Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imarisha Tumaini Lako Katika Yehova

Imarisha Tumaini Lako Katika Yehova

Imarisha Tumaini Lako Katika Yehova

Njama ya mauaji inapangwa. Maofisa wote wenye vyeo vikubwa nchini wamekutana pamoja na kukubaliana watunge sheria mpya. Wanataka mtu yeyote atakayejihusisha na ibada isiyokubaliwa na Serikali ahukumiwe kifo.

JE, UMEWAHI kusikia simulizi hilo? Katika historia kuna mifano mingi ya watu waliotunga madhara kwa njia ya sheria. Kisa kilicho juu kilitukia katika Milki ya Uajemi katika siku za nabii Danieli. Sheria hiyo, iliyotiwa sahihi na Mfalme Dario iliweka masharti haya: “Mtu ye yote atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme, atatupwa katika tundu la simba.”—Danieli 6:7-9.

Danieli angefanya nini chini ya tisho hilo la kifo? Je, angeendelea kumtumaini Mungu wake Yehova, au angeridhiana na kufanya vile mfalme alivyoamuru? Simulizi hilo latuambia hivi: “Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake; (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu), akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo.” (Danieli 6:10) Sehemu inayosalia ya simulizi hilo yajulikana vema. Danieli alitupwa katika tundu la simba kwa sababu ya imani yake, lakini Yehova ‘aliziba vinywa vya simba’ na kumwokoa mtumishi wake mwaminifu.—Waebrania 11:33; Danieli 6:16-22.

Wakati wa Kujichunguza

Leo, watumishi wa Yehova wanaishi katika ulimwengu wenye uhasama na wanakabili hali zinazohatarisha hali yao ya kimwili na ya kiroho. Kwa mfano, katika nchi fulani ambapo kumetokea chuki ya kijamii, Mashahidi wengi wameuawa. Kwingineko, watumishi wa Yehova wamekabili upungufu wa chakula, magumu ya kiuchumi, misiba ya asili, magonjwa mabaya, na hali nyingine zenye kutishia uhai. Isitoshe, wamelazimika kukabili mnyanyaso, mikazo kutoka kazini, na vishawishi mbalimbali vya kufanya mabaya, mambo ambayo yanaweza kuhatarisha hali yao ya kiroho. Kwa kweli, Mpinzani Mkuu, Shetani, ameazimia kuwaharibu watumishi wa Yehova kwa kutumia njia yoyote ile itakayofaulu.—1 Petro 5:8.

Tunaweza kufanya nini tunapokabiliwa na hali hizo? Ingawa ni jambo la kawaida kuogopa uhai wako unapohatarishwa, twaweza kukumbuka maneno yenye kutia-moyo ya mtume Paulo: “[Yehova] amesema: ‘Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.’ Ili kwamba tupate kuwa wenye moyo mkuu na kusema: ‘Yehova ni msaidiaji wangu; hakika sitaogopa. Mwanadamu aweza kunifanya nini?’” (Waebrania 13:5, 6) Twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova huhisi vivyo hivyo kuelekea watumishi wake leo. Hata hivyo, kujua ahadi za Yehova si sawa na kuwa na uhakikisho kwamba atatenda kwa niaba yetu. Kwa hiyo ni muhimu sana tuchunguze msingi wa kujenga tumaini katika Yehova na kuhakikisha kwamba tunafanya yote tuwezayo kuimarisha na kudumisha tumaini hilo. Tukifanya hivyo, “amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:7) Kisha majaribu yatokeapo, tutaweza kufikiri ifaavyo na kukabiliana nayo kwa hekima.

Msingi wa Kumtumaini Yehova

Bila shaka tuna sababu nyingi za kumtumaini Muumba wetu, Yehova. Sababu ya kwanza ni kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo anayewajali kikweli watumishi wake. Kuna mifano mingi sana katika Biblia inayoonyesha jinsi Yehova anavyowajali watumishi wake. Akieleza jinsi Yehova alivyowatendea Waisraeli, watu wake wateule, Musa aliandika hivi: “Alimkuta katika nchi ya ukame, na katika jangwa tupu litishalo; alimzunguka, akamtunza; akamhifadhi kama mboni ya jicho.” (Kumbukumbu la Torati 32:10) Katika nyakati za kisasa, Yehova anaendelea kuwajali watumishi wake, wakiwa kikundi na wakiwa mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, Mashahidi fulani walipokabili ukosefu mkubwa wa chakula wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe huko Bosnia, Yehova alihakikisha kwamba wamepokea msaada waliohitaji kupitia ndugu zao wajasiri kutoka Kroatia na Austria. Ndugu hao walihatarisha uhai wao kwa kusafiri na kupita katika maeneo hatari sana ili kuwapelekea ndugu zao msaada. *

Kwa kuwa Yehova Mungu ni Mweza Yote, bila shaka anaweza kuwalinda watumishi wake chini ya hali zozote zile. (Isaya 33:22; Ufunuo 4:8) Lakini hata wakati ambapo Yehova huruhusu baadhi ya watumishi wake wathibitishe uaminifu wao hadi kifo, bado huwategemeza na kuwasaidia wadumishe uaminifu-maadili wao, akiwawezesha wadumu wakiwa imara, wenye shangwe, na wenye utulivu hadi mwisho. Kwa hiyo, twaweza kuwa na uhakika kama mtunga-zaburi: “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari.”—Zaburi 46:1, 2.

