Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Muda Ambao Mungu Ameruhusu Kuteseka Wakaribia Kwisha

Muda Ambao Mungu Ameruhusu Kuteseka Wakaribia Kwisha

Muda Ambao Mungu Ameruhusu Kuteseka Wakaribia Kwisha

KILA mahali utazamapo, watu wanateseka. Watu fulani huteseka kwa sababu ya matendo yao wenyewe. Wanapatwa na maradhi ya kuambukizwa kingono au athari za kutumia vibaya dawa za kulevya, vileo, au kuvuta sigareti. Au huenda wakapatwa na matatizo ya afya kwa sababu ya mazoea mabaya ya kula. Hata hivyo, kuteseka kwingi hutokana na mambo au matukio yanayozidi uwezo wa mwanadamu wa kawaida: vita, vita vya kikabila, uhalifu, umaskini, njaa kali, na maradhi. Wanadamu hawawezi pia kuzuia kuteseka kunakosababishwa na uzee na kifo.

Biblia hutuhakikishia kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Kwa nini basi, Mungu mwenye upendo ameruhusu kuteseka huku kote kuendelee kwa karne nyingi hivyo? Atarekebisha hali hiyo lini? Ili kujibu maswali hayo twapaswa kuchunguza kusudi la Mungu kuhusu wanadamu. Kufanya hivyo kutatusaidia tuelewe sababu inayofanya Mungu aruhusu kuteseka na jambo atakalofanya.

Uwezo wa Kujiamulia Mambo

Mungu alipoumba mwanadamu wa kwanza, hakuumba tu mwili wenye ubongo. Isitoshe, Mungu hakuumba Adamu na Hawa wawe kama mashine zisizotumia akili. Aliwapa uwezo wa kujiamulia mambo. Na hiyo ilikuwa zawadi bora kabisa, kwa kuwa ‘Mungu aliona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.’ (Mwanzo 1:31) Naam, “kazi yake ni kamilifu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Sisi sote huthamini uwezo huu wa kujiamulia mambo kwa sababu hatutaki matendo na mawazo yetu yote yaamuliwe na mtu mwingine na hivyo tusiwe na uwezo wa kuamua lolote.

Lakini, je, uwezo mzuri wa kujiamulia mambo ulipasa kutumiwa bila mipaka? Katika mwelekezo uliotolewa kwa Wakristo wa mapema, Neno la Mungu lajibu: “Iweni kama watu huru, na bado mkishika uhuru wenu, si kama kisetiri cha ubaya, bali kama watumwa wa Mungu.” (1 Petro 2:16) Ili watu wote wanufaike, lazima kuwe na mipaka. Kwa hiyo, uwezo wa kujiamulia mambo ulipasa kuelekezwa na utawala wa sheria. La sivyo, kungekuwa na mchafuko.

Sheria ya Nani?

Ni sheria ya nani ambayo ingetumiwa kuamua mipaka ifaayo ya uhuru? Jibu la swali hilo lahusiana na sababu ya msingi ambayo imemfanya Mungu aruhusu kuteseka. Kwa kuwa Mungu ndiye aliyeumba wanadamu, anajua sheria wanazohitaji kutii kwa ajili ya faida yao na ya wengine. Biblia yasema hivi: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—Isaya 48:17.

Bila shaka, hili ndilo jambo muhimu: Wanadamu hawakuumbwa wajitegemee bila Mungu. Aliwaumba kwa njia ambayo wangepata furaha na mafanikio kwa kutii sheria zake za uadilifu. Yeremia aliyekuwa nabii wa Mungu alisema hivi: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.

Mungu aliwaumba wanadamu watii sheria zake za asili, kama vile nguvu za uvutano. Vivyo hivyo, aliumba wanadamu watii sheria zake za adili, ambazo zimekusudiwa kutokeza jamii yenye upatano. Kwa hiyo, ni kwa sababu nzuri Neno la Mungu huhimiza: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe.”—Mithali 3:5.

Kwa hiyo, familia ya kibinadamu haingeweza kamwe kufaulu kujiongoza pasipo utawala wa Mungu. Kwa kujaribu kujitegemea pasipo Mungu, watu wangebuni mifumo ya kijamii, kiuchumi, kisiasa, na kidini ambayo ingehitilafiana, na ‘mtu angekuwa na mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’—Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989.

Kwa Nini Mambo Yalienda Mrama?

