Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunapata Nguvu na Shangwe kwa Kuendelea Kufuata Njia ya Yehova

Tunapata Nguvu na Shangwe kwa Kuendelea Kufuata Njia ya Yehova

Simulizi la Maisha

Tunapata Nguvu na Shangwe kwa Kuendelea Kufuata Njia ya Yehova

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA LUIGGI D. VALENTINO

“Njia ni hii, ifuateni,” Yehova anashauri. (Isaya 30:21) Nimeazimia kufuata ushauri huo tangu nilipobatizwa miaka 60 iliyopita. Nilifanya azimio hilo mapema kutokana na kielelezo cha wazazi wangu ambao mwaka wa 1921 walihamia Cleveland, Ohio, Marekani kutoka Italia. Walilelea watoto watatu huko—mimi, kaka yangu, Mike, na dada yangu mdogo, Lydia.

WAZAZI wangu walichunguza dini mbalimbali lakini hatimaye wakakata tamaa. Kisha siku moja mwaka wa 1932, Baba alikuwa anasikiliza kipindi fulani cha Kiitalia kwenye redio. Kipindi hicho kilikuwa kinatangazwa na Mashahidi wa Yehova naye Baba alipendezwa na mambo aliyosikia. Aliandika barua ili apate habari zaidi, hivyo Shahidi mmoja Mwitalia, kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, akaja kututafuta. Baada ya mazungumzo machangamfu yaliyoendelea hadi mapambazuko, wazazi wangu walikuwa na hakika kwamba walikuwa wamepata dini ya kweli.

Baba na Mama walianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuwakaribisha nyumbani waangalizi wasafirio. Japo nilikuwa kivulana tu, wanaume hao walikubali niandamane nao katika kazi ya kuhubiri, nao wakafanya nifikirie kumtumikia Yehova wakati wote. Carey W. Barber, ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikuwa mmoja wa waangalizi waliotutembelea. Muda si muda, nikabatizwa Februari 1941 nikiwa na umri wa miaka 14, na mwaka wa 1944 nikaanza kutumikia nikiwa painia huko Cleveland. Mike na Lydia pia walijifunza kweli ya Biblia. Mike alimtumikia Yehova hadi alipokufa, naye Lydia aliandamana na mume wake, Harold Weidner, kwa miaka 28 katika huduma ya kusafiri. Leo, wanatumikia wakati wote wakiwa wahudumu wa pekee.

Kifungo Chaimarisha Azimio Langu la Kuendelea

Mapema mwaka wa 1945, nilifungwa katika gereza la Chillicothe Federal Prison huko Ohio kwa kuwa dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia ilinichochea kutenda kulingana na andiko la Isaya 2:4, ambalo lazungumza juu ya kufua panga kuwa majembe. Wakati fulani, wasimamizi wa gereza waliwaruhusu wafungwa Mashahidi kuwa na vichapo vichache tu vinavyotegemea Biblia ambavyo hu chapishwa na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, Mashahidi wa kutaniko moja la karibu walisaidia. Nyakati fulani, waliangusha vichapo kadhaa katika eneo lililokuwa karibu na gereza. Asubuhi iliyofuata, wafungwa walipokuwa wakipelekwa mahali pao pa kazi, walitafuta-tafuta vichapo hivyo na wakafaulu kuviingiza gerezani. Nilipofika tu gerezani, tuliruhusiwa kuwa na vichapo zaidi. Ijapokuwa hivyo, nilijifunza kuthamini hata zaidi chakula cha kiroho ambacho Yehova huandaa—jambo ambalo mimi hulikumbuka kila mara nipokeapo toleo jipya la Mnara wa Mlinzi au Amkeni!

Ingawa tuliruhusiwa kufanya mikutano ya kutaniko gerezani, ni Mashahidi tu ndio walioruhusiwa kuhudhuria. Hata hivyo, maofisa na wafungwa fulani walihudhuria kisiri, na baadhi yao hata wakajifunza kweli. (Matendo 16:30-34) Ziara za Ndugu A. H. Macmillan zilitufariji sana. Sikuzote alituhakikishia kwamba wakati tuliotumikia gerezani ulikuwa na manufaa kwa sababu ulitupa mazoezi kwa ajili ya migawo ya baadaye. Ndugu huyo mpendwa, aliyekuwa na umri mkubwa, aliimarisha azimio langu la kuendelea kutembea katika njia ya Yehova.

