Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ikiwa Mungu Yuko Upande Wetu, Nani Atakayekuwa Dhidi Yetu?”

“Ikiwa Mungu Yuko Upande Wetu, Nani Atakayekuwa Dhidi Yetu?”

“Ikiwa Mungu Yuko Upande Wetu, Nani Atakayekuwa Dhidi Yetu?”

“Basi, tutasema nini kuhusu mambo haya? Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu?”—WAROMA 8:31.

1. Ni nani walioondoka Misri pamoja na Waisraeli, na ni nini kilichowafanya waondoke?

WAISRAELI walipokuwa wakitoka Misri wakaishi wakiwa watu huru, baada ya kuishi Misri kwa miaka 215—mwingi wa muda huo wakiwa utumwani—‘kundi kubwa la watu wengine pia waliandamana nao.’ (Kutoka 12:38, BHN) Watu hao wasio Waisraeli walishuhudia mapigo kumi yenye kutia hofu ambayo yalisababisha uharibifu mkubwa nchini Misri na kufanya miungu yao ya uongo idharauliwe. Wakati huohuo, walikuwa wamejionea uwezo wa Yehova wa kuwalinda watu wake hasa kuanzia pigo la nne na kuendelea. (Kutoka 8:23, 24) Ijapokuwa hawakufahamu kikamili makusudi ya Yehova, walikuwa na uhakika kuhusu jambo hili: Miungu ya Misri ilishindwa kuwalinda Wamisri, ilhali Yehova alithibitika kuwa mwenye nguvu kwa niaba ya Waisraeli.

2. Kwa nini Rahabu aliwaunga mkono wapelelezi Waisraeli, na kwa nini uhakika wake katika Mungu wao haukuwa bure?

2 Miaka 40 baadaye, kabla Waisraeli hawajaingia katika Bara Lililoahidiwa, Yoshua aliyekuwa mwandamizi wa Musa, aliwatuma wanaume wawili wakaipeleleze nchi hiyo. Walipofika huko, walikutana na Rahabu mkazi wa Yeriko. Kwa sababu ya mambo aliyokuwa amesikia kuhusu matendo ya Yehova yenye nguvu ya kuwalinda Waisraeli kwa muda wa miaka 40 baada ya kutoka Misri, alijua kwamba ingekuwa lazima kuunga mkono watu wa Mungu iwapo angetaka kubarikiwa naye. Kwa sababu ya uamuzi wake wa hekima, yeye na watu wa nyumba yake waliokolewa wakati Waisraeli walipoteka jiji hilo. Kuokolewa kwao kimuujiza kulithibitisha wazi kwamba Mungu alikuwa pamoja nao. Kwa hiyo, uhakika ambao Rahabu alikuwa nao katika Mungu wa Waisraeli haukuwa bure.—Yoshua 2:1, 9-13; 6:15-17, 25.

3. (a) Yesu alifanya muujiza gani karibu na jiji lililojengwa upya la Yeriko, nao viongozi wa kidini Wayahudi waliitikiaje? (b) Wayahudi fulani, na baadaye watu wengi wasio Wayahudi, walikuja kutambua nini?

3 Karne 15 baadaye, Yesu Kristo alimponya mwombaji kipofu karibu na jiji lililojengwa upya la Yeriko. (Marko 10:46-52; Luka 18:35-43) Mwanamume huyo alimwomba Yesu amwonyeshe rehema, jambo linaloonyesha kwamba alitambua kuwa Mungu alimkubali na kumwunga mkono Yesu. Kwa upande mwingine, viongozi wa kidini Wayahudi pamoja na wafuasi wao kwa ujumla, walikataa miujiza ya Yesu kuwa uthibitisho kwamba alikuwa akifanya kazi ya Mungu. Badala yake walimchambua. (Marko 2:15, 16; 3:1-6; Luka 7:31-35) Hata baada ya kuthibitishiwa kwamba Yesu waliyemwua amefufuliwa, hawakutaka kukubali kwamba hiyo ilikuwa kazi ya Mungu. Badala yake, walikuwa katika mstari wa mbele kuwanyanyasa wafuasi wa Yesu, na kujaribu kuzuia kazi yao ya ‘kutangaza habari njema ya Bwana Yesu.’ Lakini Wayahudi fulani, na baadaye watu wengi wasio Wayahudi, waliyazingatia mambo hayo na kuyachanganua kwa usahihi. Ilikuwa wazi kwao kwamba Mungu alikuwa amewakataa viongozi Wayahudi waliojiona kuwa waadilifu na alikuwa akiunga mkono wafuasi wanyenyekevu wa Yesu Kristo.—Matendo 11:19-21.

