Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Wajane Wakabiliane na Majaribu Yao

Kuwasaidia Wajane Wakabiliane na Majaribu Yao

Kuwasaidia Wajane Wakabiliane na Majaribu Yao

SIMULIZI la Biblia kuhusu Ruthu na mkwe wake Naomi, ni mojawapo ya masimulizi yanayojulikana zaidi kuhusu wajane. Wanawake hao wawili walikuwa wajane. Hata hivyo, mume wa Naomi alikuwa amekufa na vilevile wanawe wawili. Mmoja wa wana hao waliokufa alikuwa mume wa Ruthu. Kwa kuwa waliishi katika jamii iliyotegemea kilimo ambacho kilifanywa hasa na wanaume, hali yao ilikuwa mbaya kwelikweli.—Ruthu 1:1-5, 20, 21.

Hata hivyo, Naomi alikuwa na rafiki wa pekee na mfariji, mkwe wake Ruthu, aliyekataa kumwacha. Baada ya muda, Ruthu akawa ‘anamfaa [Naomi] kuliko wana saba’—si kwa sababu tu ya kumpenda sana Naomi bali pia kwa sababu ya kumpenda Mungu. (Ruthu 4:15) Naomi alipopendekeza Ruthu arudi kwa familia na rafiki zake Wamoabu, Ruthu alijibu kwa maneno ya uaminifu na yenye kugusa moyo zaidi ambayo yamepata kuandikwa: “Wewe uendako nitakwenda, na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu; pale utakapokufa nitakufa nami, na papo hapo nitazikwa; BWANA anitende vivyo na kuzidi, ila kufa tu kutatutenga wewe nami.”—Ruthu 1:16, 17.

Yehova Mungu aliona mtazamo wa Ruthu. Alibariki jamaa ya Naomi na Ruthu iliyokuwa na watu wachache, na hatimaye Ruthu akaolewa na Mwisraeli aliyeitwa Boazi. Mtoto wao, ambaye alikuja kuwa babu ya Yesu Kristo, alitunzwa na Naomi kana kwamba alikuwa wake mwenyewe. Simulizi hilo laonyesha jinsi Yehova anavyowathamini wajane ambao humkaribia na kumtumaini. Zaidi ya hilo, Biblia hutuambia kwamba Yehova huthamini sana wale ambao kwa kuchochewa na upendo husaidia wajane katika majaribu yao. Kwa hiyo, leo twawezaje kutegemeza wajane miongoni mwetu?—Ruthu 4:13, 16-22; Zaburi 68:5.

Toa Msaada Hususa Pasipo Kutawala Maisha Yake

Unapomsaidia mjane, ni afadhali utoe msaada hususa pasipo kutawala maisha yake. Epuka kusema mambo kijuu-juu tu kama vile, “Ukihitaji kitu chochote nijulishe.” Hiyo ni sawa na kusema, “Fulizeni kujipasha moto na kulishwa vizuri” kwa mtu anayehisi baridi na njaa bila kumsaidia hata kidogo. (Yakobo 2:16) Watu wengi hawaombi msaada wanapohitaji kitu fulani; badala yake wao huteseka tu bila kusema chochote. Ili kusaidia watu wa namna hiyo, unahitaji kuwa na busara na kutambua mahitaji yao. Kwa upande mwingine, kutawala—hasa kudhibiti maisha ya mjane—kwaweza kumwudhi au kutokeza hali ya kutoelewana. Kwa hiyo, Biblia hukazia uhitaji wa kuwa na usawaziko tunaposhughulika na wengine. Ingawa inatutia moyo tupendezwe kibinafsi na masilahi ya wengine, inatukumbusha tusiwe wadaku.—Wafilipi 2:4; 1 Petro 4:15.

Ruthu alikuwa na mtazamo uliosawazika kama huo kuelekea Naomi. Ingawa alishikamana kwa uaminifu na mkwe wake, Ruthu hakumshinikiza au kumtawala. Alitenda kwa busara, kama vile kutafuta chakula chake na cha Naomi, na pia kutii maagizo ya Naomi.—Ruthu 2:2, 22, 23; 3:1-6.

