Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shangilieni kwa Kumjua Yehova

Shangilieni kwa Kumjua Yehova

Shangilieni kwa Kumjua Yehova

“Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—LUKA 11:28.

1. Yehova alianza kuwasiliana na wanadamu lini?

YEHOVA anawapenda wanadamu na anapendezwa sana na hali yao njema. Kwa hiyo, haishangazi kwamba anawasiliana nao. Alianza kuwasiliana nao katika bustani ya Edeni. Kulingana na Mwanzo 3:8, katika pindi moja “wakati wa jua kupunga,” Adamu na Hawa ‘walisikia sauti ya BWANA Mungu.’ Watu fulani wanadokeza kwamba hilo laonyesha kwamba lilikuwa jambo la kawaida kwa Yehova kuwasiliana na Adamu wakati huo, labda kila siku. Kwa vyovyote vile, Biblia yaonyesha waziwazi kwamba Mungu alikuwa amempa mwanadamu wa kwanza maagizo na pia kumfundisha mambo aliyopaswa kujua ili kutekeleza majukumu yake.—Mwanzo 1:28-30.

2. Wanadamu wa kwanza wawili walijitenga namna gani na mwongozo wa Yehova, na matokeo yakawa nini?

2 Yehova aliwapa Adamu na Hawa uhai na kuwapa mamlaka juu ya wanyama na dunia nzima. Walikuwa wamekatazwa kitu kimoja tu—hawakuruhusiwa kula kutokana na mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Kwa kushawishiwa na Shetani, Adamu na Hawa walikosa kutii amri ya Mungu. (Mwanzo 2:16, 17; 3:1-6) Waliamua kufanya mambo kwa kujitegemea, na kujiamulia lililo jema na lililo baya. Kwa upumbavu wakajitenga na mwongozo wa Muumba wao mwenye upendo. Matokeo yakawa mabaya sana kwao na kwa wazao wao ambao hawakuwa wamezaliwa. Hatimaye, Adamu na Hawa walizeeka na kufa bila tumaini la ufufuo. Wazao wao wakarithi dhambi na matokeo yake mabaya ambayo ni kifo.—Waroma 5:12.

3. Kwa nini Yehova aliwasiliana na Kaini, naye Kaini aliitikiaje?

3 Licha ya uasi katika Edeni, Yehova aliendelea kuwasiliana na viumbe wake wa kibinadamu. Kaini, mwana mzaliwa wa kwanza wa Adamu na Hawa, alikuwa anaelekea kutumbukia kwenye dhambi. Yehova alimwonya kwamba huenda akapatwa na msiba na kumshauri ‘atende vyema.’ Kaini alikataa shauri hilo lenye upendo na kumwua nduguye. (Mwanzo 4:3-8) Kwa hiyo, wanadamu wa kwanza watatu walikataa mwongozo ulio wazi kutoka kwa yule aliyewapa uhai, yaani, Mungu ambaye huwafundisha watu wake ili wapate faida. (Isaya 48:17) Lazima Yehova awe alisikitishwa sana na jambo hilo!

Yehova Ajitambulisha kwa Wanaume wa Kale Wenye Imani

4. Yehova alikuwa na uhakika gani kuhusu wazao wa Adamu, naye alitoa ujumbe gani wa tumaini, akiwa na kusudi gani?

4 Hata ingawa Yehova alikuwa na haki ya kukatisha kabisa mawasiliano na wanadamu, yeye hakufanya hivyo. Alikuwa na uhakika kwamba baadhi ya wazao wa Adamu wangefuata mwongozo Wake kwa hekima. Kwa mfano, alipokuwa akitangaza hukumu dhidi ya Adamu na Hawa, Yehova alitabiri kutokea kwa “mbegu” ambaye angempinga Nyoka, Shetani Ibilisi. Baada ya muda, Shetani angepondwa kichwa. (Mwanzo 3:15, NW ) Unabii huo ulikuwa ujumbe wa furaha na tumaini kwa “wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika.”—Luka 11:28.

5, 6. Ni katika njia zipi Yehova aliwasiliana na watu wake kabla ya karne ya kwanza W.K., nao walinufaikaje?