Ni Nani Wanaoungwa Mkono na Mungu Leo?

4, 5. (a) Watu fulani wana maoni gani kuhusu kuchagua dini? (b) Ni swali gani muhimu linalohusika katika kutambua dini ya kweli?

4 Kasisi mmoja alisema hivi katika mahojiano yaliyofanywa hivi karibuni kwenye televisheni kuhusu dini ya kweli: “Dini ya kweli humfanya mtu awe mzuri zaidi anapoishi kulingana na sheria zake.” Ni kweli kwamba dini ya kweli hufanya watu wawe wazuri zaidi. Je, tunaweza kusema dini fulani inaungwa mkono na Mungu kwa kuwa tu inafanya watu wawe wazuri? Je, hiyo ndiyo kanuni pekee ya kuamua kama dini fulani ni ya kweli?

5 Kila mtu huthamini kuwa na uhuru wa kujichagulia mambo, kutia ndani kuchagua dini atakayofuata. Lakini uhuru wa kujichagulia haumaanishi kwamba mtu atafanya uchaguzi unaofaa. Kwa mfano, watu fulani huchagua dini kwa sababu ya idadi ya wafuasi wake, utajiri wake, sherehe zake zenye madoido mengi, au kwa sababu ya uhusiano wao na familia zao. Kati ya mambo yanayotajwa juu hakuna hata moja linalosaidia kuamua iwapo dini fulani ni ya kweli au la. Swali muhimu kuhusiana na habari hiyo ni: Ni dini gani inayowahimiza wafuasi wake wafanye mapenzi ya Mungu na inayothibitisha waziwazi kwamba inaungwa mkono na Mungu, hivi kwamba wafuasi wake wanaweza kusema hivi kwa uhakika, “Mungu yuko upande wetu”?

6. Ni maneno gani ya Yesu yanayotambulisha dini ya kweli na dini isiyo ya kweli?

6 Yesu aliweka kanuni ya kutofautisha ibada ya kweli na isiyo ya kweli aliposema hivi: “Iweni wenye kulinda kuhusu manabii wasio wa kweli ambao huja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwa-mwitu walafi. Kwa matunda yao mtawatambua.” (Mathayo 7:15, 16; Malaki 3:18) Acheni tuchunguze baadhi ya “matunda,” au mambo yanayotambulisha dini ya kweli, ili tuweze kuamua kwa unyofu ni nani leo wanaoungwa mkono na Mungu.

Mambo Yanayotambulisha Wale Wanaoungwa Mkono na Mungu

7. Inamaanisha nini kufundisha tu mambo yanayotegemea Biblia?

7 Mafundisho yao yanategemea Biblia. Yesu alisema: “Kile nifundishacho si changu, bali ni chake yeye aliyenituma. Ikiwa yeyote atamani kufanya mapenzi Yake, atajua kuhusu fundisho kama ni la kutoka kwa Mungu au mimi nasema kwa ubuni wangu mwenyewe.” Pia alisema: “Yeye atokaye kwa Mungu husikiliza semi za Mungu.” (Yohana 7:16, 17; 8:47) Kwa kupatana na akili, ili mtu aungwe mkono na Mungu, ni lazima afundishe tu mambo ambayo Mungu amefunua katika Neno lake na kukataa mafundisho yanayotegemea hekima au mapokeo ya wanadamu.—Isaya 29:13; Mathayo 15:3-9; Wakolosai 2:8.

