Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwongozo wa Mungu Katika Kuchagua Mwenzi wa Ndoa

Mwongozo wa Mungu Katika Kuchagua Mwenzi wa Ndoa

Mwongozo wa Mungu Katika Kuchagua Mwenzi wa Ndoa

“Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.”—ZABURI 32:8.

1. Ni mambo gani muhimu yanayofanya ndoa ifanikiwe?

WAPIGA-NGOMA waanza kupiga ngoma zao. Kwa ustadi, mwimbaji mwenye sauti tamu ajiunga nao. Matokeo yanakuwa muziki wenye kupendeza. Wanaume wawili wanapakua makatoni mazito ya bidhaa kutoka kwenye lori kubwa. Mmoja anamtupia mwenzake katoni naye analidaka kwa urahisi kisha anangojea atupiwe lingine. Inaonekana kana kwamba mambo hayo mawili yanafanywa kwa urahisi tu. Hata hivyo, ni nani anayeweza hata kujaribu kufanya jambo kama hilo bila mazoezi, bila mwenzi stadi, na hasa mwongozo au mafundisho yafaayo. Vivyo hivyo, huenda ndoa yenye mafanikio ikaonekana kana kwamba hutokea tu. Lakini ndoa pia hutegemea mwenzi mzuri, ushirikiano, na hasa ushauri wenye hekima. Kwa kweli mwongozo ufaao ni muhimu.

2. (a) Ni nani aliyeanzisha mpango wa ndoa naye alikuwa na kusudi gani? (b) Mipango fulani ya ndoa imefanywaje?

2 Ni jambo la kawaida kwa mwanamume au mwanamke kijana kufikiria kuwa na mwenzi wa ndoa maishani. Tangu Yehova Mungu aanzishe mpango wa ndoa, limekuwa jambo la kawaida kwa wanaume na wanawake kufunga ndoa. Lakini mwanamume wa kwanza, Adamu, hakujichagulia mke. Kwa upendo Yehova alimpa mke. (Mwanzo 2:18-24) Alitaka wenzi hao wa kwanza wazae na hatimaye waijaze dunia. Baada ya ndoa hiyo ya kwanza, kwa kawaida mipango ya ndoa ilifanywa na wazazi wa bibi-arusi na bwana-arusi, nyakati nyingine baada ya kupata kibali cha waliohusika. (Mwanzo 21:21; 24:2-4, 58; 38:6; Yoshua 15:16, 17) Ingawa ndoa za kupangwa bado ni jambo la kawaida katika nchi na tamaduni fulani, wengi leo hujichagulia mwenzi wao wa ndoa.

3. Mwenzi wa ndoa apasa kuchaguliwaje?

3 Tunapaswa kuchaguaje mwenzi wa ndoa? Watu wengine huvutiwa na sura yenye kupendeza. Wengine hutafuta manufaa za kimwili, wakitaka mtu atakayewatunza vizuri na kutimiza mahitaji yao na tamaa zao. Lakini je, kuchagua mwenzi wa ndoa kwa kutegemea mambo hayo tu kutatuwezesha tuwe na ndoa yenye furaha na yenye kuridhisha? “Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; bali mwanamke amchaye BWANA, ndiye atakayesifiwa,” lasema andiko la Mithali 31:30. Tunajifunza jambo muhimu katika andiko hilo: Mzingatie Yehova unapochagua mwenzi.

Mwongozo Wenye Upendo Kutoka kwa Mungu

4. Mungu hutoa msaada gani kuhusiana na kuchagua mwenzi wa ndoa?

4 Yehova Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo ameandaa Neno lake lililoandikwa ili kutuongoza katika mambo yote. Yeye asema: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.” (Isaya 48:17) Si ajabu kwamba katika Biblia kuna miongozo ya kuchagua mwenzi wa ndoa ambayo kwa muda mrefu imethibitika kuwa yenye matokeo. Yehova anataka ndoa zetu zidumu na ziwe zenye furaha. Kwa hiyo, ameandaa msaada ili tuweze kuelewa na kutumia miongozo hiyo. Je, hatungetazamia Muumba wetu mwenye upendo afanye hivyo?—Zaburi 19:8.

