikali, na wengine waliteswa hadi kufa kufuatia amri ya Maliki Nero. Bila shaka, walipokuwa wakiteseka walitegemezwa na imani yao kwamba Mungu angewapa taji la uhai alilowaahidi. Namna gani sisi leo?

5 Tukiwa Wakristo, sisi pia twatarajia kunyanyaswa. (2 Timotheo 3:12) Zaidi ya hilo, twatambua kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote. (Mhubiri 9:11, NW) Mtu tumpendaye anaweza kufa kwenye aksidenti. Mzazi au rafiki wa karibu aweza kufa kutokana na ugonjwa usiotibika. Tusipozingatia tumaini letu la Ufalme, hali yetu ya kiroho yaweza kuhatarishwa majaribu hayo yatupatapo. Basi yafaa tujiulize, ‘Je “[ninashangilia] katika tumaini”? Mimi hutafakari juu ya tumaini hilo mara nyingi kadiri gani? Je, Paradiso itakayokuja ni halisi kwangu? Je, ninawazia nikiwa katika Paradiso hiyo? Je, ningali na hamu ileile niliyokuwa nayo hapo mwanzo nilipojifunza kweli, kuona mfumo wa sasa wa mambo ukiisha?’ Twapaswa kufikiria sana swali hilo la mwisho. Kwa nini? Kwa sababu ikiwa tuna afya njema, tuna pesa za kutosha, na tunaishi katika nchi isiyo na vita, isiyo na upungufu wa chakula, au misiba ya asili huenda—angalau kwa sasa—tukakosa kutambua uhitaji wa kuja upesi kwa ulimwengu mpya wa Mungu.

6. (a) Paulo na Sila walipopatwa na dhiki, walifikiria mambo gani? (b) Kielelezo cha Paulo na Sila chaweza kututiaje moyo leo?

6 Paulo alizidi kuwashauri Waroma ‘wavumilie chini ya dhiki.’ (Waroma 12:12) Paulo alijua dhiki ni nini. Wakati fulani katika maono Paulo aliona mtu aliyemwalika ‘avuke na kuingia Makedonia’ ili kusaidia watu wa hapo wajifunze juu ya Yehova. (Matendo 16:9) Baada ya hapo, Paulo, pamoja na Luka, Sila, na Timotheo walisafiri hadi Ulaya. Mishonari hao wenye bidii wangepatwa na nini? Na dhiki! Baada ya kuhubiri katika jiji la Makedonia la Filipi, Paulo na Sila walipigwa viboko na kutiwa gerezani. Ni wazi kwamba baadhi ya raia wa Filipi hawakuwa na ubaridi tu kuelekea ujumbe wa Ufalme bali waliupinga sana. Je, mishonari hao wenye bidii walipoteza shangwe yao baada ya mambo kubadilika? La. Baada ya kupigwa na kutiwa gerezani, “karibu na katikati ya usiku Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo.” (Matendo 16:25, 26) Bila shaka, Paulo na Sila hawakufurahia maumivu waliyopata kutokana na kupigwa, hata hivyo, mishonari hao wawili hawakuzingatia mambo hayo. Walifikiri juu ya Yehova na jinsi alivyokuwa akiwabariki. Kwa ‘kuvumilia kwa shangwe chini ya dhiki,’ Paulo na Sila waliweka kielelezo kizuri kwa ndugu zao katika Filipi na kwingineko.

7. Kwa nini tushukuru pia tunaposali?

7 Paulo aliandika hivi: “Dumuni katika sala.” (Waroma 12:12) Je, wewe husali unapokuwa na mahangaiko? Wewe husali kuhusu nini? Labda unataja tatizo lako hususa na kumwomba Yehova akusaidie. Lakini pia unaweza kushukuru kwa ajili ya baraka unazofurahia. Kutafakari wema ambao Yehova ametufanyia hutusaidia ‘kushangilia katika tumaini,’ matatizo yanapotokea. Daudi ambaye maisha yake yalijaa matatizo, aliandika hivi: “Ee BWANA, Mungu wangu, umefanya kwa wingi miujiza yako na mawazo yako kwetu; hakuna awezaye kufananishwa nawe; kama ningependa kuyatangaza na kuyahubiri, ni mengi sana hayahesabiki.” (Zaburi 40:5) Bila shaka, tutaendelea kuwa na shangwe ikiwa tutamwiga Daudi kwa kutafakari kwa ukawaida baraka ambazo tumepokea kutoka kwa Yehova.

