Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Kwa Hekima Siku Zetu Zitazidishwa’

‘Kwa Hekima Siku Zetu Zitazidishwa’

‘Kwa Hekima Siku Zetu Zitazidishwa’

NI NANI ambaye angekataa kwamba hekima ni muhimu sana ili kushughulikia matatizo maishani? Hekima ya kweli ni uwezo wa kutenda ifaavyo kulingana na ujuzi na uelewevu. Hekima ni kinyume kabisa cha upumbavu, ujinga, na ukichaa. Kwa hiyo, Maandiko hutusihi tujipatie hekima. (Mithali 4:7) Kitabu cha Mithali cha Biblia kiliandikwa hasa kitufundishe hekima na kututia nidhamu. Maneno yake ya kwanza yasema hivi: “Mithali za Sulemani, mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli. Kujua hekima na [“nidhamu,” BHN]; kutambua maneno ya ufahamu.”—Mithali 1:1, 2.

Fikiria mafundisho timamu ya sura chache za kwanza za kitabu cha Mithali. Kama baba anayempenda mwana wake, Sulemani anasihi wasomaji wake wakubali nidhamu na kusikiliza hekima. (Sura ya 1 na 2) Anatuelezea jinsi ya kukuza uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kulinda moyo wetu. (Sura ya 3 na 4) Tunasihiwa tudumishe usafi wa maadili. (Sura ya 5 na 6) Naam, kuelewa mbinu za mwasherati ni ulinzi mkubwa sana. (Sura ya 7) Na jinsi tunavyovutiwa na hekima inayofananishwa na mtu mwenye hekima! (Sura ya 8) Kabla ya kuanza kuandika mithali moja-moja fupi za sura zinazofuata, Mfalme Sulemani hujumlisha kwa njia yenye kusisimua mambo ambayo amezungumzia katika sura zilizotangulia.—Sura ya 9.

“Njoo, Ule Mkate Wangu, Ukanywe Divai Niliyoichanganya”

Umalizio wa sehemu ya kwanza ya kitabu cha Mithali si muhtasari tu wa ushauri uliotolewa mapema katika kitabu hicho. Badala yake, umalizio huo umetolewa kama kielelezi kizuri chenye kusisimua, ambacho humtia moyo msomaji afuatie hekima.

Sura ya 9 ya kitabu cha Mithali cha Biblia huanza na maneno haya: “Hekima [a]meijenga nyumba yake, amezichonga nguzo zake saba.” (Mithali 9:1) Maneno “nguzo saba,” apendekeza msomi mmoja “hudokeza kwamba kile kinachozungumziwa ni jumba ambalo limezungukwa kwa ua. Na jengo hilo limetegemezwa kwa nguzo tatu kwenye pande mbili, na nguzo nyingine moja katikati ya upande wa tatu, unaoelekea upande wenye mlango.” Kwa vyovyote vile, hekima amejenga nyumba imara ili wageni wengi wakaribishwe.

Mipango yote ya karamu imekamilika. Nyama iko, na pia divai. Hekima mwenyewe ametayarisha chakula na kupanga meza. “Amechinja nyama zake, [a]mechanganya divai yake, ameiandalia meza yake pia.” (Mithali 9:2) Bila shaka chakula chenye kuelimisha kiroho kinachostahili kuzingatiwa kwa makini hupatikana kwenye meza hiyo ya mfano.—Isaya 55:1, 2.

Ni nani ambao wamekaribishwa kwenye karamu iliyotayarishwa na hekima ya kweli? “Amewatuma wajakazi wake, analia, mahali pa mjini palipoinuka sana, kila aliye mjinga na aingie humu. Tena amwambia mtu aliyepungukiwa na akili [“asiye na ufahamu,” “Zaire Swahili Bible”], njoo ule mkate wangu, ukanywe divai niliyoichanganya. Enyi wajinga, acheni ujinga, mkaishi, mkaende katika njia ya ufahamu.”Mithali 9:3-6.

Hekima amewatuma wanawali wake wakatoe mwaliko. Wamekwenda kwenye mahali pa umma, ambapo wanaweza kuita watu wengi. Wote wamekaribishwa—wale ‘wasio na ufahamu,’ au wasio na uelewevu, kutia ndani wale wasio na ujuzi. (Mithali 9:4) Nao wanatolewa ahadi ya uhai. Karibu watu wote wanaweza kujipatia hekima ya Neno la Mungu, kutia ndani hekima inayopatikana katika kitabu cha Mithali. Leo, Mashahidi wa Yehova ambao ni wajumbe wa hekima ya kweli, wanajitahidi sana kuwaalika watu kila mahali wajifunze Biblia. Kutwaa ujuzi huo, kunaweza kuongoza kwenye uhai udumuo milele.—Yohana 17:3.

