Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahitaji Yake ya Kiroho Yalitoshelezwa

Mahitaji Yake ya Kiroho Yalitoshelezwa

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

Mahitaji Yake ya Kiroho Yalitoshelezwa

KISIWA cha Cyprus kiko sehemu ya kaskazini-mashariki mwa Bahari ya Mediterania. Katika siku za Biblia, kisiwa cha Cyprus kilijulikana kwa sababu ya shaba na mbao zake nzuri. Paulo na Barnaba walitangaza habari njema ya Ufalme huko katika safari yao ya kwanza ya mishonari. (Matendo 13:4-12) Leo, habari njema ina matokeo mazuri katika maisha ya watu wengi wa Cyprus, kutia ndani Lucas mwanamume aliye katika miaka yake ya 40. Yeye anasema hivi:

“Wazazi wangu walikuwa wafugaji wa ng’ombe na walikuwa na watoto saba. Tangu utotoni nilikuwa na hamu ya kusoma. Nilipenda sana kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, mimi na rafiki kadhaa tulianzisha kikundi cha kujifunza Biblia. Hata hivyo, kikundi hicho hakikuendelea kwa muda mrefu kwa kuwa wazee fulani kijijini walituita waasi-imani.

“Baadaye, nilipokuwa shuleni huko Marekani nilikutana na wafuasi wa dini mbalimbali. Jambo hilo liliamsha upya tamaa yangu ya mambo ya kiroho. Nilitumia siku nyingi kujifunza kuhusu dini mbalimbali katika maktaba ya chuo kikuu. Nilikwenda vilevile kwenye makanisa kadhaa, lakini ijapokuwa jitihada zangu zote, sikutoshelezwa kiroho.

“Baada ya kumaliza masomo yangu nilirudi Cyprus na kupata kazi kama mkurugenzi wa maabara ya kitiba. Mwanamume mzee aitwaye Antonis, aliyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alinitembelea kazini kwa ukawaida. Hata hivyo, makasisi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki walipata kujua juu ya ziara zake.

“Punde, mwanatheolojia alikuja kunitembelea, akanikatisha tamaa nisiendelee kuongea na Mashahidi wa Yehova. Nilikuwa nimefundishwa tangu utotoni kwamba Kanisa Othodoksi la Ugiriki ni kanisa la kweli, kwa hiyo niliacha mazungumzo pamoja na Antonis, na kuanza mazungumzo juu ya Biblia pamoja na yule mwanatheolojia. Nilitembelea pia makao mengi ya watawa huku Cyprus. Hata nilisafiri hadi sehemu ya kaskazini mwa Ugiriki kutembelea Mlima Athos, ambao ni mlima mtakatifu sana kwa Wakristo Waothodoksi. Hata hivyo, maswali yangu ya Biblia hayakujibiwa.

“Kisha nikaomba Mungu anisaidie kujua kweli. Muda mfupi baadaye Antonis alikuja tena kunitembelea kazini, nikaona kwamba sala yangu imejibiwa. Kwa hiyo niliacha kumtembelea yule mwanatheolojia na kuanza kujifunza Biblia pamoja na Antonis. Nikafanya maendeleo, na katika mwezi wa Oktoba 1997 nikaonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova kupitia ubatizo wa maji.

“Mke wangu na binti zetu wa kwanza na wa pili, wenye umri wa miaka 14 na 10, walinipinga mwanzoni. Lakini mke wangu alipoona mwenendo wangu bora aliamua kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Alivutiwa sana na urafiki wa Mashahidi na jinsi walivyopendezwa naye binafsi. Hasa alivutiwa kuona jinsi walivyotumia Biblia. Kwa hiyo, mke wangu na binti zetu wawili walikubali kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Wazia furaha yangu wakati wote watatu walipobatizwa kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa “Neno la Mungu la Kiunabii” katika mwaka wa 1999!

“Naam, jitihada yangu ya kutafuta kweli ilifanikiwa. Sasa, mimi, mke wangu na watoto wetu wote wanne, tumeungana katika ibada safi ya Yehova.”