Mungu alimwumba Adamu na Hawa wakiwa wakamilifu. Walikuwa na akili na miili mikamilifu na makao ya bustani ya paradiso. Kama wangejitiisha kwa utawala wa Mungu, wangebaki wakiwa wakamilifu na wenye furaha. Baada ya muda, wangekuwa wazazi wa familia ya wanadamu wakamilifu na wenye furaha ambao wangeishi katika paradiso duniani. Hilo ndilo lililokuwa kusudi la Mungu kwa wanadamu.—Mwanzo 1:27-29; 2:15.

Hata hivyo, wazazi wetu wa kwanza walitumia vibaya uhuru wao wa kujiamulia mambo. Walifikiri kimakosa kwamba wangeweza kufanikiwa pasipo kumtegemea Mungu. Waliamua wenyewe kuvunja sheria zake. (Mwanzo, sura ya 3) Kwa sababu walikataa utawala wake, hakuwajibika tena kuendelea kuwadumisha wakiwa wakamilifu. ‘Walitenda mambo ya uharibifu, hawakuwa watoto wake, hii ikawa ila yao.’—Kumbukumbu la Torati 32:5.

Tangu wakati walipokosa kumtii Mungu, Adamu na Hawa walianza kudhoofika mwili na akili. Yehova ndiye chemchemi ya uzima. (Zaburi 36:9) Kwa sababu ya kujitenga na Yehova, wenzi wa kwanza wa kibinadamu wakawa wasio wakamilifu na hatimaye wakafa. (Mwanzo 3:19) Kupatana na sheria za urithi, wazao wao wangerithi tu kile ambacho wazazi wao walikuwa nacho. Ni nini hicho? Ni kutokamilika na kifo. Kwa hiyo mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

Suala Kuu Kuhusu Enzi Kuu

Adamu na Hawa walipomwasi Mungu, walipinga enzi yake kuu, yaani, haki yake ya kutawala. Yehova angaliweza kuwaangamiza na kuumba tena wanadamu wengine wawili, lakini kufanya hivyo hakungalitatua suala kuhusu ni utawala wa nani ulio bora na unaowafaa watu. Kwa kupewa muda wa kuanzisha jamii zao kulingana na mawazo yao wenyewe, wanadamu wangaliweza kudhihirisha bila shaka yoyote kama utawala pasipo kumtegemea Mungu unaweza kufaulu.

Historia ya wanadamu ambayo imedumu kwa maelfu ya miaka imefunua nini? Kwa karne hizo zote, watu wamejaribu mifumo mbalimbali ya kijamii, kisiasa, na kidini. Hata hivyo, uovu na kuteseka kumeendelea. Kwa kweli, ‘watu waovu wameendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi,’ hasa katika wakati wetu.—2 Timotheo 3:13.

Kumekuwa na mafanikio ya hali ya juu zaidi ya kisayansi na kiviwanda katika karne ya 20. Lakini wanadamu waliteseka zaidi katika karne hiyo kuliko karne nyingine yoyote katika historia. Licha ya maendeleo ya kitiba ambayo yamefanywa, bado sheria ya Mungu ni ya kweli: Wanadamu ambao wamejitenga na Mungu—chanzo cha uhai—huwa wagonjwa, huzeeka, na kufa. Ni wazi kwamba wanadamu hawawezi ‘kuongoza hatua zao’!

Enzi ya Mungu Yatetewa

Mara moja na basi, jaribio hili lenye kuhuzunisha la kujitegemea pasipo Mungu limedhihirisha kwamba utawala wa wanadamu hauwezi kufanikiwa kamwe. Ni utawala wa Mungu peke yake unaoweza kuleta furaha, umoja, afya, na uhai. Isitoshe, Neno la Yehova Mungu lisilokosea, Biblia Takatifu, laonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za utawala wa kibinadamu pasipo kumtegemea Mungu. (2 Timotheo 3:1-5) Muda ambao Yehova ameruhusu wanadamu wajitawale, akaruhusu uovu na kuteseka, wakaribia kwisha.

Hivi karibuni Mungu ataingilia mambo ya wanadamu. Maandiko hutuambia hivi: “Katika siku za wafalme hao [utawala wa wanadamu uliopo sasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake [wanadamu hawatatawala dunia tena kamwe]; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.