5 Yehova aliwasiliana na wazee waaminifu wa ukoo, kama vile Noa, Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yobu kuhusu mapenzi yake. (Mwanzo 6:13; Kutoka 33:1; Ayubu 38:1-3) Baadaye, alilipa taifa la Israeli mfumo wa sheria kupitia Musa. Sheria ya Kimusa iliwanufaisha katika njia nyingi. Kwa kutii Sheria hiyo, Waisraeli walitenganishwa na mataifa mengine na kuwa watu wa pekee wa Mungu. Mungu aliwahakikishia Waisraeli kwamba iwapo wangetii Sheria hiyo, angewabariki kimwili na kiroho pia, na kuwafanya kuwa ufalme wa makuhani, taifa takatifu. Sheria hiyo ilitoa kanuni kuhusu vyakula na usafi ambazo ziliwasaidia wawe na afya njema. Hata hivyo, Yehova aliwaonya pia kuhusu matokeo mabaya ambayo yangewapata iwapo wangekosa kutii.—Kutoka 19:5, 6; Kumbukumbu la Torati 28:1-68.

6 Baada ya muda, vitabu vingine vilivyopuliziwa viliongezwa vikawa sehemu ya vitabu vya Biblia vinavyokubaliwa. Masimulizi ya kihistoria yalitaja jinsi Yehova alivyoshughulika na mataifa na watu. Vitabu vya kishairi vilieleza sifa zake kwa njia yenye kupendeza. Vitabu vya kiunabii vilitabiri jinsi ambavyo mapenzi ya Yehova yangetimizwa wakati ujao. Wanaume wa kale wenye imani walisoma kwa makini maandiko yaliyopuliziwa na kuyatumia. Mmoja wao aliandika hivi: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” (Zaburi 119:105) Yehova aliwaelimisha na kuwapa nuru wale waliokubali kumsikiliza.

Nuru Yazidi Kung’aa

7. Ijapokuwa Yesu alifanya miujiza, alijulikana hasa kwa mambo gani, na kwa nini?

7 Kufikia karne ya kwanza, vikundi vya kidini vya Wayahudi walikuwa wameongeza mapokeo kwenye Sheria. Sheria ilitumiwa vibaya, na badala ya kuwa chanzo cha nuru, ikawa mzigo kwa sababu ya mapokeo hayo. (Mathayo 23:2-4) Hata hivyo, katika mwaka wa 29 W.K., Yesu alitokea akiwa Mesiya. Kazi yake ilihusisha kutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu na pia ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli.’ Ingawa alifanya miujiza, alijulikana hasa kuwa “Mwalimu.” Mafundisho yake yalikuwa kama nuru katika giza la kiroho lililofunika akili za watu. Yesu mwenyewe alisema hivi kwa kufaa: “Mimi ni nuru ya ulimwengu.”—Yohana 8:12; 11:28; 18:37.

8. Ni vitabu gani vilivyopuliziwa ambavyo viliandikwa katika karne ya kwanza W.K., navyo viliwanufaishaje Wakristo wa mapema?

8 Baadaye vitabu vya Injili viliongezwa, yaani masimulizi manne kuhusu maisha ya Yesu, na kitabu cha Matendo kinachosimulia jinsi Ukristo ulivyoenea baada ya kifo cha Yesu. Pia kulikuweko barua zilizopuliziwa ambazo ziliandikwa na wanafunzi wa Yesu, na vilevile kitabu cha unabii cha Ufunuo. Vitabu hivyo, pamoja na Maandiko ya Kiebrania, vilikamilisha vitabu vya Biblia vinavyokubaliwa. Kwa msaada wa vitabu hivyo vilivyopuliziwa, Wakristo wangeweza “kufahamu kiakili pamoja na watakatifu wote ni nini ulio upana na urefu na kimo na kina” cha kweli. (Waefeso 3:14-18) Wangeweza kuwa na “akili ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16) Hata hivyo, Wakristo hao wa mapema hawakuelewa kikamili kila jambo lililohusu makusudi ya Yehova. Mtume Paulo aliwaandikia waamini wenzake hivi: “Wakati wa sasa twaona katika njia isiyo ya waziwazi kupitia kioo cha madini.” (1 Wakorintho 13:12) Kioo hicho hakingeeleza mambo yote waziwazi. Ufahamu kamili wa Neno la Mungu ungepatikana baadaye.

9. Kumekuwa na nuru gani ya kiroho katika “siku za mwisho”?

9 Leo, tunaishi katika kipindi kinachoitwa “siku za mwisho,” kipindi kinachoashiriwa na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Nabii Danieli alitabiri kwamba katika wakati huu ‘maarifa yangeongezeka.’ (Danieli 12:4) Kwa hiyo, Yehova, Mwasiliani Mkuu, amewasaidia watu wenye mioyo minyofu waelewe Neno lake. Watu wengi sasa wanaelewa kwamba Kristo Yesu alitawazwa katika mbingu zisizoonekana mwaka wa 1914. Pia wanajua kwamba hivi karibuni atakomesha uovu wote na kugeuza dunia kuwa paradiso. Jambo hilo muhimu kuhusu habari njema za Ufalme sasa linahubiriwa duniani pote.—Mathayo 24:14.

