Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shiriki Shangwe ya Kutoa!

Shiriki Shangwe ya Kutoa!

Shiriki Shangwe ya Kutoa!

“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—MATENDO 20:35.

1. Yehova huonyeshaje shangwe ya kutoa?

SHANGWE ya kujua kweli na manufaa yanayotokana na kujua kweli ni zawadi zenye thamani kutoka kwa Mungu. Wale ambao wamemjua Yehova wana sababu nyingi za kushangilia. Lakini, ingawa kuna shangwe ya kupokea zawadi, pia kuna shangwe katika kutoa zawadi. Yehova ni Mpaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu,” naye ni “Mungu mwenye furaha.” (Yakobo 1:17; 1 Timotheo 1:11) Yeye hutoa mafundisho yenye manufaa kwa wote wanaosikiliza na anapendezwa na utii wa watu anaowafundisha, kama vile wazazi hufurahi watoto wao wanapokubali mafundisho yao yenye upendo.—Mithali 27:11.

2. (a) Yesu alisema nini kuhusu kutoa? (b) Tunapata furaha gani tunapowafundisha wengine kweli ya Biblia?

2 Vivyo hivyo, Yesu alipokuwa duniani alifurahi kuona watu wakikubali mafundisho yake. Mtume Paulo alimnukuu Yesu aliposema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Furaha tunayopata tunapofundisha wengine kweli ya Biblia inatia ndani mengi zaidi ya ule uradhi kwamba mtu amekubali imani yetu ya kidini. Zaidi ya hilo, tunapata shangwe kujua kwamba tunatoa kitu fulani chenye thamani ya kweli na ya kudumu. Tunaweza kuwasaidia watu wajinufaishe sasa na milele kwa kuwapa kitu chenye thamani ya kiroho.—1 Timotheo 4:8.

Kutoa Huleta Shangwe

3. (a) Mtume Paulo na mtume Yohana walionyeshaje shangwe yao katika kuwasaidia wengine kiroho? (b) Kwa nini kuwafundisha watoto wetu kweli ya Biblia ni wonyesho wa upendo?

3 Ndiyo, kama vile Yehova na Yesu hupata shangwe kwa kutoa zawadi za kiroho, ndivyo na Wakristo pia. Mtume Paulo alifurahi kujua kwamba alikuwa amewasaidia wengine wajifunze kweli ya Neno la Mungu. Aliandikia kutaniko la Thesalonike maneno haya: “Ni nini tumaini letu au shangwe au taji la mchachawo—kwani, je, kwa kweli si nyinyi?—mbele ya Bwana wetu Yesu kwenye kuwapo kwake? Nyinyi hakika ni utukufu na shangwe yetu.” (1 Wathesalonike 2:19, 20) Vivyo hivyo, mtume Yohana, alipokuwa akirejezea watoto wake wa kiroho, aliandika hivi: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 4) Fikiria pia shangwe tunayopata kwa kuwasaidia watoto wetu wawe watu wa kiroho! Wazazi wanaonyesha upendo wanapowalea watoto wao katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Kwa hiyo wazazi huonyesha kwamba wanajali hali njema ya milele ya watoto wao. Watoto hao wanapokubali mafundisho, wazazi hupata shangwe na uradhi mwingi.

4. Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha shangwe ya kutoa kwa njia ya kiroho?

4 Dell, ni mhudumu painia, mtumishi wa wakati wote, ambaye ni mama mwenye watoto watano. Asema hivi: “Naweza kuelewa vizuri kilichomfanya mtume Yohana aseme maneno aliyosema kwa sababu mimi ninashukuru sana kwamba watoto wangu wanne ‘wanatembea katika kweli.’ Ninajua kwamba familia zinapoungana katika ibada ya kweli zinamletea Yehova heshima na utukufu, kwa hiyo ninaridhika sana kuona akibariki jitihada zangu za kufundisha watoto wangu kweli. Taraja zuri la kuishi milele katika Paradiso pamoja na familia yangu hunipa tumaini na hunichochea kuvumilia licha ya magumu na vizuizi mbalimbali.” Kwa kusikitisha, mmojawapo wa binti za Dell alitengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo kwa sababu ya kufuatia mwenendo usio wa Kikristo. Hata hivyo, Dell hujitahidi kudumisha mtazamo ufaao. “Natumaini kwamba siku moja binti yangu atamrudia Yehova kwa unyenyekevu na kwa unyofu,” asema. “Lakini ninamshukuru Mungu kwamba wengi wa watoto wangu wanaendelea kumtumikia kwa uaminifu. Shangwe ninayopata hunitia nguvu kwelikweli.”—Nehemia 8:10.