Dumisha Mtazamo Unaofaa

8. Ni nini humsaidia Mkristo aendelee kuwa na furaha anaponyanyaswa?

8 Yesu anawatia moyo wafuasi wake wadumishe mtazamo unaofaa wanapokabiliana na majaribu mbalimbali. Asema hivi: “Wenye furaha ni nyinyi watu wawashutumupo na kuwanyanyasa nyinyi na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo ovu dhidi yenu kwa ajili yangu.” (Mathayo 5:11) Tuna sababu gani ya kufurahi chini ya hali hizo? Uwezo wetu wa kuvumilia upinzani huthibitisha kwamba tuna roho ya Yehova. Mtume Petro aliwaambia hivi Wakristo wenzake katika siku zake: “Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, nyinyi ni wenye furaha, kwa sababu roho ya utukufu, naam, roho ya Mungu, inatulia juu yenu.” (1 Petro 4:13, 14) Kupitia roho yake, Yehova atatusaidia pia kuvumilia na hivyo kudumisha shangwe yetu.

9. Ni nini kilichowasaidia ndugu fulani wapate shangwe walipokuwa gerezani kwa sababu ya imani yao?

9 Hata tunapokuwa chini ya hali mbaya sana, twaweza kuwa na sababu za kushangilia. Mkristo aitwaye Adolf alitambua ukweli wa jambo hilo. Anaishi katika nchi ambayo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku kwa miaka mingi. Adolf na wenzake kadhaa walikamatwa na kufungwa kwa muda mrefu kwa sababu hawakukana imani yao inayotegemea Biblia. Maisha ya gerezani yalikuwa magumu, lakini kama Paulo na Sila, Adolf na wenzake walikuwa na sababu za kumshukuru Mungu. Walisema kwamba mambo waliyokabili gerezani yaliwasaidia kuimarisha imani yao na kusitawisha sifa za Kikristo zinazofaa, kama vile ukarimu, huruma, na shauku ya kidugu. Kwa mfano, mfungwa alipopokea kifurushi kutoka nyumbani, aliwagawia waamini wenzake vitu vilivyokuwamo ndani, nao wakaona vitu hivyo vya ziada kuwa vinatoka kwa Yehova, Mpaji mkuu wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” Mpaji na wapokeaji walipata shangwe kwa sababu ya matendo hayo ya fadhili. Kwa hiyo ingawa walitiwa gerezani ili kuvunja imani yao, mambo yaliyowapata yalifanya wawe na nguvu zaidi za kiroho.—Yakobo 1:17; Matendo 20:35.

10, 11. Dada mmoja alitendaje alipohojiwa mfululizo na kufungwa kwa muda mrefu?

10 Ella, anayeishi pia katika nchi ambayo kazi ya Ufalme ilipigwa marufuku kwa muda mrefu, alikamatwa kwa sababu ya kuwajulisha wengine tumaini lake la Kikristo. Alihojiwa mfululizo kwa muda wa miezi minane. Hatimaye alipopelekwa mahakamani, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika gereza ambalo halikuwa na mwabudu mwingine wa Yehova. Wakati huo, Ella alikuwa na umri wa miaka 24 tu.

11 Bila shaka, si kwamba Ella alifurahia kutumia muda mwingi wa ujana wake gerezani. Lakini kwa kuwa hangeweza kubadili hali yake, aliamua kubadili maoni yake. Kwa hiyo alianza kuona gereza hilo kuwa eneo lake la kibinafsi la kutoa ushahidi. “Nilihubiri sana hivi kwamba miaka ilipita upesi sana,” asema. Baada ya miaka zaidi ya mitano, Ella alihojiwa tena. Watu waliokuwa wakimhoji walipotambua kwamba imani yake haikuvunjwa licha ya kufungwa gerezani, walimwambia hivi: “Hatuwezi kukuachilia; hujabadilika.” Ella alijibu hivi kwa uthabiti, “lakini nimebadilika! Sasa nina mtazamo mzuri kuliko wakati nilipotiwa gerezani, na imani yangu ni yenye nguvu kuliko hapo awali!” Kisha akaongezea: “Msipotaka kuniachilia, nitaendelea kukaa hapa hadi Yehova aonapo inafaa kunikomboa.” Ella hakupoteza shangwe yake kwa sababu ya kufungwa gerezani kwa muda wa miaka mitano na nusu! Alijifunza kuridhika na hali zozote zilizompata. Je, unaweza kujifunza jambo fulani kutokana na kielelezo chake?—Waebrania 13:5.