Kichwa kikuu cha Biblia ni kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova Mungu kupitia Ufalme wa kimbingu. Hilo ndilo lililokuwa fundisho kuu la Yesu. Alisema hivi: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Utawala wa Mungu utakapochukua mahali pa utawala wa wanadamu, ni nani watakaookoka na ni nani ambao hawataokoka? Kwenye Mithali 2:21, 22 twahakikishiwa hivi: “Maana wanyofu [wanaounga mkono utawala wa Mungu] watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu [watu wasiounga mkono utawala wa Mungu] watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” Mtunga-zaburi aliyepuliziwa na Mungu aliimba hivi: “Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani. Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:10, 11, 29.

Ulimwengu Mpya Mzuri Sana

Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, waokokaji wa mwisho wa mfumo huu wa mambo wataingizwa katika dunia isiyo na uovu wala kuteseka. Wanadamu watapewa maagizo kutoka kwa Mungu, kisha baada ya muda “dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9) Fundisho hili lenye kuimarisha na linalofaa litatokeza jamii ya kibinadamu yenye amani na upatano. Hivyo, hakutakuwa tena na vita, mauaji, jeuri, kubakwa, wizi, au uhalifu mwingine wowote.

Wanadamu watiifu watakaoishi katika ulimwengu mpya wa Mungu watanufaika sana kimwili. Matokeo yote mabaya ya uasi dhidi ya utawala wa Mungu yataondolewa. Kutokamilika, ugonjwa, uzee, na kifo havitakuwako tena. Biblia hutuhakikishia hivi: “Hapana mwenyeji atakayesema, mimi mgonjwa.” Isitoshe, Maandiko huahidi hivi: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.” (Isaya 33:24; 35:5, 6) Itapendeza kama nini kufurahia afya njema kila siku—milele!

Chini ya uongozi wa Mungu wenye upendo, wakazi wa dunia mpya watatumia nishati na stadi zao kufanya dunia yote iwe paradiso. Umaskini, njaa, ukosefu wa makao hautakuwapo tena kwa kuwa Isaya atabiri hivi: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine.” (Isaya 65:21, 22) Kwa kweli, “wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Mika 4:4.

Dunia itabadilika kwa sababu ya utunzaji wenye upendo kutoka kwa Mungu na kwa wanadamu watiifu. Tuna uhakikisho huu wa Kimaandiko: “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kam waridi. . . . Katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani.” (Isaya 35:1, 6) “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.

Vipi juu ya mabilioni ya watu ambao wamekufa? Wale walio katika kumbukumbu la Mungu watahuishwa, kwa kuwa “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Naam, wafu watafufuliwa. Watafundishwa kweli nzuri kuhusu utawala wa Mungu na kupewa fursa ya kuishi milele katika Paradiso.—Yohana 5:28, 29.

Kupitia ufufuo, Yehova Mungu atatangua kabisa hali mbaya ya kuteseka, ugonjwa, na kifo ambayo imewapata wanadamu kwa maelfu ya miaka. Hakuna ugonjwa tena! Hakuna ulemavu tena! Hakuna kifo tena! Mungu “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani [yatakuwa] yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.

Hivyo ndivyo Mungu atakavyokomesha kuteseka. Ataharibu ulimwengu huu uliopotoka na kuleta mfumo mpya kabisa wa mambo ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Hizo ni habari njema kama nini! Twahitaji sana ulimwengu huo mpya. Na tutauona hivi karibuni. Kutokana na kutimizwa kwa unabii wa Biblia, twajua kwamba ulimwengu mpya unakaribia sana, na muda ambao Mungu ameruhusu kuteseka umekaribia kwisha.—Mathayo 24:3-14.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

Kushindwa kwa Utawala wa Kibinadamu

Helmut Schmidt aliyekuwa Waziri Mkuu wa Ujerumani, alisema hivi kuhusu utawala wa binadamu: “Sisi wanadamu . . . sikuzote tumetawala ulimwengu kwa kadiri fulani, na mara nyingi tumetawala kwa njia mbaya sana. . . . Hatujawahi kutawala ulimwengu kwa amani kamili.” Kichapo Human Development Report 1999 kilisema hivi: “Nchi zote zinaripoti kuzorota kwa maadili, jambo ambalo limetokeza mahitilafiano ya kijamii, uhalifu mwingi zaidi, jeuri nyingi zaidi ya kinyumbani. . . . Mataifa yote yanashindwa kukabiliana na vitisho vinavyoongezeka duniani pote.”

[Picha katika ukurasa wa 8]

“Watajifurahisha kwa wingi wa amani.” —Zaburi 37:11

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

Picha ya tatu kutoka juu, mama na mtoto: FAO photo/B. Imevbore; chini, mlipuko: U.S. National Archives photo