Wakristo wanapaswa kukubali kwa unyenyekevu nidhamu ambayo hutolewa na hekima. Jambo hilo ni kweli hasa kuhusu vijana na wale ambao wameanza majuzi kujifunza juu ya Yehova. Kwa sababu hawana ujuzi mwingi kuhusu njia za Mungu huenda ‘wasiwe na ufahamu.’ Haimaanishi kwamba makusudio yao yote ni mabaya. Lakini ili nia na makusudio yao ya moyoni yampendeze Yehova Mungu, kutumia wakati na jitihada nyingi huhitajika. Wanahitaji kurekebisha mawazo, tamaa, mapendezi, na miradi yao ili kuzipatanisha na mapenzi ya Mungu. Lazima ‘wafanyize hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno.’—1 Petro 2:2.

Sisi sote tunapaswa ‘kuacha fundisho la msingi.’ Lazima sisi sote tusitawishe upendezi kwa “mambo yenye kina kirefu ya Mungu” na kupata lishe kutokana na chakula kigumu ambacho ni cha watu wakomavu. (Waebrania 5:12–6:1; 1 Wakorintho 2:10) “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” ambaye anaongozwa moja kwa moja na Yesu Kristo, anaandaa kwa bidii chakula cha kiroho cha wakati unaofaa kwa wote. (Mathayo 24:45-47) Acheni tule kwenye meza iliyopangwa na hekima kwa kujifunza kwa bidii Neno la Mungu na vichapo vya Biblia ambavyo vimeandaliwa na jamii ya mtumwa mwaminifu.

“Usimkaripie Mwenye Dharau”

Mafundisho ya hekima yanatia ndani pia nidhamu na karipio. Hayo hayapendwi na wengi. Kwa hiyo, umalizio wa sehemu ya kwanza ya kitabu cha Mithali unatia ndani onyo hili: “Amkemeaye mwenye dharau hujipatia fedheha; amkaripiaye mtu mbaya hujipatia aibu. Usimkaripie mwenye dharau, asije akakuchukia.”Mithali 9:7, 8a.

Mtu mwenye dharau humwekea kinyongo na kumchukia yule anayejaribu kumsaidia kurekebisha njia zake. Mtu mwovu hathamini karipio. Ni kukosa hekima kama nini kujaribu kumfundisha yule anayechukia au kudhihaki ukweli wa ajabu wa Neno la Mungu! Mtume Paulo alipohubiri mjini Antiokia, alikutana na kundi la Wayahudi ambao hawakupenda ukweli hata kidogo. Walijaribu kumwingiza katika mabishano kwa kumpinga kwa kukufuru, lakini Paulo alisema tu hivi: “Kwa kuwa mnalisukuma [neno la Mungu] mbali kutoka kwenu na hamjihukumu wenyewe kuwa mwastahili uhai udumuo milele, tazameni! twawageukia mataifa.”—Matendo 13:45, 46.

Tunapojitahidi kufikia watu wenye mioyo myeupe na habari njema ya Ufalme, na tujihadhari tusijiingize katika mabishano na wadhihaki. Kristo Yesu aliamuru wanafunzi wake hivi: “Mnapokuwa mkiingia ndani ya hiyo nyumba, salimuni hao watu wa nyumbani; na ikiwa hiyo nyumba inastahili, acheni amani mwitakiayo ije juu yayo; lakini ikiwa haistahili, acheni amani itokayo kwenu irudi juu yenu. Popote pale ambapo yeyote hawakaribishi nyinyi au hasikilizi maneno yenu, mnapoenda kutoka katika nyumba hiyo au jiji hilo yakung’uteni mavumbi kutoka kwenye miguu yenu.”—Mathayo 10:12-14.

Mwenye hekima anakubali nidhamu lakini mwenye dharau huikataa. Sulemani asema: “Mkaripie mwenye hekima, naye atakupenda. Mwelimishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima.” (Mithali 9:8b, 9a) Mwenye hekima anajua kwamba “hakuna nidhamu ionekanayo kwa wakati wa sasa kuwa yenye shangwe, bali yenye kihoro; lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo hutoa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Waebrania 12:11) Huenda ikawa ushauri unaumiza, lakini kwa nini tulipize kisasi au kujitetea ikiwa kuukubali ushauri utafanya tuwe wenye hekima?

“Mfundishe mwenye haki, naye atazidi kuwa na elimu,” aongeza mfalme huyo mwenye hekima. (Mithali 9:9b) Hakuna aliye mwenye hekima mno au mzee mno asihitaji kuendelea kujifunza. Inafurahisha kama nini kuwaona hata wazee wakikubali ukweli na kujiweka wakfu kwa Yehova! Na sisi pia tudumishe mwelekeo wa kutaka kujifunza na kuwa na akili nyepesi.

