Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iweni Wavunaji Wenye Furaha!

Iweni Wavunaji Wenye Furaha!

Iweni Wavunaji Wenye Furaha!

“Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.”—MATHAYO 9:37, 38.

1. Ni nini hutusaidia kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu?

TUNAPOKUMBUKA siku tulipobatizwa tukawa watumishi wa Yehova, iwe tulibatizwa miaka mingi au miaka michache iliyopita, huenda tukaona kana kwamba tulibatizwa juzi tu. Baada ya ubatizo, kumsifu Yehova kukawa jambo muhimu zaidi katika maisha yetu tuliyoweka wakfu kwake. Hangaiko letu kuu likawa kumtumikia Yehova kwa furaha huku tukinunua kabisa wakati unaofaa ili kuwasaidia wengine wasikie na ikiwezekana wakubali ujumbe wa Ufalme. (Waefeso 5:15, 16) Hata sasa, sisi huona wakati ukipita haraka sana tunapokuwa na shughuli nyingi, ‘tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Wakorintho 15:58) Ingawa tunapata matatizo, furaha yetu katika kufanya mapenzi ya Yehova hutuchochea kuendelea kufanya kazi ya Bwana.—Nehemia 8:10.

2. Ni nini kinachochangia furaha tunayopata katika kazi ya uvunaji wa mfano?

2 Tukiwa Wakristo, tunashiriki katika kazi ya uvunaji wa mfano. Yesu Kristo alifananisha kukusanywa kwa watu kwa ajili ya uhai udumuo milele na kazi ya kuvuna. (Yohana 4:35-38) Kwa kuwa tunashiriki kazi hiyo ya kuvuna, itatia moyo kuchunguza furaha waliyopata Wakristo wa mapema katika kazi ya kuvuna. Tutachunguza mambo matatu yanayochangia furaha ambayo sisi hupata katika kazi ya kuvuna leo. Mambo hayo ni (1) ujumbe wetu wa tumaini, (2) jinsi ya kufanikiwa katika utafutaji wetu, na (3) jinsi ya kuwa na mtazamo wa kudumisha amani katika kazi ya kuvuna.

Waliotumwa Kuwa Wavunaji

3. Wafuasi wa mapema wa Yesu walipata furaha katika njia gani?

3 Maisha ya wavunaji wa mapema—hasa mitume 11 wa Yesu waliokuwa waaminifu—yalibadilika sana mwaka wa 33 W.K., siku walipoenda mlimani huko Galilaya kuonana na Kristo aliyekuwa amefufuliwa. (Mathayo 28:16) Huenda “zaidi ya ndugu mia tano” walikuwepo pindi hiyo. (1 Wakorintho 15:6) Walikuwa wangali wanakumbuka kazi ambayo Yesu aliwaagiza wafanye. Aliwaambia: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Licha ya mnyanyaso mkali, walipata furaha nyingi katika kazi ya kuvuna walipoona makutaniko ya wafuasi wa Kristo yakianzishwa mahali kwingi. Baada ya muda, ‘habari njema ikahubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’—Wakolosai 1:23; Matendo 1:8; 16:5.

4. Wanafunzi wa Kristo walitumwa chini ya hali gani?

4 Awali katika huduma yake huko Galilaya, Yesu alikuwa amewaita mitume wake 12 na kuwatuma hasa wakatangaze hivi: “Ufalme wa mbingu umekaribia.” (Mathayo 10:1-7) Yeye mwenyewe ‘aliondoka ili kutalii majiji na vijiji vyote vya Galilaya, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme na kuponya kila namna ya maradhi na kila namna ya udhaifu.’ Yesu alihurumia umati “kwa sababu ulikuwa umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:35, 36) Kisha akiwa ameguswa moyo sana akawaambia wanafunzi wake: “Ndiyo, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno [Yehova Mungu] atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:37, 38) Miezi sita tu kabla ya kumaliza huduma yake duniani, Yesu aliona kulikuwa na uhitaji wa kuwa na wavunaji huko Yudea pia. (Luka 10:2) Katika pindi zote mbili, aliwatuma wafuasi wake wafanye kazi ya kuvuna.—Mathayo 10:5; Luka 10:3.

Ujumbe Wetu wa Tumaini

5. Sisi hutangaza ujumbe wa aina gani?

5 Tukiwa watumishi wa Yehova wa siku hizi, sisi huitikia kwa furaha mwito wa kuwa wavunaji. Jambo moja ambalo huchangia sana furaha yetu ni kwamba sisi huwapelekea ujumbe wa tumaini wale waliokata tamaa na kushuka moyo. Kama wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza, tuna pendeleo lililoje kutangaza habari njema—ujumbe wa kweli wenye tumaini—kwa wale ambao ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji’!

