Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusonga Mbele Hadi Ushindi Kamili!

Kusonga Mbele Hadi Ushindi Kamili!

Kusonga Mbele Hadi Ushindi Kamili!

“Tazama! farasi mweupe; na yeye aketiye juu yake alikuwa na upinde; naye akapewa taji, naye akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.”—UFUNUO 6:2.

1. Yohana aliona matukio gani ya wakati ujao katika maono?

KWA kupuliziwa na Mungu, mtume Yohana aliona kimbele na kueleza kutawazwa kwa Kristo kuwa Mfalme miaka 1,800 mapema. Yohana alihitaji imani ili kuamini mambo aliyoona katika maono. Sisi leo tuna uthibitisho ulio wazi kwamba kutawazwa huko kulikotabiriwa kulitokea mwaka wa 1914. Kwa macho ya imani twamwona Yesu Kristo akienda na ‘kushinda na kukamilisha ushindi wake.’

2. Shetani alitendaje Ufalme uliposimamishwa, na jambo hilo lathibitisha nini?

2 Baada ya Ufalme kusimamishwa, Shetani alifukuzwa kutoka mbinguni na kuanzisha vita kali sana kwa sababu ya hasira nyingi, lakini hatafanikiwa hata kidogo. (Ufunuo 12:7-12) Hasira yake imefanya hali ulimwenguni ziwe mbaya hata zaidi. Ustaarabu wa jamii ya kibinadamu unazorota. Kwa Mashahidi wa Yehova huo ni uthibitisho wazi kwamba Mfalme wao anasonga mbele ‘akakamilishe ushindi wake.’

Jamii ya Ulimwengu Mpya Yaanzishwa

3, 4. (a) Ni marekebisho gani ya kitengenezo ambayo yamefanywa katika kutaniko la Kikristo tangu Ufalme usimamishwe, na kwa nini ilikuwa lazima yafanywe? (b) Marekebisho hayo yameleta manufaa gani kama ilivyotabiriwa na Isaya?

3 Ufalme uliposimamishwa, wakati uliwadia wa kupatanisha kutaniko la Kikristo lililoanzishwa upya—ambalo sasa lilikuwa na madaraka zaidi ya Ufalme—na kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Hivyo, matoleo ya Mnara wa Mlinzi ya Juni 1 na 15, 1938 yalichanganua jinsi tengenezo la Kikristo linavyopaswa kutenda. Baadaye, toleo la Desemba 15, 1971, lilifafanua zaidi Baraza Linaloongoza la kisasa katika makala yenye kichwa “Jinsi Baraza Linaloongoza Linavyotofautiana na Shirika la Kisheria” (“A Governing Body as Different From a Legal Corporation”). Mnamo mwaka wa 1972, mabaraza ya wazee yaliwekwa rasmi ili kuandaa msaada na mwelekezo kwa ajili ya makutaniko.

4 Kutaniko la Kikristo liliimarishwa sana baada ya kurudishwa kwa usimamizi unaofaa. Kutaniko pia liliimarishwa na mipango iliyofanywa na Baraza Linaloongoza kuwafundisha wazee madaraka yao, kutia ndani kuwazoeza katika mambo ya kihukumu. Marekebisho ya hatua kwa hatua katika tengenezo la Mungu la kidunia na matokeo yake mazuri yalitabiriwa katika Isaya 60:17: “Badala ya shaba nitaleta dhahabu, na badala; ya chuma nitaleta fedha, na badala ya mti, shaba, na badala ya mawe, chuma; tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.” Marekebisho hayo yalidhihirisha baraka za Mungu na kibali chake kwa wale waliojitoa kuunga mkono Ufalme wake kwa bidii.

5. (a) Shetani alitendaje Yehova alipowabariki watu Wake? (b) Kupatana na Wafilipi 1:7, watu wa Yehova wametendaje kuhusiana na hasira ya Shetani?

