Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msaada wa Kuielewa Biblia

Msaada wa Kuielewa Biblia

Msaada wa Kuielewa Biblia

BIBLIA ni kitabu cha pekee. Waandishi wake hudai kwamba walipuliziwa na Mungu, na yaliyomo hutoa uthibitisho wa kutosha kwamba dai hilo ni kweli. (2 Timotheo 3:16) Biblia hueleza tulitoka wapi, kwa nini tupo hapa, na tunaelekea wapi. Bila shaka, Biblia ni kitabu ambacho kinastahili kuchunguzwa!

Labda umejaribu kuisoma Biblia lakini ukaona kwamba ni vigumu kuielewa. Labda hujui jinsi ya kupata majibu ya maswali yako. Ikiwa ndivyo, kuna wengine walio kama wewe. Hali yako ni kama ya yule mtu aliyeishi katika karne ya kwanza. Alikuwa anasafiri kwenye gari la kukokotwa na farasi kutoka Yerusalemu kwenda Ethiopia, nchi ya kwao. Ofisa huyo Mwethiopia alikuwa akisoma kwa sauti kubwa kitabu cha Biblia cha Isaya, kilichokuwa kimeandikwa zaidi ya miaka 700 awali.

Kwa ghafula akasalimiwa na mwanamume fulani aliyekuwa anakimbia kandokando ya gari hilo. Mwanamume huyo alikuwa Filipo, mwanafunzi wa Yesu, naye alimwuliza hivi Mwethiopia huyo: “Je, wewe kwa hakika wajua unayoyasoma?” Huyo Mwethiopia akamjibu: “Kwa kweli, ningewezaje kufanya hivyo, isipokuwa mtu fulani angeniongoza?” Kisha akamwalika Filipo ndani ya gari. Filipo alimweleza maana ya sehemu hiyo aliyokuwa anasoma na kumwambia “habari njema juu ya Yesu.”—Matendo 8:30-35.

Kama vile Filipo alivyomsaidia Mwethiopia huyo kulielewa Neno la Mungu hapo zamani, Mashahidi wa Yehova huwasaidia watu kuielewa Biblia leo. Watafurahia kukusaidia pia. Kwa kawaida, ni vizuri kujifunza Biblia kwa utaratibu, ukianza na mafundisho ya msingi ya Kimaandiko. (Waebrania 6:1) Unapofanya maendeleo, utaweza kula kile Paulo alichokiita “chakula kigumu”—yaani, kweli zenye kina. (Waebrania 5:14) Ingawa Biblia ndiyo unayojifunza, kuna vichapo vingine vinavyoweza kukusaidia kupata na kuelewa maandiko ya Biblia kuhusu habari mbalimbali.

Kwa kawaida funzo linaweza kupangwa wakati na mahali panapokufaa. Wengine hata hujifunza kupitia simu. Funzo hilo sio kama mafunzo ya darasani; ni mpango wa kibinafsi unaorekebishwa ufaane na hali zako, kutia ndani malezi na elimu yako. Huhitaji kulipia funzo hilo la Biblia. (Mathayo 10:8) Hakuna mitihani, na hutaaibishwa. Maswali yako yatajibiwa, na utajifunza namna ya kumkaribia Mungu. Basi, kwa nini ujifunze Biblia? Chunguza sababu kadhaa zinazoonyesha kwamba funzo la Biblia linaweza kukuongezea shangwe maishani.