Pia Biblia huonyesha kwamba Yehova ni Mungu anayesema kweli. Hiyo yamaanisha kwamba sikuzote yeye hutimiza ahadi zake. Kwa kweli, Biblia humtaja kuwa Mungu “asiyeweza kusema uwongo.” (Tito 1:2) Kwa kuwa Yehova amerudia kusema mara kadhaa juu ya utayari wake wa kulinda na kuokoa watumishi wake, twaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba mbali na kuwa ana uwezo, yuko tayari kutimiza ahadi zake pia.—Ayubu 42:2.

Njia za Kuimarisha Tumaini Letu

Ingawa tuna kila sababu ya kumtumaini Yehova, hatupaswi kuchukua jambo hilo kivivi hivi tu. Sababu ni kwamba kwa ujumla ulimwengu una imani ndogo katika Mungu, na mtazamo kama huo unaweza kudhoofisha tumaini letu katika Yehova. Kwa hiyo, tunahitaji kujitahidi vilivyo ili kuimarisha na kudumisha tumaini hilo. Yehova anafahamu jambo hilo, na ametuandalia njia za kudumisha tumaini letu.

Kwanza kabisa, ameandaa Neno lake lililoandikwa, Biblia, ambayo husimulia matendo mengi sana makubwa aliyofanya kwa niaba ya watumishi wake. Ebu fikiria, unaweza kumtumaini kadiri gani mtu unayemjua kwa jina tu? Labda hutamtumaini sana. Unahitaji kujua namna anavyofanya mambo na matendo yake ndiposa uweze kumtumaini, sivyo? Tusomapo na kutafakari masimulizi hayo ya Biblia, ujuzi wetu juu ya Yehova na njia zake za ajabu huongezeka, na tunapata kuthamini zaidi jinsi anavyotumainika. Hivyo tumaini letu katika Yehova huimarishwa. Mtunga-zaburi aliweka kielelezo kizuri aliposali hivi kwa Mungu kwa bidii: “Nitayakumbuka matendo ya BWANA; naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako.”—Zaburi 77:11, 12.

Mbali na Biblia, pia tuna chakula kingi cha kiroho katika vichapo vinavyotegemea Biblia ambavyo huchapishwa na tengenezo la Yehova. Kati ya mambo mengi yanayosimuliwa, mara nyingi vichapo hivyo vina masimulizi yenye kugusa moyo ya watumishi wa Mungu wa nyakati za kisasa. Masimulizi hayo huonyesha jinsi Yehova alivyowaandalia msaada walipokabili hali zenye kukatisha tamaa. Kwa mfano, Martin Poetzinger, ambaye baadaye alipata kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikuwa mgonjwa sana alipokuwa akitumikia akiwa painia katika maeneo fulani ya Ulaya mbali na nchi ya kwao. Hakuwa na pesa zozote, na hakuna daktari aliyetaka kumtibu. Lakini Yehova hakumwacha. Hatimaye daktari mkuu wa hospitali hiyo alitembelewa. Kwa kuwa aliamini Biblia kwa dhati, mwanamume huyo mwenye fadhili alimtunza Ndugu Poetzinger kama mwana wake, bila malipo yoyote. Bila shaka, kusoma masimulizi hayo ya kibinafsi kwaweza kuimarisha tumaini letu katika Baba yetu wa mbinguni.

Msaada mwingine wenye thamani sana ambao Yehova hutupa ili kuimarisha tumaini letu katika yeye ni pendeleo lenye thamani la sala. Mtume Paulo atuambia hivi kwa upendo: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu.” (Wafilipi 4:6) “Kila jambo” linaweza kutia ndani hisia zetu, mahitaji yetu, hofu zetu, na mahangaiko yetu. Kadiri tusalivyo mara nyingi na kutoka moyoni ndivyo tumaini letu katika Yehova litakavyoimarika.

Wakati Yesu Kristo alipokuwa duniani, nyakati fulani alienda mahali pasipokuwa na watu ili asali bila kusumbuliwa. (Mathayo 14:23; Marko 1:35) Kabla ya kufanya maamuzi makubwa, hata alisali kwa Baba yake usiku kucha. (Luka 6:12, 13) Haishangazi kwamba tumaini la Yesu katika Yehova lilikuwa lenye nguvu sana hivi kwamba aliweza kuvumilia jaribu kali zaidi ambalo halijawahi kumpata yeyote. Maneno yake ya mwisho akiwa kwenye mti wa mateso yalikuwa: “Baba, ndani ya mikono yako naikabidhi roho yangu.” Wonyesho huo wa uhakika ulithibitisha kwamba tumaini lake katika Baba yake halikufifia, hata ingawa Yehova hakuingilia kati ili kumwokoa.—Luka 23:46.

