Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shangilieni Pamoja na Mungu Mwenye Furaha

Shangilieni Pamoja na Mungu Mwenye Furaha

Shangilieni Pamoja na Mungu Mwenye Furaha

“Mwishowe, akina ndugu, endeleeni kushangilia, . . . na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.”—2 WAKORINTHO 13:11.

1, 2. (a) Kwa nini watu wengi hawana shangwe maishani? (b) Shangwe ni nini, nasi twaweza kuisitawishaje?

KATIKA siku hizi zenye kuhuzunisha, watu wengi hawaoni jambo la kuwafurahisha. Watu hao au wapendwa wao wanapopatwa na msiba, huenda wakahisi kama Yobu wa kale, aliyesema hivi: “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.” (Ayubu 14:1) Wakristo hupatwa na mikazo ya “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na haishangazi kwamba nyakati nyingine watumishi waaminifu wa Yehova huvunjika moyo.—2 Timotheo 3:1.

2 Hata hivyo, Wakristo wanaweza kuwa na shangwe, hata wanapopatwa na majaribu. (Matendo 5:40, 41) Ili kuelewa jinsi wanavyoweza kuwa na shangwe, fikiria kwanza maana ya neno shangwe. Shangwe imefafanuliwa kuwa ‘furaha ya kuwa na kitu kizuri au ya kutazamia kitu kizuri.’ * Kwa sababu hiyo, tunapofikiria mambo mazuri tuliyo nayo sasa na vilevile kutafakari shangwe tutakayopata katika ulimwengu mpya wa Mungu, twaweza kuwa wenye shangwe.

3. Ni katika maana gani inaweza kusemwa kwamba kila mtu ana sababu fulani za kushangilia?

3 Kila mtu amebarikiwa kwa njia fulani ambayo yapasa kumfanya ashukuru. Huenda kichwa cha familia akapoteza kazi yake. Bila shaka, atakuwa na wasiwasi. Anataka kuwaruzuku wapendwa wake. Hata hivyo, ikiwa ana nguvu za kimwili na afya njema, ana sababu za kushukuru. Akipata kazi ataweza kuifanya kwa bidii. Kwa upande mwingine, huenda mwanamke Mkristo akapatwa na ugonjwa wenye kudhoofisha. Hata hivyo, anaweza kushukuru kwa ajili ya msaada kutoka kwa marafiki na washiriki wa familia wenye upendo ambao humsaidia kukabiliana na ugonjwa wake kwa utulivu na ujasiri. Hata hali zao ziweje, Wakristo wote wa kweli wanaweza kushangilia katika pendeleo la kumjua Yehova, “Mungu mwenye furaha,” na Yesu Kristo, ‘Mtawala pekee na mwenye furaha.’ (1 Timotheo 1:11; 6:15) Naam, Yehova Mungu na Yesu Kristo ni wenye furaha kwelikweli. Wamedumisha shangwe yao licha ya uhakika kwamba hali zilizopo duniani zatofautiana kabisa na jinsi Yehova alivyokusudia hapo mwanzoni. Kielelezo chao chaweza kutufundisha mengi kuhusu jinsi tunavyoweza kudumisha shangwe yetu.

Hawajawahi Kupoteza Shangwe Yao

4, 5. (a) Yehova alihisije wanadamu wa kwanza walipoasi? (b) Yehova alidumishaje mtazamo mzuri kuelekea wanadamu?

4 Katika bustani ya Edeni, Adamu na Hawa walikuwa na afya nzuri na akili kamilifu. Waliishi katika mazingira mazuri na walikuwa na kazi yenye kuthawabisha. Zaidi ya yote, walikuwa na pendeleo la kuwasiliana na Yehova kwa ukawaida. Mungu alikusudia wawe na wakati ujao wenye furaha. Lakini wazazi wetu wa kwanza hawakuridhika na zawadi hizo nzuri; waliiba tunda lililokatazwa kutoka katika “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Tendo hilo la kutotii lilisababisha hali ya huzuni ambayo sisi wazao wao hupatwa nayo leo.—Mwanzo 2:15-17; 3:6; Waroma 5:12.