5. Ni mambo gani ambayo ni ya lazima ili ndoa iwe na furaha yenye kudumu?

5 Yehova alipoanzisha mpango wa ndoa, alitaka uwe wenye kudumu. (Marko 10:6-12; 1 Wakorintho 7:10, 11) Hiyo ndiyo sababu ‘anachukia talaka.’ Yeye huiruhusu tu kwa msingi wa “uasherati.” (Malaki 2:13-16, Biblia Habari Njema; Mathayo 19:9) Kwa hiyo, kuchagua mwenzi wa ndoa ni jambo zito ambalo hatupaswi kulichukulia kivivi hivi tu. Ndoa ni mojawapo ya maamuzi ambayo yanaweza kukuletea furaha au huzuni. Ingawa uchaguzi mzuri unaweza kuboresha maisha ya mtu na kuyafanya yawe yenye kuridhisha, uchaguzi mbaya unaweza kuleta huzuni ya kudumu. (Mithali 21:19; 26:21) Ili furaha iendelee, ni muhimu kufanya uchaguzi kwa busara na kuwa tayari kuwajibika kabisa, kwa kuwa Mungu alianzisha ndoa iwe muungano ambao ungefanikiwa kukiwepo upatano na ushirikiano.—Mathayo 19:6.

6. Kwa nini wanaume na wanawake vijana hasa wanahitaji kuwa waangalifu wanapochagua mwenzi, nao wanawezaje kufanya uamuzi wa hekima zaidi?

6 Wanaume na wanawake vijana hasa wapaswa kuwa waangalifu wanapochagua mwenzi ili uwezo wao wa kuchanganua mambo usipotoshwe na sura na tamaa yenye nguvu ya ngono. Kwa kweli, ndoa inayotegemea mambo hayo tu inaweza kutokeza dharau au hata chuki. (2 Samweli 13:15) Kwa upande mwingine, upendo wenye kudumu unaweza kusitawishwa tunapopata kumjua mwenzi wetu na vilevile kujijua vema zaidi. Tunahitaji kutambua kwamba mwanzoni moyo wetu unaweza kutamani kitu ambacho huenda kisitufae. (Yeremia 17:9) Hiyo ndiyo sababu mwongozo wa Mungu unaopatikana katika Biblia ni muhimu sana. Hutusaidia kufahamu jinsi tuwezavyo kufanya maamuzi yenye hekima zaidi maishani. Mtunga-zaburi alisema hivi akimwakilisha Yehova: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.” (Zaburi 32:8; Waebrania 4:12) Ingawa ndoa inaweza kutosheleza uhitaji tuliozaliwa nao wa kupendwa na kuwa na rafiki, pia ina magumu ambayo hutaka mtu awe mkomavu na mwenye busara.

7. Kwa nini watu wengine hawakubali ushauri wa Biblia kuhusu kuchagua mwenzi wa ndoa, lakini kufanya hivyo kunaweza kusababisha nini?

7 Ni hekima kutii yale ambayo Mwanzilishi wa ndoa anasema kuhusu kuchagua mwenzi. Hata hivyo, huenda tukakataa ushauri wa Biblia unaotolewa na wazazi au wazee Wakristo. Huenda tukahisi kwamba hawatuelewi kikamili, na huenda hisia zenye nguvu zikatuchochea tufanye vile moyo wetu unavyotaka. Hata hivyo, tukabilipo ukweli wa mambo, huenda tukaona kwamba hatukufuata ushauri wenye hekima uliotolewa kwa manufaa yetu. (Mithali 23:19; 28:26) Huenda tukajikuta katika ndoa ambayo haina upendo, tukiwa na watoto ambao ni vigumu kuwalea, na labda hata tukiwa na mwenzi asiyeamini. Lingekuwa jambo la kusikitisha kama nini ikiwa mpango ambao ungetuletea furaha kubwa ungesababisha huzuni!

