Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ungamo Liletalo Ponyo la Kiroho

Ungamo Liletalo Ponyo la Kiroho

Ungamo Liletalo Ponyo la Kiroho

“NILIPONYAMAZA mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana kutwa. Kwa maana mchana na usiku mkono wako ulinilemea. Jasho langu likakauka hata nikawa kama nchi kavu wakati wa kaskazi.” (Zaburi 32:3, 4) Huenda maneno hayo yenye kugusa moyo yalionyesha maumivu ya kihisia aliyokuwa nayo Mfalme Daudi wa Israeli la kale, maumivu ambayo alijiletea mwenyewe kwa kuficha dhambi nzito badala ya kuiungama.

Daudi alikuwa na uwezo mbalimbali wenye kutokeza. Alikuwa mpiganaji jasiri, kiongozi stadi, mshairi, na mwanamuziki. Hata hivyo, yeye alimtegemea Mungu badala ya kutegemea uwezo wake mbalimbali. (1 Samweli 17:45, 46) Alitajwa kuwa mtu ambaye moyo wake ulikuwa “mkamilifu kwa BWANA.” (1 Wafalme 11:4) Lakini alifanya dhambi moja ambayo hasa ilistahili adhabu, na huenda aliitaja kwenye Zaburi 32. Tunaweza kujifunza mengi kwa kuchunguza hali zilizofanya Daudi atende dhambi hiyo. Tutatambua mitego ya kuepuka na pia uhitaji wa kuungama dhambi zetu ili turekebishe uhusiano wetu na Mungu.

Mfalme Mwaminifu-Mshikamanifu Afanya Dhambi

Taifa la Israeli lilikuwa linapigana na Waamoni, lakini Daudi alikuwa Yerusalemu. Jioni moja alipokuwa akitembea-tembea kwenye paa ya jumba lake la kifalme, aliona mwanamke mrembo akioga kwenye nyumba iliyokuwa karibu. Alishindwa kujidhibiti na badala yake akaanza kumtamani sana. Alipojua kwamba mwanamke huyo alikuwa Bath-sheba, mke wa Uria ambaye alikuwa askari katika jeshi lake, Daudi aliagizwa aletwe kwake kisha akafanya uzinzi naye. Baada ya muda, Bath-sheba alimjulisha Daudi kwamba alikuwa na mimba.—2 Samweli 11:1-5.

Daudi alikuwa amenaswa. Iwapo dhambi yao ingefunuliwa, wote wawili wangepata adhabu ya kifo. (Mambo ya Walawi 20:10) Hivyo akapanga njama. Alimwita Uria, mume wa Bath-sheba, arudi kutoka vitani. Baada ya kumhoji kwa muda kuhusu vita, Daudi alimwagiza Uria arudi nyumbani kwake. Daudi alitumaini kwamba jambo hilo lingefanya ionekane kwamba Uria ndiye aliyekuwa baba wa mtoto wa Bath-sheba.—2 Samweli 11:6-9.

Daudi alihuzunika sana Uria alipokataa kumtembelea mke wake. Uria alisema kwamba haingewezekana arudi nyumbani huku jeshi likiendelea kukabiliana na hali ngumu vitani. Wakati jeshi la Waisraeli lilipokuwa vitani, wanaume waliepuka kufanya ngono, hata na wake zao. Iliwapasa wadumu wakiwa safi kidesturi. (1 Samweli 21:5) Ndipo Daudi akamwalika Uria kwa chakula na kumlewesha, lakini bado akakataa kumtembelea mke wake. Kwa mwenendo wake mwaminifu, Uria alishutumu dhambi nzito ya Daudi.—2 Samweli 11:10-13.

Daudi alizidi kunaswa na matokeo ya dhambi yake. Kwa kukosa matumaini Daudi aliona suluhisho moja tu. Alimwambia Uria arudi vitani na kumpa barua ampelekee Yoabu, mkuu wa jeshi. Madhumuni ya barua hiyo fupi yalikuwa wazi: “Mwekeni Uria mbele ya watu penye vita vikali, kisha ondokeni, mmwache, ili apigwe akafe.” Kwa barua hiyo fupi, ilionekana kana kwamba mfalme huyu mwenye nguvu alikuwa ameficha matendo yake kwa kufanya Uria auawe.—2 Samweli 11:14-17.