10. Watu wameitikiaje shauri la Yehova katika karne zote ambazo zimepita?

10 Naam, katika muda wote ambao umepita Yehova amewajulisha watu hapa duniani mapenzi na makusudi yake. Biblia hueleza jinsi wengi walivyobarikiwa kwa kusikiliza na kutumia hekima ya kimungu. Inaonyesha pia juu ya wengine waliokataa shauri la Mungu lenye upendo, na kufuata mwenendo wa uharibifu wa Adamu na Hawa. Yesu alieleza hali hiyo alipozungumza juu ya barabara mbili za mfano. Moja inaongoza kwenye uharibifu. Kwa kuwa barabara hiyo ni pana na yenye nafasi, inafuatwa na wengi wanaolikataa Neno la Mungu. Barabara ile nyingine huongoza kwenye uhai udumuo milele. Ingawa imefinyana, njia hiyo inafuatwa na watu wachache wanaoikubali Biblia kuwa Neno la Mungu, na kuishi kupatana nayo.—Mathayo 7:13, 14.

Kuthamini Kile Tulicho Nacho

11. Ujuzi na imani yetu katika Biblia huthibitisha nini?

11 Je, wewe ni mmoja wa wale ambao wamechagua barabara inayoongoza kwenye uhai? Ikiwa ndivyo, bila shaka ungependa kubaki katika barabara hiyo. Unawezaje kubaki katika barabara hiyo? Tafakari kwa ukawaida na kwa uthamini baraka ambazo umepata maishani kwa sababu ya kujua kweli za Biblia. Kwa kuwa umekubali habari njema, huo ni uthibitisho wa kwamba Mungu amekubariki. Yesu alionyesha hivyo aliposali hivi kwa Baba yake: “Nakusifu wewe hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa vitoto.” (Mathayo 11:25) Wavuvi na wakusanya-kodi walielewa mafundisho ya Yesu, lakini viongozi wa kidini waliokuwa na elimu ya juu hawakuyafahamu. Yesu aliongezea kusema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Ikiwa unaifahamu Biblia na unaiamini na kutii mafundisho yake, huo ni uthibitisho wa kwamba Yehova amekuvuta kwake. Hiyo ni sababu moja ya kushangilia.

12. Biblia hutoa nuru katika njia gani?

12 Neno la Mungu lina kweli zinazotoa nuru na kuweka watu huru. Wale wanaoishi kupatana na ujuzi wa Biblia wako huru kutokana na ushirikina, mafundisho yasiyo ya kweli, na ukosefu wa ujuzi ambao unadhibiti maisha ya mamilioni ya watu. Kwa mfano, kufahamu ukweli kuhusu nafsi hutuweka huru na hofu yoyote kwamba wafu wanaweza kutudhuru au kwamba wapendwa wetu waliokufa wanateseka. (Ezekieli 18:4) Kujua ukweli kuhusu malaika waovu hutusaidia tuepuke hatari za uwasiliani-roho. Fundisho la ufufuo hufariji wale ambao wamefiwa na wapendwa wao. (Yohana 11:25) Unabii wa Biblia hutuonyesha mahali ambapo tumefikia kuhusiana na wakati na hutupa uhakika katika ahadi za Mungu za wakati ujao. Pia huimarisha tumaini letu la kuishi milele.

13. Kutii Neno la Mungu hutunufaishaje kimwili?

13 Kanuni za kimungu zilizo katika Biblia hutufundisha kuishi kwa njia ambayo inatunufaisha kimwili. Kwa mfano, tunajifunza kuepuka mazoea ambayo huchafua miili yetu, kama vile matumizi mabaya ya dawa za kulevya na tumbaku. Tunaepuka kutumia vileo isivyofaa. (2 Wakorintho 7:1) Kutii sheria za Mungu za maadili hutulinda tusipatwe na magonjwa yanayoambukizwa kingono. (1 Wakorintho 6:18) Kwa kutii shauri la Mungu la kuepuka kupenda fedha, hatuharibu amani yetu ya akili, kama vile wengine wameiharibu kwa kufuatia utajiri. (1 Timotheo 6:10) Umenufaika katika njia gani kwa sababu ya kutumia Neno la Mungu katika maisha yako?

14. Roho takatifu huathirije maisha yetu?

14 Tukiishi kupatana na Neno la Mungu, tunapokea roho takatifu ya Yehova. Tunasitawisha utu kama wa Kristo unaodhihirishwa na sifa zenye kuvutia kama vile rehema na huruma. (Waefeso 4:24, 32) Roho ya Mungu pia hutusaidia tusitawishe matunda ya roho—upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti. (Wagalatia 5:22, 23) Sifa hizo hutufanya tuwe na furaha na uhusiano mzuri pamoja na wengine, kutia ndani washiriki wa familia. Tunapata nguvu ambayo hutusaidia kukabiliana na magumu kwa ujasiri. Je, unatambua jinsi ambavyo roho takatifu imeathiri maisha yako yakawa bora?

