Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa kuwa Yehova yuko tayari kusamehe dhambi kwa sababu ya manufaa ya dhabihu ya fidia, kwa nini ni lazima Wakristo waungame kwa wazee katika kutaniko?

Kama tuonavyo katika kisa cha Daudi na Bath-sheba, Yehova alimsamehe Daudi dhambi zake japo zilikuwa nzito, kwa sababu Daudi alionyesha toba ya kweli. Nathani alipozungumza naye, Daudi alikiri hivi waziwazi: “Nimemfanyia BWANA dhambi.”—2 Samweli 12:13.

Hata hivyo, mbali na kukubali ungamo la kweli la mtenda-dhambi na kumsamehe, Yehova hutoa maandalizi ya upendo ili kumsaidia mkosaji afanye maendeleo na kurudia hali nzuri ya kiroho. Katika kisa cha Daudi, msaada ulitolewa kupitia nabii Nathani. Leo, katika kutaniko la Kikristo, kuna wazee wakomavu kiroho. Mtume Yakobo aeleza hivi: “Je, kuna yeyote mgonjwa [kiroho] miongoni mwenu? Acheni awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, na acheni wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamfanya huyo asiyejisikia vizuri apone, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”—Yakobo 5:14, 15.

Wazee wenye uzoefu wanaweza kusaidia sana kupunguza huzuni ya moyoni ambayo humpata mkosaji mwenye kutubu. Wao hujitahidi kumwiga Yehova wanaposhughulika na mkosaji. Hawawi wakali kamwe hata ingawa huenda nidhamu kali ikahitajiwa. Badala yake, wao hufikiria mahitaji ya mtu huyo kwa huruma. Wao hujitahidi kwa subira kurekebisha kufikiri kwa mkosaji wakitumia Neno la Mungu. (Wagalatia 6:1) Hata mtu asipotaka kuungama dhambi zake, huenda akachochewa atubu wazee wanapozungumza naye, kama vile Daudi alivyofanya alipozungumziwa na Nathani. Kwa hiyo utegemezo unaotolewa na wazee humsaidia mkosaji aepuke hatari ya kurudia dhambi na kupatwa na matokeo mabaya ya kuwa mtenda-dhambi aliye sugu.—Waebrania 10:26-31.

Bila shaka si rahisi kuungama kwa wengine dhambi zenye kuaibisha na pia kutafuta msamaha. Unahitaji ujasiri. Hata hivyo, fikiria jinsi mambo yanavyoweza kuwa usipofanya hivyo. Mtu mmoja ambaye alishindwa kufunulia wazee wa kutaniko dhambi yake nzito alisema hivi: “Nilihisi maumivu moyoni ambayo hayakuisha. Nilijitahidi kuhubiri zaidi, lakini maumivu hayo hayakuisha.” Alifikiri kwamba ilitosha kuungama dhambi kwa Mungu kupitia sala, lakini bila shaka hiyo haikutosha, kwa kuwa alihisi kama Mfalme Daudi. (Zaburi 51:8, 11) Ni afadhali kama nini kukubali msaada wenye upendo unaotolewa na Yehova kupitia wazee!