5 Shetani alitambua mwongozo na uangalifu wenye upendo ambao Mungu aliwapa watu wake baada ya kusimamishwa kwa Ufalme. Kwa mfano, katika mwaka wa 1931, kikundi hiki kidogo cha Wakristo walitangaza hadharani kwamba hawakuwa Wanafunzi wa Biblia tu. Kupatana na Isaya 43:10, walikuwa Mashahidi wa Yehova! Iwe jambo hilo lilitukia kwa mpango au la, Ibilisi alianzisha mnyanyaso usio na kifani ulimwenguni pote. Hata katika nchi zinazojulikana kuwa na uhuru wa ibada, kama vile Marekani, Kanada, na Ujerumani, Mashahidi walilazimika kuchukua hatua za kisheria mara kwa mara ili kutetea uhuru wao wa ibada. Kufikia mwaka wa 1988, Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani ilikuwa imechunguza kesi zipatazo 71 zilizohusu Mashahidi wa Yehova, nao wakashinda thuluthi mbili ya kesi hizo. Leo, hatua za kisheria zinaendelea kuchukuliwa ulimwenguni pote na kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, kumekuwa na “kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema.”—Wafilipi 1:7.

6. Je, marufuku na vizuizi vilizuia watu wa Yehova wasisonge mbele? Toa mfano.

6 Katika miaka ya 1930, kabla ya Vita ya Pili ya Ulimwengu, serikali za kidikteta zilipiga marufuku au kuzuia kazi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani, Hispania, na Japani. Lakini katika mwaka wa 2000, nchi hizi tatu peke yake zilikuwa na watangazaji wenye bidii wa Ufalme wa Mungu wapatao 500,000. Idadi hiyo ilikuwa karibu mara kumi ya idadi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote katika mwaka wa 1936! Ni wazi kwamba marufuku na vizuizi haviwezi kuzuia watu wa Yehova kusonga mbele chini ya Kiongozi wao mshindi, Yesu Kristo.

7. Ni jambo gani lenye kutokeza lililotukia mwaka wa 1958, na kumekuwa na badiliko gani kubwa tangu wakati huo?

7 Kusonga mbele huko kulidhihirishwa kwa njia kubwa katika mwaka wa 1958, wakati wa mkusanyiko mkubwa zaidi uliopata kufanywa na Mashahidi wa Yehova. Mkusanyiko huo wa Kimataifa wenye kichwa, Mapenzi ya Mungu, ulifanywa huko New York City na kuhudhuriwa na watu 253,922. Kufikia mwaka wa 1970 kazi yao ilikuwa inafanywa katika nchi tatu zilizotajwa juu, bila kutia ndani nchi iliyokuwa Ujerumani Mashariki. Lakini Mashahidi bado walikuwa chini ya marufuku katika nchi kubwa sana ya Muungano wa Sovieti na nchi zilizoiunga mkono ambazo zilikuwa wanachama wa Mkataba wa Warsaw. Leo, katika nchi hizo zilizokuwa za Kikomunisti, kuna Mashahidi watendaji zaidi ya nusu milioni.

8. Baraka za Yehova zimewanufaishaje watu wake, na gazeti Mnara wa Mlinzi la 1950 lilisema nini kuhusu jambo hilo?

8 Mashahidi wa Yehova wamebarikiwa kupata ongezeko kwa sababu wameendelea ‘kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wa Mungu.’ (Mathayo 6:33) Tayari unabii wa Isaya umetimizwa kwa njia halisi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Na ongezeko linaendelea. Katika mwongo uliopita peke yake, idadi ya wateteaji wenye bidii wa Ufalme iliongezeka kwa watu zaidi ya 1,750,000. Kwa hiari watu hao wamekuwa sehemu ya kikundi ambacho gazeti Mnara wa Mlinzi la 1950 lilisema hivi kukihusu: “Sasa Mungu anaandaa jamii ya ulimwengu mpya. . . . Kikundi hiki kitaokoka Har-Magedoni, . . . kikiwa cha kwanza kuingia katika ‘dunia mpya’ . . . , iliyopangwa kitheokrasi, na kinachofahamu utaratibu wa kitengenezo.” Makala hiyo ilimalizia kwa kusema hivi: “Kwa hiyo, acheni sisi sote kwa pamoja, tusonge mbele hatua kwa hatua tukiwa jamii ya ulimwengu mpya!”