Napata Mwenzi

Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kwisha, tuliachiliwa kutoka gerezani, nami nikaanza tena upainia, huduma ya wakati wote. Lakini mwaka wa 1947 babangu akafa. Ili kutegemeza familia yetu, nilianza kufanya kazi na pia nikawa stadi katika matibabu ya kukanda mwili—ustadi ambao ungenisaidia wakati mgumu ambao mimi na mke wangu tulikabili miaka 30 baadaye. Lakini nimeanza kuzungumzia mambo ambayo sipaswi kuzungumzia sasa. Kwanza, acheni niwaeleze kuhusu mke wangu.

Nilipokuwa kwenye Jumba la Ufalme, alasiri moja mwaka wa 1949, simu ililia. Nilipoichukua nilisikia sauti tamu ikisema: “Jina langu ni Christine Genchur. Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nimehamia Cleveland kutafuta kazi, na nataka kujiunga na mojawapo ya makutaniko.” Jumba letu la Ufalme lilikuwa mbali na mahali alipoishi, lakini nilipendezwa na sauti yake, kwa hiyo nikampa maelezo ya jinsi ambavyo angefika kwenye jumba letu na kumtia moyo aje Jumapili hiyohiyo—siku ambayo ningetoa hotuba ya watu wote. Jumapili, mimi ndiye niliyekuwa wa kwanza kufika kwenye Jumba la Ufalme, lakini sikuona dada ambaye sikumfahamu. Muda wote niliotoa hotuba hiyo, nilitazama-tazama kwenye mlango lakini hakuna mtu aliyeingia. Nilimpigia simu siku iliyofuata, naye akaniambia kwamba hakujua angetumia basi gani kuja. Hivyo nikajitolea kukutana naye ili nimwelezee mambo vizuri zaidi.

Nilipata kujua kwamba wazazi wake, waliokuwa wahamiaji kutoka Chekoslovakia, walikuwa wameanza kushirikiana na Wanafunzi wa Biblia baada ya kusoma kijitabu Wafu Wako Wapi? (Where are the Dead?) Wazazi wake walibatizwa mwaka wa 1935. Katika mwaka wa 1938, babake Christine akawa mtumishi wa kampuni (ambaye sasa anaitwa mwangalizi-msimamizi) wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova huko Clymer, Pennsylvania, Marekani. Christine alibatizwa mwaka wa 1947 akiwa na umri wa miaka 16. Muda si muda, nikaanza kumpenda dada huyo wa kiroho, mwenye sura nzuri. Tulioana Juni 24, 1950, na tangu wakati huo Christine amekuwa mwenzi wangu mwaminifu, na wakati wote yeye yu tayari kutanguliza masilahi ya Ufalme wa Mungu. Ninamshukuru Yehova kwamba Christine, ambaye ni mwenzi mwenye ujuzi, alikubali nimwoe.—Mithali 31:10.

Mshangao Mkubwa

Tulianza kupainia pamoja Novemba 1, 1951. Miaka miwili baadaye, kwenye mkusanyiko huko Toledo, Ohio, Ndugu Hugo Riemer na Ndugu Albert Schroeder walizungumza na mapainia kadhaa waliopendezwa na utumishi wa mishonari. Tulikuwa miongoni mwao. Tulitiwa moyo kuendelea kupainia huko Cleveland, lakini mwezi uliofuata, tulishangaa sana kupokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 23 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, lililoanza Februari 1954!

Tukiwa njiani kwenda Shule ya Gileadi, iliyokuwa South Lansing, New York, Christine alikuwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba aliniambia tena na tena niendeshe gari polepole. Nami nikamwambia, “Christine, nikiendesha polepole zaidi, gari litasimama.” Hata hivyo, muda mfupi baada ya kufika Gileadi, wasiwasi ulipungua. Ndugu Nathan Knorr ndiye aliyekikaribisha kikundi chetu cha wanafunzi na kututembeza. Alitueleza jinsi ya kutumia maji na umeme kwa uangalifu, akikazia kwamba kufanya hivyo ni sifa njema tunaposhughulikia masilahi ya Ufalme. Hatujasahau ushauri huo. Bado tunaufuata.

