Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uwasiliani-roho Waweza Kutosheleza Mahitaji Yetu ya Kiroho?

Je, Uwasiliani-roho Waweza Kutosheleza Mahitaji Yetu ya Kiroho?

Je, Uwasiliani-roho Waweza Kutosheleza Mahitaji Yetu ya Kiroho?

SOTE tuna mahitaji ya kiroho na pia ya kimwili. Hiyo ndiyo sababu watu wengi huuliza maswali kama, Ni nini kusudi la maisha, kwa nini watu huteseka na inakuwaje tunapokufa? Watu wengi wenye moyo mweupe hutafuta majibu ya maswali hayo na mengine kama hayo kwenye mikutano ya uwasiliani-roho, ambako hutafuta ushauri wa wawasiliani-roho, wakitumaini kuwasiliana na roho za wafu. Zoea hilo linaitwa uwasiliani-roho.

Wale wanaowasiliana na roho wanapatikana katika nchi nyingi, nao hukusanyika katika makundi mbalimbali na makanisa. Kwa mfano, nchini Brazili, kuna watu wapatao 4,000,000 wanaowasiliana na roho. Watu hao hufuata mafundisho ya Hyppolyte Léon Denizard Rivail, mwalimu na mwanafalsafa Mfaransa wa karne ya 19, ambaye aliandika mafundisho hayo kwa kutumia jina bandia, Allan Kardec. Kardec alianza kupendezwa na uwasiliani-roho mwaka wa 1854. Baadaye aliwauliza maswali wawasiliani-roho kutoka sehemu nyingi na kuandika majibu yao katika kitabu, The Book of Spirits, kilichochapishwa mwaka wa 1857. Aliandika vitabu vingine viwili, The Mediums’ Book na The Gospel According to Spiritism.

Uwasiliani-roho umehusianishwa na mazoea ya kidini kama uchawi, ulogi, mazingaombwe, au Ibada ya Shetani. Hata hivyo, wale wanaofuata mafundisho ya Allan Kardec wanasema kwamba imani yao ni tofauti. Mara nyingi vichapo vyao hunukuu Biblia, nao humrejezea Yesu kuwa “kiongozi na kielelezo cha wanadamu wote.” Wanasema kwamba mafundisho ya Yesu ndiyo “sheria ya Mungu iliyo safi kushinda zote.” Allan Kardec aliyaona maandishi ya uwasiliani-roho kuwa ufunuo wa tatu wa sheria ya Mungu kwa wanadamu, ufunuo wa kwanza na wa pili ukiwa ule wa Musa na wa Yesu.

Uwasiliani-roho huvutia watu wengi kwa sababu hukazia upendo kwa jirani na kazi ya kutoa misaada. Mojawapo ya itikadi za wanaowasiliana na roho ni: “Bila kutoa misaada hakuna wokovu.” Wengi wanaowasiliana na roho wanashiriki kwa bidii huduma za kijamii, wakisaidia kujenga hospitali, shule, na mashirika mengine. Kazi kama hizo zastahili pongezi. Lakini je, imani ya wale wanaowasiliana na roho yapatana na mafundisho ya Yesu kama yalivyoandikwa katika Biblia? Acheni tuchunguze mifano miwili: tumaini la wafu na sababu ya kuteseka.

Wafu Wana Tumaini Gani?

Wengi wanaowasiliana na roho wanaamini katika kuzaliwa upya katika umbo jingine. Kichapo kimoja cha uwasiliani-roho chasema: “Kuzaliwa upya katika umbo jingine ndilo fundisho pekee ambalo lapatana na jinsi tunavyoelewa haki ya Mungu; ndilo fundisho pekee linaloweza kufafanua wakati ujao na kuimarisha matumaini yetu.” Wale wanaowasiliana na roho husema kwamba watu wanapokufa wanakuwa viumbe wa roho na kuacha mwili—kama vile kipepeo aachapo kifukofuko chake. Wanaamini kwamba baadaye viumbe hao wa roho huzaliwa upya wakiwa wanadamu ili kuondolea mbali dhambi walizofanya katika maisha ya awali. Lakini dhambi hizo za awali hazikumbukwi tena. “Mungu aliona inafaa dhambi zilizofanywa katika maisha ya awali zisahauliwe,” yasema The Gospel According to Spiritism.