Kujipatia Marafiki wa Kudumu

5. Tunapojitoa katika kazi ya kufanya wanafunzi, tunapata uradhi kwa kujua jambo gani?

5 Yesu aliwaagiza wafuasi wake wafanye wanafunzi Wakristo na kuwafundisha kuhusu Yehova na matakwa yake. (Mathayo 28:19, 20) Yehova na Yesu wamesaidia watu bila ubinafsi wajifunze kweli. Kwa hiyo tunapojitoa katika kazi ya kufanya wanafunzi, tunapata uradhi wa kujua kwamba tunaiga kielelezo cha Yehova na cha Yesu, kama walivyofanya Wakristo wa mapema. (1 Wakorintho 11:1) Kwa hiyo tunaposhirikiana na Mungu Mweza Yote na Mwana wake mpendwa, maisha yetu yanakuwa na kusudi halisi. Ni baraka iliyoje kuwa miongoni mwa “wafanyakazi wenzi” wa Mungu! (1 Wakorintho 3:9) Je, si jambo lenye kusisimua kwamba hata malaika wanashiriki kuhubiri habari njema?—Ufunuo 14:6, 7.

6. Tunakuwa marafiki wa nani tunaposhiriki kutoa kitu chenye thamani ya kiroho?

6 Kwa hakika, kwa kushiriki kazi hii ya kutoa kitu chenye thamani ya kiroho, tunaweza kuwa wafanyakazi wenzi wa Mungu na pia marafiki wake wa kudumu. Abrahamu aliitwa rafiki ya Yehova kwa sababu ya imani yake. (Yakobo 2:23) Tunapojitahidi kufanya mapenzi ya Mungu, sisi pia tunaweza kuwa marafiki wa Mungu. Tunapokuwa marafiki wa Mungu, tunakuwa marafiki wa Yesu pia. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nimewaita nyinyi marafiki, kwa sababu mambo yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu nimewajulisha nyinyi.” (Yohana 15:15) Watu wengi hufurahia kuwa marafiki wa watu mashuhuri au wa maofisa wenye vyeo vikubwa, lakini tunaweza kuwa marafiki wa watu wawili wakubwa zaidi katika ulimwengu wote!

7. (a) Mwanamke fulani alipataje rafiki wa kweli? (b) Je, umewahi kupata rafiki wa kweli kama alivyopata mwanamke huyo?

7 Isitoshe, tunapowasaidia watu kumjua Mungu, wanakuwa marafiki wetu pia, na hivyo tunapata furaha ya pekee. Joan, anayeishi Marekani, alianza kujifunza Biblia na mwanamke mmoja anayeitwa Thelma. Ingawa Thelma alipingwa na familia yao asijifunze, alivumilia na kubatizwa mwaka mmoja baadaye. Joan aliandika hivi: “Uhusiano wetu haukuishia hapo; badala yake, sasa tumekuwa marafiki kwa muda wa miaka 35. Mara nyingi tumeenda kwenye huduma na kwenye mikusanyiko pamoja. Hatimaye, nilihamia nyumba mpya iliyo umbali wa kilometa 800. Lakini, Thelma anaendelea kunitumia barua za upendo na ambazo hunichangamsha sana, akiniambia kwamba ananifikiria kwa upendo na kunishukuru kwa kuwa rafiki na mfano mzuri kwake na kwa kumfundisha kweli ya Biblia. Nimepata thawabu nzuri ya kuwa na rafiki mpendwa na wa karibu namna hiyo kwa sababu ya jitihada niliyofanya ya kumsaidia ajifunze juu ya Yehova.”