Ujitoaji Kimungu Ni Muhimu

8. Ujitoaji kimungu unasaidiaje ndoa iwe yenye kudumu na yenye furaha?

8 Ni kweli kwamba uvutano kati ya watu wawili huchangia kuwa na ndoa imara. Lakini ili ndoa iwe yenye kudumu na yenye furaha ni muhimu sana kwa watu waliooana kufuata maadili yaleyale. Wote wawili wanapojitoa kwa Yehova Mungu, jambo hilo huleta muungano wenye kudumu na huchangia umoja kwa njia isiyo na kifani. (Mhubiri 4:12) Wenzi Wakristo wanapozingatia ibada ya kweli ya Yehova katika maisha yao, wanaungana kiroho, kiakili, na kiadili. Wanajifunza Neno la Mungu pamoja. Wanasali pamoja, na kufanya hivyo huunganisha mioyo yao. Huandamana kwenda kwenye mikutano ya Kikristo na kuhubiri pamoja katika huduma ya shambani. Mambo hayo yote husaidia kutokeza muungano wa kiroho unaowafanya wawe na ukaribu zaidi. Na jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba kufanya hivyo huleta baraka za Yehova.

9. Abrahamu alifanya nini kwa habari ya kumtafutia Isaka mke, na matokeo yakawaje?

9 Abrahamu, mzee wa ukoo mwaminifu, alikuwa mwenye ujitoaji kimungu. Kwa sababu hiyo, alitaka kumpendeza Mungu wakati ulipofika wa kumchagulia mwanawe Isaka mke. Abrahamu alimwambia hivi mtumishi wake wa nyumbani mwaminifu: “Nitakuapisha kwa BWANA, Mungu wa mbingu, na Mungu wa nchi, kwamba hutamtwalia mwanangu mke katika binti za Wakanaani ambao nakaa kati yao; bali enenda hata nchi yangu, na kwa jamaa zangu, ukamtwalie mwanangu Isaka mke. . . . [Yehova] atampeleka malaika wake mbele yako, nawe utamtwalia mwanangu mke tokea huko.” Rebeka alikuwa mke bora, naye Isaka alimpenda sana.—Mwanzo 24:3, 4, 7, 14-21, 67.

10. Waume na wake wana majukumu gani ya Kimaandiko?

10 Ikiwa sisi ni Wakristo ambao hatujafunga ndoa, ujitoaji kimungu utatusaidia kusitawisha sifa ambazo zitatuwezesha kutimiza matakwa ya Kimaandiko ya ndoa. Mtume Paulo anataja baadhi ya majukumu ya waume na wake: “Acheni wake wawe katika ujitiisho kwa waume zao kama kwa Bwana . . . Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujikabidhi mwenyewe kwa ajili yalo . . . Waume wapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. . . . Acheni kila mtu mmoja-mmoja kati yenu ampende hivyo mke wake kama yeye mwenyewe; kwa upande mwingine, mke apaswa kuwa na staha yenye kina kirefu kwa mume wake.” (Waefeso 5:22-33) Kama tuwezavyo kuona, maneno ya Paulo yaliyopuliziwa yakazia uhitaji wa kuwa na upendo na staha. Kufuata ushauri huo kwahusisha kumcha Yehova. Kunahitaji uwajibikaji wa moyo wote hata hali ziwe nzuri au mbaya. Wakristo wanaofikiria kufunga ndoa wapaswa kuwa na uwezo wa kutimiza jukumu hilo.

Kuamua Wakati wa Kufunga Ndoa

11. (a) Ni ushauri gani kuhusu wakati wa kufunga ndoa ambao umetolewa katika Maandiko? (b) Ni mfano gani unaoonyesha hekima ya kufuata ushauri wa Biblia katika 1 Wakorintho 7:36?

11 Ni muhimu kujua wakati ambapo tuko tayari kufunga ndoa. Kwa kuwa watu hutofautiana katika jambo hilo, Maandiko hayatoi masharti yoyote kuhusu umri. Hata hivyo, yanaonyesha kwamba ni vizuri kungojea hadi tuwe ‘tumepita mchanuko wa ujana,’ wakati ambapo tamaa zenye nguvu za ngono zinaweza kupotosha uwezo wa mtu wa kuchanganua mambo ifaavyo. (1 Wakorintho 7:36) Michelle asema hivi: “Nyakati nyingine ilikuwa vigumu kwangu kufuata ushauri huo hasa nilipoona marafiki wangu wakifanya miadi ya kimapenzi na kufunga ndoa, wengi wao wakiwa bado matineja. Lakini nilitambua kwamba ushauri huo unatoka kwa Yehova, naye hutuambia tu mambo yanayotunufaisha. Kwa kutoharakisha kufunga ndoa, niliweza kusitawisha uhusiano wangu pamoja na Yehova na kuwa na uzoefu maishani, ambao mtu hawezi kuwa nao anapokuwa tineja. Miaka kadhaa baadaye, niliweza kushughulikia vema zaidi majukumu na pia matatizo yanayotokea katika ndoa.”