“Kukana kwamba watu hawazaliwi upya katika umbo jingine ni sawa na kukana maneno ya Kristo,” akaandika Allan Kardec. Hata hivyo, Yesu hakutaja kamwe kuhusu “kuzaliwa upya katika umbo jingine” wala hakutaja dhana kama hiyo. (Ona “Je, Biblia Hufundisha Juu ya Kuzaliwa Upya Katika Umbo Jingine?” kwenye ukurasa wa 22.) Badala yake, Yesu alifundisha juu ya kufufuliwa kwa wafu. Wakati wa huduma yake ya kidunia, Yesu alifufua watu watatu—Lazaro, rafiki yake wa karibu, mwana wa mjane huko Naini, na binti ya ofisa-msimamizi wa sinagogi. (Marko 5:22-24, 35-43; Luka 7:11-15; Yohana 11:1-44) Acheni tufikirie mojawapo ya matukio hayo yenye kutokeza na tuone Yesu alimaanisha nini kwa neno “ufufuo.”

Ufufuo wa Lazaro

Yesu alisikia kwamba rafiki yake Lazaro alikuwa mgonjwa. Siku mbili baadaye, akawaambia wanafunzi wake: “Lazaro rafiki yetu ameenda kupumzika, lakini ninafunga safari huko ili kumwamsha kutoka usingizini.” Wanafunzi wake hawakuelewa Yesu alikuwa anamaanisha nini, kwa hiyo akasema waziwazi: “Lazaro amekufa.” Lazaro alikuwa mfu kwa siku nne wakati Yesu alipofika kwenye kaburi lake. Hata hivyo, Yesu aliamuru jiwe lililokuwa limefunika lango la kaburi liondolewe. Kisha akapaaza sauti: “Lazaro, njoo huku nje!” Wakati huo, jambo la ajabu likatukia. “Mtu aliyekuwa amekuwa mfu akatoka miguu na mikono yake ikiwa imefungwa vitambaa, na sura yake ilifungwa-fungwa kwa nguo. Yesu akawaambia: ‘Mfungueni mmwache aende.’”—Yohana 11:5, 6, 11-14, 43, 44.

Bila shaka, tukio hilo halikuwa kuzaliwa upya katika umbo jingine. Yesu alisema kwamba Lazaro aliyekuwa mfu alikuwa analala, bila ufahamu. Kama Biblia isemavyo, ‘mawazo yake yalikuwa yamepotea.’ ‘Hakujua neno lolote.’ (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5) Lazaro aliyefufuliwa hakuwa mtu tofauti aliyezaliwa upya akiwa na roho nyingine tofauti. Alikuwa na utu uleule, umri uleule, na kumbukumbu lilelile. Alirudia maisha yake ya kawaida aliyoishi kabla ya kifo chake cha mapema na kurudi kwa wapendwa wake waliokuwa wakiomboleza kifo chake.—Yohana 12:1, 2.

Lazaro alikufa tena baadaye. Kwa hiyo, kifo chake kilikuwa na maana gani? Ufufuo huo pamoja na ufufuo mwingine mbalimbali ambao Yesu alifanya, waimarisha tumaini letu katika ahadi ya Mungu kwamba watumishi Wake waaminifu watafufuliwa kwa wakati Wake alioweka. Miujiza hiyo ya Yesu yakazia sana maneno yake: “Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.”—Yohana 11:25.

Kuhusiana na ufufuo huo wa wakati ujao, Yesu alisema: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti [yangu] na kutoka, wale waliofanya mambo mema kwenye ufufuo wa uhai, wale waliozoea kufanya mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28, 29) Kama ilivyokuwa katika kisa cha Lazaro, huo utakuwa ufufuo wa wafu. Ufufuo huo hautakuwa wa kuunganisha roho zilizo hai na miili iliyofufuliwa ambayo imeoza na ambayo huenda hata ikawa imekuwa sehemu ya viumbe wengine. Muumba wa mbingu na dunia, ambaye ana hekima na uwezo usio na kifani, anaweza kufufua wafu.

Je, mafundisho ya Yesu Kristo juu ya ufufuo hayadhihirishi kwamba Mungu anapendezwa sana na kila mmoja wetu? Lakini vipi swali la pili lililoulizwa hapo awali?

Kwa Nini Watu Wanateseka?

Wanadamu wengi huteseka sana kwa sababu ya mambo yanayofanywa na watu wasio na hekima, uzoefu, au watu waovu. Namna gani maafa ambayo hayasababishwi na watu? Kwa mfano, kwa nini kuna aksidenti na misiba ya asili? Kwa nini watoto wengine huzaliwa wakiwa na kasoro? Allan Kardec aliona mambo hayo kuwa adhabu. Aliandika: “Ikiwa tunaadhibiwa basi ni lazima tuwe tulifanya kosa fulani. Ikiwa kosa hilo si la wakati huu basi lilifanywa katika maisha yetu ya awali.” Wale wanaowasiliana na roho wanafunzwa kusali hivi: “Bwana, Wewe ni mwenye haki yote. Lazima iwe ninastahili kupatwa na ugonjwa uliochagua unipate . . . naukubali kuwa adhabu kwa makosa niliyofanya katika maisha ya awali na majaribu ya imani na ujitiisho wangu kwa mapenzi Yako matakatifu.”—The Gospel According to Spiritism.

