Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msifuni Yehova kwa Vitendo Vyake Vikubwa!

Msifuni Yehova kwa Vitendo Vyake Vikubwa!

Msifuni Yehova kwa Vitendo Vyake Vikubwa!

“Nafsi yangu yamtukuza Yehova . . . kwa sababu Aliye Mwenye nguvu amenifanyia vitendo vikubwa.”—LUKA 1:46-49.

1. Yehova anastahili sifa zetu kwa sababu ya vitendo gani vikubwa?

YEHOVA anastahili kusifiwa kwa sababu ya vitendo vyake vikubwa. Nabii Musa alisema hivi wakati alipokuwa akisimulia kuhusu ukombozi wa Waisraeli kutoka Misri: “Macho yenu yameiona kazi kubwa [“vitendo vikubwa,” NW] ya BWANA aliyoifanya, yote.” (Kumbukumbu la Torati 11:1-7) Vivyo hivyo, malaika Gabrieli alipomjulisha Maria, msichana bikira, kuhusu kuzaliwa kwa Yesu, Maria alisema hivi: “Nafsi yangu yamtukuza Yehova . . . kwa sababu Aliye Mwenye nguvu amenifanyia vitendo vikubwa.” (Luka 1:46-49) Sisi Mashahidi wa Yehova humsifu kwa sababu ya vitendo vyake vikubwa kama vile kuwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri na kufanya mimba ya Mwana wake mpendwa itungwe kimuujiza.

2. (a) “Kusudi la milele” la Mungu lamaanisha nini kwa wanadamu watiifu? (b) Yohana aliona nini akiwa kwenye kisiwa kidogo cha Patmosi?

2 Vitendo vingi vikubwa vya Yehova vimehusianishwa na ‘kusudi lake la milele’ la kuwabariki wanadamu watiifu kupitia Mesiya na utawala wake wa Ufalme. (Waefeso 3:8-13) Kusudi hilo lilikuwa likiendelea kutimizwa hatua kwa hatua wakati mtume Yohana aliyezeeka aliporuhusiwa katika njozi kuchungulia mbinguni kupitia mlango uliokuwa umefunguliwa. Alisikia sauti kama ya tarumbeta ikisema: “Panda uje huku, nami nitakuonyesha mambo ambayo lazima yatukie.” (Ufunuo 4:1) Yohana alipokea “ufunuo kupitia Yesu Kristo” akiwa kwenye kisiwa kidogo cha Patmosi alikohamishiwa na serikali ya Roma “[kwa sababu ya kusema] juu ya Mungu na kutoa ushahidi kuhusu Yesu.” Yale ambayo mtume huyo aliona na kusikia yalifunua mambo mengi sana kuhusu kusudi la Mungu la milele na hivyo kutoa uelewevu wa kiroho na kitia-moyo cha wakati ufaao kwa Wakristo wote wa kweli.—Ufunuo 1:1, 9, 10.

3. Wazee 24 ambao Yohana aliona katika njozi wanawakilisha nani?

3 Kupitia mlango huo uliokuwa umefunguliwa mbinguni, Yohana aliona wazee 24, waliotawazwa na kuvishwa taji kama wafalme. Walianguka chini mbele ya Mungu na kusema: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” (Ufunuo 4: 11) Wazee hao wanawakilisha Wakristo wote watiwa-mafuta ambao tayari wamefufuliwa kwenye cheo cha juu sana ambacho waliahidiwa na Mungu. Wanachochewa kumsifu Yehova kwa sababu ya vitendo vyake vikubwa vya uumbaji. Sisi pia hustaajabia mambo yanayothibitisha ‘nguvu za Yehova za milele na Uungu’ wake. (Waroma 1:20) Na tunapozidi kujifunza juu ya vitendo vikubwa vya Yehova tunapata sababu zaidi za kumsifu.

Tangaza Vitendo vya Yehova Vinavyostahili Sifa!

4, 5. Toa mifano ya jinsi Daudi alivyomsifu Yehova?