“Miaka ya Maisha Yako Itaongezwa”

Anapokazia jambo kuu la habari inayozungumziwa, Sulemani anatia ndani sifa ambayo lazima tuwe nayo tukitaka kuwa wenye hekima. Anaandika hivi: “Kumcha BWANA ni mwanzo wa hekima; na kumjua Mtakatifu ni ufahamu.” (Mithali 9:10) Mtu hawezi kuwa na hekima ya kimungu asipomcha Mungu wa kweli na kumheshimu. Huenda mtu akawa na ujuzi mwingi akilini, hata hivyo, ikiwa hamchi Yehova, atashindwa kutenda kulingana na ujuzi huo na kukosa kumheshimu Muumba. Hata huenda akakata kauli mbaya akitumia ujuzi alio nao, na hivyo kuonekana mpumbavu. Isitoshe, kumjua Yehova, aliye Mtakatifu, ni muhimu ili kupata uelewevu kwa kuwa bila uelewevu mtu hawezi kuwa mwenye hekima.

Hekima inazaa matunda gani? (Mithali 8:12-21, 35) Mfalme wa Israeli asema: “Maana, kwa msaada wangu siku zako zitazidishwa; na miaka ya maisha yako itaongezwa.” (Mithali 9:11) Siku nyingi na miaka mingi ya maisha ni matokeo ya kuwa mwenye hekima. Naam, “hekima humhifadhi yeye aliye nayo.”—Mhubiri 7:12.

Kujitahidi kujipatia hekima ni daraka la binafsi la kila mmoja wetu. Sulemani anasema hivi, akikazia jambo hilo: “Kama una hekima, una hekima kwa nafsi yako; na kama una dharau, utaichukua peke yako.” (Mithali 9:12) Mwenye hekima hunufaika kutokana na hekima yake, lakini mwenye dharau hujiletea mwenyewe mateso. Ndiyo, tunavuna kile tunachopanda. Acheni, basi, ‘tusikilize hekima.’—Mithali 2:2.

“Mwanamke Mpumbavu Hupiga Kelele”

Kisha Sulemani husimulia jambo ambalo ni kinyume cha hekima, akisema hivi: “Mwanamke mpumbavu hupiga kelele, ni mjinga, hajui kitu. Hukaa mlangoni pa nyumba yake, juu ya kiti mahali pa mjini palipoinuka, apate kuwaita wapitao njiani, waendao moja kwa moja katika njia zao. Kila aliye mjinga [“asiye na ujuzi,” “NW”] na aingie humu.”Mithali 9:13-16a.

Upumbavu huelezwa kuwa mwanamke mjinga asiyejizuia na mwenye kelele. Yeye vilevile amejenga nyumba. Naye amejipatia kazi ya kuwaita wote wasio na ujuzi. Kwa hiyo, wale wapitao wanaweza kuchagua la kufanya. Je, watakubali mwaliko wa hekima au ule wa ujinga?

“Maji Yaliyoibiwa Ni Matamu”

Hekima na upumbavu hualika wasikilizaji ‘waingie humu.’ Hata hivyo, uvutio ni tofauti. Hekima hukaribisha watu kwenye karamu ya divai, nyama, na mkate. Uvutio ambao upumbavu hutolea watu hutukumbusha njia za mwanamke mwasherati. Sulemani anasema hivi: “Tena amwambia mtu aliyepungukiwa na akili [“asiye na ufahamu,” “ZSB”], maji yaliyoibiwa ni matamu, na mkate ulioliwa kwa siri hupendeza.”Mithali 9:16b, 17.

Badala ya divai iliyochanganywa “mwanamke mpumbavu” hutolea watu maji yaliyoibiwa. (Mithali 9:13) Maandiko yanaifananisha raha ambayo huletwa na uhusiano wa ngono pamoja na mke mpendwa na maji yenye kuburudisha. (Mithali 5:15-17) Kwa hiyo, maji yaliyoibiwa yanafananisha uasherati, ambao hufanywa sirini. Maji hayo yanaonekana ni matamu—bora kuliko divai—eti, kwa sababu yameibwa, na wenye kuiba hawakukamatwa. Mkate na nyama ambazo huliwa sirini huonekana kuwa tamu kuliko mkate na nyama ya hekima kwa sababu tu zimepatikana kwa njia isiyo halali. Kuona kilichokatazwa na kutendwa sirini kuwa chenye kupendeza ni ishara ya upumbavu.

Mwaliko wa hekima unatia ndani ahadi ya uhai. Walakini yule mwanamke mpumbavu hataji kamwe matokeo ya kuzifuata njia zake. Lakini Sulemani anaonya hivi: “Lakini huyo hajui ya kuwa wafu wamo humo; ya kuwa wageni wake wamo chini kuzimuni [“kaburini,” “NW”].” (Mithali 9:18) “Nyumba ya mwanamke mpumbavu si mahali pa kuishi bali ni kaburi,” aandika msomi mmoja. “Ukiingia humo utafia humo.” Kuishi maisha yasiyo na maadili si jambo la hekima; bali maisha ya aina hiyo huleta kifo.

Yesu Kristo alisema hivi: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Na tujilishe daima kwenye meza ya hekima na kuwa miongoni mwa wale walioko kwenye njia inayoongoza kwenye uhai.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mwenye hekima hukubali kurekebishwa

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kujipatia hekima ni daraka la kibinafsi la kila mmoja wetu