Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Katika Kazi ya Kuvuna!

Endeleeni Katika Kazi ya Kuvuna!

Endeleeni Katika Kazi ya Kuvuna!

“Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.”—ZABURI 126:5.

1. Kwa nini ‘tumwombe Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi’ leo?

BAADA ya safari ya tatu ya Yesu Kristo kwenda kuhubiri huko Galilaya, aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” (Mathayo 9:37) Hali ilikuwa vivyo hivyo huko Yudea. (Luka 10:2) Hali ikoje leo, ikiwa mavuno yalikuwa mengi karibu miaka 2,000 iliyopita? Katika mwaka uliopita wa utumishi, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 6,000,000 waliendelea na kazi yao ya uvunaji wa mfano miongoni mwa watu 6,000,000,000 ulimwenguni, ambao wengi wao ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ Kwa hiyo, kama ilivyokuwa karne zilizopita, leo himizo la Yesu kwamba ‘tuombe Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake’ linafaa.—Mathayo 9:36, 38.

2. Ni nini ambacho hufanya tutambuliwe na watu?

2 Yehova Mungu aliye Bwana-mkubwa wa mavuno, amejibu ombi la kutuma wafanyakazi zaidi. Inafurahisha kama nini kushiriki katika kazi hii ya kuvuna inayoelekezwa na Mungu! Ingawa sisi ni wachache tukilinganishwa na mataifa, kuhubiri Ufalme kwa bidii na kufanya wanafunzi hufanya tutambuliwe na watu. Katika nchi nyingi tunatajwa sana katika vyombo vya habari. Katika vipindi fulani vya televisheni waigizaji wamesikika wakisema, ‘hao ni Mashahidi wa Yehova,’ mlango unapobishwa. Naam, utendaji wetu wa Kikristo tukiwa wavunaji wa mfano unajulikana sana katika karne hii ya 21.

3. (a) Tunajuaje kwamba kazi ya kuhubiri Ufalme ya karne ya kwanza ilitambuliwa? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba malaika wanategemeza huduma yetu?

3 Katika karne ya kwanza watu pia walitambua kuhubiriwa kwa Ufalme nao waliwanyanyasa watangazaji wa habari njema. Hivyo, mtume Paulo aliandika: “Yaonekana kwangu kwamba Mungu ametuweka sisi mitume mwisho katika wonyesho wa hadharani kama watu waliowekewa kifo, kwa sababu [sisi mitume] tumekuwa kitu cha kutazamwa mahali pa michezo kwa ulimwengu, na kwa malaika, na kwa wanadamu.” (1 Wakorintho 4:9) Vivyo hivyo, kuendelea kwetu kutangaza Ufalme licha ya mnyanyaso hufanya tutambuliwe na watu, jambo ambalo ni muhimu kwa malaika. Andiko la Ufunuo 14:6 lasema: “Nami [mtume Yohana] nikaona malaika mwingine akiruka katika mbingu ya kati, naye alikuwa na habari njema idumuyo milele ili aitangaze kuwa taarifa za mteremo kwa wale wakaao juu ya dunia, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” Naam, tunategemezwa na malaika katika huduma yetu—kazi yetu ya kuvuna!—Waebrania 1:13, 14.

“Vitu vya Kuchukiwa”

4, 5. (a) Yesu aliwapa wanafunzi wake onyo gani? (b) Kwa nini watumishi wa Mungu wa leo ni “vitu vya kuchukiwa”?

4 Mitume wa Yesu walipotumwa kuwa wavunaji, walitii agizo lake la kuwa “wenye hadhari kama nyoka na bado kuwa wasio na hatia kama njiwa.” Yesu aliongezea kusema: “Jilindeni dhidi ya watu; kwa maana watawakabidhi nyinyi kwenye mahakama za mtaa, nao watawapiga nyinyi mijeledi katika masinagogi yao. Naam, mtaburutwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa. . . . Nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu; lakini yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Mathayo 10:16-22.