Twasafiri kwa Ndege Kwenda Rio

Tulihitimu baada ya muda mfupi, na mnamo Desemba 10, 1954 tukapanda ndege huko New York City, ambako kulikuwa na baridi kali. Tulikuwa na hamu nyingi ya kusafiri kwenda kwenye mgawo wetu jiji lenye jua kali la Rio de Janeiro, Brazili. Tulisafiri pamoja na mishonari wenzetu, Peter na Billie Carrbello. Safari hiyo ilitarajiwa kuchukua muda wa saa 24, na tungesimama Puerto Rico, Venezuela, na Belém, kaskazini mwa Brazili. Hata hivyo, kwa kuwa ndege hiyo ilikuwa na matatizo ya injini, ilichukua muda wa saa 36 kufika Rio de Janeiro. Jiji hilo lilivutia kama nini! Taa zake zilimetameta kama almasi kwenye kitambaa cheusi, nao mwangaza wa mwezi ukafanya maji ya Ghuba ya Guanabara yametemete kama fedha.

Washiriki kadhaa wa familia ya Betheli walikuwa wanatungojea kwenye uwanja wa ndege. Baada ya kutukaribisha kwa uchangamfu, walitupeleka kwa gari hadi ofisi ya tawi ambako tulilala mwendo wa saa tisa usiku. Muda wa saa chache baadaye, kengele ya kuamsha watu ikatukumbusha kwamba siku yetu ya kwanza tukiwa mishonari ilikuwa imeanza!

Twajifunza Mapema

Baada ya muda mfupi tulijifunza jambo muhimu. Familia moja ya Mashahidi ilikuwa imetualika kwao jioni. Tulitaka kutembea kwa miguu kurudi Betheli, lakini mwenye kutualika akakataa akisema, “La, hamwezi kuondoka; kunanyesha,” na kusisitiza tulale huko. “Mahali tunakotoka, hunyesha pia,” nikasema na kuondoka huku nikipuuza maneno yake kwa kucheka tu.

Kwa sababu ya milima inayozunguka Rio, maji ya mvua hukusanyika upesi na kutiririka kuingia jijini, mara nyingi yakisababisha mafuriko. Muda si muda tulikuwa tunatembea ndani ya maji yaliyokuwa yamefika kwenye magoti. Karibu na ofisi ya tawi, barabara zilikuwa kama mito inayoenda kwa nguvu sana nayo maji yalifika kwenye kifua. Hatimaye tulipofika Betheli, tulikuwa tumelowa maji. Siku iliyofuata, Christine alikuwa mnyonge na baadaye akapatwa na homa ya matumbo. Ni wazi kwamba, tukiwa mishonari wapya, tulipaswa kusikiliza ushauri wa Mashahidi wenyeji wenye uzoefu zaidi.

Hatua za Kwanza Katika Kazi ya Mishonari na ya Kusafiri

Baada ya matatizo hayo ya mwanzo-mwanzo, tulianza huduma yetu ya shambani kwa hamu. Tulisomea kila mtu tuliyekutana naye ujumbe ambao tulikuwa tumeandika kwa Kireno, jambo lililotusaidia pia kufanya maendeleo katika kuzungumza lugha hiyo. Mwenye nyumba mmoja angemwambia Christine hivi huku akininyoshea kidole, ‘Ninakuelewa wewe, lakini simwelewi mume wako.’ Mwenye nyumba mwingine angeniambia hivi: ‘Ninakuelewa, lakini simwelewi mke wako.’ Hata hivyo, tulifurahi kupata maandikisho 100 ya Mnara wa Mlinzi katika majuma machache ya kwanza. Kwa kweli, baadhi ya wanafunzi wetu wa Biblia walibatizwa katika mwaka wetu wa kwanza nchini Brazili, jambo lililodhihirisha matokeo ambayo tungepata katika mgawo huo wa mishonari.

Katikati ya miaka ya 1950, makutaniko mengi nchini Brazili hayakutembelewa kwa ukawaida na waangalizi wa mzunguko kwa sababu hakukuwa na ndugu wenye kustahili. Kwa hiyo, japo nilikuwa ninajifunza lugha na sikuwa nimewahi kutoa hotuba ya watu wote katika Kireno, nilipewa mgawo wa kuzunguka katika jimbo la São Paulo mwaka wa 1956.