5 Hata hivyo, Yehova hakupoteza shangwe yake kwa sababu ya mtazamo wa Adamu na Hawa wa kukosa shukrani. Alikuwa na uhakika kwamba baadhi ya wazao wao wangechochewa na mioyo yao kumtumikia. Alikuwa na uhakika mwingi sana hivi kwamba hata kabla Adamu na Hawa hawajapata mtoto wao wa kwanza, alitangaza kusudi lake la kukomboa wazao wao watiifu! (Mwanzo 1:31; 3:15) Katika karne zilizofuata, wengi walitenda kama Adamu na Hawa, lakini Yehova hakuwakataa wanadamu kwa sababu ya kutotii huko kulikoenea sana. Badala yake, alielekeza fikira zake kwa wanaume na wanawake ‘walioufurahisha moyo wake,’ wale waliojitahidi kwelikweli kumpendeza kwa sababu walimpenda.—Mithali 27:11; Waebrania 6:10.

6, 7. Ni mambo gani yaliyomsaidia Yesu kudumisha shangwe?

6 Namna gani Yesu—yeye alidumishaje shangwe yake? Akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu huko mbinguni, Yesu alikuwa na fursa ya kutazama matendo ya wanaume na wanawake duniani. Hali yao ya kutokuwa wakamilifu ilikuwa wazi, hata hivyo Yesu aliwapenda. (Mithali 8:31) Baadaye, alipokuja duniani na “[ku]kaa miongoni” mwa wanadamu, hakubadili maoni yake kuelekea wanadamu. (Yohana 1:14) Ni nini kilichomwezesha Mwana mkamilifu wa Mungu adumishe mtazamo huo mzuri kuelekea wanadamu wenye dhambi?

7 Kwanza kabisa, Yesu alikuwa na maoni ya kiasi kujihusu na kuhusu wengine. Alijua kwamba hangeweza kugeuza imani ya watu wote ulimwenguni. (Mathayo 10:32-39) Kwa hiyo alishangilia hata kama ni mtu mmoja tu mnyofu aliyekubali ujumbe wa Ufalme. Ingawa wakati fulani mwenendo na mtazamo wa wanafunzi wake haukupendeza, Yesu alijua kwamba walitaka kufanya mapenzi ya Mungu kutoka moyoni, na aliwapenda kwa sababu hiyo. (Luka 9:46; 22:24, 28-32, 60-62) Katika sala aliyomtolea Baba yake wa kimbingu, twaweza kuona kwamba Yesu alitaja jinsi wanafunzi wake walivyojiendesha ifaavyo kufikia wakati huo: “Nao wameshika neno lako.”—Yohana 17:6.

8. Taja baadhi ya njia ambazo twaweza kumwiga Yehova na Yesu katika kudumisha shangwe yetu.

8 Bila shaka, sote twaweza kunufaika kwa kuiga mfano uliowekwa na Yehova Mungu na Kristo Yesu kuhusu jinsi ya kudumisha shangwe. Je, twaweza kumwiga Yehova kwa ukamili zaidi labda kwa kutokuwa na wasiwasi kupita kiasi mambo yasipotukia kama tulivyotarajia? Je, twaweza kufuata kwa ukaribu zaidi hatua za Yesu kwa kudumisha mtazamo unaofaa kuelekea hali zetu za sasa, na vilevile kuwa wenye kiasi katika mambo tunayotarajia kutoka kwetu na kwa wengine? Acheni tuone jinsi baadhi ya kanuni hizi zinavyoweza kutumiwa ifaavyo katika huduma ya shambani ambayo inapendwa sana na Wakristo wenye bidii kila mahali.

Dumisha Mtazamo Unaofaa Kuhusu Huduma

9. Shangwe ya Yeremia ilichochewaje upya, na kielelezo chake chaweza kutusaidiaje?

9 Yehova anataka tuwe wenye shangwe katika utumishi wake. Shangwe yetu haipasi kutegemea matokeo tunayopata. (Luka 10:17, 20) Nabii Yeremia alihubiri kwa miaka mingi katika eneo ambalo halikuwa na matokeo. Alipofikiria jinsi watu walivyoitikia vibaya, alipoteza shangwe yake. (Yeremia 20:8) Lakini alipofikiria uzuri wa ujumbe huo, shangwe yake ilichochewa upya. Yeremia alimwambia Yehova hivi: “Maneno yako yalionekana, nami nikayala; na maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina lako, Ee BWANA, Mungu wa majeshi.” (Yeremia 15:16) Naam, Yeremia alifurahia pendeleo lake la kuhubiri neno la Mungu. Sisi pia twaweza kulifurahia.

