Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Baraka kwa Waadilifu’

‘Baraka kwa Waadilifu’

‘Baraka kwa Waadilifu’

“NALIKUWA kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki [“mwadilifu,” NW] ameachwa wala mzao wake akiomba chakula,” mtunga-zaburi Daudi alisema maneno hayo alipokuwa mzee. (Zaburi 37:25) Yehova Mungu hupenda waadilifu na kuwatunza sana. Katika Neno lake, Biblia, anawasihi waabudu wa kweli watafute uadilifu.—Sefania 2:3.

Uadilifu humaanisha kuwa na kibali cha Mungu, kwa sababu ya kutii sheria zake za mema na mabaya. Ili kututia moyo kufanya mapenzi ya Mungu, sura ya 10 ya kitabu cha Biblia cha Mithali inaonyesha baraka nyingi za kiroho ambazo wale wanaofanya mapenzi ya Mungu hupokea. Miongoni mwa hizo ni chakula kingi cha kiroho kinachojenga, kazi inayoridhisha yenye faida, na uhusiano mzuri pamoja na Mungu na wanadamu. Basi, tuchunguze Mithali 10:1-14.

Kichocheo Bora

Maneno ya utangulizi ya sura hiyo huonyesha wazi jina la mwandishi wa sehemu inayofuata ya kitabu cha Mithali. Yanasema hivi: “Mithali za Sulemani.” Mfalme Sulemani wa Israeli ya kale anataja kichocheo bora cha kufanya mema anaposema hivi: “Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye.”Mithali 10:1.

Wazazi wanahuzunika sana wakati mmoja wa watoto wao anapoacha kumwabudu Mungu wa kweli aliye hai! Mfalme huyo mwenye hekima anataja hasa huzuni ya mama, huenda akataka kuonyesha kwamba huzuni ya mama ni kubwa kuliko ya baba. Ndivyo Doris alivyoona. * Doris anasema hivi: “Mwana wetu mwenye umri wa miaka 21 alipoacha kweli, mimi na mume wangu, Frank, tulihuzunika sana. Mimi nimeumia moyoni zaidi kuliko Frank. Ijapokuwa miaka 12 imepita, huzuni hiyo haijaisha bado.”

Watoto wanaweza kuathiri furaha ya baba yao na kumhuzunisha mama yao. Na tuwe wenye hekima ili tuwafurahishe wazazi wetu. Na kwa vyovyote, tufurahishe moyo wa Baba yetu wa mbinguni, Yehova.

‘Nafsi ya Mwadilifu Imetoshelezwa’

“Hazina za uovu hazifaidii kitu; bali haki [“uadilifu,” “NW”] huokoa na mauti,” mfalme huyo asema. (Mithali 10:2) Wakristo wa kweli wanaoishi katika umalizio kabisa wa siku za mwisho wanathamini sana maneno hayo. (Danieli 12:4) Uharibifu wa ulimwengu huu wenye dhambi umekaribia sana. Njia za wanadamu za kujiletea usalama wa—kimwili, kifedha, au kijeshi—hazitakuwa kinga wakati wa “dhiki kubwa” iliyo karibu. (Ufunuo 7:9, 10, 13, 14) “Wanyofu [pekee] watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake.” (Mithali 2:21) Na tuendelee, basi, “kutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu].”—Mathayo 6:33.

Si lazima watumishi wa Yehova wangoje hadi ulimwengu mpya ulioahidiwa ili wapokee baraka za Mungu. “BWANA hataiacha nafsi ya mwenye haki [“mwadilifu,” “NW”] ife na njaa; bali tamaa ya mtu mwovu huisukumia mbali.” (Mithali 10:3) Yehova ameandaa chakula tele cha kiroho kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Waadilifu wana sababu nzuri za ‘kuimba kwa furaha ya moyo.’ (Isaya 65:14) Ujuzi hufurahisha moyo wake. Kutafuta hazina za kiroho ni furaha yake. Mwovu haoni kamwe furaha hiyo.

‘Bidii Hutajirisha’

Mwadilifu amebarikiwa kwa njia nyingine pia. “Atendaye mambo kwa mkono mlegevu huwa maskini; bali mkono wake aliye na bidii hutajirisha. Akusanyaye wakati wa hari ni mwana mwenye hekima; bali asinziaye wakati wa mavuno ni mwana mwenye kuaibisha.”Mithali 10:4, 5.

Maneno ya mfalme kwa wafanyakazi wa mavuno yana maana mahususi. Majira ya mavuno si wakati wa kusinzia. Ni wakati wa kufanya kazi kwa saa nyingi. Ndio wakati wa haraka.