Punde baada ya Bath-sheba kumaliza kipindi cha kumwomboleza mume wake, Daudi alimwoa. Wakati ulipita na mtoto wao akazaliwa. Wakati huo wote Daudi hakusema chochote kuhusu dhambi zake. Labda kimawazo alikuwa akijaribu kuhalalisha matendo yake. Je, Uria hakufa kiheshima vitani kama wengine? Isitoshe, je, hakukosa kumtii mfalme kwa kukataa kwenda kumtembelea mke wake? ‘Moyo mdanganyifu’ utajaribu kusababu katika kila njia ili kujaribu kuhalalisha dhambi.—Yeremia 17:9; 2 Samweli 11:25.

Matendo Yanayoongoza Kwenye Dhambi

Daudi, mpenda uadilifu, angewezaje kujishusha chini hivyo kiasi cha kuua na kufanya uzinzi? Ni wazi kwamba kuna mambo aliyokuwa amefanya kwa kipindi fulani ambayo yalimwongoza kwenye dhambi hiyo. Huenda tukashangaa ni kwa nini Daudi hakuwa pamoja na wanajeshi wake, akiwasaidia katika vita vyao na adui za Yehova. Kinyume cha hilo, Daudi alikuwa anastarehe kwenye jumba lake la kifalme, ambako ingekuwa vigumu sana kufikiria yaliyokuwa yakiendelea vitani, jambo ambalo lingemsaidia kuondoa akilini mwake tamaa mbaya ya mke wa askari mwaminifu. Leo, Wakristo wa kweli wanapata ulinzi kwa kushiriki kwa bidii katika mambo ya kiroho pamoja na makutaniko yao na pia kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kueneza injili.—1 Timotheo 6:12.

Mfalme mwisraeli aliagizwa kuandika nakala ya Sheria na kuisoma kila siku. Biblia husema ni kwa nini aliagizwa kufanya hivyo: “Ili apate kujifunza kumcha BWANA, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii na amri hizi, kwa kuyafanya; moyo wake usije ukainuliwa juu ya ndugu zake, wala asikengeuke katika maagizo, kwa mkono wa kuume wala wa kushoto.” (Kumbukumbu la Torati 17:18-20) Inaonekana kwamba Daudi hakuwa akifuata agizo hilo wakati alipotenda dhambi hizo nzito. Bila shaka kujifunza na kutafakari Neno la Mungu kwa ukawaida kutatulinda tusitende mabaya nyakati hizi za hatari.—Mithali 2:10-12.

Isitoshe, amri ya mwisho kati ya zile Amri Kumi yasema waziwazi hivi: “Usimtamani mke wa jirani yako.” (Kutoka 20:17) Wakati huo Daudi alikuwa na wake na masuria kadhaa. (2 Samweli 3:2-5) Lakini jambo hilo halikumzuia asitamani mwanamke mwingine mwenye kuvutia. Simulizi hilo linatukumbusha uzito wa maneno haya ya Yesu: “Kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Badala ya kuwaza juu ya tamaa hizo zisizofaa, acheni tuziondoe kabisa katika akili na mioyo yetu.

Toba na Rehema

Bila shaka, simulizi la Biblia lililo wazi kuhusu dhambi ya Daudi halikusudiwi kuamsha tamaa za mtu za kingono. Simulizi hilo linatusaidia kuona, kwa njia yenye nguvu na yenye kugusa moyo, rehema ya Yehova ambayo ni mojawapo ya sifa zake zenye kutokeza.—Kutoka 34:6, 7.

Baada ya Bath-sheba kuzaa mwana, Yehova alimtuma nabii Nathani akamkabili Daudi. Hilo lilikuwa tendo la rehema. Kama Daudi angeendelea kunyamaza na kama Nathani hangeongea naye kuhusu dhambi hiyo, inawezekana kwamba hali hiyo ingefanya moyo wake uwe mgumu asiache kutenda dhambi. (Waebrania 3:13) Inafurahisha kwamba Daudi aliitikia rehema ya Mungu. Maneno Nathani aliyosema kwa ustadi na waziwazi yalichoma dhamiri ya Daudi na kumfanya akubali kwa unyenyekevu kwamba alikuwa amemtenda Mungu dhambi. Zaburi 51 inayozungumzia dhambi ya Daudi na Bath-sheba, iliandikwa baada ya Daudi kutubu na kuungama dhambi yake nzito. Na tusiruhusu kamwe mioyo yetu iwe migumu iwapo tumetenda dhambi nzito.—2 Samweli 12:1-13.