5 Leo sisi ni “vitu vya kuchukiwa” kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu,” Shetani Ibilisi, ambaye ni adui mkuu wa Mungu na watu Wake. (1 Yohana 5:19) Ingawa adui zetu huona mafanikio yetu ya kiroho wao hawakubali kwamba mafanikio hayo yametokana na Yehova. Wapinzani huona jinsi tunavyofurahia kazi ya kuvuna. Wao hustaajabu kuona jinsi tulivyo na umoja! Huenda wakakiri shingo upande kwamba tuna umoja wanaposafiri nchi nyingine na kuona kwamba kazi ile Mashahidi wa Yehova wanayofanya huko ndiyo ileile wanayofanya nchini mwao. Bila shaka, tunajua kwamba katika wakati ufaao, hata adui zetu watamtambua Yehova, ambaye ndiye mtegemezaji wetu na chanzo cha umoja wetu.—Ezekieli 38:10-12, 23.

6. Tuna uhakikisho gani tunaposhiriki katika kazi ya kuvuna, lakini ni swali gani linalozuka?

6 Bwana-mkubwa wa mavuno amempa Mwana wake, Yesu Kristo, “mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia.” (Mathayo 28:18) Hivyo, Yehova humtumia Yesu kuelekeza kazi ya kuvuna hapa duniani kupitia malaika wa mbinguni na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye ametiwa mafuta. (Mathayo 24:45-47; Ufunuo 14:6, 7) Lakini tunawezaje kukabili upinzani wa adui zetu na bado tudumishe furaha yetu tunapoendelea na kazi ya kuvuna?

7. Yatupasa kujitahidi kudumisha mtazamo gani tunapopingwa au kunyanyaswa?

7 Tunapokabili upinzani au hata mnyanyaso wa moja kwa moja, acheni tutafute msaada wa Mungu ili tudumishe mtazamo kama wa Paulo. Aliandika: “Tunapotukanwa, twabariki; tunaponyanyaswa, twahimili; tunapoharibiwa sifa, twasihi sana.” (1 Wakorintho 4:12, 13) Mara kwa mara mtazamo huo pamoja na huduma yetu ya hadharani tunayofanya kwa busara, hubadili mtazamo wa wapinzani.

8. Unapata uhakikisho gani kutokana na maneno ya Yesu kwenye Mathayo 10:28?

8 Hata tisho la kifo halipunguzi bidii yetu tukiwa wavunaji. Tunatangaza kwa ujasiri ujumbe wa Ufalme waziwazi kadiri iwezekanavyo. Nasi hupata uhakikisho wenye kutia moyo kutokana na maneno haya ya Yesu: “Msiwe wenye kuwahofu wale wauuao mwili lakini hawawezi kuiua nafsi; lakini badala ya hivyo mhofuni yeye awezaye kuangamiza vyote viwili nafsi na mwili katika Gehena.” (Mathayo 10:28) Tunajua kwamba Baba yetu wa mbinguni ndiye Mpaji wa uhai. Yeye huwathawabisha wale wanaodumisha uaminifu-maadili kwake na kuendelea kuvuna kwa uaminifu.

Ujumbe Wenye Kuokoa Uhai

9. Watu wengine waliyaonaje maneno ya Ezekieli, na hali ikoje leo?

9 Nabii Ezekieli alipotangaza kwa ujasiri ujumbe wa Yehova kwa “mataifa wanaoasi,” yaani, falme za Israeli na Yuda, watu fulani walipendezwa na yale aliyosema. (Ezekieli 2:3) “Tazama,” Yehova akasema, “wewe umekuwa kwao kama wimbo mzuri sana, wa mtu mwenye sauti ipendezayo, awezaye kupiga kinanda vizuri.” (Ezekieli 33:32) Ingawa walipendezwa na maneno ya Ezekieli, walishindwa kutenda kupatana nayo. Hali ikoje leo? Wakati watiwa-mafuta na wenzao wanapotangaza ujumbe wa Yehova kwa ujasiri, wengine hupenda kusikia juu ya baraka za Ufalme, lakini hawaitikii kwa uthamini, wawe wanafunzi, na kujiunga na kazi ya kuvuna.

10, 11. Katika nusu ya kwanza ya karne ya 20, ni nini kilichofanywa ili kutangaza ujumbe wetu wenye kuokoa uhai, na matokeo yalikuwa nini?