Je, Yesu alifundisha jambo kama hilo? La. Yesu alifahamu vema maneno haya ya Biblia: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhubiri 9:11, NW) Alijua kwamba wakati mwingine mambo mabaya hutokea. Si lazima tuwe tunaadhibiwa kwa sababu ya dhambi.

Fikiria jambo hili lililotukia katika maisha ya Yesu: “[Yesu] alipokuwa akipita aliona mtu aliye kipofu tangu kuzaliwa. Nao wanafunzi wake wakamwuliza: ‘Rabi, ni nani aliyefanya dhambi, mtu huyu au wazazi wake, hivi kwamba akazaliwa kipofu?’” Jibu alilotoa Yesu lilikuwa lenye kuarifu sana: “Mtu huyu hakufanya dhambi wala wazazi wake, bali ilikuwa ili kazi za Mungu zipate kufanywa dhahiri katika kisa chake. Baada ya kusema mambo haya, alitema mate chini akafanya udongo wa mfinyanzi kwa hayo mate, akaweka udongo wake wa mfinyanzi juu ya macho ya mtu huyo na kumwambia: ‘Nenda kajioshe katika dimbwi la Siloamu.’ . . . Na kwa hiyo akaenda na kujiosha, akarudi akiona.”—Yohana 9:1-3, 6, 7.

Maneno ya Yesu yalionyesha kwamba siyo mtu huyo wala wazazi wake waliofanya azaliwe akiwa kipofu. Kwa hiyo, Yesu hakuunga mkono wazo la kwamba mtu huyo alikuwa akiadhibiwa kwa sababu ya dhambi alizofanya katika maisha yake ya awali. Ni kweli kwamba Yesu alijua kuwa wanadamu wote wamerithi dhambi. Lakini wanarithi dhambi ya Adamu, si dhambi fulani walizofanya kabla ya kuzaliwa. Kwa sababu ya dhambi ya Adamu, wanadamu wote huzaliwa wakiwa watu wasio wakamilifu na wanaweza kupatwa na ugonjwa na kifo. (Ayubu 14:4; Zaburi 51:5; Waroma 5:12; 9:11) Bila shaka, Yesu alitumwa kurekebisha hali hiyo. Yohana Mbatizaji alisema kwamba Yesu alikuwa “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” *Yohana 1:29.

Ona pia kwamba, Yesu hakusema kwamba Mungu alifanya mtu huyo azaliwe akiwa kipofu kimakusudi ili Yesu aweze kuja kumponya siku fulani. Hilo lingekuwa tendo la ukatili na lenye kutweza kama nini! Je, jambo hilo lingemletea Mungu sifa? La. Kuponywa kimuujiza kwa mwanamume huyo kipofu ‘kulifanya kazi za Mungu ziwe dhahiri.’ Kama maponyo mengi ambayo Yesu alifanya, ponyo hilo lilionyesha upendo wa kweli wa Mungu kwa wanadamu wanaoteseka. Lilithibitisha pia kutegemeka kwa ahadi Yake ya kumaliza ugonjwa na kuteseka kwa wanadamu katika wakati Wake alioweka.—Isaya 33:24.

Je, si jambo lenye kufariji kujua kwamba badala ya kusababisha kuteseka, Baba yetu wa mbinguni huwapa “vitu vyema wale wanaomwomba”? (Mathayo 7:11) Aliye Juu Zaidi Sana atapata utukufu ulioje wakati macho ya vipofu yatakapofumbuliwa, na masikio ya viziwi kuzibuliwa, na walemavu kutembea, kuruka, na hata kukimbia!—Isaya 35:5, 6.

Kutosheleza Mahitaji Yetu ya Kiroho

Yesu alisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Naam, mahitaji yetu ya kiroho hutoshelezwa tusomapo Neno la Mungu, Biblia, na kuishi kulingana nayo. Kutafuta ushauri wa wawasiliani-roho hakutoshelezi kikamili mahitaji yetu ya kiroho. Kwa kweli, mazoea hayo yamekatazwa katika ule ambao Allan Kardec aliuita ufunuo wa kwanza wa sheria ya Mungu.—Kumbukumbu la Torati 18:10-13.