8. Kwa nini ni muhimu kutumia jina la Mungu katika ibada?

8 Wanatumia na kutangaza jina la Mungu, Yehova. Isaya alitabiri hivi: “Katika siku hiyo mtasema, mshukuruni BWANA, liitieni jina lake; yatangazeni matendo yake kati ya mataifa, litajeni jina lake kuwa limetukuka. Mwimbieni BWANA; kwa kuwa ametenda makuu; na yajulikane haya katika dunia yote.” (Isaya 12:4, 5) Yesu alifundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Kwa hiyo, Wakristo walipaswa kutumikia wakiwa “watu kwa ajili ya jina la [Mungu]” wawe ni Wayahudi au si Wayahudi. (Matendo 15:14) Bila shaka, Mungu anapenda kuwaunga mkono wale wanaofurahia kuwa “watu kwa ajili ya jina lake.”

9. (a) Kwa nini shangwe hutambulisha wafuasi wa dini ya kweli? (b) Isaya atofautishaje dini ya kweli na isiyo ya kweli?

9 Wanadhihirisha utu wa Mungu wenye shangwe. Akiwa mtungaji wa “habari njema,” Yehova ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Basi waabudu wake wangekosaje furaha au kuwa wenye kutazamia mabaya tu sikuzote? Kujapokuwa taabu za ulimwengu na matatizo ya kibinafsi, Wakristo wa kweli hudumisha shangwe kwa sababu wanakula kwa ukawaida chakula cha kiroho ambacho kinapatikana kwa wingi. Isaya aonyesha tofauti iliyopo kati yao na wafuasi wa dini zisizo za kweli: “BWANA Mungu asema hivi, tazama, watumishi wangu watakula, bali ninyi mtaona njaa; tazama watumishi wangu watakunywa, bali ninyi mtaona kiu; tazama watumishi wangu watafurahi, bali ninyi mtatahayarika; tazama watumishi wangu wataimba kwa furaha ya moyo, bali ninyi mtalia kwa huzuni ya moyo; mtapiga kelele kwa sababu ya uchungu wa roho zenu.”—Isaya 65:13, 14.

10. Wafuasi wa dini ya kweli huepukaje kujifunza mambo kwa kujaribu-jaribu tu?

10 Mwenendo na maamuzi yao hutegemea kanuni za Biblia. Mwandishi wa Mithali atushauri hivi: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Mungu huwaunga mkono watu wanaomtegemea ili kupata mwongozo badala ya kutegemea nadharia zinazotofautiana za wanadamu ambao hupuuza hekima ya Mungu. Iwapo mtu yu tayari kuishi kupatana na Neno la Mungu basi ataepuka kujifunza mambo kwa kujaribu-jaribu tu.—Zaburi 119:33; 1 Wakorintho 1:19-21.

11. (a) Kwa nini wafuasi wa dini ya kweli hawawezi kugawanywa kuwa vikundi viwili, cha makasisi na cha watu wa kawaida? (b) Wale wanaoongoza miongoni mwa watu wa Mungu wanapaswa kuwekea kundi kielelezo gani?

11 Wamepangwa kitengenezo kama kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Yesu aliweka kanuni ifuatayo: “Msiitwe Rabi, kwa maana mmoja ni mwalimu wenu, lakini nyinyi nyote ni akina ndugu. Zaidi ya hayo, msiite yeyote baba yenu duniani, kwa maana mmoja ni Baba yenu, Aliye wa kimbingu. Wala msiitwe ‘viongozi,’ kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo. Lakini aliye mkubwa zaidi sana miongoni mwenu lazima awe mhudumu wenu.” (Mathayo 23:8-11) Katika kutaniko la akina ndugu hakuna makasisi wenye kiburi ambao hujitukuza kwa majina ya fahari na kujiinua juu ya watu wa kawaida. (Ayubu 32:21, 22) Wale wanaochunga kundi la Mungu wanaambiwa wafanye hivyo “si kwa kushurutishwa, bali kwa nia ya kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; wala si kama kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali [kuwa] vielelezo kwa kundi.” (1 Petro 5:2, 3) Wachungaji Wakristo wa kweli hawajifanyi kuwa wakubwa wa imani ya wengine. Wakiwa wafanyakazi wenzi katika utumishi wa Mungu, wao hujitahidi kuwa vielelezo vizuri.—2 Wakorintho 1:24.