10. Tunaweza kudumishaje shangwe yetu katika huduma hata ikiwa eneo letu halina matokeo wakati wa sasa?

10 Hata wengi wakikataa kukubali habari njema, tuna sababu kubwa sana ya kushangilia tunapokuwa katika huduma ya shambani. Kumbuka kwamba Yehova alikuwa na uhakika kabisa kwamba baadhi ya wanadamu wangechochewa kumtumikia. Kama vile Yehova, hatupaswi kukata tamaa kamwe kwamba huenda hatimaye watu fulani wakatambua suala la enzi kuu na kukubali ujumbe wa Ufalme. Hatupaswi kusahau kwamba hali za watu hubadilika. Mtu anapopatwa na msiba au tatizo fulani ambalo hakutarajia, hata kama alikuwa ameridhika na maisha kadiri gani, huenda akaanza kufikiria kwa uzito kusudi la maisha. Je, utakuwa tayari kusaidia wakati mtu kama huyo atakapoona ‘uhitaji wake wa kiroho’? (Mathayo 5:3) Kwani, huenda mtu fulani katika eneo lenu akakubali kusikiliza habari njema utakapomtembelea wakati ujao!

11, 12. Ni nini kilichotukia katika mji fulani, nasi twaweza kujifunza nini kutokana na jambo hilo?

11 Aina ya watu wanaoishi katika eneo letu wanaweza kubadili maoni yao pia. Fikiria kielelezo kimoja. Katika mji mmoja mdogo, paliishi kikundi cha wenzi wa ndoa wachanga waliokuwa na watoto na ambao walikuwa na uhusiano wa karibu. Mashahidi wa Yehova walipowatembelea, walipata jibu lilelile kwenye kila mlango, “Hatupendezwi!” Mtu fulani alipoonyesha upendezi wa kweli katika ujumbe wa Ufalme, majirani walimvunja moyo mara moja asiendelee kuwasiliana na Mashahidi. Bila shaka, ilikuwa vigumu sana kuhubiri eneo hilo. Hata hivyo, Mashahidi hawakukata tamaa; waliendelea kuhubiri. Matokeo yakawaje?

12 Baada ya muda, watoto wengi katika mji huo walikua, wakafunga ndoa na kuendelea kuishi katika mji huo. Walipotambua kwamba njia yao ya maisha haikuwaletea furaha ya kweli, baadhi ya vijana hao walianza kutafuta kweli. Waliipata kweli walipokubali habari njema zinazotangazwa na Mashahidi. Kwa hiyo baada ya miaka mingi kutaniko dogo likaanza kukua. Hebu wazia jinsi wahubiri wa Ufalme walivyoshangilia kwa sababu hawakukata tamaa! Acheni tupate shangwe vilevile kwa kuhubiri kwa bidii ujumbe wa Ufalme wenye utukufu!

Waamini Wenzako Watakutegemeza

13. Tunaweza kuwaendea nani tunapovunjika moyo?

13 Mikazo inapoongezeka au unapopatwa na msiba, unaweza kutafuta faraja wapi? Watumishi wengi waliojiweka wakfu kwa Yehova, humwendea kwanza katika sala, kisha huwaendea ndugu na dada zao Wakristo. Alipokuwa duniani, Yesu mwenyewe alithamini utegemezo wa wanafunzi wake. Usiku uliotangulia kifo chake, alisema kwamba wao ndio ‘walioshikamana naye katika majaribu yake.’ (Luka 22:28) Bila shaka, wanafunzi hao hawakuwa wakamilifu, lakini uaminifu-mshikamanifu wao ulimfariji Mwana wa Mungu. Sisi pia twaweza kupata faraja kutoka kwa waamini wenzetu.

14, 15. Ni nini kilichowasaidia wenzi fulani wa ndoa kukabiliana na kifo cha mwana wao, nawe unajifunza nini kutokana na jambo lililowapata?