8. Ni mtazamo gani unaofaa utakaotusaidia katika huduma?

8 Tazamio la kupata mtu ambaye anataka kujifunza kweli laweza kutusaidia kuvumilia hata ikiwa watu wengi tunaowapata hawapendezwi sana au hawapendezwi kabisa na Neno la Yehova. Imani yetu na uvumilivu wetu waweza kujaribiwa kwa sababu ya kutopendezwa huko. Hata hivyo, mtazamo unaofaa utatusaidia. Fausto, kutoka Guatemala, alisema hivi: “Ninapowatolea wengine ushahidi, mimi hufikiri jinsi inavyoweza kuwa jambo lenye kufurahisha ikiwa mtu ninayezungumza naye atakuwa ndugu au dada wa kiroho. Mimi husababu kwamba angalau nitakutana na mtu mmoja ambaye hatimaye atakubali kweli ya Neno la Mungu. Ninapofikiria jambo hilo linanisaidia niendelee kutoa ushahidi na ninapata shangwe ya kweli.”

Kujiwekea Hazina Mbinguni

9. Yesu alisema nini kuhusu hazina za mbinguni, nasi twaweza kujifunza nini kutokana na maneno yake?

9 Si jambo rahisi kufanya wanafunzi, wawe ni watoto wetu au ni watu wengine. Huenda kufanya hivyo kukahitaji tuwe wenye saburi, wavumilivu, na huenda kukachukua muda pia. Hata hivyo, kumbuka kwamba wengi wako tayari kufanya kazi kwa bidii ili kulundika vitu vya kimwili, vitu ambavyo kwa kawaida haviwaletei furaha na havidumu milele. Yesu aliwaambia wasikilizaji wake kwamba ni afadhali kujitahidi kupata vitu vya kiroho. Alisema hivi: “Komeni kujiwekea akiba ya hazina duniani, ambako nondo na kutu hula kabisa, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala ya hivyo, jiwekeeni akiba ya hazina mbinguni, ambako wala nondo wala kutu haili kabisa, na ambako wezi hawavunji na kuiba.” (Mathayo 6:19, 20) Kwa kufuatia miradi ya kiroho—ambayo inatia ndani kushiriki kazi ya maana ya kufanya wanafunzi—tunaweza kupata uradhi wa kujua kwamba tunafanya mapenzi ya Mungu na kwamba atatuthawabisha. Mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Waebrania 6:10.

10. (a) Kwa nini Yesu alikuwa na hazina za kiroho? (b) Yesu alijitoaje, na kujitoa kwake kungewaletea wengine faida gani kubwa?

10 Tukifanya wanafunzi kwa bidii, tunajiwekea “akiba ya hazina mbinguni,” kupatana na maneno aliyosema Yesu. Kufanya hivyo hutupa shangwe ya kupokea. Hali yetu inakuwa bora tunapotoa bila ubinafsi. Yesu alikuwa amemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka isiyohesabika. Fikiria hazina alizojiwekea mbinguni! Hata hivyo, Yesu hakutafuta masilahi yake mwenyewe. Mtume Paulo aliandika hivi: “[Yesu] alijitoa mwenyewe kwa ajili ya dhambi zetu ili kulingana na mapenzi ya Mungu na Baba yetu apate kutukomboa kutoka katika mfumo mwovu wa mambo uliopo.” (Wagalatia 1:4) Yesu alijitoa bila ubinafsi katika huduma yake na pia akatoa uhai wake mwenyewe kuwa fidia ili wengine wapate fursa ya kujiwekea hazina mbinguni.

11. Kwa nini zawadi za kiroho ni bora kuliko zawadi za kimwili?

11 Kwa kufundisha watu kuhusu Mungu, tunawasaidia waone jinsi wao pia wanavyoweza kujiwekea hazina za kiroho zisizoharibika. Ni zawadi gani kubwa kuliko hiyo ambayo unaweza kutoa? Ukimpa rafiki saa ghali sana, gari, au hata nyumba, yaelekea rafiki huyo atathamini na kufurahi, nawe utapata shangwe kwa sababu ya kutoa. Lakini zawadi hiyo itakuwa katika hali gani baada ya miaka 20? Baada ya miaka 200? Baada ya miaka 2,000? Kwa upande mwingine, ukijitoa kusaidia mtu fulani amtumikie Yehova, mtu huyo anaweza kunufaika na zawadi hiyo milele.