Kwa kuwa kutaniko tulilozuru halikuwa limepata mwangalizi wa mzunguko kwa muda wa miaka miwili, kila mmoja alitarajia kwa hamu kubwa hotuba ya watu wote. Nilitayarisha hotuba hiyo kwa kukata visehemu fulani katika makala mbalimbali za gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kireno na kuvibandika kwenye makaratasi. Jumapili hiyo, Jumba la Ufalme lilijaa pomoni. Watu wengine hata waliketi kwenye jukwaa, wote wakingojea hotuba hiyo muhimu. Hotuba, au niseme usomaji ukaanza. Mara kwa mara, nilitazama wasikilizaji na kushangaa kuona kwamba kila mmoja wao, hata watoto walikuwa wameketi tuli. Wote walikuwa wakinitazama kwa mshangao. Nikawaza: ‘Lo, nimefanya maendeleo yaliyoje katika Kireno! Watu hawa wanasikiliza.’ Miaka kadhaa baadaye, nilipotembelea kutaniko hilo tena, ndugu aliyekuwepo nilipozuru mara ya kwanza alisema: “Je, unakumbuka hotuba ya watu wote uliyotoa? Hatukuelewa chochote.” Nilikiri kwamba hata mimi sikuielewa.

Mwaka huo wa kwanza katika kazi ya kuzunguka, nilisoma andiko la Zekaria 4:6 mara nyingi. Maneno, ‘Si kwa nguvu bali kwa roho,’ yalinikumbusha kwamba roho ya Yehova ndiyo pekee iliyofanya kazi ya Ufalme iendelee. Na kazi hiyo iliendelea licha ya udhaifu wetu mbalimbali uliokuwa wazi.

Matatizo na Baraka Tulizopata Katika Migawo Yetu

Kazi ya kuzunguka ilimaanisha kusafiri kotekote nchini, huku tumebeba mashine ya chapa, katoni za vichapo, masanduku, na mifuko. Kwa hekima, Christine alitia alama mizigo yetu ili isisahaulike tuliposhuka basi moja kupanda nyingine. Ili kufika tulikokuwa tunaenda, lilikuwa jambo la kawaida kusafiri kwa basi kwa muda wa saa 15 kwenye barabara za mchanga. Mara kwa mara iliogopesha sana, hasa wakati mabasi mawili yalipovuka daraja lenye kuyumbayumba kwa wakati mmoja, huku yakikaribiana sana. Pia tulisafiri kwa gari-moshi, kwa meli, na kwa farasi.

Katika mwaka wa 1961 tulianza kutumikia katika kazi ya wilaya, tukisafiri kutoka mzunguko mmoja hadi mwingine badala ya kusafiri kutoka kutaniko moja hadi jingine. Jioni kadhaa kwa juma, tulionyesha filamu zilizotengenezwa na tengenezo la Yehova—kila mara katika eneo tofauti. Mara nyingi tulihitaji kuchukua hatua haraka ili kuwashinda akili makasisi wenyeji ambao walijaribu kuzuia maonyesho hayo ya filamu. Katika mji mmoja, kasisi alimlazimisha mmiliki wa jumba fulani afutilie mbali mkataba tuliokuwa tumefanya naye. Baada ya kutafuta kwa muda mrefu, tulipata jumba mahali pengine, lakini hatukuambia yeyote. Tuliendelea kualika watu wote kwenda kwenye lile jumba la kwanza. Kabla ya programu kuanza, Christine alienda kwenye jumba hilo na kuwaelekeza kimyakimya wale waliotaka kutazama sinema hiyo kwenda kwenye hilo jengo jingine. Jioni hiyo, watu 150 walitazama sinema hiyo, ambayo ilikuwa na kichwa kifaacho, Jamii ya Ulimwengu Mpya Inatenda (The New World Society in Action).

Wakati mwingine kazi ya kusafiri kwenda maeneo yaliyo mbali ilikuwa ngumu lakini ndugu wanyenyekevu walioishi huko walithamini sana ziara zetu. Walitukaribisha kwa uchangamfu sana kwenye nyumba zao, ambazo hazikuwa za gharama kubwa, nasi tulimshukuru Yehova sikuzote kwa kuwa tungeweza kuwa pamoja nao. Tulipata baraka nyingi kwa kufanya urafiki pamoja nao. (Mithali 19:17; Hagai 2:7) Kwa hiyo tulisikitika kama nini wakati siku zetu za utumishi wa mishonari nchini Brazili zilipoisha baada ya kutumikia huko kwa muda wa miaka 21!