12. Kwa nini si jambo la hekima kukimbilia kufunga ndoa ukiwa bado mchanga?

12 Mara nyingi wale wanaokimbilia kufunga ndoa wakiwa bado wachanga sana hutambua kwamba mahitaji yao na tamaa zao hubadilika wanapokomaa. Ndipo wang’amuapo kwamba mambo yaliyowapendeza pale mwanzoni si muhimu sana. Mkristo mmoja kijana alikuwa ameazimia kuolewa akiwa na umri wa miaka 16. Nyanya yake na pia mama yake waliolewa wakiwa na umri huo. Mwanamume mmoja kijana, ambaye msichana huyo alipendezwa naye, alipokataa kumwoa wakati huo, alichagua mtu mwingine aliyekuwa tayari kufanya hivyo. Hata hivyo, baadaye alijuta sana kwa sababu ya kuamua mambo harakaharaka.

13. Mara nyingi wale wanaofunga ndoa kabla hawajakomaa wanapungukiwa katika mambo gani?

13 Unapofikiria kufunga ndoa, ni muhimu kuelewa kikamili yanayohusika. Wanapofunga ndoa kabla hawajakomaa, wenzi wa ndoa wachanga wanaweza kupata matatizo mengi sana ambayo yaelekea inakuwa vigumu kwao kuyatatua. Huenda wasiwe na uzoefu na ukomavu unaohitajika kushughulika na mikazo ya ndoa na kulea watoto. Twapaswa kufunga ndoa tu tunapokuwa tayari kimwili, kiakili, na kiroho kuweza kudumisha muungano huo.

14. Ni nini kinachohitajiwa ili kushughulikia hali zenye mkazo katika ndoa?

14 Paulo aliandika kwamba wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Kutatokea matatizo kwa kuwa ndoa ni ya watu wawili walio tofauti, na maoni yatatofautiana. Kwa sababu ya kutokamilika, huenda ikawa vigumu kutimiza jukumu letu la Kimaandiko katika mpango wa ndoa. (1 Wakorintho 11:3; Wakolosai 3:18, 19; Tito 2:4, 5; 1 Petro 3:1, 2, 7) Tunahitaji ukomavu na usawaziko wa kiroho ili tuweze kutafuta na kufuata mwongozo wa Mungu na kushughulikia kwa upendo hali zenye mkazo.

15. Wazazi wanaweza kuwatayarishaje watoto wao kwa ajili ya ndoa? Toa mfano.

15 Wazazi wanaweza kuwatayarisha watoto wao kwa ajili ya ndoa kwa kuwasaidia kuelewa umuhimu wa kufuata mwongozo wa Mungu. Kwa kutumia kwa ustadi Maandiko na vichapo vya Kikristo, wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao kuamua kama wao au mtu wanayetazamia kufunga ndoa naye yuko tayari kuwajibika katika ndoa. * Blossom aliyekuwa na umri wa miaka 18 alidhani alimpenda mwanamume mmoja kijana katika kutaniko lao. Mwanamume huyo alikuwa mhudumu painia wa wakati wote, nao walitaka kufunga ndoa. Lakini wazazi wake wakamwomba angoje kwa mwaka mmoja kwa kuwa walihisi kwamba alikuwa mchanga mno. Blossom aliandika hivi baadaye: “Ninashukuru sana kwamba nilisikiliza ushauri huo wa hekima. Katika mwaka huo, nilikomaa kwa kiasi fulani na kutambua kwamba mwanamume huyo hakuwa na sifa za mwenzi wa ndoa afaaye. Hatimaye aliacha tengenezo, nami nikaokoka kile ambacho kingekuwa msiba mkubwa maishani mwangu. Ni jambo zuri kama nini kuwa na wazazi ambao maoni yao yanaweza kutegemeka!”

‘Oa au Olewa Katika Bwana Tu’

16. (a) Wakristo wanaweza kupata jaribu gani kuhusiana na ‘kuoa au kuolewa katika Bwana’? (b) Wakristo wapaswa kufikiria nini wanaposhawishwa kufunga ndoa na mtu asiyeamini?