14 Wenzi wa ndoa Wakristo, Michel na Diane, walijifunza jinsi utegemezo wa ndugu na dada zao uwezavyo kuwa wenye thamani. Mwana wao mwenye umri wa miaka 20 anayeitwa Jonathan, Mkristo mwenye nguvu na mataraja mema, alipimwa na kupatikana kuwa na uvimbe wa ubongo. Madaktari walijaribu juu chini kumwokoa, lakini hali ya Jonathan ilizorota hadi akafa alasiri moja. Michel na Diane walihuzunika kwelikweli. Walitambua kwamba Mkutano wa Utumishi, uliokuwa unafanywa siku hiyo, ulikuwa unakaribia kwisha. Hata hivyo, kwa kuwa walihitaji kufarijiwa sana, walimwomba mzee aliyekuwa pamoja nao aambatane nao hadi kwenye Jumba la Ufalme. Waliwasili tu wakati ambapo kutaniko lilikuwa likijulishwa habari za kifo cha Jonathan. Baada ya mkutano, wazazi hao waliokuwa wamejaa majonzi walizungukwa na ndugu na dada zao waliowakumbatia na kuwafariji. Diane akumbuka hivi: “Tulikuwa na huzuni nyingi sana tulipofika kwenye jumba, lakini tulipata faraja iliyoje kutoka kwa akina ndugu—walitutia moyo kama nini! Ingawa hawangeweza kutuondolea maumivu, walitusaidia kuvumilia chini ya mkazo!”—Waroma 1:11, 12; 1 Wakorintho 12:21-26.

15 Msiba huo ulifanya Michel na Diane wawe na uhusiano wa karibu zaidi na ndugu zao. Pia uliwafanya wawe na uhusiano wa karibu zaidi wao kwa wao. Michel asema hivi: “Nimejifunza kumthamini zaidi mke wangu mpendwa. Tunapovunjika moyo, tunazungumza kuhusu kweli ya Biblia na jinsi Yehova anavyotutegemeza.” Diane aongezea hivi: “Tumaini la Ufalme lina maana kubwa hata zaidi kwetu leo.”

16. Kwa nini ni muhimu kuchukua hatua ya kwanza kuwajulisha ndugu zetu mahitaji yetu?

16 Naam, ndugu na dada zetu Wakristo wanaweza kuwa “msaada wenye ku[tu]tia nguvu” wakati wenye magumu maishani na hivyo kutusaidia tudumishe shangwe yetu. (Wakolosai 4:11) Bila shaka, hawawezi kujua mambo tunayofikiri. Kwa hiyo, tunapohitaji utegemezo, ni vizuri kuwajulisha mahitaji yetu. Ndipo tutakapoweza kuonyesha uthamini halisi kwa faraja tunayopata kutoka kwa ndugu zetu, na kuiona kuwa inatoka kwa Yehova.—Mithali 12:25; 17:17.

Angalia Vielelezo Katika Kutaniko Lako

17. Mama mmoja asiye na mwenzi hukabili magumu gani, nasi twawaonaje watu kama yeye?

17 Kadiri uangaliavyo vielelezo vya waamini wenzako, ndivyo utakavyojifunza kuwathamini zaidi na kupata shangwe kwa kushirikiana nao. Angalia vielelezo katika kutaniko lako. Unaona nini? Je, kuna mzazi asiye na mwenzi ambaye anajitahidi kulea watoto wake katika njia ya kweli? Je, umewahi kufikiria kwa makini kielelezo kizuri anachoweka? Jaribu kuwazia baadhi ya matatizo anayokabili. Jeanine, ambaye ni mama asiye na mwenzi, ataja baadhi ya matatizo hayo: upweke, kutongozwa na wanaume kazini, kutokuwa na fedha za kutosha. Lakini asema jambo lililo gumu kuliko yote ni kushughulikia mahitaji ya kihisia-moyo ya watoto wake, kwa kuwa kila mtoto ni tofauti na mwingine. Jeanine ataja tatizo jingine: “Inaweza kuwa vigumu sana kukinza mwelekeo wa kutaka mwanao atende kama kichwa cha nyumba yako ili kujazia pengo la kutokuwa na mume. Nina binti, na nyakati nyingine ninasahau na kumlemea kwa kumweleza matatizo yangu ya ndani kabisa.” Sawa na maelfu ya wazazi wasio na wenzi na wanaomhofu Mungu, Jeanine anafanya kazi ya wakati wote na kutunza familia yake. Pia huwafundisha watoto wake Biblia, huwazoeza katika huduma, na kuwapeleka katika mikutano ya kutaniko. (Waefeso 6:4) Lazima Yehova awe anafurahi kama nini aonapo kila siku jitihada ya familia hii ya kudumisha uaminifu-maadili! Je, hatufurahi kuwa na watu kama hao miongoni mwetu? Bila shaka, tunafurahi.

