Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usiruhusu Imani Yako Iharibiwe na Shaka

Usiruhusu Imani Yako Iharibiwe na Shaka

Usiruhusu Imani Yako Iharibiwe na Shaka

Siku moja unafikiri una afya nzuri. Siku inayofuata unakuwa mgonjwa. Kwa ghafula unaishiwa na nguvu. Unaumwa na kichwa na kupatwa na maumivu mwilini. Kumetokea nini? Virusi hatari vinavyosababisha maradhi vimeingia mwilini mwako na kudhoofisha kinga ya mwili wako na kushambulia viungo muhimu. Usipotibiwa, vijidudu hivyo vyaweza kuharibu afya yako kabisa—hata kukuua.

BILA shaka, ukiambukizwa ugonjwa unapokuwa na afya mbaya utapatwa na madhara zaidi. Ikiwa, kwa mfano, mwili wako umedhoofishwa na utapiamlo, uwezo wa kujikinga “huwa mdogo sana hivi kwamba ambukizo dogo sana laweza kuwa hatari,” asema mwandishi wa kitiba Peter Wingate.

Ikiwa mambo yako hivyo, ni nani angependa kuishi maisha ya njaa? Yaelekea, unafanya yote uwezayo kula chakula kifaacho ili uendelee kuwa na afya. Yaelekea pia unafanya yote uwezayo ili kujilinda na maambukizo. Hata hivyo, je, unafanya hivyohivyo ili kuendelea kuwa ‘mwenye afya katika imani’? (Tito 2:2) Kwa mfano, je, uko macho kuelekea hatari zinazotokezwa na shaka zenye kudhuru? Shaka hizo zaweza kuingia kwa urahisi katika akili na moyo wako na kuharibu imani yako na uhusiano wako pamoja na Yehova. Watu wengine hawafahamu hatari hiyo. Wanapatwa na shaka kwa urahisi kwa sababu ya kutojilisha kiroho. Je, inawezekana kwamba unafanya hivyo?

Shaka—Je, Hudhuru Sikuzote?

Kwa kweli, shaka zote si mbaya. Nyakati nyingine, unahitaji kuchunguza jambo kabla ya kuliamini. Dini zinazohimiza watu waamini tu mambo bila kuwa na shaka juu ya jambo lolote ni hatari na ni za udanganyifu. Ni kweli kwamba, Biblia husema kuwa upendo “huamini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Bila shaka, Mkristo mwenye upendo anakuwa tayari kuamini watu ambao ni wenye kutumainika tangu zamani. Lakini, Neno la Mungu pia hutuonya dhidi ya ‘kuamini kila neno.’ (Mithali 14:15) Nyakati nyingine mambo ambayo mtu alifanya wakati uliopita yaweza kufanya atiliwe shaka. “[Mtu mdanganyifu] anenapo maneno mazuri usimsadiki,” yaonya Biblia.—Mithali 26:24, 25.

Mtume Yohana pia awaonya Wakristo wasiamini mambo vivi hivi tu. Aandika hivi: “Msiamini kila usemi uliopuliziwa.” Badala yake, “jaribuni semi zilizopuliziwa ili kuona kama hizo zatokana na Mungu.” (1 Yohana 4:1) “Usemi,” fundisho au maoni, yaweza kuonekana kana kwamba yanatoka kwa Mungu. Lakini je, kweli yanatoka kwake? Kuwa na shaka ya kiasi fulani au kutoamini kila jambo tu kwaweza kuwa ulinzi kwelikweli kwa sababu kama asemavyo mtume Yohana, ‘wadanganyi wengi wameingia katika ulimwengu.’—2 Yohana 7.