10 Kwa upande mwingine, wengine wameitikia ifaavyo kazi ya kuvuna na wameshiriki kutangaza ujumbe wa Mungu. Kwa mfano, wakati wa mfululizo wa mikusanyiko ya Kikristo iliyoanza mwaka wa 1922 hadi 1928, ujumbe wa hukumu juu ya mfumo wa mambo wa Shetani ulio mwovu ulitangazwa waziwazi. Vituo vya redio vilitangaza hukumu hizo zilizotolewa kwenye makusanyiko. Baadaye, watu wa Mungu waligawanya mamilioni ya nakala zenye ujumbe huo.

11 Mwishoni mwa miaka ya 1930, kazi ya kutoa ushahidi ilianza kufanywa kwa njia nyingine—maandamano ya kutangaza habari. Mwanzoni, watu wa Yehova walivaa mabango yaliyotangaza hotuba za watu wote. Baadaye walibeba mabango yakiwa na maneno kama “Dini ni mtego na hila” na “Mtumikie Mungu na Kristo Mfalme.” Walipoandamana barabarani, walivutia wapita-njia. ‘Jambo hilo lilifanya Mashahidi wa Yehova wajulikane sana na kuwafanya wawe jasiri,’ akaeleza ndugu mmoja ambaye alishiriki kwa ukawaida katika kazi hiyo kwenye barabara zenye watu wengi za London, Uingereza.

12. Mbali na ujumbe wa hukumu ya Mungu, tumekazia nini katika huduma yetu, na ni nani ambao sasa wameungana kuhubiri habari njema?

12 Tunapotangaza ujumbe wa hukumu ya Mungu, sisi pia hukazia baraka zilizoahidiwa ambazo ni sehemu ya ujumbe wa Ufalme. Kutoa ushahidi kwa ujasiri ulimwenguni hutusaidia kutafuta wanaostahili. (Mathayo 10:11) Wengi wa mabaki ya watiwa-mafuta waliitikia wito wa kuvuna katika miaka ya 1920 na 1930. Kisha kwenye mkusanyiko wa mwaka wa 1935, habari nzuri zilitolewa kuhusu baraka ambazo “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” watapata katika paradiso duniani wakati ujao. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Wamesikiliza ujumbe wa hukumu ya Mungu na wameungana na watiwa-mafuta katika kuhubiri habari njema zenye kuokoa uhai.

13, 14. (a) Tunaweza kupata faraja gani kutokana na Zaburi 126:5, 6? (b) Tukiendelea kupanda na kutia maji matokeo yatakuwa nini?

13 Watu wanaofanya kazi ya Mungu ya kuvuna, na hasa wale wanaonyanyaswa, wanapata faraja kubwa kutokana na maneno haya ya Zaburi 126:5, 6: “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha. Ingawa mtu anakwenda zake akilia, azichukuapo mbegu za kupanda. Hakika atarudi kwa kelele za furaha, aichukuapo miganda yake.” Maneno ya mtunga-zaburi kuhusu kupanda na kuvuna yanaonyesha jinsi Yehova alivyowajali na kuwabariki mabaki ambao walirudi kutoka utekwani Babiloni ya kale. Walifurahia sana kuwekwa huru, lakini huenda walilia walipopanda mbegu kwenye ardhi iliyokuwa ukiwa ambayo haikuwa imelimwa kwa muda wa miaka 70 walipokuwa uhamishoni. Hata hivyo, wale walioendelea na kazi ya kupanda na kujenga walipata matokeo na uradhi.

14 Huenda tukalia tunapojaribiwa au wakati sisi au waamini wenzetu wanapoteseka kwa sababu ya uadilifu. (1 Petro 3:14) Huenda mwanzoni kazi yetu ya kuvuna isiwe rahisi kwa sababu inaweza kuonekana kana kwamba jitihada zetu katika huduma hazina matokeo. Lakini tukiendelea kupanda na kutia maji, mara nyingi Mungu atakuza kwa kadiri tusiyotarajia. (1 Wakorintho 3:6) Jambo hilo linadhihirishwa na matokeo ya ugawanyaji wetu wa Biblia na vichapo vinavyotegemea Maandiko.