12. Mkristo anayekabili magumu aweza kupataje amani ya akili?

12 Usifikiri kwamba Ella ana kipawa fulani kisicho cha kawaida ambacho humwezesha kukabiliana na magumu hayo. Akirejezea kipindi alichohojiwa miezi kadhaa kabla ya kuhukumiwa, Ella akiri hivi: “Nakumbuka meno yangu yakigongana-gongana, na nilihisi kama ndege mdogo aliyeshtuliwa.” Hata hivyo, Ella ana imani yenye nguvu katika Yehova. Amejifunza kumtumaini. (Mithali 3:5-7) Kwa sababu hiyo amemwona Mungu kuwa halisi kwake kuliko hapo awali. Aeleza hivi: “Kila mara nilipoingia katika chumba cha kuhojiwa, nilihisi nikiwa na amani. . . . Kadiri hali ilivyozidi kuwa yenye kutisha, ndivyo nilivyohisi amani nyingi zaidi.” Yehova ndiye aliyekuwa chanzo cha amani hiyo. Mtume Paulo aeleza hivi: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

13. Tuna uhakikisho gani kwamba iwapo tutakabiliana na dhiki, tutakuwa na nguvu za kuvumilia?

13 Ella, ambaye tayari ameachiliwa, alidumisha shangwe yake licha ya magumu. Alivumilia kwa kutegemea nguvu alizopewa na Yehova wala si kwa kutegemea nguvu zake mwenyewe. Mtume Paulo, ambaye hakutegemea nguvu zake mwenyewe, aliandika hivi: “Kwa hiyo, kwa mteremo zaidi sana afadhali nijisifu kwa habari ya udhaifu wangu, ili nguvu ya Kristo ipate kubaki juu yangu. . . . Kwa maana niwapo dhaifu, ndipo niwapo mwenye nguvu.”—2 Wakorintho 12:9, 10.

14. Eleza jinsi Mkristo anavyoweza kuwa na maoni yafaayo kuhusu hali fulani yenye kujaribu na matokeo yake yaweza kuwa nini.

14 Huenda mikazo unayokabili leo ikatofautiana kidogo na ile ambayo tumetaja. Hata hivyo, hata mikazo hiyo iwe ya namna gani, si rahisi kukabiliana nayo. Kwa mfano, huenda mwajiri wako akachambua sana kazi yako kuliko anavyochambua kazi ya wafanyakazi wa dini nyingine. Huenda usiweze kupata kazi nyingine. Unaweza kudumishaje shangwe yako? Kumbuka Adolf na marafiki wake waliositawisha sifa muhimu kwa sababu ya mambo yaliyowapata gerezani. Ukijitahidi kwa unyofu kumpendeza mwajiri wako—hata yule ambaye ni “mgumu kupendeza”—utasitawisha sifa za Kikristo kama vile uvumilivu na ustahimilivu. (1 Petro 2:18) Isitoshe, huenda ukawa mfanyakazi anayefaa zaidi, jambo ambalo laweza kukusaidia kupata kazi yenye kuridhisha zaidi wakati fulani. Acheni sasa tuchunguze njia nyingine zinazoweza kutusaidia kudumisha shangwe yetu katika utumishi wa Yehova.

Kufanya Maisha Yawe Sahili Huleta Shangwe

15-17. Wenzi fulani wa ndoa walijifunza nini ambacho kingeweza kupunguza mkazo, hata ingawa kisababishi cha mkazo huo hakingeweza kukomeshwa kabisa?

15 Huenda usiweze kubadili kazi unayofanya au mahali pako pa kazi, lakini huenda ikawa unaweza kubadili mambo fulani maishani. Fikiria jambo lililoonwa lifuatalo.

16 Wenzi wa ndoa Wakristo walikaribisha mzee fulani nyumbani kwao kwa chakula. Jioni hiyo, ndugu na mke wake walimwambia mzee huyo kwamba hivi karibuni wamekuwa wakilemewa na mikazo ya maisha. Ingawa wote wawili walikuwa na kazi ya wakati wote iliyowataka watumie muda mwingi na jitihada nyingi, hawangeweza kutafuta kazi nyingine. Hawakujua wangeendelea kukabiliana na hali hiyo mpaka lini.

17 Alipoulizwa shauri, mzee huyo alijibu, “Fanyeni Maisha Yenu Yawe Sahili.” Jinsi gani? Mume na mke huyo walikuwa wakitumia muda wa saa tatu kila siku kwenda na kurudi kutoka kazini. Mzee huyo ambaye aliwajua vizuri wenzi hao wa ndoa aliwadokezea wahame na kuishi karibu na mahali pao pa kazi ili wapunguze muda wanaotumia kwenda kazini kila siku. Wangeweza kutumia muda huo wa ziada kushughulikia mambo mengine muhimu au kupumzika tu. Ikiwa unapoteza shangwe yako kwa kiasi fulani kwa sababu ya mikazo ya maisha, kwa nini usifikirie kama unaweza kupata kitulizo kwa kufanya marekebisho fulani?