12. Wale wanaotaka kuungwa mkono na Mungu wanapaswa kuwa na mtazamo gani uliosawazika kuhusu serikali za kibinadamu?

12 Wao hujitiisha kwa serikali za kibinadamu na bado hudumisha msimamo wa kutokuwamo. Mtu anayekosa ‘kujitiisha kwa mamlaka zilizo kubwa’ hawezi kutarajia kuungwa mkono na Mungu. Kwa nini? Kwa sababu “mamlaka zilizopo zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusu. Kwa hiyo yeye aipingaye mamlaka amechukua msimamo dhidi ya mpango wa Mungu.” (Waroma 13:1, 2) Hata hivyo, Yesu alitambua kwamba huenda mapendezi ya Kaisari yakatofautiana na ya Mungu aliposema: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:17) Wale wanaotaka kuungwa mkono na Mungu lazima ‘wafulize kutafuta kwanza ufalme wa Mungu na uadilifu wake,’ huku wakitii sheria za nchi zinazopatana na mamlaka ya Mungu iliyo kuu zaidi. (Mathayo 6:33; Matendo 5:29) Yesu alikazia msimamo wa kutokuwamo aliposema hivi kwa wanafunzi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” Baadaye aliongezea kusema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.”—Yohana 17:16; 18:36.

13. Upendo hutimiza fungu gani katika kuwatambua watu wa Mungu?

13 Hawana ubaguzi wanapofanya “lililo jema kuelekea wote.” (Wagalatia 6:10) Upendo wa Kikristo haubagui, unakubali watu wote bila kujali rangi ya ngozi yao, hali yao ya kiuchumi au kielimu, taifa, au lugha. Kufanya lililo jema kuelekea wote na hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zao husaidia kutambua wale wanaoungwa mkono na Mungu. Yesu alisema hivi: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.”—Yohana 13:35; Matendo 10:34, 35.

14. Je, ni lazima watu walio na kibali cha Mungu wakubaliwe na watu wote? Eleza.

14 Wako tayari kunyanyaswa kwa sababu ya kufanya mapenzi ya Mungu. Yesu aliwaonya kimbele wafuasi wake: “Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia; ikiwa wameshika neno langu, watashika lenu pia.” (Yohana 15:20; Mathayo 5:11, 12; 2 Timotheo 3:12) Wale wanaoungwa mkono na Mungu wamechukiwa sikuzote kama Noa, aliyeuhukumu ulimwengu kupitia imani yake. (Waebrania 11:7) Leo, wale wanaotaka kuungwa mkono na Mungu hawaridhiani kanuni za Mungu ili kuepuka mnyanyaso. Maadamu wanamtumikia Mungu kwa uaminifu wanajua kwamba watu ‘watatatanishwa na kuendelea kuwasema wao kwa maneno yenye kuudhi.’—1 Petro 2:12; 3:16; 4:4.

Wakati wa Kuchanganua Mambo ya Hakika

15, 16. (a) Ni maswali gani yatakayotusaidia kutambua dini inayoungwa mkono na Mungu? (b) Mamilioni ya watu wamefikia mkataa gani, na kwa nini?