4 Mtunga-zaburi Daudi alimsifu Mungu kwa vitendo Vyake vikubwa. Kwa mfano, Daudi aliimba hivi: “Mwimbieni BWANA akaaye Sayuni, yatangazeni kati ya watu matendo yake. Wewe, BWANA, unifadhili, tazama mateso niteswayo na wanaonichukia; wewe uniinuaye katika malango ya mauti, ili nizisimulie sifa zako zote; katika malango ya binti Sayuni nitaufurahia wokovu wako.” (Zaburi 9:11, 13, 14) Baada ya kumpa mwanaye Solomoni ramani ya ujenzi wa hekalu, Daudi alimhimidi na kumsifu Mungu akisema: “Ee BWANA, ukuu ni wako, na uweza, na utukufu, na kushinda, na enzi . . . Ufalme ni wako, Ee BWANA, nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote. . . . Basi sasa, Mungu wetu, twakushukuru na kulisifu jina lako tukufu.”—1 Mambo ya Nyakati 29:10-13.

5 Maandiko hutuhimiza tena na tena tumsifu Mungu kama Daudi alivyofanya. Kitabu cha Zaburi kina semi nyingi za kumsifu Mungu, na yadhaniwa kwamba nusu ya nyimbo hizo ziliandikwa na Daudi. Alimsifu na kumshukuru Yehova daima. (Zaburi 69:30) Isitoshe, tangu zamani, nyimbo zilizopuliziwa na Mungu ambazo ziliandikwa na Daudi na wengineo zimetumiwa kumsifu Yehova.

6. Tunanufaikaje kutokana na Zaburi zilizopuliziwa?

6 Zaburi ni zenye manufaa kama nini kwa waabudu wa Yehova! Tunapotaka kumshukuru Mungu kwa vitendo vikubwa alivyotenda kwa niaba yetu, tunaweza kufikiria maneno mazuri tupatayo katika Zaburi. Kwa mfano, tunapoamka na kuona siku mpya, huenda tukachochewa kusema maneno kama haya: “Ni neno jema kumshukuru BWANA, na kuliimbia jina lako, Ee Uliye juu. Kuzitangaza rehema zako asubuhi, na uaminifu wako wakati wa usiku. . . . kwa kuwa umenifurahisha, BWANA, kwa kazi yako; nitashangilia kwa ajili ya matendo ya mikono yako.” (Zaburi 92:1-4) Tunaposhinda jambo linalotuzuia tusifanye maendeleo ya kiroho, huenda tukataka kuonyesha shangwe na shukrani katika sala kama vile mtunga-zaburi alivyofanya alipoimba: “Njoni, tumwimbie BWANA, tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu. Tuje mbele zake kwa shukrani, tumfanyie shangwe kwa zaburi.”—Zaburi 95:1, 2.

7. (a) Yafaa kuzingatia nini kuhusu nyimbo nyingi zinazoimbwa na Wakristo? (b) Kwa nini tufike mikutanoni mapema na kukaa hadi mwisho?

7 Mara nyingi sisi humsifu Yehova kwa nyimbo kwenye mikutano yetu ya kutaniko, makusanyiko na mikusanyiko. Yafaa kuzingatia kwamba nyingi za nyimbo hizo zimetungwa kutokana na mawazo yaliyopuliziwa ya kitabu cha Zaburi. Tunafurahi kama nini kuwa na nyimbo zifaazo na zenye kuchangamsha za kumsifu Yehova! Kumsifu Mungu kwa nyimbo ni sababu moja nzuri ya kufika mikutanoni mapema na kuwepo hadi mwisho, hivyo kushiriki na waabudu wenzetu katika kumsifu Yehova kwa nyimbo na sala.

“Msifuni Yah, Enyi Watu!”

8. Neno “Haleluya” lamaanisha nini, nalo kwa kawaida hutafsiriwaje?

8 Neno “Haleluya,” linalomaanisha kumsifu Yehova, linalotokana na neno la Kiebrania ambalo karibu kila mara hutafsiriwa “Msifuni Yah, enyi watu.” Kwa mfano, kwenye Zaburi 135:1-3, twapata wito huu mchangamfu na wenye mkazo: “Haleluya [“msifuni Yah, enyi watu!” NW]. Lisifuni jina la BWANA, enyi watumishi wa BWANA, sifuni. Ninyi msimamao nyumbani mwa BWANA, nyuani mwa nyumba ya Mungu wenu. Msifuni kwa kuwa BWANA ni mwema, liimbieni jina lake kwa maana lapendeza.”