Kutafuta Wale Wanaotaka Kweli

12. Wengi wamejitoaje kuwasaidia wengine kiroho?

12 Ili kushiriki shangwe ya kuwapa watu kitu chenye thamani ya kiroho, watu wa Yehova wamehubiri katika sehemu zote za dunia. Maelfu wameacha nyumba na familia zao wakawe mishonari katika nchi ambako imewabidi kujifunza lugha na tamaduni mpya. Wengine wamehamia kwenye maeneo katika nchi zao ambapo pana uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Na bado, wengine wamejifunza lugha ya kigeni, wakapata fursa mpya za kuhubiria watu ambao wamehamia maeneo yao. Kwa mfano, baada ya kulea watoto wawili ambao sasa wanatumikia katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, wenzi fulani wa ndoa huko New Jersey, Marekani, walianza kufanya upainia na kujifunza Kichina. Kwa muda unaozidi miaka mitatu waliweza kuongoza mafunzo ya Biblia 74 ya watu wanaozungumza Kichina waliokuwa wakisomea kwenye chuo fulani kilicho karibu na eneo hilo. Je, unaweza kupanua huduma yako kwa njia fulani ili upate shangwe zaidi katika kazi ya kufanya wanafunzi?

13. Unaweza kufanya nini ikiwa ungependa huduma yako iwe yenye matokeo zaidi?

13 Labda unatamani kuongoza funzo la Biblia lakini hujafanikiwa. Katika nchi fulani, ni vigumu kupata watu wenye kupendezwa. Labda watu unaowapata hawapendezwi na Biblia. Ikiwa ndivyo, labda unaweza kutaja jambo hilo mara nyingi katika sala, ukifahamu kwamba Yehova na Yesu Kristo wanapendezwa sana na kazi hiyo na wanaweza kukuelekeza kwa mtu mwenye mfano wa kondoo. Tafuta madokezo kutoka kwa wale ambao wana uzoefu zaidi katika kutaniko lenu au wale ambao wana matokeo zaidi katika huduma. Tumia mazoezi na madokezo yanayotolewa kwenye mikutano ya Kikristo. Nufaika na shauri la waangalizi wasafirio na wake zao. Zaidi ya yote, usikate tamaa. Mtu mwenye hekima aliandika hivi: “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa.” (Mhubiri 11:6) Wakati huohuo, kumbuka wanaume wenye imani kama vile Noa na Yeremia. Ijapokuwa ni watu wachache waliokubali mahubiri yao, huduma yao ilikuwa na matokeo. Zaidi ya yote, huduma yao ilimpendeza Yehova.

Kufanya Yote Uwezayo

14. Yehova huonaje watu ambao wamezeeka wakimtumikia?

14 Huenda hali zako zisikuruhusu kufanya mengi kadiri ambavyo ungependa kufanya katika huduma. Kwa mfano, uzee waweza kukuzia usifanye mambo ambayo ungependa kufanya katika utumishi wa Yehova. Hata hivyo, kumbuka maneno yaliyoandikwa na mtu mwenye hekima: “Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, kama kikionekana katika njia ya haki.” (Mithali 16:31) Yehova hufurahi anapoona tukimtumikia katika maisha yetu yote. Zaidi ya hilo, Maandiko husema: “Mimi ni yuleyule hata katika uzee wenu; hata katika uzee wenu mimi nitawabeba. Nilifanya hivyo kwanza, nitafanya hivyo tena. Nitawabeba nyinyi na kuwaokoa.” (Isaya 46:4, Biblia Habari Njema) Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo anaahidi kuwategemeza na kuwaunga mkono waaminifu-washikamanifu wake.