Daudi alisamehewa, lakini hakuepuka nidhamu au matokeo ya dhambi yake. (Mithali 6:27) Daudi angeepukaje nidhamu? Kama Mungu angepuuza tu matendo ya Daudi, basi viwango vyake vingetiliwa shaka. Yehova angekuwa dhaifu kama Eli, Kuhani wa Cheo cha Juu, ambaye aliwakemea kwa upole tu wanaye waovu na kuwaachilia waendelee na vitendo vyao vibaya. (1 Samweli 2:22-25) Lakini Yehova humwonyesha fadhili-upendo mtu anayetubu. Rehema Yake, kama maji baridi yenye kuburudisha, itamsaidia aliyekosa avumilie matokeo ya dhambi yake. Hali nzuri inayotokana na kusamehewa na Mungu na ushirika wenye kujenga pamoja na waabudu wenzake unaweza kumponya kiroho mtu aliyekosa. Naam, kwa msingi wa fidia ya Kristo, mtu anayetubu anaweza kupata “utajiri wa fadhili [ya Mungu] isiyostahiliwa.”—Waefeso 1:7.

“Moyo Safi” na “Roho Mpya”

Baada ya Daudi kuungama, yeye hakujiruhusu apatwe na hali ya kuhisi kwamba hafai kitu. Maneno aliyoandika katika zaburi kuhusu maungamo yaonyesha kitulizo alichopata na pia azimio lake la kumtumikia Mungu kwa uaminifu. Kwa mfano, tazama Zaburi ya 32. Twasoma hivi kwenye mstari wa 1: “Heri aliyesamehewa dhambi, na kusitiriwa makosa yake.” Hata dhambi iwe nzito namna gani, inawezekana kuwe na matokeo mazuri ikiwa mtu anatubu kwa unyofu. Njia moja ya kuonyesha unyofu huo ni kukubali matendo yako yote, kama vile Daudi alivyofanya. (2 Samweli 12:13) Hakujaribu kujitetea mbele ya Yehova au kujaribu kulaumu wengine. Mstari wa 5 unasema: “Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuficha upotovu wangu. Nalisema, Nitayakiri maasi yangu kwa BWANA, nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu.” Toba ya kweli huleta kitulizo, kwa hiyo mtu hachomwi na dhamiri yake kwa sababu ya makosa ya wakati uliopita.

Baada ya kumsihi Yehova amsamehe, Daudi alisihi: “Uniumbie moyo safi, ee Mungu, uweke ndani yangu roho mpya na thabiti.” (Zaburi 51:10, BHN) Kuomba “moyo safi” na “roho mpya” kwaonyesha kwamba Daudi alitambua mwelekeo wa dhambi uliokuwa ndani yake na kwamba alihitaji msaada wa Mungu ili asafishe moyo wake na kuanza maisha upya. Badala ya kuanza kujisikitikia, aliazimia kusonga mbele katika utumishi wake kwa Mungu. Alisali hivi: “Ee Bwana, uifumbue midomo yangu, na kinywa changu kitazinena sifa zako.”—Zaburi 51:15.

Yehova aliitikiaje toba ya unyofu na azimio la Daudi la kumtumikia? Alimpa Daudi hakikisho hili lenye kuchangamsha moyo: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.” (Zaburi 32:8) Hapa tunahakikishiwa kwamba Yehova anajali sana hisia na mahitaji ya mtu anayetubu. Yehova alichukua hatua za kumwongezea Daudi ufahamu, uwezo wa kuona mambo kwa undani zaidi. Iwapo angepatwa na kishawishi wakati ujao, angeweza kutambua matokeo ya matendo yake na jinsi yangeathiri wengine, na angeweza kutenda kwa busara.

Jambo hilo lililotokea katika maisha ya Daudi ni kitia moyo kwa wote ambao wamefanya dhambi nzito. Kwa kuungama dhambi yetu na kutubu kwa unyofu, tunaweza kupata tena kitu kilicho cha thamani zaidi kwetu, uhusiano wetu na Yehova Mungu. Maumivu ya muda mfupi na aibu ambayo huenda tukapata haiwezi kulinganishwa na maumivu makali yanayotokana na kuficha dhambi, au matokeo mabaya sana ya kufuata mwenendo wa uasi kwa kuruhusu mioyo yetu iwe migumu. (Zaburi 32:9) Badala yake, tunaweza kusamehewa na Mungu mwenye upendo na rehema, “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 Wakorintho 1:3.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Daudi alitumaini kuepuka matokeo ya dhambi yake kwa kufanya Uria auawe