Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watazame Mayatima na Wajane Katika Dhiki Yao

Watazame Mayatima na Wajane Katika Dhiki Yao

Watazame Mayatima na Wajane Katika Dhiki Yao

Ni wazi kabisa kwamba tunaishi katika ulimwengu usio na upendo. Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu watu ambao wangeishi katika “siku za mwisho”: “Nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na shauku ya kiasili.” (2 Timotheo 3:1-3) Maneno hayo ni ya kweli kabisa.

HALI ya maadili ya siku hizi ni mojawapo ya sababu zinazofanya watu wengi wakose huruma. Watu wengi hawajali wengine, na baadhi yao hawajali hata watu wa jamaa yao wenyewe.

Jambo hilo linaathiri wengi ambao wamekuwa maskini kwa sababu mbalimbali. Idadi ya wajane na mayatima inaongezeka daima kwa sababu ya vita, misiba ya asili, na wakimbizi wanaotafuta makao. (Mhubiri 3:19) Ripoti moja ya Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa yasema hivi: “Zaidi ya [watoto] milioni 1 wamepoteza wazazi au kutenganishwa na jamaa zao kwa sababu ya vita.” Pia, kuna mama wengi wasio na wenzi na mama ambao waume zao wamewataliki au wamewaacha. Mama hao wana kazi ngumu ya kujiruzuku na kulea watoto wao. Hali ni ngumu zaidi katika nchi zenye matatizo ya uchumi. Katika nchi hizo watu wengi ni maskini sana.

Je, kuna tumaini lolote kwa wale ambao wanateseka? Wajane na mayatima wanaweza kusaidiwaje? Je, tatizo hilo litakuja kutatuliwa?

Utunzaji Wenye Upendo Katika Siku za Biblia

Katika siku za Biblia wale ambao walimwabudu Mungu, walitunza wajane na mayatima na kutosheleza uhitaji wao wa kimwili na wa kiroho. Waisraeli walipovuna nafaka au matunda yao, hawakuruhusiwa kukusanya mavuno yaliyobaki shambani. Waliamriwa wasichume mara ya pili. ‘Mgeni, yatima, na mjane’ waliachiwa yaliyobaki. (Kumbukumbu la Torati 24:19-21) Sheria ya Musa ilisema: “Usimtese mjane ye yote aliyefiwa na mumewe, wala mtoto yatima.” (Kutoka 22:22, 23) Katika Biblia wajane na mayatima huwakilisha kwa kufaa watu maskini kwa kuwa mume na baba, au wazazi wote wawili wanapokufa, huenda waliofiwa wakawa maskini. Ayubu alisema hivi: “Nalimwokoa maskini aliyenililia; yatima naye, na yule asiyekuwa na mtu wa kumsaidia.”—Ayubu 29:12.

Kutunza waliokuwa wanateseka na waliokuwa wenye uhitaji kwa sababu walikuwa wamefiwa na wazazi au wamefiwa na mume, kulikuwa sehemu muhimu ya ibada ya kweli katika siku za mapema za kutaniko la Kikristo. Maneno yafuatayo yaliyoandikwa na mwanafunzi Yakobo yanaonyesha kwamba aliwajali sana wajane na mayatima: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kutazama mayatima na wajane katika dhiki yao, na kufuliza kujitunza mwenyewe bila doa kutokana na ulimwengu.”—Yakobo 1:27.

Mbali na kutaja wajane na mayatima, Yakobo pia alihangaikia sana wengine waliokuwa maskini na wenye uhitaji. (Yakobo 2:5, 6, 15, 16) Mtume Paulo aliwahangaikia vivyo hivyo. Paulo na Barnaba waliagizwa ‘wakumbuke walio maskini,’ walipotumwa wahubirie mataifa. “Jambo hilihili mimi pia nimejitahidi sana kwa bidii kulifanya,” Paulo aliweza kusema kwa dhamiri safi. (Wagalatia 2:9, 10) Simulizi kuhusu utendaji wa kutaniko la Kikristo muda mfupi baada ya kuanzishwa, lasema hivi: “Hapakuwa hata mmoja mwenye uhitaji miongoni mwao . . . Nao ugawanyaji ulikuwa ukifanywa kwa kila mmoja, kama vile alivyokuwa na uhitaji.” (Matendo 4:34, 35) Naam, mpango wa kutunza mayatima, wajane, na maskini uliokuwapo katika Israeli la kale hutumika pia katika kutaniko la Kikristo.