Njia nyingine ya kujenga tumaini katika Yehova ni kushirikiana kwa ukawaida na wale wanaomtumaini kwa moyo wote. Yehova aliwaamuru watu wake wakusanyike kwa ukawaida ili kujifunza mengi zaidi juu yake, na kutiana moyo. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Waebrania 10:24, 25) Ushirika wa aina hiyo uliimarisha tumaini lao katika Yehova na kuwawezesha wavumilie majaribu makali ya imani. Katika nchi moja ya Afrika ambapo kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku, Mashahidi wa Yehova walinyimwa ulinzi wa polisi, hati za kusafiria, vyeti vya ndoa, matibabu ya hospitali, na kazi. Vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipozuka katika eneo moja, washiriki 39 wa kutaniko jirani, kutia ndani watoto, waliishi chini ya daraja dogo jangwani. Walikaa huko kwa muda wa miezi mitano hivi, ili kukwepa mashambulizi ya mabomu katika mji wao. Chini ya hali hizo ngumu, walipata nguvu nyingi kwa kuzungumzia andiko la Biblia kila siku na kufanya mikutano mingine. Hivyo waliweza kuvumilia majaribu hayo na kudumisha hali nzuri ya kiroho. Bila shaka, jambo hilo lililoonwa laonyesha umuhimu wa kukutanika pamoja na watu wa Yehova.

Mwishowe, ili kuimarisha tumaini letu katika Yehova, twapaswa kuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kuwa tayari sikuzote kuwaeleza wengine habari njema. Jambo hilo ladhihirishwa na kisa chenye kugusa moyo cha mhubiri mchanga mwenye bidii huko Kanada aliyekuwa na ugonjwa usiotibika wa lukemia. Licha ya ugonjwa wake mbaya alitaka kuwa painia wa kawaida, yaani, mhudumu wa wakati wote. Alipopata nafuu kwa muda mfupi, alikuwa na nguvu za kutosha kutumikia akiwa painia-msaidizi kwa mwezi mmoja. Kisha hali yake ikazorota, akafa miezi michache baadaye. Hata hivyo, alidumu akiwa mwenye nguvu kiroho hadi mwisho, tumaini lake katika Yehova halikuyumba-yumba hata kidogo. Mamake akumbuka hivi: “Hadi kifo chake, aliwahangaikia wengine zaidi kuliko alivyojihangaikia. Aliwatia moyo wajifunze Biblia, na kuwaambia, ‘Tutakuwa pamoja katika Paradiso.’”

Kuthibitisha Tumaini Letu Katika Yehova

“Kama vile mwili bila roho umekufa, ndivyo pia imani bila kuwa na kazi imekufa.” (Yakobo 2:26) Mambo aliyosema Yakobo kuhusu imani katika Mungu yanaweza kuhusu pia tumaini letu katika Yehova. Hata tuseme twamtumaini Mungu kadiri gani, ni bure tusipodhihirisha tumaini hilo kwa matendo. Abrahamu alimtumaini Yehova kabisa na kuthibitisha tumaini hilo kwa kutii amri zake bila kusitasita, hata akawa tayari kumdhabihu Isaka, mwana wake. Kwa sababu ya tumaini na utii huo wenye kutokeza, Abrahamu akawa rafiki ya Yehova.—Waebrania 11:8-10, 17-19; Yakobo 2:23.

Si lazima tungoje hadi tupatwe na jaribu kali ndipo tuonyeshe tumaini letu katika Yehova. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni asiye mwaminifu katika lililo kubwa pia.” (Luka 16:10) Twapaswa kujifunza kumtumaini Yehova katika shughuli zetu za kila siku na kumtii hata katika mambo yanayoonekana kuwa madogo. Tunapoona manufaa yanayotokana na utii huo,tumaini letu katika Baba yetu wa kimbingu huimarishwa, na tutaweza kukabiliana na majaribu makubwa au magumu zaidi.

Ulimwengu unapoelekea mwisho wenye msiba, watu wa Yehova watazidi kupatwa na majaribu. (Matendo 14:22; 2 Timotheo 3:12) Kwa kusitawisha tumaini imara na kamili katika Yehova sasa, tunaweza kutarajia kuokoka na kuingia katika ulimwengu wake mpya—ama kwa kupita dhiki kubwa tukiwa hai au kwa kufufuliwa. (2 Petro 3:13) Na tusiruhusu kamwe ukosefu wa tumaini uharibu uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Yehova. Kisha, itaweza kusemwa juu yetu kama ilivyosemwa kuhusu Danieli baada ya kuokolewa kutoka kwenye tundu la simba: “Dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake.”—Danieli 6:23.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kwa habari kamili ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1994, ukurasa wa 23-27.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kusoma masimulizi ya watumishi waaminifu wa Yehova, kama vile Martin Poetzinger, huimarisha imani