9. Ni nini ambacho hutuchochea kumsifu Yehova?

9 Uthamini wa kutoka moyoni hutuchochea kumsifu Mungu tunapotafakari juu ya kazi zake za ajabu za uumbaji na vitendo vyake kwa niaba yetu. Tunapofikiria miujiza ambayo Yehova aliwafanyia watu wake wakati uliopita, mioyo yetu hutuchochea kumsifu. Na tunapotafakari ahadi za mambo makuu ambayo Yehova atafanya, sisi hutafuta njia za kumsifu na kumshukuru.

10, 11. Kuwa kwetu hai hutupa sababu gani ya kumsifu Mungu?

10 Kuwa kwetu hai hutupa sababu nzuri ya kumsifu Yah. Daudi aliimba: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Naam, tumeumbwa kwa “jinsi ya ajabu” na tuna zawadi zenye thamani kama uwezo wa kuona, kusikia, na kufikiri. Kwa hiyo, je, haitupasi kuishi maisha yanayomletea Muumba wetu sifa? Paulo alikuwa na maoni kama hayo alipoandika: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo jingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.

11 Iwapo tunampenda Yehova kikweli tutafanya mambo yote kwa utukufu wake. Yesu alisema kwamba amri ya kwanza ni: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30; Kumbukumbu la Torati 6:5) Kwa hakika yatupasa kumpenda Yehova na kumsifu kwa kuwa ni Mfanyi wetu na Mpaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17; Isaya 51:13; Matendo 17:28) Inafaa kufanya hivyo kwa sababu uwezo wetu wa kusababu, uwezo wetu wa kiroho, na nguvu zetu za kimwili—sifa zetu zote na uwezo wetu wote—hutoka kwa Yehova. Naye anastahili upendo wetu na sifa zetu kwa kuwa yeye ndiye Muumba wetu.

12. Unahisije kuhusu vitendo vikubwa vya Yehova na maneno ya Zaburi 40:5?

12 Vitendo vikubwa vya Yehova hutupa sababu nyingi sana za kumpenda na kumsifu! “Ee BWANA, Mungu wangu, umefanya kwa wingi miujiza yako na mawazo yako kwetu,” akaimba Daudi. “Hakuna awezaye kufananishwa nawe; kama ningependa kuyatangaza na kuyahubiri, ni mengi sana hayahesabiki.” (Zaburi 40:5) Daudi hakuweza kuhesabu kazi zote za ajabu za Yehova. Sisi pia hatuwezi. Lakini acheni tumsifu Mungu sikuzote tunapofahamu baadhi ya vitendo vyake vikubwa.

Vitendo Vinavyohusiana na Kusudi la Milele la Mungu

13. Tumaini letu linahusianaje na vitendo vikubwa vya Mungu?

13 Tumaini letu la wakati ujao lahusiana sana na vitendo vikubwa vyenye kusifika ambavyo vyahusisha kusudi la milele la Mungu. Baada ya uasi uliotokea Edeni, Yehova alitoa unabii wa kwanza uliotokeza matumaini makubwa. Mungu alisema hivi alipomhukumu nyoka: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako [“mbegu yako,” NW] na uzao wake [“mbegu yake,” NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Tumaini katika Mbegu ya mwanamke iliyoahidiwa lilidumu katika mioyo ya wanadamu waaminifu baada ya Yehova kufanya kitendo kikubwa kwa kumwokoa Noa na familia yake wakati wa Gharika ya ulimwenguni pote ambayo iliangamiza ulimwengu mwovu. (2 Petro 2:5) Ahadi za kiunabii ambazo wanaume wenye imani kama Abrahamu na Daudi walipewa zilitoa ufahamu zaidi wa mambo ambayo Yehova angetimiza kupitia Mbegu hiyo.—Mwanzo 22:15-18; 2 Samweli 7:12.