Yesu alirejezea mavuno ya watu, wala si ya nafaka, alipowaambia wanafunzi wake hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno [Yehova Mungu] atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:35-38) Zaidi ya watu milioni 14 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu mwaka wa 2000—zaidi ya maradufu ya idadi ya Mashahidi wa Yehova. Ni nani awezaye kukataa kwamba ‘mashamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa’? (Yohana 4:35) Waabudu wa kweli huomba Bwana-mkubwa atume wafanyakazi zaidi, huku wakiwa na bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi kwa kupatana na sala zao. (Mathayo 28:19, 20) Na Yehova amebariki sana jitihada zao. Katika mwaka wa utumishi wa 2000, zaidi ya watu 280,000 walibatizwa. Hao pia wanajitahidi kuwa walimu wa Neno la Mungu. Na tuwe na furaha na turidhike katika majira haya ya mavuno tukishiriki kwa bidii kazi ya kufanya wanafunzi.

‘Baraka Humkalia Kichwani’

Sulemani anaendelea kusema, “Baraka humkalia mwenye haki [“mwadilifu,” “NW”] kichwani; bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu.”Mithali 10:6

Mtu mwadilifu mwenye moyo mnyofu huonyesha uadilifu wake wazi. Mazungumzo yake ni yenye urafiki na yenye kujenga, na hutenda kwa njia yenye kujenga na kwa ukarimu. Wengine wanapenda kushirikiana naye. Mtu huyo huheshimiwa na wengine—anapokea baraka zao—kwa kuwa wanasema mema juu yake.

Mtu mwovu kwa upande mwingine ni mwenye chuki, naye hunuia kuwadhuru wengine. Huenda ikawa usemi wake unapendeza, na ‘kufunika uovu’ uliomo moyoni mwake, lakini hatimaye atatenda na kusema maovu. (Mathayo 12:34, 35) Au, huenda ikawa “jeuri itafunika [au kufunga] kinywa cha watu waovu.” (Mithali 10:6, NW, kielezi chini) Jambo hilo lamaanisha kwamba mtu mwovu mara nyingi hutendewa na wengine jinsi anavyowatendea, yaani kwa uhasama. Kwa njia hiyo kinywa chake kinafunikwa, au kufungwa, naye ananyamazishwa. Mtu huyo hawezi kutarajia baraka zozote kutoka kwa wengine.

Mfalme wa Israeli aandika, “Kuwakumbuka wenye haki [“waadilifu,” “NW”] huwa na baraka; bali jina la mtu mwovu litaoza.” (Mithali 10:7) Waadilifu hukumbukwa kwa furaha na wengine, hasa zaidi na Yehova Mungu. Kwa kuwa Yesu alikuwa mwaminifu hadi kifo “amerithi jina bora kabisa” kuliko la malaika. (Waebrania 1:3, 4) Wanaume na wanawake waaminifu walioishi kabla ya enzi ya Ukristo, wanakumbukwa leo na Wakristo wa kweli kama mifano inayostahili kuigwa. (Waebrania 12:1, 2) Hiyo ni tofauti jinsi gani na jina la waovu ambalo hukirihiwa na kuchukiwa! Naam, “heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; na neema kuliko fedha na dhahabu.” (Mithali 22:1) Na tujifanyie jina jema pamoja na Yehova na wanadamu wenzetu.

“Aendaye kwa Unyofu Huenda Salama”

Sulemani anasema hivi akibainisha mwenye hekima na mpumbavu: “Aliye na akili moyoni mwake atapokea agizo; bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka.” (Mithali 10:8) Mwenye hekima anajua vizuri kwamba “kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Anatambua uhitaji wa kutafuta mwongozo kutoka kwa Yehova na hukubali amri za Mungu bila kusita. Lakini mpumbavu mwenye maneno mengi, kwa upange mwingine, hatambui jambo hilo la msingi. Maneno yake mengi humwongoza kwenye uharibifu.

Mwadilifu ana usalama fulani ambao mwovu hana. “Aendaye kwa unyofu huenda salama; bali apotoshaye njia zake atajulikana. Akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko; bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka.”Mithali 10:9, 10.

Mtu mwaminifu anatenda kwa unyofu. Anajipatia heshima na wengine wanamtumaini. Mtu mnyofu huthaminiwa na mwajiri wake na mara nyingi yeye hupewa daraka kubwa zaidi. Mtu anayejulikana kuwa mnyofu hatafutwa kazi au itakuwa rahisi kwake kupata kazi mpya hata wakati ambapo kazi hazipatikani kwa urahisi. Mbali na hayo, unyofu wake huchangia hali yenye kupendeza na ya amani nyumbani. (Zaburi 34:13, 14) Anakaa kwa usalama na watu wengine wa familia yake. Naam, usalama unatokana na uaminifu.