9. Mashahidi wa Yehova wamenufaikaje na mambo ambayo wamejifunza kwa miaka mingi?

9 Kufikia sasa, jamii ya ulimwengu mpya inayoongezeka daima imejipatia ujuzi ambao umekuwa wenye thamani sana leo na ambao huenda hata ukatumika katika kazi itakayofanywa baada ya Har-Magedoni. Kwa mfano, Mashahidi wamejifunza kupanga mikusanyiko mikubwa, kutoa misaada ya dharura, na kujenga majengo haraka. Utendaji huo umefanya watu wengi wawathamini na kuwastahi Mashahidi wa Yehova.

Kusahihisha Maoni Yenye Makosa

10, 11. Eleza jinsi maoni mabaya kuhusu Mashahidi wa Yehova yalivyosahihishwa.

10 Hata hivyo, kuna watu wanaowashutumu Mashahidi wa Yehova kuwa tofauti na jamii ya kibinadamu. Wanakuwa hivyo kwa sababu hasa ya msimamo wao unaotegemea Biblia kuhusiana na masuala kama vile kutiwa damu mishipani, kutokuwamo, kuvuta sigareti, na maadili. Lakini umma unazidi kukiri kwamba maoni ya Mashahidi yapasa kufikiriwa. Kwa mfano, daktari mmoja nchini Poland alipiga simu kwenye ofisi ya usimamizi ya Mashahidi wa Yehova na kusema kwamba yeye pamoja na wafanyakazi wenzake hospitalini walikuwa wakijadiliana kwa saa kadhaa kuhusu suala la kutiwa damu mishipani. Mazungumzo hayo yalianza kwa sababu ya habari iliyochapishwa katika gazeti la kila siku la Poland Dziennik Zachodni. “Mimi binafsi nasikitika kwamba damu inatumiwa kupita kiasi kwa ajili ya matibabu,” akakiri daktari huyo. “Lazima zoea hilo liachwe, na ninafurahi kwamba mtu fulani ameanzisha mazungumzo kuhusu jambo hilo. Ningependa habari zaidi.”

11 Kwenye mkutano uliofanywa mwaka jana, wataalamu wa mambo ya kitiba kutoka Israel, Kanada, Marekani, na Ulaya walizungumzia habari iliyokusudiwa kusaidia madaktari kutibu wagonjwa pasipo kutumia damu. Kwenye mkutano huo uliofanywa nchini Uswisi, ilisemekana kwamba tofauti na vile wengi wanavyoamini, idadi ya wagonjwa wanaokufa kwa kutiwa damu inazidi idadi ya wagonjwa ambao hawakutiwa damu. Kwa kawaida wagonjwa ambao ni Mashahidi hukaa hospitalini siku chache kuliko wagonjwa waliotiwa damu, na kwa sababu hiyo gharama ya matibabu ya Mashahidi huwa ndogo.

12. Toa mfano kuhusu jinsi ambavyo watu fulani mashuhuri wamesifu msimamo uliochukuliwa na Mashahidi wa Yehova kuhusu kutokuwamo katika mambo ya kisiasa.

12 Pia maelezo mengi mazuri yametolewa kuhusu msimamo wa kutokuwamo ambao Mashahidi wa Yehova walichukua kabla na baada ya Vita ya Pili ya Ulimwengu waliponyanyaswa vikali na Wanazi. Video Jehovah’s Witnesses Stand Firm Against Nazi Assault, iliyotayarishwa na Mashahidi wa Yehova na kuonyeshwa mara ya kwanza kwenye kambi ya mateso ya Ravensbrück, Ujerumani, Novemba 6, 1996, imesifiwa sana. Kwenye sherehe za kufungua maonyesho ya video hiyo katika kambi ya mateso yenye sifa mbaya ya Bergen-Belsen, katika Aprili 18, 1998, mkurugenzi wa Kituo cha Elimu ya Kisiasa huko Lower Saxony, Dakt. Wolfgang Scheel, alikiri hivi: “Mojawapo ya mambo ya kweli yenye kushtua zaidi katika historia ni kwamba makanisa ya Kikristo hayakupinga katakata harakati za Usoshalisti wa Kitaifa kama walivyofanya Mashahidi. . . . Hata tuwe na maoni gani kuhusu mafundisho na bidii ya kidini ya Mashahidi wa Yehova, uimara wao wakati wa utawala wa Nazi unafanya wastahili kuheshimiwa.”