15 Jiulize hivi, ‘Ni dini gani inayojulikana kwa kutii kabisa Neno la Mungu, hata wakati mafundisho yake yanapotofautiana na imani ya watu wengi? Ni nani wanaokazia umuhimu wa jina la kibinafsi la Mungu, hata kulitumia kujitambulisha wenyewe? Ni nani ambao hukazia kwa uhakika kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee kwa matatizo yote ya wanadamu? Ni nani wanaodumisha viwango vya Biblia kuhusu mwenendo bila kujali kwamba wataonwa kuwa watu wa kizamani? Ni kikundi gani kinachojulikana kwa kutokuwa na makasisi wanaolipwa, ambacho wafuasi wake wote ni wahubiri? Ni nani wanaosifiwa kuwa raia wanaotii sheria, ijapokuwa hawajihusishi katika siasa? Ni nani wanaotumia pesa na wakati wao kwa upendo ili kusaidia watu wengine wajifunze juu ya Mungu na makusudi yake? Na licha ya mambo hayo yote ya hakika, ni nani ambao bado hudharauliwa, hudhihakiwa, na kunyanyaswa?’

16 Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wamechanganua mambo hayo ya hakika na kusadiki kwamba Mashahidi wa Yehova peke yao ndio wanaofuata dini ya kweli. Wamefikia mkataa huo kwa kutegemea mambo ambayo Mashahidi wa Yehova hufundisha na jinsi wanavyojiendesha. Pia kwa sababu ya manufaa ambayo yametokana na dini yao. (Isaya 48:17) Kwa kweli, mamilioni ya watu wanasema hivi kama ilivyotabiriwa kwenye Zekaria 8:23: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”

17. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawana kimbelembele wasemapo kwamba dini yao ndiyo ya kweli?

17 Je, Mashahidi wa Yehova wana kimbelembele wasemapo kwamba ni wao tu wanaoungwa mkono na Mungu? Kwa kweli sivyo, dai lao ni sawa na la Waisraeli waliokuwa Misri ambao walidai kwamba wanaungwa mkono na Mungu licha ya imani ya Wamisri. Au ni sawa na la Wakristo wa karne ya kwanza wakati walipodai kuungwa mkono na Mungu na kusema kwamba wanadini Wayahudi hawakuungwa mkono na Mungu. Mambo ya hakika huthibitisha ukweli wa dai hilo. Katika nchi 235 Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi ambayo Yesu alitabiri ingefanywa na wafuasi wake wa kweli wakati wa mwisho: “Na habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

18, 19. (a) Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawapaswi kuacha kufanya kazi yao ya kuhubiri licha ya upinzani? (b) Zaburi 41:11 yathibitishaje uhakika wa kwamba Mashahidi wanaungwa mkono na Mungu?

18 Mashahidi wa Yehova wataendelea kufanya kazi hiyo, pasipo kuruhusu kamwe mnyanyaso au upinzani uzuie utendaji wao. Ni lazima kazi ya Yehova ifanywe na itafanywa. Kila jitihada ambayo imefanywa na wengine katika karne iliyopita kuzuia Mashahidi wasitimize kazi ya Mungu hatimaye imeambulia patupu, kwa kuwa Yehova aliahidi hivi: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa BWANA, na haki yao inayotoka kwangu mimi.”—Isaya 54:17.

19 Uhakika wa kwamba Mashahidi wa Yehova ni wenye nguvu na wenye bidii kuliko wakati mwingine wowote—licha ya upinzani kutoka ulimwenguni pote—huthibitisha kwamba Yehova anafurahia kazi wanayofanya. Mfalme Daudi alisema hivi: “Kwa neno hili nimejua ya kuwa wapendezwa nami, kwa kuwa adui wangu hasimangi kwa kunishinda.” (Zaburi 41:11; 56:9, 11) Maadui wa Mungu hawataweza kamwe kushangilia kwa sababu ya kuwashinda watu wa Yehova, kwa kuwa Kiongozi wao Yesu Kristo, anasonga mbele ili kupata ushindi kamili!

Je, Unaweza Kujibu?

• Kuna mifano gani ya watu wa kale walioungwa mkono na Mungu?

• Ni mambo gani yanayotambulisha dini ya kweli?

• Kwa nini unasadiki kwamba Mashahidi wa Yehova wanaungwa mkono na Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Lazima mafundisho ya wale wanaotaka kuungwa mkono na Mungu yategemee Neno lake pekee

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wazee Wakristo huwekea kundi kielelezo kizuri