15. Toa mfano wa manufaa ya vichapo vya Kikristo katika kazi ya kuvuna.

15 Fikiria mfano wa mwanamume aitwaye Jim. Mamake alipokufa, alipata miongoni mwa vitu vyake nakala ya kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? * Alikisoma kwa makini. Alipozungumza na Shahidi mmoja aliyekutana naye barabarani, Jim alikubali Shahidi huyo amtembelee na funzo la Biblia likaanzishwa. Jim alifanya maendeleo ya kiroho haraka, akajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Aliwaambia watu wengine katika familia yake mambo aliyokuwa amejifunza. Hivyo, dada yake na ndugu yake wakawa Mashahidi wa Yehova, na baadaye Jim akapata pendeleo la kujitolea kutumikia wakati wote kwenye Betheli huko London.

Wadumisha Furaha Licha ya Mnyanyaso

16. (a) Kwa nini tumefanikiwa katika kazi ya kuvuna? (b) Yesu alitoa onyo gani kuhusu matokeo ya habari njema, lakini sisi huzungumza na watu tukiwa na mtazamo gani?

16 Kwa nini kumekuwa na mafanikio hayo katika kazi ya kuvuna? Kwa sababu Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao wametii maagizo ya Yesu: “Lile niwaambialo nyinyi katika giza, lisemeni katika nuru; na lile msikialo lanong’onwa, lihubirini kutoka paa za nyumba.” (Mathayo 10:27) Hata hivyo, tunaweza kutarajia magumu, kwa kuwa Yesu alionya: “Ndugu atakabidhi ndugu kwenye kifo, na baba mtoto wake, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na kufanya wauawe.” Yesu aliendelea kusema: “Msifikiri nilikuja kuweka amani juu ya dunia; nilikuja kuweka, si amani, bali upanga.” (Mathayo 10:21, 34) Yesu hakuwa na nia ya kutenganisha familia kimakusudi. Lakini nyakati nyingine habari njema zingetenganisha familia. Ndivyo ilivyo kwa watumishi wa Mungu leo. Tunapotembelea familia, nia yetu si kuzitenganisha. Tunatamani kila mtu akubali habari njema. Kwa hiyo, tunajaribu kuzungumza na kila mshiriki wa familia kwa njia ya fadhili na ya huruma na hilo hufanya ujumbe wetu uvutie wale ‘walio na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.’—Matendo 13:48.

17. Wale wanaouunga mkono enzi kuu ya Mungu wanakuwaje tofauti, na tuna mfano gani wa jambo hilo?

17 Ujumbe wa Ufalme umewafanya wale wanaounga mkono enzi kuu ya Mungu wawe tofauti. Kwa mfano, fikiria jinsi waabudu wenzetu walivyojitokeza kuwa tofauti kwa sababu ‘walilipa Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu’ wakati wa Utawala wa Nazi huko Ujerumani. (Luka 20:25) Tofauti na viongozi wa kidini na wafuasi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ambao ni Wakristo kwa jina tu, watumishi wa Yehova walikuwa thabiti, wakakataa kuvunja kanuni za Biblia. (Isaya 2:4; Mathayo 4:10; Yohana 17:16) Profesa Christine King, mwandishi wa kitabu The Nazi State and the New Religions, alisema: ‘Utawala wa [Nazi] ulishindwa na Mashahidi pekee, kwa kuwa ingawa utawala huo uliwaua kwa wingi, wao waliendelea na kazi yao ya kutoa ushahidi na mnamo Mei 1945, Mashahidi wa Yehova walikuwa bado wanaendelea na kazi yao ilhali Utawala wa Nazi ulikuwa umetoweka.’

18. Watu wa Yehova huonyesha mtazamo gani licha ya mnyanyaso?

18 Mtazamo ambao huonyeshwa na watu wa Yehova wanapokabili mnyanyaso ni muhimu sana. Ingawa huenda wenye mamlaka katika ulimwengu wakavutiwa na imani yetu, wao hustaajabu kwamba sisi hatuna chuki wala uchungu. Kwa mfano, mara nyingi Mashahidi waliookoka yale Maangamizi Makubwa ya Nazi huonyesha furaha na uradhi wanapokumbuka mambo yaliyowapata. Wanajua kwamba Yehova aliwapa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Baadhi yetu ambao ni watiwa-mafuta wana uhakika kwamba ‘majina yao yameandikwa mbinguni.’ (Luka 10:20) Uvumilivu wao hutokeza tumaini ambalo haliongozi kwenye kukata tamaa, nao wavunaji waaminifu wanaotarajia kuishi duniani wana uhakika huo.—Waroma 5:4, 5.