Hali ya mtu anayewadanganya wengine kwa sababu ya faida ya binafsi ni tofauti. Mdanganyifu huenda akajaribu kufunika udanganyifu wake kwa maneno ya uwongo au ishara za mwili. (Mithali 6:12-14) Mdanganyifu anayekonyeza jicho lake ili kudanganya na kwa nia ovu, anaweza kuwaumiza wengine sana kiakili. Lakini siku moja udanganyifu wa mtu huyo utajulikana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Dhambi za watu wengine hudhihirika waziwazi kwa watu wote, zikiongoza moja kwa moja kwenye hukumu, lakini kwa habari ya watu wengine pia dhambi zao hudhihirika baadaye. Katika njia ileile pia kazi zilizo bora hudhihirika waziwazi kwa watu wote na zile zilizo tofauti haziwezi kuwekwa zikiwa zimefichwa.” (1 Timotheo 5:24, 25) Haidhuru ni nani anayehusika—kama ni mzazi, rafiki, mwenzi wa ndoa, au mtu unayemfahamu kidogo tu—hatimaye, udanganyifu utakuja kufichuliwa. Ni nani awezaye kumwamini mtu ambaye anajulikana kuwa mdanganyifu?

‘Kinywa Chake Ni Chemchemi ya Uzima’

Sulemani asema, “Kinywa chake mwenye haki [“mwadilifu,” “NW”] ni chemchemi ya uzima, bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu.” (Mithali 10:11) Maneno yanayotoka kinywani yaweza ama kutuliza au kuumiza. Yanaweza kuburudisha na kumchangamsha mtu, au yanaweza kumvunja moyo.

Mfalme wa Israeli anasema hivi akionyesha kichocheo cha maneno yanayosemwa: “Kuchukiana huondokesha fitina; bali kupendana husitiri makosa yote.” (Mithali 10:12) Chuki hutokeza fitina na mizozano katika jamii ya wanadamu. Lazima wanaompenda Yehova waondoe kabisa chuki maishani mwao. Vipi? Kwa kuibadilisha na upendo. “Upendo hufunika wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8) Upendo “huhimili mambo yote,” yaani, “mambo yote ambayo hufunika.” (1 Wakorintho 13:7, Kingdom Interlinear) Upendo wa kimungu hautarajii ukamilifu kutokana na watu wasiokamilika. Badala ya kutangaza makosa ya wengine, upendo huo hutusaidia kutozingatia makosa yao, ila makosa mazito. Upendo hufanya tustahimili hata tunapotendwa vibaya katika huduma ya shambani, kazini, au shuleni.

Mfalme mwenye hekima aendelea kusema hivi: “Hekima hupatikana midomoni mwa mwenye ufahamu; bali fimbo hufaa kwa mgongo wake asiye na ufahamu.” (Mithali 10:13) Hekima ya mtu mwenye uelewevu humwongoza. Maneno yenye kujenga mdomoni mwake husaidia wengine kutembea kwenye njia ya uadilifu. Wala yeye wala wale wanaomsikiliza hawatalazimishwa—kwa fimbo ya nidhamu—kutembea kwa njia inayofaa.

‘Hifadhi Ujuzi’

Ni nini kitakachofanya maneno yetu yawe ‘kijito kibubujikacho hekima’ badala ya kuwa kijito kinachoropoka maneno matupu? (Mithali 18:4) Sulemani ajibu hivi: “Wenye hekima huhifadhi maarifa [“ujuzi” “NW”], lakini kuropoka kwa mpumbavu huleta maangamizi haraka.” Mithali 10:14, Biblia Habari Njema.

Takwa la kwanza ni kwamba akili yetu ijazwe ujuzi wenye kujenga wa Mungu. Ujuzi huo unapatikana mahali pamoja tu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Lazima tuweke akiba ya ujuzi na kuchimba katika Neno la Mungu kana kwamba tunachimba hazina iliyofichwa. Jinsi utafutaji huo ulivyo wenye kuchochea na wenye faida!

Ili tuweze kusema kwa hekima, lazima ujuzi wa Maandiko uwe moyoni mwetu. Yesu aliwaambia wasikilizaji wake hivi: “Mtu mwema hutokeza mema katika hazina njema ya moyo wake, lakini mtu mwovu hutokeza ambayo ni maovu katika hazina yake mbovu; kwa maana katika wingi wa moyo kinywa chake husema.” (Luka 6:45) Kwa hiyo, lazima tutafakari kwa ukawaida juu ya yale ambayo tunajifunza. Kwa kweli, kujifunza na kutafakari kwataka jitihada, lakini kwaleta faida kubwa sana ya kiroho. Hakuna haja kwa yeyote kuwa mropokaji wa maneno matupu yanayodhuru.

Naam, mtu mwenye hekima anafanya yaliyo mema machoni pa Mungu na ana uvutano mzuri juu ya wengine. Ana chakula kingi cha kiroho na ana mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana yenye faida. (1 Wakorintho 15:58) Kwa sababu yeye ni mtu mwaminifu, anaishi kwa usalama, naye ana kibali cha Mungu. Ndiyo, baraka za mwadilifu ni nyingi. Na tutafute uadilifu kwa kufuata sheria za Mungu za mema na mabaya.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Jina limebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Unyofu huchangia maisha ya familia yenye furaha

[Picha katika ukurasa wa 26]

‘Wenye hekima huweka akiba ya ujuzi’