14. Yehova alidhihirishaje kwa njia kuu kabisa vitendo vyake vikubwa kwa niaba ya wanadamu?

14 Yehova alidhihirisha kwa njia kuu kabisa kuwa yeye ni mtekelezaji wa vitendo vikubwa kwa niaba ya wanadamu alipomtoa Mwana wake wa pekee—Yesu Kristo, Mbegu iliyoahidiwa—kuwa dhabihu ya fidia. (Yohana 3:16; Matendo 2:29-36) Fidia hiyo iliandaa msingi wa kupatanishwa na Mungu. (Mathayo 20:28; Waroma 5:11) Yehova aliwakusanya watu wa kwanza waliokuwa wamepatanishwa naye kwenye kutaniko la Kikristo, lililoanzishwa Pentekoste 33 W.K. Kwa msaada wa roho takatifu, watu hao walihubiri habari njema kila mahali, wakionyesha jinsi kifo na ufufuo wa Yesu zinavyotolea wanadamu watiifu fursa ya kupokea baraka za milele chini ya utawala wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu.

15. Yehova ametendaje kwa njia ya ajabu siku hizi?

15 Siku hizi, Yehova ametenda kwa njia ya ajabu ili kuwakusanya Wakristo watiwa-mafuta wanaobaki. Pepo za uharibifu zimezuiliwa ili mabaki ya wale 144,000 ambao watatawala na Kristo mbinguni, waweze kutiwa muhuri. (Ufunuo 7:1-4; 20:6) Mungu amehakikisha kwamba Wakristo watiwa-mafuta walikombolewa kutoka katika utumwa wa kiroho wa “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini zisizo za kweli. (Ufunuo 17:1-5) Ukombozi huo wa mwaka wa 1919 na ulinzi ambao wamepata kutoka kwa Mungu tangu wakati huo, umewawezesha mabaki ya watiwa-mafuta wafanye nini? Wajitokeze katika kutoa ushahidi wa mwisho kabla Yehova hajamaliza mfumo mwovu wa mambo wa Shetani katika “dhiki kubwa” inayokuja kwa kasi sana.—Mathayo 24:21; Danieli 12:3; Ufunuo 7:14.

16. Kazi ya kuhubiri Ufalme ulimwenguni pote siku hizi ina matokeo gani?

16 Mashahidi wa Yehova waliotiwa mafuta wameongoza kwa bidii kazi ya kuhubiri Ufalme ulimwenguni pote. Matokeo yamekuwa kwamba idadi inayoongezeka ya “kondoo wengine” sasa wanakuwa waabudu wa Yehova. (Yohana 10:16) Tunafurahi kwamba bado kuna fursa kwa wanyenyekevu wa dunia kujiunga nasi kumsifu Yehova. Wale wanaoitikia mwaliko “njoo” watahifadhiwa katika dhiki kubwa, wakiwa na matarajio ya kumsifu Yehova kwa umilele.—Ufunuo 22:17.

Maelfu Wanamiminika Kwenye Ibada ya Kweli

17. (a) Yehova anafanyaje vitendo vikubwa kuhusiana na kazi yetu ya kuhubiri? (b) Andiko la Zekaria 8:23 linatimizwaje?

17 Sasa Yehova anatekeleza vitendo vikubwa na vinavyostahili sifa kuhusiana na kazi yetu ya kuhubiri. (Marko 13:10) Katika miaka ya karibuni, yeye ‘amefungua milango mikubwa iongozayo kwenye utendaji.’ (1 Wakorintho 16:9) Jambo hilo limefanya iwezekane kutangaza habari njema katika maeneo makubwa ambako maadui wa ile kweli walizuia zisitangazwe. Wengi walioishi katika giza la kiroho sasa wanakubali mwaliko wa kumwabudu Yehova. Wanatimiza maneno haya ya kiunabii: “BWANA wa majeshi asema hivi, Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” (Zekaria 8:23) ‘Watu hao kumi’ wanaongea na Wayahudi wa kiroho, mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta wa siku zetu. Kwa kuwa kumi yaweza kuwakilisha utimilifu kuhusiana na mambo ya duniani, ‘watu hao kumi’ wanawakilisha “umati mkubwa” ambao wameungana pamoja na “Israeli wa Mungu” kufanyiza “kundi moja.” (Ufunuo 7:9, 10; Wagalatia 6:16) Inafurahisha kama nini kuona watu wengi sana leo wakitoa utumishi mtakatifu pamoja wakiwa waabudu wa Yehova Mungu!