6. Mitume walifanya kazi gani katika karne ya kwanza?

6 Kufikia katikati ya karne ya kwanza, mtume Paulo alikuwa na shughuli nyingi za kuhubiri habari njema. Hapana shaka alifanikiwa katika kazi yake ya kuvuna, kwa kuwa alipowaandikia Wakristo wa Korintho yapata mwaka wa 55 W.K., alisema: “Nawajulisha nyinyi, akina ndugu, habari njema niliyowatangazia, mliyoipokea pia, ambayo katika hiyo mwasimama pia.” (1 Wakorintho 15:1) Mitume na Wakristo wengine wa mapema walikuwa wavunaji wenye bidii. Ingawa Biblia haituambii ni mitume wangapi waliookoka matukio yenye kuogofya yaliyomalizika kwa kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., tunajua kwamba mtume Yohana alikuwa bado anahubiri miaka 25 hivi baadaye.—Ufunuo 1:9.

7, 8. Ni ujumbe gani wa tumaini ambao watumishi wa Yehova wamekuwa wakitangaza kwa uharaka zaidi sasa kuliko wakati mwingineo wowote?

7 Kisha kwa karne nyingi, makasisi waasi-imani wa Jumuiya ya Wakristo ambao ndio “mtu wa uasi-sheria” wakawa ndio wenye kuongoza. (2 Wathesalonike 2:3) Hata hivyo, mwishoni mwa karne ya 19, wale waliojitahidi kuishi kupatana na mafundisho ya Ukristo wa awali, walianza kutangaza ujumbe wa tumaini, ujumbe wa Ufalme. Kwa kweli, tangu toleo lake la kwanza (Julai 1879), gazeti hili limekuwa na vichwa ambavyo vimetia ndani maneno, “Unaotangaza Kuwapo kwa Kristo,” “Unaotangaza Ufalme wa Kristo,” au “Unaotangaza Ufalme wa Yehova.”

8 Ufalme wa mbinguni wa Mungu ulisimamishwa mwaka wa 1914 mikononi mwa Yesu Kristo, na sasa tunatangaza ujumbe wa tumaini kwa uharaka zaidi kuliko wakati mwingineo wowote. Kwa nini? Kwa sababu mojawapo ya mambo mazuri yatakayotimizwa na utawala wa Ufalme huo wa Mungu ni kuondolewa hivi karibuni kwa mfumo huu mwovu. (Danieli 2:44) Je, kunaweza kuwa na ujumbe mwingine bora zaidi? Tunapata furaha nyingi sana kwa kushiriki kutangaza Ufalme kabla ya “dhiki kubwa” kuanza.—Mathayo 24:21; Marko 13:10.

Jinsi ya Kufanikiwa Katika Utafutaji

9. Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo gani, nao watu waliitikiaje ujumbe wa Ufalme?

9 Jambo jingine ambalo huchangia furaha yetu tukiwa wavunaji ni mafanikio tunayopata katika kutafuta wale wanaokuwa wanafunzi na kujiunga nasi katika kazi ya kuvuna. Katika mwaka wa 31-32 W.K., Yesu aliwaagiza wanafunzi wake hivi: “Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mwingiamo, tafuteni kabisa ni nani humo anayestahili.” (Mathayo 10:11) Kama ionyeshwavyo na itikio lao kwa ujumbe wa Ufalme, si watu wote waliostahili. Hata hivyo, wanafunzi wa Yesu walihubiri kwa bidii habari njema kokote ambako watu wangepatikana.

10. Paulo alitafutaje wale wanaostahili?

10 Baada ya kifo na ufufuo wa Yesu, kazi ya kutafuta wanaostahili iliendelea kwa bidii. Paulo alisababu na Wayahudi katika masinagogi yao na pia watu waliokuwa sokoni huko Athene. Alipotoa ushahidi kwenye Areopago katika jiji hilo la Ugiriki, “wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini, miongoni mwao pia wakiwamo Dionisio, hakimu wa mahakama ya Areopago, na mwanamke mmoja aitwaye jina Damarisi, na wengine mbali na hao.” Kokote ambako Paulo alienda, aliweka kielelezo kizuri katika kuhubiri “hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.”—Matendo 17:17, 34; 20:20.

11. Ni njia zipi za kufanya huduma zilizotumiwa miaka iliyopita?

11 Katika miongo ya mwisho ya karne ya 19, Wakristo watiwa-mafuta walitafuta kwa ujasiri wale wanaostahili. Katika makala yenye kichwa, “Walitiwa Mafuta Kuhubiri,” gazeti la Kiingereza Zion’s Watch Tower la Julai/Agosti 1881 lilisema: “Habari njema zinahubiriwa ‘wapole’ walio tayari na wanaoweza kusikiliza ili kutokeza miongoni mwao watawala wenzi wa Kristo ambao ni mwili wake.” Mara nyingi watu waliofanya kazi ya Mungu ya kuvuna waliwafikia watu waliokuwa wakitoka katika makanisa yao na kuwapa trakti zenye ujumbe wa Kimaandiko uliokusudiwa kuamsha upendezi wa wale wanaostahili. Baada ya kuchunguza kwa makini matokeo mazuri ya kutoa ushahidi kwa njia hiyo, gazeti la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1903, liliwasihi wavunaji wagawanye trakti “kutoka nyumba hadi nyumba, Jumapili alasiri.”