15. Tunanufaikaje kwa kupatanisha maisha yetu na mapenzi ya Mungu?

15 Tunapopatanisha maisha yetu na mapenzi ya Mungu, tunaimarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Tunakuwa na uhakika zaidi kwamba anatuelewa na kutupenda. Kupitia mambo yanayotupata tunajifunza kwamba anatutegemeza wakati wa magumu. (Zaburi 18:18) Tunafahamu kwamba kwa kweli yeye husikiliza sala zetu. (Zaburi 65:2) Kisha sisi hutegemea mwongozo wake, tukiwa na uhakika kwamba utatunufaisha. Na tuna tumaini zuri kwamba kwa wakati wake, Mungu atafanya watumishi wake waaminifu wawe wakamilifu na kuwapa zawadi ya uhai udumuo milele. (Waroma 6:23) Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Je, umehisi kwamba uhusiano wako na Yehova umeimarishwa kwa sababu ya kumkaribia?

Hazina Isiyo na Kifani

16. Wakristo fulani wa karne ya kwanza walifanya mabadiliko gani?

16 Paulo aliwakumbusha Wakristo watiwa-mafuta wa karne ya kwanza kwamba wakati fulani baadhi yao walikuwa waasherati, wazinzi, wanaume walalao pamoja na wanaume, wezi, watu wenye pupa, walevi, watukanaji, na wanyang’anyi. (1 Wakorintho 6:9-11) Walifanya mabadiliko makubwa kwa sababu ya kweli ya Biblia; ‘walioshwa wakawa safi.’ Jaribu kuwazia jinsi ambavyo maisha yako yangekuwa bila kweli zenye kuweka watu huru ambazo umejifunza katika Biblia. Bila shaka ukweli ni hazina isiyo na kifani. Tunafurahi kama nini kwamba Mungu huwasiliana nasi!

17. Mashahidi wa Yehova wamelishwaje kiroho kwenye mikutano ya Kikristo?

17 Isitoshe, fikiria baraka tulizo nazo katika udugu wetu wenye jamii nyingi! “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huandaa chakula cha kiroho kwa wakati wake, kutia ndani Biblia, magazeti, na vichapo vingine katika lugha nyingi sana. (Mathayo 24:45-47) Kwenye mikutano ya kutaniko katika mwaka wa 2000, Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingi walipitia mambo makuu katika vitabu vinane vikuu vya Maandiko ya Kiebrania. Walisoma karibu robo ya kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi na karibu kitabu chote cha Sikiliza Unabii wa Danieli! Mbali na zile makala 52 za funzo la Mnara wa Mlinzi, tulisoma makala 36 kutoka katika gazeti hilo. Isitoshe, watu wa Yehova waliandaliwa matoleo 12 ya Huduma Yetu ya Ufalme na hotuba za watu wote za kila juma zilizohusu mambo mbalimbali katika Biblia. Tumeandaliwa ujuzi mwingi wa kiroho kama nini!

18. Tunasaidiwa katika njia gani kwenye kutaniko la Kikristo?

18 Ulimwenguni pote, makutaniko zaidi ya 91,000 huandaa utegemezo na kitia-moyo kupitia mikutano na ushirika. Pia tunapata utegemezo kutoka kwa Wakristo wenzetu waliokomaa ambao wako tayari kutusaidia kiroho. (Waefeso 4:11-13) Naam, tumenufaika sana kwa kupokea ujuzi wa ile kweli. Ni shangwe kujua na kumtumikia Yehova. Jinsi maneno haya yaliyoandikwa na mtunga-zaburi yalivyo ya kweli: “Heri watu wenye BWANA kuwa Mungu wao”!—Zaburi 144:15.

Je, Unakumbuka?

• Yehova aliwasiliana na nani kabla ya Ukristo?

• Nuru ya kiroho iliangazaje zaidi katika karne ya kwanza? katika nyakati za kisasa?

• Tunapata baraka gani kwa kuishi kupatana na ujuzi juu ya Yehova?

• Kwa nini tunashangilia kumjua Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Yehova aliwasiliana na Noa, Abrahamu, na Musa kuhusu mapenzi yake

[Picha katika ukurasa wa 9]

Katika siku zetu, Yehova ameangaza nuru kwa Neno lake

[Picha katika ukurasa wa 10]

Fikiria baraka tulizo nazo katika udugu wetu wenye jamii nyingi!