18, 19. Kuna uthibitisho gani kwamba Yehova anabariki kazi ya kuhubiri?

18 Tunafurahi sana kwamba makumi ya maelfu—naam, mamia ya maelfu—wanajiunga na ibada ya kweli katika nchi ambako dini isiyo ya kweli ilikuwa imeenea sana hivi kwamba ilionekana kana kwamba watu hawangekubali kamwe habari njema. Tazama kitabu Yearbook of Jehovah’s Witnesses cha karibuni uone nchi ambazo zinaripoti wahubiri wa Ufalme kati ya 100,000 hadi 1,000,000. Idadi hiyo ni uthibitisho wenye nguvu kwamba Yehova anabariki kazi ya kuhubiri Ufalme.—Mithali 10:22.

19 Tukiwa watu wa Yehova, sisi humsifu na kumshukuru Baba yetu wa mbinguni kwa kutupa kusudi halisi maishani, kazi yenye kuridhisha katika utumishi wake, na matarajio mema ya wakati ujao. Tunatazamia kwa hamu kutimizwa kwa ahadi zote za Mungu na tumeazimia ‘kujitunza wenyewe katika upendo wa Mungu, tukitazamia uhai udumuo milele.’ (Yuda 20, 21) Tunafurahi kama nini kuona kwamba umati mkubwa unaomsifu Mungu sasa ni watu 6,000,000 hivi! Kwa baraka za Yehova, mabaki ya watiwa-mafuta pamoja na wenzao kondoo wengine wamepangwa katika makutaniko 91,000 katika nchi 235. Sote tunalishwa vizuri kiroho kupitia jitihada nyingi za “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Tengenezo la kitheokrasi linalosonga mbele likiwa na waangalizi wenye upendo linasimamia kazi katika ofisi za tawi 110 za Mashahidi wa Yehova. Tunashukuru kwamba Yehova amechochea mioyo ya watu wake ili ‘wamheshimu kwa mali yao.’ (Mithali 3:9, 10) Kwa hiyo, kazi yetu ya ulimwenguni pote ya kuhubiri inaendelea. Majengo ya uchapaji, makao ya Betheli na ya mishonari, na Majumba ya Makusanyiko yanajengwa kunapokuwa na uhitaji.

20. Kutafakari vitendo vikuu vya Yehova vinavyostahili sifa kwapasa kutuathirije?

20 Hatuwezi kutaja vitendo vyote vikubwa na vinavyostahili sifa vya Baba yetu wa mbinguni. Lakini je, yeyote aliye na moyo mnyofu anaweza kukataa kujiunga na umati mkubwa unaomsifu Yehova? La, hasha! Kwa hiyo, acheni wote wanaompenda Mungu wapaaze sauti kwa furaha: “Haleluya [“msifuni Yah, enyi watu!”NW]. Msifuni BWANA kutoka mbinguni; msifuni katika mahali palipo juu. Msifuni enyi malaika wake wote . . . , vijana waume, na wanawali, wazee, na watoto; na walisifu jina la BWANA maana jina lake peke yake limetukuka; adhama yake i juu ya nchi na mbingu.” (Zaburi 148:1, 2, 12, 13) Naam, sasa na milele, acheni tumsifu Yehova kwa vitendo vyake vikubwa!

Ungejibuje?

• Ni baadhi ya vitendo gani vya Yehova vinavyostahili sifa?

• Kwa nini unahisi umechochewa kumsifu Yehova?

• Tumaini letu linahusianaje na vitendo vikubwa vya Mungu?

• Ni jinsi gani Yehova anafanya vitendo vinavyostahili sifa kuhusiana na kazi ya kuhubiri Ufalme?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, unajiunga na wengine kwa moyo wote kumsifu Yehova kwa nyimbo?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tunafurahi kwamba bado kuna fursa kwa wanyenyekevu kujiunga nasi katika kumsifu Yehova