Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Funzo la Biblia Linakufaa?

Je, Funzo la Biblia Linakufaa?

Je, Funzo la Biblia Linakufaa?

“HAIPASI kusomwa pasipo uongozi wa kasisi.” Tahadhari hii iko kwenye ukurasa wa kwanza wa baadhi ya Biblia za Wakatoliki. Kay Murdy wa Taasisi ya Biblia ya Katoliki huko Los Angeles anasema kwamba ‘Sisi Wakatoliki hatukusoma Biblia mbeleni, lakini hali hiyo inabadilika.’ Anaeleza kwamba Wakatoliki wanapotambua matokeo mazuri ambayo Maandiko Matakatifu yanaweza kuleta maishani mwao “wanasitawisha hamu yao wenyewe ya kusoma Biblia.”

Akirejezea badiliko hilo, msimamizi wa elimu ya kidini aliyenukuliwa katika Gazeti la U.S. Catholic alisema kwamba Wakatoliki waliojiunga na madarasa ya funzo la Biblia walihisi kwamba “wamenyimwa mambo mengi mazuri wanayoweza kujifunza katika Biblia, na sasa wanataka kuyapata.”

Kwa vyovyote vile, ni “mambo mengi mazuri” yapi ambayo mwanafunzi wa Biblia anaweza kujifunza? Hebu fikiri: Je, ungependa kujua jinsi ya kukabiliana na mahangaiko ya kila siku? Unawezaje kudumisha amani katika jamaa? Kwa nini watu wengi hutenda bila adabu? Kwa nini vijana wa siku hizi ni wenye vurugu sana? Majibu yenye kuaminika kwa maswali hayo na mengineyo yanapatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Na majibu hayo ni “mambo mengi mazuri,” kwelikweli, si kwa Wakatoliki wala Waprotestanti tu, bali pia kwa Wabudha, Wahindu, Waislamu, Washinto, na hata kwa wale wasioamini kwamba kuna Mungu na wale ambao wanadhani kwamba haiwezekani kuthibitisha kwamba kuna Mungu. Mtunga-zaburi alisema, ‘Neno la Mungu lilikuwa taa ya miguu yake, na mwanga wa njia yake.’ Linaweza kukuongoza wewe vilevile.—Zaburi 119:105.