18. Kwa nini ni muhimu kufikiri kwa makini kabla ya kufanya maamuzi?

18 Njia nyingine ya kupunguza mkazo ni kufikiria kwa makini kabla ya kufanya maamuzi. Kwa mfano, Mkristo mmoja aliamua kujenga nyumba. Alichagua plani ya jengo lenye vyumba vingi hata ingawa hakuwa amewahi kujenga nyumba hapo awali. Sasa anatambua kwamba angeweza kuepuka matatizo yasiyo ya lazima ikiwa ‘angeangalia sana aendavyo’ kabla ya kuchagua plani ya nyumba yake. (Mithali 14:15) Mkristo mwingine alikubali kuwa mdhamini wa mwamini mwenzake aliyepewa mkopo. Kupatana na makubaliano ya mkopo huo, ikiwa mwenye kukopeshwa angeshindwa kulipa, mdhamini angekuwa na jukumu la kuulipa. Mwanzoni, hakukuwa na matatizo yoyote, lakini baada ya muda mwenye kukopeshwa akashindwa kutimiza ahadi yake. Mkopeshaji alianza kuwa na wasiwasi na kudai mdhamini alipe mkopo wote. Mdhamini alipatwa na mkazo mkubwa sana. Je, angeweza kuepuka mikazo hiyo iwapo angefikiria kwa makini mambo yote yanayohusika kabla ya kukubali jukumu la kulipa mkopo huo?—Mithali 17:18.

19. Ni baadhi ya njia gani zinazoweza kutusaidia kupunguza mikazo maishani?

19 Tunapochoka, acheni tusifikiri kamwe kwamba tunaweza kupunguza mkazo na kupata tena shangwe yetu kwa kupunguza muda wa kufanya funzo la Biblia la kibinafsi, utumishi wa shambani, na kuhudhuria mikutano. Hayo ni mambo muhimu kwa kuwa kupitia hayo twaweza kupokea roho takatifu ya Yehova, ambayo hutokeza shangwe. (Wagalatia 5:22) Utendaji wa Kikristo huburudisha wakati wote na hauchoshi mtu kupindukia. (Mathayo 11:28-30) Huenda tunachoshwa na mambo ya kimwili au tafrija, bali si mambo ya kiroho. Kuzoea kulala mapema kwaweza kutusaidia tusichoke kupindukia. Kupumzika kwa muda mrefu zaidi kwaweza kunufaisha sana. N. H. Knorr, aliyetumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova hadi alipokufa, alizoea kuwaambia mishonari hivi: “Unapovunjika moyo, jambo la kwanza unalopaswa kufanya ni kupumzika. Utaona jambo ambalo hukuwa umetarajia, yaani itakuwa rahisi kutatua karibu kila tatizo baada ya kulala vizuri!”

20. (a) Taja kifupi baadhi ya njia zinazoweza kutusaidia tudumishe shangwe yetu. (b) Ni sababu gani zinazoweza kukufanya uwe mwenye shangwe? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 17.)

20 Wakristo wana pendeleo la kutumikia “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Kama vile tumeona, tunaweza kudumisha shangwe yetu hata tunapokabiliana na matatizo makubwa. Acheni tuendelee kufikiri juu ya tumaini la Ufalme, turekebishe mtazamo wetu inapokuwa lazima, na tufanye maisha yetu yawe sahili. Kisha, hata tujikute katika hali gani, tutatii maneno haya ya mtume Paulo: “Sikuzote shangilieni katika Bwana. Mara moja tena hakika nitasema, Shangilieni!”—Wafilipi 4:4.

Fikiria Maswali Haya kwa Makini:

• Kwa nini Wakristo wafikirie kwa uzito tumaini la Ufalme?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia tudumishe shangwe yetu wakati wa magumu?

• Kwa nini tujitahidi kufanya maisha yetu yawe sahili?

• Wengine wamefanya maisha yao yawe sahili katika njia gani?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 17]

Sababu Nyingine Zinazotufanya Tuwe Wenye Shangwe:

Tukiwa Wakristo, tuna sababu nyingi za kushangilia. Fikiria sababu zifuatazo:

1. Twamjua Yehova.

2. Tumejifunza kweli ya Neno la Mungu.

3. Tunaweza kusamehewa dhambi zetu kupitia imani katika dhabihu ya Yesu.

4. Ufalme wa Mungu unatawala —ulimwengu mpya utakuja hivi karibuni!

5. Yehova ametuingiza katika paradiso ya kiroho.

6. Tunafurahia ushirika ufaao wa Kikristo.

7. Tuna pendeleo la kushiriki kazi ya kuhubiri.

8. Tuko hai, na tuna nguvu kwa kiasi fulani.

Unaweza kutaja sababu ngapi nyingine za kuwa na shangwe?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Paulo na Sila walikuwa na shangwe hata walipokuwa gerezani

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, unakazia fikira tumaini lenye shangwe la ulimwengu mpya wa Mungu?