Watu wengi, kutia ndani wale wanaowasiliana na roho, wanatambua kwamba Mungu ni Mkuu Kuliko Wote, anaishi milele, ni mkamilifu kabisa, ni mwenye fadhili, ni mwema, na ni mwenye haki. Lakini Biblia hufunua mengi zaidi. Hufunua kwamba Mungu ana jina la kibinafsi, Yehova, ambalo lazima tulistahi kama Yesu alivyofanya. (Mathayo 6:9; Yohana 17:6) Jina hilo laonyesha kwamba Mungu ni mtu halisi ambaye wanadamu wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Waroma 8:38, 39) Kwa kusoma Biblia, sisi hujifunza kwamba Mungu ni mwenye rehema na kwamba “hakututenda sawasawa na hatia zetu, wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu.” (Zaburi 103:10) Kupitia Neno la Mungu lililoandikwa, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hufunua upendo wake, ukuu wake, na busara yake. Yeye ndiye huongoza na kulinda wanadamu watiifu. Kumjua Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo, ‘kwamaanisha uhai udumuo milele.’—Yohana 17:3.

Biblia hutoa habari zote tunazohitaji kuhusu makusudi ya Mungu, nayo hutuambia yale tupaswayo kufanya tukitaka kumpendeza. Tutapata majibu ya kweli na yenye kuridhisha kwa maswali yetu tukiichunguza Biblia kwa makini. Biblia pia hutupatia mwongozo juu ya yaliyo mema na yaliyo mabaya, na hutoa tumaini hakika. Hutuhakikishia kwamba karibuni, Mungu “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho [ya wanadamu], na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani [yatakuwa] yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Kupitia Yesu Kristo, Yehova atawakomboa wanadamu kutokana na dhambi na hali ya kutokamilika waliyorithi, nao wanadamu watiifu watarithi uhai udumuo milele kwenye dunia paradiso. Wakati huo, mahitaji yao ya kimwili na ya kiroho yatatoshelezwa kabisa.—Zaburi 37:10, 11, 29; Mithali 2:21, 22; Mathayo 5:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Ili upate habari zaidi juu ya chanzo cha dhambi na kifo, soma sura ya 6 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

JE, BIBLIA HUFUNDISHA JUU YA KUZALIWA UPYA KATIKA UMBO JINGINE?

Je, kuna maandiko yoyote ya Biblia yanayounga mkono fundisho la kuzaliwa upya katika umbo jingine? Ona baadhi ya maandiko yanayotumiwa na wale wanaoamini mafundisho hayo:

“Manabii na Sheria, walitoa unabii mpaka Yohana . . . Yeye mwenyewe ndiye ‘Eliya ambaye akusudiwa kuja.’”—Mathayo 11:13, 14.

Je, Yohana Mbatizaji alikuwa Eliya aliyekuwa amezaliwa upya? Alipoulizwa: “Je, wewe ndiwe Eliya?” Yohana alijibu waziwazi hivi: “Mimi siye.” (Yohana 1:21) Hata hivyo, ilikuwa imetabiriwa kwamba Yohana angemtangulia Mesiya “kwa roho na nguvu ya Eliya.” (Luka 1:17; Malaki 4:5, 6) Yaani, Yohana Mbatizaji alilinganishwa na Eliya kwa sababu alifanya kazi iliyofanana na ya Eliya.

“Isipokuwa yeyote azaliwe tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu. Usistaajabu kwa sababu nimekuambia wewe, Nyinyi watu lazima mzaliwe tena.”—Yohana 3:3, 7.

Baadaye, mmoja wa mitume aliandika hivi: “Asifiwe Mungu na Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo! Kwa huruma yake kuu alitufanya tuzaliwe upya kwa kumfufua Yesu kutoka wafu. Ametujalia tumaini lenye uhai.” (1 Petro 1:3, 4, Biblia Habari Njema; Yohana 1:12, 13) Ni wazi kwamba kuzaliwa upya ambako Yesu alirejezea ni jambo fulani la kiroho ambalo lingetukia wafuasi wake wakiwa wangali hai, si kuzaliwa upya katika umbo jingine wakati ujao.

“Mwanadamu anapokufa, anaishi milele; wakati siku zangu za kuishi Duniani zitakwisha, nitangoja, kwa kuwa nitarudi tena.”—“Tafsiri ya Kigiriki” ya andiko la Ayubu 14:14 iliyonukuliwa katika The Gospel According to Spiritism.

Andiko hilo limetafsiriwa hivi katika Biblia ya Union Version: “Mtu akifa je! atakuwa hai tena? Mimi ningengoja siku zote za vita vyangu, hata kufunguliwa kwangu kunifikilie.” Hebu soma muktadha wa andiko hilo. Utaona kwamba wafu wanangoja kaburini ili waje “kufunguliwa.” (Mstari wa 13) Hawangoji wakiwa hai. “Lakini mtu hufa na huo ndio mwisho wake. Akisha toa roho anabakiwa na nini tena?”—Ayubu 14:10, BHN.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Tumaini la ufufuo hudhihirisha kwamba Mungu anapendezwa sana na kila mmoja wetu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mungu atakomesha kuteseka kote kwa wanadamu