Bila shaka, kila mtu ana mahitaji tofauti kabisa na ya mwingine. Sandra, aliyetajwa mwanzoni, asema: “Wakati wa huzuni nilipata nilichohitaji—marafiki wapendwa sana walikuja kwa wingi.” Kwa upande mwingine, Elaine aliyetajwa mapema, alihitaji wakati wa faragha. Kwa hiyo, mtu mwenye kujali ni mtambuzi na mwenye kudumisha usawaziko kuhusu kuheshimu wakati wa faragha wa wengine na kujitoa kusaidia inapohitajika.

Utegemezo wa Familia

Ikiwa kuna familia fulani changamfu na yenye upendo yaweza kufanya mengi ili kumhakikishia mjane kwamba anaweza kukabiliana na hali yake. Ingawa washiriki fulani wa familia wanaweza kutoa msaada mkubwa kuliko wengine, wote wanaweza kutimiza fungu fulani. “Ikiwa mjane yeyote ana watoto au wajukuu, acha hawa wajifunze kwanza kuzoea ujitoaji-kimungu kwa watu wa nyumbani mwao wenyewe na kufuliza kulipa wazazi na babu na nyanya zao fidia ipasayo, kwa maana hili ni lenye kukubalika machoni pa Mungu.”—1 Timotheo 5:4.

Huenda nyakati nyingine msaada wa kifedha au “marupurupu” yasihitajiwe. Wajane fulani wana pesa za kutosha kujikimu, na katika nchi fulani wengine hupokea msaada wa kifedha kutoka kwa serikali. Lakini mahali ambapo wajane wana uhitaji, washiriki wa familia wapaswa kusaidia. Ikiwa mjane hana watu wa jamaa wa karibu wa kumsaidia, au watu hao wa jamaa hawawezi kusaidia, Maandiko huwatia moyo waamini wenzake wamsaidie: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kutazama mayatima na wajane katika dhiki yao.”—Yakobo 1:27.

Wale wanaotenda kupatana na kanuni hizi za Biblia kwa kweli ‘huheshimu wajane.’ (1 Timotheo 5:3) Kwa kweli, kuheshimu mtu kwamaanisha kumwonyesha staha. Watu wanaoheshimiwa huhisi kwamba wanathaminiwa, wanapendwa, wanatambuliwa. Hawawi na maoni ya kwamba wengine wanawasaidia kwa sababu ni wajibu tu. Ingawa Ruthu alikuwa mjane kwa kipindi fulani, alimheshimu Naomi kwelikweli kwa hiari na kwa upendo kwa kuhakikisha kwamba amemtimizia Naomi mahitaji yake ya kimwili na ya kihisia-moyo. Kwa kweli, mtazamo wa Ruthu ulimpa sifa njema, hivi kwamba mwanamume aliyekuja kuwa mume wake alimwambia hivi: “Kila mtu katika mji wa watu wangu anakujua ya kwamba u mwanamke mwema.” (Ruthu 3:11, kielezi-chini) Bila shaka, Ruthu alifurahi kumsaidia Naomi kwa sababu Naomi alimpenda Mungu, hakudai mengi mno na alithamini sana jitihada za Ruthu za kumsaidia. Naomi ni kielelezo kizuri kama nini kwa wajane leo!

Mkaribie Mungu

Bila shaka, washiriki wa familia na marafiki hawawezi kuziba pengo lililoachwa na mwenzi aliyekufa. Kwa sababu hiyo ni muhimu mtu aliyefiwa amkaribie hasa “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Fikiria kielelezo cha Ana, mjane mcha Mungu aliyekuwa na umri wa miaka 84 wakati wa kuzaliwa kwa Yesu.

Mume wa Ana alipokufa miaka saba baada ya ndoa yao, alimgeukia Yehova ili kupata faraja. “Alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana kwa mifungo na dua.” (Luka 2:36, 37) Je, Yehova aliona ujitoaji-kimungu wa Ana? Ndiyo! Alimwonyesha upendo kwa njia ya pekee sana kwa kumruhusu aone mtoto ambaye baadaye alikuja kuwa Mwokozi wa ulimwengu. Jambo hilo lilimsisimua na kumfariji Ana kama nini! Bila shaka, alijionea ukweli wa Zaburi 37:4: “Nawe utajifurahisha kwa BWANA, naye atakupa haja za moyo wako.”