13, 14. (a) Ni maoni gani yenye busara kuhusu Wakristo wa mapema yaliyotolewa na mtu ambaye hakutarajiwa kufanya hivyo? (b) Toa mifano ya maelezo mazuri yaliyotolewa kuhusu watu wa Mungu leo.

13 Watu mashuhuri au mahakama zinapowaunga mkono Mashahidi wa Yehova kuhusu masuala yenye kubishaniwa, huenda hali hiyo ikapunguza ubaguzi na kufanya watu wawe na maoni yanayofaa kuelekea Mashahidi. Mara nyingi hilo huwapa Mashahidi fursa ya kuzungumza na watu ambao hapo awali hawakutaka kuwasikiliza. Kwa hiyo hatua hizo zinapendeza, na Mashahidi wa Yehova huzithamini kwelikweli. Hilo latukumbusha jambo lililotukia huko Yerusalemu katika karne ya kwanza. Wakati Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi, ilipotaka kuwaua Wakristo kwa sababu ya bidii yao ya kuhubiri, Gamalieli, “mwalimu wa sheria mwenye kustahiwa na watu wote,” alitoa onyo na kusema: “Wanaume wa Israeli, jiangalieni nyinyi wenyewe kuhusu lile mkusudialo kufanya kwa habari ya watu hawa. . . . Msijiingize katika mambo ya watu hawa, bali waacheni; (kwa sababu, ikiwa mpango huu au kazi hii ni kutoka kwa wanadamu, itapinduliwa; lakini ikiwa ni kutoka kwa Mungu, hamtaweza kuwapindua;) ama sivyo, huenda mkaonwa kuwa wapiganaji dhidi ya Mungu kwa kweli.”—Matendo 5:33-39.

14 Kama vile Gamalieli, hivi karibuni watu fulani mashuhuri wamesema kwa ujasiri kwamba Mashahidi wa Yehova wapewe uhuru wa kidini. Kwa mfano, aliyekuwa mwenyekiti wa Chuo cha Kimataifa cha Uhuru wa Kidini na Imani alisema hivi: “Dini haipasi kunyimwa haki zake kwa sababu tu imani yake inaonwa na jamii kuwa isiyokubalika au isiyo ya kawaida.” Na profesa mmoja anayechunguza masuala ya kidini kwenye chuo kikuu cha Leipzig aliuliza swali muhimu kuhusu tume fulani iliyoanzishwa na serikali ya Ujerumani kuchunguza yale yanayoitwa madhehebu. Aliuliza hivi: “Kwa nini dini ndogo-ndogo tu ndizo zinazopasa kuchunguzwa wala si makanisa mawili makubwa [Kanisa Katoliki na Kanisa la Kilutheri]?” Twaweza kupata jibu kwa urahisi kutokana na maneno ya aliyekuwa ofisa wa Ujerumani, ambaye aliandika hivi: “Bila shaka, waumini wenye msimamo mkali walifanya mambo kichinichini na hivyo kuchangia msimamo wa kisiasa uliochukuliwa na tume ya serikali.”

Tunatafuta Kitulizo Kutoka kwa Nani?

15, 16. (a) Kwa nini hatua ya Gamalieli ilikuwa na matokeo ya muda tu? (b) Kwa nini wale watu watatu mashuhuri hawangeweza kufanya mengi kwa ajili ya Yesu?