Shaka Zisizo na Msingi

Naam, mara nyingi tunahitaji kuchunguza mambo ili kuthibitisha kama ni ya kweli. Hata hivyo, hiyo si sawa na kuruhusu shaka zisizo na msingi na zenye kudhuru zisitawi katika akili na mioyo yetu, yaani, shaka zinazoweza kuharibu imani na uhusiano wetu wenye msingi thabiti. Shaka hiyo yafafanuliwa kuwa ‘hali ya kutokuwa na imani au maoni thabiti’ na mara nyingi huathiri uwezo wetu wa kufanya maamuzi.’ Je, unakumbuka jinsi Shetani alivyotia shaka akilini mwa Hawa kuhusu Yehova? Aliuliza, “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, msile matunda ya miti yote ya bustani?” (Mwanzo 3:1) Hali ya kukosa uhakika iliyotokezwa na swali hilo lililoonekana kuwa lenye nia nzuri, ilivuruga uwezo wake wa kufanya maamuzi. Jambo hilo laonyesha jinsi mbinu za Shetani zilivyo. Kama vile mtu aliyezoea kuandika barua za uchongezi, Shetani ni stadi katika kutumia uchongezi, usemi wenye ukweli nusu, na uwongo. Kwa kutumia njia hiyo ya kupanda shaka zenye hila, Shetani ameharibu mahusiano mengi mazuri.—Wagalatia 5:7-9.

Mwanafunzi Yakobo alifahamu waziwazi madhara yanayosababishwa na shaka ya namna hiyo. Aandika juu ya pendeleo zuri tulilo nalo la kumfikia Mungu kwa uhuru wakati wa jaribu. Lakini, Yakobo aonya, unaposali kwa Mungu, ‘fuliza kuomba katika imani, bila kutia shaka hata kidogo.’ Kunapokuwa na shaka katika uhusiano wetu na Mungu tunakuwa “kama wimbi la bahari liendeshwalo na upepo na kupeperushwa huku na huku.” Tunakuwa kama “mtu wa kusitasita kuamua, asiye imara katika njia zake zote.” (Yakobo 1:6-8) Tunasitasita kuamua mambo kwa sababu tunakosa uhakika kuhusu jambo tunaloamini. Kisha, kama ilivyotukia kwa Hawa, inakuwa rahisi kuathiriwa na kila namna ya mafundisho na falsafa za roho waovu.

Kudumisha Afya Nzuri ya Kiroho

Hivyo, basi, twaweza kujilindaje dhidi ya shaka zenye kudhuru? Jibu ni rahisi sana: ni kwa kukataa katakata propaganda ya kishetani na kutumia kikamili maandalizi ya Mungu ambayo hutufanya tuwe “thabiti katika imani.”—1 Petro 5:8-10.

Jambo lililo muhimu kabisa ni kujilisha vizuri kiroho. Mwandishi Wingate, aliyetajwa mapema, aeleza hivi: “Hata wakati mwili unapopumzika unahitaji nguvu daima ili kemikali na viungo muhimu viendelee kufanya kazi; na tishu ziweze kufanyizwa upya.” Ndivyo ilivyo na afya yetu ya kiroho. Tusipojilisha kiroho kwa ukawaida, imani yetu, kama vile mwili ambao haujalishwa, itadhoofika hatua kwa hatua na hatimaye itakufa. Yesu Kristo alikazia jambo hilo aliposema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.”—Mathayo 4:4.

Ebu fikiria jambo hilo. Tulisitawishaje imani yenye nguvu hapo mwanzoni? Mtume Paulo aandika kwamba “imani hufuata jambo lisikiwalo.” (Waroma 10:17) Amaanisha kwamba hapo mwanzoni tulisitawisha imani na uhakika wetu katika Yehova, ahadi zake, na tengenezo lake kwa kujilisha Neno la Mungu. Bila shaka, hatukuamini tu kila kitu tulichosikia. Tulifanya kama vile wakazi wa jiji la Beroya walivyofanya. ‘Tuliyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo yalikuwa hivyo.’ (Matendo 17:11) ‘Tulijithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu’ na kuhakikisha kwamba yale tuliyosikia yalikuwa ya kweli. (Waroma 12:2; 1 Wathesalonike 5:21) Tangu wakati huo, yaelekea tumeimarisha imani yetu kwa kuwa tumepata kufahamu vizuri zaidi kwamba Neno la Mungu na ahadi zake haziwezi kushindwa.—Yoshua 23:14; Isaya 55:10, 11.