16 Mwelekezo wa Yehova kwa Wakristo ni wazi kabisa: ‘Oa au olewa katika Bwana tu.’ (1 Wakorintho 7:39) Huenda wazazi Wakristo na watoto wao wakapata jaribu kuhusiana na jambo hilo. Vipi? Huenda vijana wanaotaka kufunga ndoa wasipate wenzi katika kutaniko. Angalau hali inaonekana hivyo. Katika eneo fulani huenda idadi ya wanaume ikawa ndogo ikilinganishwa na ya wanawake, au huenda kusiwe na mwanamume yeyote anayeonekana anafaa kuwa mwenzi wa ndoa. Huenda mwanamume kijana au mwanamke kijana ambaye si mshiriki aliyejiweka wakfu wa kutaniko akapendezwa na kijana Mkristo na kukawa na mkazo wa kupuuza viwango ambavyo Yehova ameweka. Katika hali kama hizo, ingefaa kufikiria kielelezo cha Abrahamu. Njia moja ambayo alidumisha uhusiano mzuri pamoja na Mungu ni kwa kuhakikisha kwamba mwana wake Isaka alioa mwabudu wa kweli wa Yehova. Isaka alifanya vivyo hivyo kuhusiana na mwanaye Yakobo. Haikuwa rahisi kufanya hivyo lakini Mungu alipendezwa na jitihada zao na kuwabariki.—Mwanzo 28:1-4.

17. Kwa nini kufunga ndoa na mtu asiyeamini kwaweza kuwa na matokeo mabaya sana, na ni nini iliyo sababu muhimu hata zaidi ya ‘kuoa au kuolewa katika Bwana tu’?

17 Katika ndoa chache mwenzi asiyeamini hatimaye amekuwa Mkristo. Hata hivyo, mara nyingi kufunga ndoa na watu wasioamini kumekuwa na matokeo mabaya. Unapofunga ndoa na mtu asiyeamini mnakuwa na imani, kanuni, au miradi tofauti. (2 Wakorintho 6:14) Jambo hilo linaweza kuathiri vibaya mawasiliano na furaha ya ndoa. Kwa mfano, mwanamke mmoja Mkristo alihuzunika sana kwa kuwa baada ya mikutano yenye kujenga, hangeweza kwenda nyumbani na kuzungumzia mambo ya kiroho na mwenzi wake asiyeamini. Bila shaka, jambo la muhimu hata zaidi ni kwamba ‘unapooa au kuolewa katika BWANA’ unaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova. Tunapotii Neno la Mungu, mioyo yetu haitushutumu, kwa kuwa tunafanya mambo “yanayopendeza machoni pake.”—1 Yohana 3:21, 22.

18. Unapofikiria kufunga ndoa, wapaswa kuzingatia mambo gani muhimu, na kwa nini?

18 Unapofikiria kufunga ndoa, ni muhimu sana kuzingatia sifa nzuri na hali ya kiroho ya yule unayetazamia kufunga ndoa naye. Utu wa Kikristo, pamoja na kumpenda Mungu na kujitoa kwake kwa nafsi yote, ni mambo muhimu zaidi kuliko sura yenye kuvutia. Wale wanaothamini na kutimiza jukumu la kuwa wenzi wa ndoa wenye nguvu kiroho, hupata kibali cha Mungu. Ndoa inaweza kuwa thabiti sana wenzi wanaposhirikiana katika ujitoaji wao kwa Muumba na kufuata kikamili mwongozo wake. Kwa njia hiyo Yehova huheshimiwa, na ndoa inakuwa na msingi imara kiroho ambao utasaidia muungano huo uwe wenye kudumu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Soma gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 1999, ukurasa wa 4-8.

Ungejibuje?

• Kwa nini mwongozo wa Mungu unahitajiwa katika kuchagua mwenzi mzuri wa ndoa?

• Ujitoaji kimungu utasaidiaje kuimarisha kifungo cha ndoa?

• Wazazi wanaweza kuwatayarishaje watoto wao kwa ajili ya ndoa?

• Kwa nini ni muhimu ‘kuoa au kuolewa katika Bwana tu’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kufuata ushauri wa Mungu katika kuchagua mwenzi wako kunaweza kutokeza furaha nyingi

[Picha katika ukurasa wa 18]

‘Kuoa au kuolewa katika Bwana tu’ huleta baraka nyingi