Bila shaka, msaada uliotolewa ulikuwa wa kadiri na kulingana na uwezo wa makutaniko. Fedha hazikutumiwa ovyoovyo, na wale waliosaidiwa walikuwa na uhitaji wa kweli. Wakristo hawakupaswa kujinufaisha isivyofaa na mpango huo, wala kutaniko halikupasa kutwikwa mzigo huo isivyo lazima. Paulo alitoa maagizo yaliyo wazi kuhusu habari hii katika andiko la 1 Timotheo 5:3-16. Andiko hilo laonyesha kwamba ikiwa watu wa ukoo wa yule mwenye uhitaji walikuwa na uwezo wa kumsaidia, basi, ilikuwa daraka lao kufanya hivyo. Wajane maskini walihitaji kutimiza matakwa fulani ili kustahili kupokea msaada. Hayo yote ni mpango wa busara wa Yehova kutunza wale wenye uhitaji. Hata hivyo, yanaonyesha pia kwamba lazima kuwe na usawaziko ili mtu yeyote asijinufaishe isivyofaa kwa mpango huo.—2 Wathesalonike 3:10-12.

Kutunza Mayatima na Wajane Leo

Kanuni zinazohusu kuwajali na kuwasaidia wanaoteseka, ambazo zilifuatwa na watumishi wa Mungu zamani, zinafuatwa hata leo katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Upendo wa kidugu ni sifa inayowatambulisha kama Yesu alivyosema: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Ikiwa baadhi ya Wakristo ni wenye uhitaji au wamepatwa na misiba au wameathiriwa na vita au mapambano ya kiraia, ndugu wao ulimwenguni pote wanajitahidi kutoa msaada wa kiroho na wa kimwili. Acheni tuchunguze visa vya siku zetu ambavyo vinaonyesha kile kinachofanywa leo kuhusiana na kusaidia wajane na mayatima.

Pedro hamkumbuki mama yake aliyekufa alipokuwa na umri wa mwaka mmoja na nusu. Alipokuwa na umri wa miaka mitano babake pia akafa. Kwa hiyo Pedro na ndugu zake waliachwa bila wazazi. Mashahidi wa Yehova walikuwa wamemtembelea baba yao, kwa hiyo Pedro na ndugu zake wote wakubwa walianza kujifunza Biblia.

Pedro asimulia: “Juma lililofuata, tulianza kuhudhuria mikutano. Tuliposhirikiana na ndugu, tuliweza kuona jinsi walivyotupenda. Kutaniko lilikuwa kimbilio langu kwa kuwa ndugu na dada walinipenda kana kwamba walikuwa wazazi wangu.” Pedro anakumbuka kwamba mzee mmoja Mkristo alikuwa akimkaribisha nyumbani kwake, na aliweza kushiriki mazungumzo na burudisho pamoja na familia ya mzee huyo. “Nakumbuka pindi hizo na ninazithamini sana,” Pedro anasema. Pedro alianza kuhubiri juu ya imani yake alipokuwa na umri wa miaka 11, na kubatizwa alipokuwa na umri wa miaka 15. Ndugu zake wakubwa pia walisaidiwa na ndugu kutanikoni kufanya maendeleo makubwa ya kiroho.

David ni mfano mwingine. David na dada yake, ambao ni mapacha, waliachwa peke yao wazazi wao walipotengana. Walilelewa na babu na nyanya zao na dada mmoja ya mama yao. “Tulipokua na kutambua hali yetu, tulipatwa na wasiwasi na huzuni nyingi sana. Tulihitaji tegemezo. Dada huyo wa mama yangu akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, kwa hiyo tukafundishwa kweli ya Biblia. Ndugu walituonyesha upendo na urafiki. Walitupenda sana, na kututia moyo kufikia miradi na kuendelea kumtumikia Yehova. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, mtumishi wa huduma mmoja alikuwa akija kunichukua tuhubiri pamoja. Ndugu mwingine alinisaidia kifedha nilipohudhuria mikusanyiko. Ndugu mmoja hata alinipa fedha niweze kutoa michango kwenye Jumba la Ufalme.”

David alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 17, na baadaye akaanza kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico. Anasema hivi: “[Hata sasa] kuna wazee kadhaa ambao wananielimisha na kunitolea ushauri unaonisaidia. Kwa njia hiyo ninaweza kushinda wasiwasi na upweke.”

Abel, ambaye ni mzee katika kutaniko moja huko Mexico lenye wajane kadhaa wanaohitaji msaada, anasema hivi: “Ninaamini kabisa kwamba wajane wanahitaji kusaidiwa kihisia hasa. Mara nyingine wanavunjika moyo na kujisikia wapweke. Kwa hiyo, ni muhimu sana kuwasaidia kwa kuwasikiliza. Sisi [wazee wa kutaniko] huwatembelea mara kwa mara. Ni muhimu kusikiliza wanapoeleza matatizo yao. Kwa njia hiyo wanapata faraja ya kiroho.” Hata hivyo, nyakati nyingine msaada wa kifedha unahitajika vilevile. Majuzi Abel alisema hivi: “Kwa sasa tunamjengea dada mjane nyumba. Tunatumia Jumamosi kadhaa kujenga nyumba yake, na vilevile alasiri kadhaa katikati ya juma.”

Mzee mwingine wa kutaniko ambaye amezoea kuwasaidia mayatima na wajane anasema hivi: “Ninaamini kwamba mayatima wana uhitaji mkubwa zaidi wa upendo wa Kikristo kuliko hata wajane. Nimeona kwamba mayatima wengi wanahisi wamepuuzwa kuliko watoto na vijana walio na wazazi wawili. Wanahitaji kuonyeshwa upendo mara nyingi. Ni vyema kuwatafuta baada ya mikutano na kuwajulia hali. Kuna ndugu aliyeoa ambaye alipoteza wazazi alipokuwa mvulana mdogo. Huwa ninamsalimu kwa uchangamfu mikutanoni, na yeye hunikumbatia anaponiona. Jambo hilo huimarisha upendo wa kidugu.”

Yehova “Atamkomboa Mhitaji”

Kumtumaini Yehova ni jambo la msingi katika kushughulikia hali za wajane na mayatima. Biblia inasema hivi kuhusu Yehova: “BWANA huwahifadhi wageni; huwategemeza yatima na mjane.” (Zaburi 146:9) Ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo ndio suluhisho kamili la matatizo hayo. Mtunga-zaburi aliandika hivi alipotabiri utawala huo wa Mesiya: “Atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:12, 13.

Mwisho wa ulimwengu huu unapokaribia, hapana shaka kwamba mikazo ambayo Wakristo wanakabili itazidi. (Mathayo 24:9-13) Ni lazima Wakristo wajali Wakristo wenzao zaidi na zaidi kila siku na ‘kuwa na upendo wenye juhudi nyingi wao kwa wao.’ (1 Petro 4:7-10) Wanaume Wakristo, hasa wazee, wanahitaji kuwajali mayatima na kuwaonyesha huruma. Na wanawake waliokomaa katika kutaniko wanaweza kuwasaidia sana na kuwafariji wajane. (Tito 2:3-5) Kila mmoja anaweza kutoa msaada kwa kuonyesha wazi kwamba anawajali wanaoteseka.

Wakristo wa kweli ‘hawafungi mlango wa huruma zao nyororo wanapomwona ndugu yao akiwa na uhitaji.’ Wanajitahidi sana kutii maneno haya ya mtume Yohana: “Watoto wadogo, acheni tupende, si katika neno wala kwa ulimi, bali katika kitendo na kweli.” (1 Yohana 3:17, 18) Kwa hiyo, acheni ‘tutazame mayatima na wajane katika dhiki yao.’—Yakobo 1:27.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Acheni tupende, si katika neno wala kwa ulimi, bali katika kitendo na kweli.”—1 Yohana 3:18

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakristo wa kweli hutunza wajane na mayatima kimwili, kiroho, na kihisia