Epuka Njaa ya Kiroho

Sasa kazi iliyo ngumu ni kudumisha imani yetu na kuepuka shaka yoyote inayoweza kudhoofisha uhakika wetu katika Yehova na tengenezo lake. Ili tufaulu katika jambo hilo twapaswa kuendelea kuyachunguza Maandiko kila siku. Mtume Paulo aonya kwamba “katika vipindi vya wakati vya baadaye wengine [ambao huenda hapo mwanzoni walionekana kuwa na imani yenye nguvu] wataanguka kutoka kwenye imani, wakikazia uangalifu matamko yaliyopuliziwa yenye kuongoza vibaya na mafundisho ya roho waovu.” (1 Timotheo 4:1) Matamko na mafundisho hayo yenye kupotosha hufanya wengine wawe na shaka na kuwatenganisha na Mungu. Ni nini kinachoweza kutulinda? Kuendelea “kulishwa maneno ya imani na fundisho bora ambalo [tume]fuata kwa ukaribu.”—1 Timotheo 4:6.

Hata hivyo, kwa kusikitisha, wengine leo wanaamua ‘wasilishwe maneno ya imani’—hata wakati lishe hiyo inapopatikana bila malipo. Kama vile mwandikaji mmoja wa kitabu cha Mithali asemavyo, inawezekana kuwa na chakula kingi cha kiroho, karamu ya kiroho, na bado mtu akose kula na kumeng’enya chakula hicho.—Mithali 19:24; 26:15.

Jambo hilo ni hatari. Mwandishi Wingate asema: “Afya huathiriwa mara tu mwili uanzapo kutumia protini zake.” Unapokosa chakula, mwili wako huanza kutumia akiba ya nguvu iliyo katika sehemu zote za mwili. Akiba hiyo inapomalizika, mwili huanza kutumia protini iliyo muhimu kwa ukuzi na kurekebisha upya tishu. Viungo muhimu huanza kuchakaa. Kisha afya yako inazorota upesi.

Ndivyo ilivyotukia kwa watu fulani katika kutaniko la Kikristo la mapema katika maana ya kiroho. Walijaribu kujilisha kutokana na akiba yao ya kiroho. Yaelekea, walipuuza funzo la kibinafsi, wakawa dhaifu kiroho. (Waebrania 5:12) Mtume Paulo alieleza hatari ya kufanya hivyo alipowaandikia Wakristo Waebrania hivi: “Ni lazima kwetu kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa nasi, ili tusipate kamwe kupeperushwa mbali.” Alijua jinsi ilivyo rahisi kusitawisha mazoea mabaya ikiwa “tumepuuza wokovu wa ukubwa wa namna hii.”—Waebrania 2:1, 3.

Inashangaza kwamba, si lazima mtu mwenye utapiamlo aonekane kuwa dhaifu au mwembamba. Vivyo hivyo, huenda isijulikane mara moja kwamba mtu fulani ana njaa ya kiroho. Unaweza kuonekana kuwa mwenye afya nzuri ya kiroho hata wakati ambapo haujilishi vizuri—lakini utaonekana hivyo kwa muda mfupi tu! Bila shaka, utakuwa dhaifu kiroho, utapatwa na shaka zisizo na msingi, na kushindwa kupigana vita vikali kwa ajili ya imani. (Yuda 3) Ni wewe tu unayejua kadiri ambayo unajilisha kiroho.