Endelea na Kazi ya Kuvuna

19. Ni njia zipi zenye matokeo ambazo zimetumiwa katika huduma ya Kikristo?

19 Hatujui ni kwa muda mrefu kadiri gani Yehova ataturuhusu tufanye kazi ya uvunaji wa mfano. Kwa sasa, yatupasa kukumbuka kwamba wavunaji wana njia mahususi za kufanya kazi yao. Vivyo hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba uaminifu wetu katika kutumia njia za kuhubiri zilizojaribiwa utakuwa na matokeo. Paulo aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Nawasihi sana nyinyi, iweni waigaji wangu.” (1 Wakorintho 4:16) Paulo alipokutana na wazee wa Efeso huko Mileto, aliwakumbusha kwamba yeye hakuepuka kuwafundisha “hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.” (Matendo 20:20, 21) Timotheo, mwandamani wa Paulo, alijifunza njia za mtume huyo za kufundisha kwa hiyo angeweza kuwafunza Wakorintho njia hizo. (1 Wakorintho 4:17) Mungu alibariki njia za Paulo za kufundisha, kama vile atakavyobariki uvumilivu wetu katika kuhubiri habari njema hadharani kutoka nyumba hadi nyumba, kwenye ziara za kurudia, kwenye mafunzo ya Biblia, na popote pale watu wanapoweza kupatikana.—Matendo 17:17.

20. Yesu alionyeshaje kwamba uvunaji mkubwa wa kiroho ulikuwa karibu, na jambo hilo limethibitikaje kuwa kweli katika miaka ya karibuni?

20 Baada ya kumtolea ushahidi mwanamke Msamaria karibu na Sikari mwaka wa 30 W.K., Yesu alizungumzia uvunaji wa kiroho. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Inueni macho yenu mtazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa. Tayari mvunaji anapokea mshahara na kukusanya matunda kwa ajili ya uhai udumuo milele, ili mpanzi na mvunaji wapate kushangilia pamoja.” (Yohana 4:34-36) Labda Yesu alikuwa tayari ameona matokeo ya mazungumzo yake na mwanamke Msamaria, kwa kuwa kutokana na ushuhuda wa mwanamke huyo, wengi walimwamini Yesu. (Yohana 4:39) Katika miaka ya karibuni, nchi mbalimbali zimeondolea Mashahidi wa Yehova vizuizi au kuhalalisha kazi yao, hivyo kutokeza maeneo mapya ya kuvunwa. Matokeo yamekuwa kwamba uvunaji mkubwa wa kiroho unaendelea. Naam, ulimwenguni pote tunapata baraka nyingi tunapoendelea kwa furaha na uvunaji wa kiroho.

21. Kwa nini tuna sababu ya kuendelea tukiwa wavunaji wenye furaha?

21 Mavuno yanapokuwa tayari, lazima wafanyakazi wavune kwa uharaka. Lazima wafanye kazi bila kukawia. Leo, tunahitaji kufanya kazi kwa bidii na kwa uharaka kwa sababu tunaishi katika “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Naam, tunakabili majaribu, lakini leo kuna uvunaji mkubwa wa waabudu wa Yehova kuliko wakati mwingine wowote. Kwa hiyo, hii ni siku ya kushangilia. (Isaya 9:3) Basi, tukiwa wavunaji wenye furaha, acheni tuendelee na kazi ya kuvuna!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kilichochapishwa na kugawanywa na Mashahidi wa Yehova.

Unaweza Kujibuje?

Bwana-mkubwa wa mavuno amejibuje ombi la kupata wafanyakazi wengi zaidi?

Ingawa sisi ni “vitu vya kuchukiwa,” tunadumisha mtazamo gani?

Kwa nini sisi tu wenye furaha licha ya mnyanyaso?

Kwa nini tunapaswa kuendelea na kazi ya kuvuna kwa uharaka?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Wale wanaoshiriki uvunaji wa kiroho wanaungwa mkono na malaika

[Picha katika ukurasa wa 18]

Maandamano ya kutangaza habari yaliwavuta wengi kwenye ujumbe wa Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tunapanda na kutia maji, lakini Mungu hukuza