Mungu Hutenda Kupitia Wakristo Wenzetu

Elaine asema: “Muda mrefu baada ya David kufa, nilikuwa na maumivu makali kama ya kisu kinachogeuzwa-geuzwa mbavuni mwangu. Nilifikiri nina shida ya kumeng’enya chakula. Siku moja maumivu hayo yalikuwa makali sana hivi kwamba nilifikiri ningelazimika kumwona daktari. Dada mmoja wa kiroho ambaye pia ni rafiki mwenye utambuzi alidokeza kwamba huenda huzuni yangu ndiyo iliyosababisha maumivu hayo. Alinitia moyo nimwombe Yehova msaada na faraja. Nilikubali shauri lake mara moja na kutoa sala kimyakimya ya kutoka moyoni, nikimwomba Yehova anitegemeze nikabiliane na huzuni yangu. Naye alinitegemeza!” Elaine alipata nafuu, na punde baada ya hapo hata maumivu yake yakaisha.

Wazee wa kutaniko wanaweza hasa kuonyesha urafiki kwa njia ya fadhili kwa wajane walio na huzuni. Kwa kuwasaidia kiroho kwa ukawaida na kuwafariji kwa njia ya busara na utambuzi, wazee wanaweza kuwasaidia wamkaribie Yehova licha ya majaribu yao. Inapohitajika, wazee wanaweza pia kupanga msaada wa kimwili utolewe. Kwa kweli wazee hao watambuzi na wenye kujali huwa “mahali pa kujificha na upepo.”—Isaya 32:2; Matendo 6:1-3.

Faraja ya Kudumu Kutoka kwa Mfalme Mpya wa Dunia

Mtoto ambaye Ana mzee-mzee alifurahia kumwona miaka elfu mbili hivi iliyopita sasa amekuwa Mfalme wa Kimesiya wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu. Hivi karibuni serikali hiyo itaondoa mambo yote yanayosababisha huzuni, kutia ndani kifo. Kwa habari hii, Ufunuo 21:3, 4 husema: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Je, umeona kwamba andiko hilo larejezea “wanadamu”? Naam, wanadamu watakombolewa kutoka katika kifo na maombolezo yote na kilio ambacho husababishwa na kifo.

Lakini kuna habari njema zaidi! Biblia inaahidi pia ufufuo wa wafu. “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake [Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Kama Lazaro aliyefufuliwa na Yesu, wafu watatoka wakiwa wanadamu, si wakiwa viumbe wa roho. (Yohana 11:43, 44) Wale ambao baada ya hapo ‘watafanya mambo mema’ watakuwa wanadamu wakamilifu na kujionea kibinafsi utunzaji wa Yehova ulio kama wa baba ‘afumbuapo mkono wake na kushibisha kila kilicho hai matakwa yake.’—Zaburi 145:16.

Wale waliofiwa na mpendwa wao na walio na imani katika tumaini hili hakika, hufarijika sana. (1 Wathesalonike 4:13) Kwa hiyo, ikiwa wewe ni mjane, hakikisha ‘unasali bila kukoma’ ili upate faraja na msaada unaohitaji kila siku wa kushughulika na majukumu yako mbalimbali. (1 Wathesalonike 5:17; 1 Petro 5:7) Tumia wakati kila siku kusoma Neno la Mungu ili mawazo ya Mungu yakufariji. Ukifanya hivyo, utaona kwamba licha ya magumu na majaribu unayokabili ukiwa mjane, kwa kweli Yehova anaweza kukusaidia upate amani.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Kuwa mwenye kujali kwamaanisha kudumisha usawaziko kuhusu kuheshimu wakati wa faragha wa wengine na kujitoa unapohitajiwa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mungu alimbariki Ana aliyekuwa mjane mzeemzee