Kwa hiyo, endelea na funzo lako la kibinafsi. Piga vita vikali dhidi ya shaka. Kupuuza jambo linaloonekana kuwa tatizo dogo tu, kutofanya lolote kuhusu shaka zenye kusumbua daima, kwaweza kuleta matokeo mabaya. (2 Wakorintho 11:3) ‘Je, kweli tunaishi katika siku za mwisho? Je, unaweza kuamini kila jambo ambalo Biblia husema? Je, kwa kweli hili ndilo tengenezo la Yehova?’ Shetani angependa kutia shaka kama hizo akilini mwako. Usiruhusu kutojilisha kiroho kufanye uathiriwe kwa wepesi na mafundisho yake ya udanganyifu. (Wakolosai 2:4-7) Fuata shauri alilopewa Timotheo. Uwe mwanafunzi mzuri wa “maandiko matakatifu” ili ‘uendelee katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishwa kuamini.’—2 Timotheo 3:13-15.

Huenda ukahitaji msaada ili kufanya hivyo. Mwandishi aliyenukuliwa mapema aendelea kusema: “Njaa inapokuwa kali sana viungo vinavyomeng’enya chakula vyaweza kudhuriwa sana na ukosefu wa vitamini na vitu vingine vya lazima hivi kwamba vitashindwa kumeng’enya chakula cha kawaida. Watu ambao wamefikia hali hiyo huenda wakahitaji kwa muda fulani kutumia chakula kinachoweza kumeng’enywa kwa urahisi .” Uangalifu wa pekee wahitajiwa ili kuondoa madhara ya utapiamlo mwilini. Vivyo hivyo, mtu ambaye amepuuza kabisa funzo lake la kibinafsi la Biblia huenda akahitaji kitia-moyo na msaada mkubwa ili asitawishe tena hamu yake ya mambo ya kiroho. Ikiwa uko katika hali hiyo, tafuta msaada na ukubali kwa moyo msaada wowote utakaopewa ili kuimarisha afya na nguvu zako za kiroho.—Yakobo 5:14, 15.

‘Usisitesite kwa Ukosefu wa Imani’

Kwa kufikiria hali za mzee wa ukoo Abrahamu, huenda wengine wakahisi kwamba Abrahamu alikuwa na sababu halali za kuwa na shaka. Huenda likasikika kuwa jambo la akili kufikia mkataa kwamba alikuwa ‘amekata tumaini kabisa la kuwa baba wa mataifa mengi’—licha ya ahadi ya Mungu. Kwa nini? Kwa kufikiria mambo kwa maoni ya kibinadamu, hakukuwa na tumaini lolote. Biblia husema kwamba ‘alifikiria mwili wake mwenyewe, ukiwa sasa tayari umefishwa na pia ufu wa tumbo la uzazi la Sara.’ Na bado, alikataa katakata kuruhusu shaka kuhusu Mungu na ahadi zake zisitawi katika akili na moyo wake. Mtume Paulo aandika hivi: “Hakupata kudhoofika katika imani,” au ‘kusitasita kwa ukosefu wa imani.’ Abrahamu aliendelea ‘kusadiki kikamili kwamba alilokuwa ameahidi Mungu alikuwa na uwezo pia wa kufanya.’ (Waroma 4:18-21) Alikuwa amesitawisha uhusiano wa kibinafsi ulio thabiti na wenye kutumainika pamoja na Yehova kwa miaka mingi. Alipuuza shaka zozote ambazo huenda zingedhoofisha uhusiano huo.

Unaweza kufanya vivyo hivyo ‘ukifuliza kushika kiolezo cha maneno yenye afya’—ukijilisha vyema kiroho. (2 Timotheo 1:13) Chukua kwa uzito hatari inayosababishwa na shaka. Shetani anapigana vita inayoweza kuitwa vita vya kutumia virusi vya kiroho. Ukipuuza kula chakula kizuri cha kiroho kupitia funzo la kibinafsi la Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, utaweza kushambuliwa kwa urahisi. Tumia chakula cha kiroho kinachoandaliwa kwa wingi na kwa wakati ufaao na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Endelea ‘kukubaliana na maneno yenye afya’ na kudumu ukiwa ‘mwenye afya katika imani.’ (1 Timotheo 6:3; Tito 2:2) Usiruhusu imani yako iharibiwe na shaka.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Unajilisha kiroho vizuri kadiri gani?