Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwenye 2 Petro 3:13 hutaja “mbingu mpya [kwa wingi] na dunia mpya,” ilhali Ufunuo 21:1 hutabiri “mbingu mpya [kwa umoja] na dunia mpya”?

Kwa msingi, hii ni habari ya ziada inayohusu sarufi ya lugha za awali. Yaonekana habari hiyo haiwezi kubadili maana.

Fikiria kwanza Maandiko ya Kiebrania. Katika maandiko ya lugha ya awali, neno la Kiebrania sha·maʹyim, lililotafsiriwa “mbingu,” linakuwa kwa wingi sikuzote. Neno hilo linapotumiwa kwa wingi, yaonekana kwamba halimaanishi wingi katika maana ya ubora, bali wingi “wa eneo lenyewe,” au “kitu kizima kilicho na sehemu au ncha nyingi zilizotengana mbalimbali.” Hilo laeleweka kwa sababu mbingu halisi zilizo mbali na dunia zimeenea kila upande na zinatia ndani mabilioni ya nyota. Wakati neno sha·maʹyim linapotanguliwa na kibainishi bayana, karibu wakati wote New World Translation hulitafsiri “mbingu” kwa wingi kama vile katika Isaya 66:22. Neno sha·maʹyim lisipokuwa na kibainishi bayana, linaweza kutafsiriwa kuwa “mbingu,” kwa umoja kama vile katika Mwanzo 1:8; 14:19, 22; Zaburi 69:34 au “mbingu” kwa wingi kama vile katika Mwanzo 49:25; Ayubu 9:8; Isaya 65:17.

Katika Isaya 65:17 na pia 66:22, neno la Kiebrania lililotafsiriwa mbingu liko katika wingi, na limetafsiriwa kwa upatano kuwa “mbingu mpya na nchi mpya.”

Neno la Kigiriki ou·ra·nosʹ lamaanisha “mbingu,” kwa umoja na neno ou·ra·noiʹ lamaanisha “mbingu” kwa wingi. Jambo la kushangaza ni kwamba watafsiri wa Septuagint ya Kigiriki walitumia neno mbingu kwa umoja katika Isaya 65:17 na pia 66:22.

Sasa vipi juu ya sehemu mbili ambapo neno “mbingu mpya [au mbingu kwa wingi] na dunia mpya” hupatikana katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo?

Katika 2 Petro 3:13, mtume alitumia neno la Kigiriki kwa wingi. Kabla ya mstari huo (katika mstari wa 7, 1012), alizungumza juu ya “mbingu” mbovu zilizopo sasa akitumia neno hilo katika wingi. Kwa hiyo alitumia kwa upatano neno hilo katika wingi kwenye mstari wa 13. Isitoshe, yaonekana alikuwa akinukuu andiko la awali la Isaya 65:17, ambapo neno la Kiebrania liko katika wingi, kama vile katika 2 Petro 2:22, ambapo alinukuu andiko la Kiebrania la Mithali 26:11. Kwa hiyo Petro alitaja “mbingu mpya [kwa wingi] na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake.”

Kwa kutofautisha kidogo, katika Ufunuo 21:1, yaonekana mtume Yohana alitumia maneno ya andiko la Isaya 65:17 katika Septuagint, ambalo kama ilivyotajwa, linatumia neno la Kigiriki “mbingu” kwa umoja. Kwa hiyo Yohana aliandika hivi: “Nikaona mbingu mpya [kwa umoja] na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali.”

Hii ni habari ya ziada ya kisarufi inayohusiana na tafsiri. Yafaa turudie kwamba hakuna tofauti yoyote katika maana kuhusiana na neno “mbingu mpya” liwe liko katika wingi au katika umoja. Maana ni ileile.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]

Nyota: Frank Zullo