Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, ‘Unanunua Kabisa Wakati Unaofaa’?

Je, ‘Unanunua Kabisa Wakati Unaofaa’?

Je, ‘Unanunua Kabisa Wakati Unaofaa’?

MTUME Paulo aliwashauri hivi Wakristo Waefeso wa karne ya kwanza: “Fulizeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia kabisa wakati unaofaa, kwa sababu siku ni za uovu.” (Waefeso 5:15, 16) Kwa nini ushauri huo ulifaa? Ili kujibu swali hilo tunahitaji kujua hali ambazo Wakristo wa jiji hilo la zamani walikabili.

Efeso lilikuwa jiji maarufu kwa sababu ya utajiri wake mwingi, ukosefu mbaya sana wa maadili, uhalifu ulioenea sana, na shughuli mbalimbali zilizohusiana na roho waovu. Isitoshe, Wakristo huko walilazimika kukabiliana na itikadi za kifalsafa zilizohusu wakati. Wagiriki walioishi Efeso ambao hawakuwa Wakristo hawakuamini kwamba wakati hufuata mkondo uleule bila kubadilika. Walikuwa wamejifunza kutokana na falsafa ya Kigiriki kwamba maisha yalikuwa mzunguko tu usio na mwisho. Mtu ambaye angetumia vibaya wakati wake katika mzunguko mmoja wa maisha angeweza kuupata tena katika mzunguko mwingine. Huenda maoni kama hayo ndiyo yaliyofanya Wakristo Waefeso wasiitilie maanani sana ratiba ya Yehova ya matukio, kutia ndani ratiba yake ya hukumu. Kwa hiyo, ushauri wa Paulo wa ‘kununua kabisa wakati unaofaa’ ulifaa.

Paulo hakuwa anazungumza juu ya wakati tu kwa jumla. Neno la Kigiriki alilotumia lamaanisha wakati uliowekwa, wakati unaofaa kwa kusudi fulani. Paulo alikuwa anawashauri Wakristo wa karne ya kwanza watumie vizuri wakati unaofaa, wakati wao wa kupendelewa, kabla haujaisha na rehema za Mungu na fursa ya wokovu kuondolewa.—Waroma 13:11-13; 1 Wathesalonike 5:6-11.

Tunaishi katika wakati kama huo ambao unafaa. Badala ya kuutumia vibaya wakati huo wa kupendelewa ambao hatutaupata tena, kwa kufuatia raha za muda za ulimwengu, ni jambo la hekima kwa Wakristo kutumia wakati wanaopata kufanya “vitendo vya ujitoaji-kimungu” na hivyo kuimarisha uhusiano wao na Muumba, Yehova Mungu.—2 Petro 3:11; Zaburi 73:28; Wafilipi 1:10.