15. Je, unaamini kwamba Yehova anaelewa hali yako? Kwa nini?

15 Labda unavumilia ugonjwa, upinzani kutoka kwa mwenzi asiyeamini, madaraka mazito ya familia, au tatizo jingine gumu. Yehova hutambua udhaifu na hali zetu, naye anatupenda kwa sababu ya jitihada nyingi tunazofanya ili kumtumikia. Anatambua jambo hilo hata ingawa huenda tusifanye mengi kama wengine. (Wagalatia 6:4) Yehova anafahamu kwamba sisi si wakamilifu, naye hatarajii tufanye mengi kuliko tuwezavyo. (Zaburi 147:11) Tukifanya yote tuwezayo, tunaweza kuwa na hakika kwamba sisi ni wenye thamani machoni pa Mungu na kwamba hatasahau matendo yetu ya imani.—Luka 21:1-4.

16. Kutaniko lote hushirikije kufanya mwanafunzi?

16 Pia, kumbuka kwamba, sote tunashirikiana katika kazi ya kufanya wanafunzi. Mtu mmoja hawezi kufanya mtu awe mwanafunzi kama vile tone moja la mvua lisivyoweza kukuza mmea. Ni kweli kwamba huenda Shahidi mmoja akapata mtu mwenye kupendezwa na kuongoza funzo la Biblia. Lakini mtu huyo anapokuja kwenye Jumba la Ufalme, kutaniko lote humsaidia kutambua ile kweli. Uchangamfu wa akina ndugu huonyesha jinsi roho ya Mungu inavyotenda. (1 Wakorintho 14:24, 25) Watoto na matineja hutoa maelezo yenye kuchochea, jambo ambalo humwonyesha mtu mpya kwamba vijana wetu ni tofauti na vijana wa ulimwengu. Walio wagonjwa, wadhaifu kimwili, na wazee-wazee katika kutaniko huwafundisha wapya maana ya uvumilivu. Licha ya umri au udhaifu wetu, sote tunashiriki fungu muhimu katika kusaidia wapya kadiri upendo wao kwa Biblia unavyoongezeka na wanapofanya maendeleo kufikia ubatizo. Huenda kila saa tunayotumia katika huduma, kila ziara ya kurudia tunayofanya, kila mara tunapozungumza na mtu anayependezwa kwenye Jumba la Ufalme, mambo hayo yakaonekana kuwa madogo, hata hivyo, ni sehemu ya kazi kubwa inayotimizwa na Yehova.

17, 18. (a) Mbali na kushiriki kazi ya kufanya wanafunzi, tunaweza kushirikije shangwe ya kutoa? (b) Tunamwiga nani tunaposhiriki shangwe ya kutoa?

17 Bila shaka, mbali na kushiriki kazi ya maana zaidi ya kufanya wanafunzi, sisi Wakristo hushiriki pia shangwe ya kutoa katika njia nyingine. Tunaweza kutenga pesa za michango ili kutegemeza ibada safi na kusaidia walio na uhitaji. (Luka 16:9; 1 Wakorintho 16:1, 2) Tunaweza kutafuta fursa za kuonyesha wengine ukarimu. (Waroma 12:13) Tunaweza kujitahidi ‘kufanya lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.’ (Wagalatia 6:10) Tunaweza kutoa kwa njia sahili tena muhimu kwa kuwaandikia wengine barua, kuwapigia simu, kuwapa zawadi, kuwasaidia, na kwa kuwatia moyo.

18 Tunapotoa, tunaonyesha kwamba tunamwiga Baba yetu wa mbinguni. Pia tunaonyesha upendo wetu wa kidugu ambao hututambulisha kuwa Wakristo wa kweli. (Yohana 13:35) Kukumbuka mambo hayo kwaweza kutusaidia kushiriki shangwe ya kutoa.

Je, Unaweza Kueleza?

• Yehova na Yesu wameweka kielelezo gani katika kutoa kitu chenye thamani ya kiroho?

• Tunawezaje kujipatia marafiki wa kudumu?

• Ni hatua gani tunazoweza kuchukua ili kufanya huduma yetu iwe yenye matokeo zaidi?

• Wote kutanikoni wanaweza kushirikije shangwe ya kutoa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Watoto wanapokubali kufundishwa, wazazi hupata shangwe na uradhi mwingi

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tunapofanya wanafunzi, tunaweza kupata marafiki wa kweli

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yehova hutubeba wakati wa uzee

[Picha katika ukurasa wa 17]

Tunapata shangwe ya kutoa katika njia sahili tena muhimu