15 Mambo aliyosema Gamalieli yakazia tu uhakika wa kwamba kazi inayoungwa mkono na Mungu haiwezi kushindwa. Bila shaka, Wakristo wa mapema walinufaika kwa maneno ambayo Gamalieli aliambia Sanhedrini, lakini hawakusahau kwamba maneno ya Yesu kwamba wafuasi wake wangenyanyaswa yalikuwa ya kweli. Hatua ya Gamalieli ilizuia viongozi wa kidini wasiwaue wanafunzi wa Yesu, lakini haikumaliza mnyanyaso kabisa, kwa kuwa twasoma: “Ndipo wakamsikiliza, nao wakawaita mitume, wakawapiga viboko, na kuwaagiza wakome kusema juu ya msingi wa jina la Yesu, na kuwaacha waende zao.”—Matendo 5:40.

16 Yesu alipokuwa akihukumiwa, Pontio Pilato, alijaribu kumwachilia kwa sababu hakumpata na kosa lolote. Lakini hakufaulu. (Yohana 18:38, 39; 19:4, 6, 12-16) Hata washiriki wawili wa Sanhedrini, Nikodemo na Yosefu wa Arimathea, waliomwunga Yesu mkono, hawangeweza kufanya mengi ili kuzuia mahakama isimchukulie Yesu hatua. (Luka 23:50-52; Yohana 7:45-52; 19:38-40) Kitulizo ambacho hupatikana wakati wanadamu wanapowatetea watu wa Yehova—kwa sababu yoyote ile—huwa cha muda tu. Ulimwengu utaendelea kuchukia wafuasi wa kweli wa Kristo, kama ulivyomchukia. Kitulizo kamili kinaweza kutoka kwa Yehova pekee.—Matendo 2:24.

17. Mashahidi wa Yehova wana maoni gani halisi, lakini kwa nini azimio lao la kuendelea kuhubiri habari njema halidhoofishwi?

17 Kwa sababu ya kuona mambo kihalisi, Mashahidi wa Yehova hutarajia mnyanyaso uendelee. Mnyanyaso utakoma tu wakati mfumo wa Shetani utakaposhindwa kikamili. Hata hivyo, japo mnyanyaso huo haupendezi, hauwazuii Mashahidi kutimiza utume wao wa kuhubiri Ufalme. Kwa nini uwazuie ilhali wanaungwa mkono na Mungu? Wanamtegemea Kiongozi wao mjasiri, Yesu Kristo, ambaye ni kielelezo kinachofaa.—Matendo 5:17-21, 27-32.

18. Ni jambo gani gumu ambalo watu wa Yehova bado watakabili, lakini wana hakika matokeo yatakuwaje?

18 Dini ya kweli imekuwa ikikabili upinzani mkali tangu mwanzo. Hivi karibuni, Gogu ambaye ni Shetani aliyetwezwa tangu afukuzwe kutoka mbinguni, atafanya shambulizi la kufa na kupona dhidi ya dini hiyo. Lakini dini ya kweli itaokoka. (Ezekieli 38:14-16) “Wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wakiongozwa na Shetani, “watapigana na Mwana-Kondoo, lakini, kwa sababu yeye ni Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme, Mwana-Kondoo atawashinda.” (Ufunuo 16:14; 17:14) Naam, Mfalme wetu anasonga mbele hadi ushindi kamili na hivi karibuni ‘atakamilisha ushindi wake.’ Ni pendeleo lililoje kusonga mbele pamoja naye, tukijua kwamba hivi karibuni hakuna mtu atakayewapinga waabudu wa Yehova wanaposema: “Mungu yuko upande wetu”!—Waroma 8:31; Wafilipi 1:27, 28.

Je, Unaweza Kueleza?

• Yehova amefanya nini ili kuimarisha kutaniko la Kikristo tangu Ufalme usimamishwe?

• Shetani amefanya nini kujaribu kuzuia Kristo asikamilishe ushindi wake, na matokeo yamekuwaje?

• Twapaswa kuwa na maoni gani yaliyosawazika kuhusu hatua nzuri iliyochukuliwa na watu ambao si Mashahidi?

• Hivi karibuni Shetani atafanya nini, na matokeo yatakuwaje?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mikusanyiko hudhihirisha kwamba watu wa Yehova wanasonga mbele

[Picha katika ukurasa wa 20]

Msimamo wa Mashahidi wa kutokuwamo wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu ungali unamletea Yehova sifa