Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Wanadamu Wanateseka?

Kwa Nini Wanadamu Wanateseka?

Kwa Nini Wanadamu Wanateseka?

“MUNGU, KWA NINI IWE HIVYO?” Kichwa hicho kikubwa cha habari kilikuwa katika ukurasa wa kwanza wa gazeti fulani ambalo huchapishwa kwa wingi, kufuatia tetemeko baya sana la ardhi huko Asia Ndogo. Ukurasa huohuo ulikuwa na picha ya baba aliyefadhaika akimbeba binti yake aliyejeruhiwa kutoka katika nyumba yao iliyoporomoka.

Vita, njaa kali, magonjwa yenye kuenea, na misiba ya asili vimesababisha maumivu mengi sana, majonzi tele, na vifo vingi. Pia kuna wale wanaoteseka kwa sababu ya kubakwa, watoto wanaotendwa vibaya, na uhalifu mwingine. Fikiria pia watu wengi sana wanaojeruhiwa au kufa katika aksidenti. Mabilioni ya watu wanapatwa na maumivu makali kwa sababu ya ugonjwa, uzee, na kifo cha wapendwa wao.

Katika karne ya 20 wanadamu wameteseka kwa njia isiyo na kifani. Kuanzia 1914 hadi 1918, karibu askari-jeshi milioni kumi walikufa katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Wanahistoria fulani wanasema kwamba raia wapatao milioni kumi pia walikufa katika vita hiyo. Katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, askari na raia wapatao milioni 50 waliuawa, kutia ndani mamilioni ya wanawake, watoto, na wanaume wazee wasio na ulinzi wowote. Katika karne yote iliyopita, mamilioni zaidi walikufa katika maangamizi ya jamii nzima-nzima, mapinduzi, ghasia za kikabila, njaa, na umaskini. Kichapo Historical Atlas of the Twentieth Century chakadiria kwamba zaidi ya watu milioni 180 walikufa kwa sababu ya ‘hali hizo zisizofurahisha.’

Homa ya Kihispania ya 1918/1919 iliua watu milioni 20. Katika miongo miwili iliyopita, watu wapatao milioni 19 walikufa kutokana na UKIMWI, na wengine wapatao milioni 35 sasa wana virusi vinavyosababisha ugonjwa huo. Mamilioni ya watoto wameachwa bila wazazi—walikufa kutokana na UKIMWI. Na watoto wengi sana wanakufa kutokana na UKIMWI ambao waliambukizwa walipokuwa ndani ya tumbo la uzazi.

Watoto wanazidi kuteseka katika njia mbalimbali. Likinukuu habari kutoka shirika la HazinayaWatoto ya Umoja wa Mataifa (UNICEF), mwishoni mwa mwaka wa 1995, gazeti la Uingereza, Manchester Guardian Weekly, lilisema hivi: “Katika vita iliyotukia mwongo uliopita, watoto milioni 2 wameuawa, milioni 4 hadi 5 wakalemazwa, milioni 12 wakaachwa bila makao, zaidi ya milioni 1 wakawa mayatima au wakatenganishwa na wazazi wao na milioni 10 wakavurugika kiakili.” Pia kuna visa vya utoaji-mimba milioni 40 hadi 50 ulimwenguni pote—kila mwaka!

Ni Nini Kitakachotukia Wakati Ujao?

Wengi wanatazamia jambo baya sana litokee wakati ujao. Kikundi fulani cha wanasayansi walisema hivi: “Shughuli za wanadamu . . . zaweza kubadili sana dunia kiasi cha kwamba itashindwa kutegemeza uhai.” Waliongezea kusema: “Hata wakati huu, mtu mmoja kati ya watano huishi katika ufukara bila chakula cha kutosha, na mmoja kati ya kumi hupatwa na utapiamlo.” Wanasayansi walichukua fursa hiyo “kuonya wanadamu wote kuhusu mambo yatakayotokea” na kusema: “Badiliko kubwa sana lahitaji kufanywa kuhusu usimamizi wa dunia na viumbe vilivyopo, ili wanadamu wasiteseke sana na pia dunia yetu isije ikaharibika kabisa.”

Kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka kwingi na uovu mwingi kadiri hiyo? Anapanga kurekebishaje hali? Lini?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

Juu, kiti cha magurudumu: UN/DPI Photo 186410C by P.S. Sudhakaran; katikati, watoto wenye njaa: WHO/OXFAM; chini, mwanamume aliyedhoofika: FAO photo/B. Imevbore