18, 19. Eleza jinsi tunavyoweza kuwaonyesha uthamini zaidi washiriki wa kutaniko.

18 Angalia tena vielelezo katika kutaniko lako. Huenda ukaona wajane wanawake au wanaume ambao ‘hawakosi kamwe’ mikutanoni. (Luka 2:37) Je, wao huhisi upweke nyakati nyingine? Bila shaka. Wanatamani sana kuwa na wenzi wao! Lakini wanakuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova na wanapendezwa kibinafsi na wengine. Mtazamo wao wenye utulivu na unaofaa huongeza shangwe ya kutaniko! Mkristo mmoja ambaye ametumikia katika huduma ya wakati wote kwa miaka zaidi ya 30 alisema hivi: “Jambo moja linalonipa shangwe kubwa zaidi ni kuona ndugu na dada wenye umri mkubwa ambao wamepatwa na majaribu mengi na bado wanamtumikia Yehova kwa uaminifu!” Naam, Wakristo wenye umri mkubwa miongoni mwetu ni kitia-moyo kikubwa kwa wachanga.

19 Namna gani wapya ambao wameanza tu kushirikiana na kutaniko hivi karibuni? Je, hatuchochewi kuona wakidhihirisha imani yao kwenye mikutano? Fikiria maendeleo ambayo wamefanya tangu waanze kujifunza Biblia. Lazima Yehova awe anapendezwa sana nao. Je, tunapendezwa nao? Je, tunaonyesha kwamba tunawaunga mkono kwa kuwapongeza kwa ajili ya jitihada zao?

20. Kwa nini tunaweza kusema kwamba kila mshiriki wa kutaniko huchangia fungu muhimu kutanikoni?

20 Je, umefunga ndoa, u mseja, au mzazi asiye na mwenzi? Je, wewe ni msichana au mvulana asiye na baba (au mama), mjane mwanamke au mwanamume? Je, umeshirikiana na kutaniko kwa miaka mingi au umeanza kushirikiana nalo hivi karibuni tu? Uwe na hakika kwamba kielelezo chako cha uaminifu hututia moyo sote. Na unaposhiriki kuimba wimbo wa Ufalme, unapotoa maelezo au hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, tunafurahi hata zaidi. Jambo la maana hata zaidi, ni kwamba unaufurahisha moyo wa Yehova.

21. Tuna sababu nyingi za kufanya nini, lakini ni maswali gani yanayozuka?

21 Naam, hata katika nyakati hizi zenye matatizo, tunaweza kuwa wenye furaha tunapomwabudu Mungu wetu mwenye furaha. Tuna sababu nyingi za kukubali kitia-moyo cha Paulo: “Endeleeni kushangilia, . . . na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.” (2 Wakorintho 13:11) Ingawa hivyo, vipi tukipatwa na msiba wa asili, mnyanyaso, au magumu ya kiuchumi? Je, tunaweza kudumisha shangwe yetu hata tunapokabiliana na hali kama hizo? Fikiria utakavyofanya uchunguzapo makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Ona kichapo Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 119, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kujibu?

• Shangwe inafafanuliwaje?

• Kudumisha mtazamo unaofaa kwaweza kutusaidiaje tuendelee kuwa wenye shangwe?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia tuwe na maoni yanayofaa kuhusu eneo la kutaniko letu?

• Ni katika njia gani mbalimbali unawathamini ndugu na dada katika kutaniko lako?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watu katika eneo letu wanaweza kubadili maoni yao

[Picha katika ukurasa wa 12]

Washiriki wa kutaniko lako hukabili magumu gani?