Yehova Alituongoza Wakati wa Matatizo

Mwaka wa 1975, Christine alifanyiwa upasuaji. Tulianza tena kazi ya kuzunguka, lakini afya ya Christine ikazidi kudhoofika. Tuliona ni vema kurudi Marekani ili akapate matibabu. Mnamo Aprili 1976, tulifika Long Beach, California, tulikokaa na mama yangu. Baada ya kuishi katika nchi za kigeni kwa miaka 20, hatukujua tufanye nini. Nilianza kazi ya kukanda mwili, na pesa nilizochuma kutokana nayo zilitutegemeza. Jimbo la California lilimtafutia Christine kitanda kwenye hospitali fulani, lakini hali yake ikaendelea kudhoofika siku baada ya siku kwa sababu madaktari walikataa kumtibu bila damu. Tulivunjika moyo na kumsihi Yehova atupe mwongozo.

Alasiri moja nilipokuwa katika utumishi wa shambani, niliona ofisi ya daktari na mara moja nikaamua kuingia ndani. Japo daktari huyo alikuwa anataka kwenda nyumbani, aliniruhusu niingie kwenye ofisi yake ambapo tulizungumza kwa muda wa saa mbili. Kisha akasema: “Ninathamini kazi yenu ya mishonari na nitamtibu mke wako bila malipo na bila damu.” Ilikuwa vigumu kuamini aliyosema.

Daktari huyo mwenye fadhili, ambaye alikuwa mtaalamu mwenye kuheshimiwa, alimhamisha Christine na kumpeleka kwenye hospitali alikofanya kazi, na hali ya Christine ikaimarika kwa sababu ya ujuzi wa daktari huyo. Tulishukuru kama nini kwamba Yehova alituongoza wakati huo wenye magumu!

Migawo Mipya

Christine alipozidi kupata nguvu, tulitumikia tukiwa mapainia na tulifurahi kuwasaidia watu kadhaa wa Long Beach kuwa waabudu wa Yehova. Katika mwaka wa 1982 tuliombwa tufanye kazi ya kuzunguka huko Marekani. Tulimshukuru Yehova kwa kututumia tena katika kazi ya kusafiri—huduma ambayo tuliipenda. Tulitumikia huko California, kisha New England. Katika mzunguko huo kulikuwa na makutaniko ya watu wenye kuzungumza Kireno. Baadaye mzunguko huo ulitia ndani Bermuda.

Baada ya miaka minne yenye kuburudisha, tulipata mgawo mwingine. Tulialikwa kutumikia tukiwa mapainia wa pekee popote tulipotaka. Japo tulihuzunika kuacha kazi ya kusafiri, tuliazimia kuendelea na mgawo wetu mpya. Lakini tungeenda kupainia wapi? Katika kazi ya kusafiri nilikuwa nimeona kwamba kutaniko la lugha ya Kireno huko New Bedford, Massachusetts, lilihitaji msaada—kwa hiyo tukaenda New Bedford.

Tulipofika, kutaniko lilitukaribisha kwa karamu kubwa sana. Tulihisi tunathaminiwa kama nini! Hata tulilia. Wenzi wawili wa ndoa wachanga, ambao walikuwa na watoto wawili wadogo, walitukaribisha tukae nao hadi tulipopata nyumba yetu wenyewe. Kwa kweli Yehova alibariki mgawo wetu wa upainia wa pekee kwa njia ambayo hatukutazamia. Tangu mwaka wa 1986 tumesaidia watu wapatao 40 katika mji huu kuwa Mashahidi. Wao ni familia yetu ya kiroho. Isitoshe, nimefurahi kuona ndugu watano wenyeji wakikua na kuwa wachungaji wa kundi wenye kujali. Imekuwa kama kutumikia katika mgawo wa mishonari wenye matokeo.

Tukumbukapo ya nyuma, tunashangilia kwamba tumemtumikia Yehova tangu ujanani na kuishi kupatana na kweli. Ni kweli kwamba umri na magonjwa yanatuathiri sasa, lakini bado tunapata nguvu na shangwe kwa kuendelea kufuata njia ya Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Baada tu ya kufika Rio de Janeiro

[Picha katika ukurasa wa 28]

Familia yetu ya kiroho huko New Bedford, Massachusetts