12. Tumefanyaje kazi yetu ya kuhubiri iwe na matokeo mazuri zaidi? Toa mfano.

12 Katika miaka ya karibuni, tumepanua huduma yetu kwa kuzungumza na watu mahali kwingineko badala ya nyumbani kwao. Njia hiyo imekuwa na matokeo mazuri katika nchi ambako kwa sababu ya hali za kiuchumi na kufuatilia mambo ya starehe, watu hawapatikani nyumbani tunapowatembelea. Wakati Mashahidi wawili kutoka Uingereza walipoona kwamba wageni walikuwa wakiondoka kwa ukawaida kwa basi baada ya kujifurahisha kwa siku moja kwenye ufuo wa bahari, walipiga moyo konde, wakapanda basi hizo na kuwatolea wasafiri magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Waligawanya nakala 229 za magazeti hayo kwa muda wa mwezi mmoja. Wanaripoti hivi: “Kwa sababu tunajua kwamba Yehova yu pamoja nasi daima, sisi hatuogopi kutoa ushahidi kwenye ufuo wa bahari, maeneo ya biashara, au maeneo mengineyo magumu.” Walipata watu waliokubali kupelekewa magazeti kwa ukawaida, wakaanzisha funzo la Biblia, na wote wawili wakatumikia wakiwa mapainia-wasaidizi.

13. Ni marekebisho gani katika huduma yetu yanayohitajika katika maeneo fulani?

13 Tunapoendelea kutafuta wanaostahili, huenda tukahitaji kuchunguza huduma yetu kwa makini katika maeneo fulani. Imekuwa kawaida kwa Mashahidi wengi kushiriki mahubiri ya kutoka nyumba hadi nyumba Jumapili asubuhi. Lakini wameona kwamba hawapati matokeo sana katika maeneo fulani wanapotembelea watu Jumapili asubuhi kwa sababu huenda wenye nyumba wakawa wanalala. Mashahidi wengi wamerekebisha ratiba yao na sasa wanatafuta watu baadaye mchana, labda baada ya mikutano ya Kikristo. Na utafutaji huo umefanikiwa kwelikweli. Mwaka uliopita idadi ya watangazaji wa Ufalme iliongezeka kwa asilimia 2.3. Jambo hilo humtukuza Bwana-mkubwa wa mavuno na hutufurahisha.

Dumisheni Amani Katika Kazi ya Kuvuna

14. Tunapeleka ujumbe wetu tukiwa na mtazamo gani, na kwa nini?

14 Sababu nyingine inayofanya tuwe wenye furaha inahusiana na mtazamo wa kudumisha amani tunapofanya kazi ya kuvuna. “Mnapokuwa mkiingia ndani ya hiyo nyumba,” Yesu akasema, “salimuni hao watu wa nyumbani; na ikiwa hiyo nyumba inastahili, acheni amani mwitakiayo ije juu yayo.” (Mathayo 10:12, 13) Salamu hiyo katika Kiebrania na pia katika Kigiriki cha Biblia humaanisha ‘Nakutakia mema.’ Mtazamo huo ndio hutuongoza tunapowahubiria watu habari njema. Tunatumaini kwamba wataitikia ifaavyo ujumbe wa Ufalme. Wale wanaoitikia wana taraja la kupatanishwa na Mungu wanapotubu dhambi zao, kugeuka na kufanya mapenzi yake. Amani pamoja na Mungu huongoza kwenye uhai udumuo milele.—Yohana 17:3; Matendo 3:19; 13:38, 48; 2 Wakorintho 5:18-20.

15. Tunawezaje kudumisha mtazamo wa amani hata watu wasipoitikia ifaavyo tunapohubiri?

15 Tunaweza kudumishaje amani yetu hata watu wasipoitikia ifaavyo? Yesu aliagiza: “Ikiwa [nyumba hiyo] haistahili, acheni amani itokayo kwenu irudi juu yenu.” (Mathayo 10:13) Simulizi la Luka kuhusu kutumwa kwa wanafunzi 70 latia ndani maneno haya ya Yesu: “Ikiwa rafiki wa amani yumo, amani yenu itatulia juu yake. Lakini ikiwa hayumo, itawarudia nyinyi.” (Luka 10:6) Tunapozungumza na watu habari njema, tunafanya hivyo kwa njia ifaayo tukiwa wachangamfu na wenye amani. Ikiwa mwenye nyumba anaonyesha ubaridi, analalamika, au anasema jambo fulani baya, basi tutaacha ujumbe wetu wa amani ‘uturudie.’ Lakini mambo hayo hayatukoseshi amani, ambayo ni mojawapo ya matunda ya roho takatifu ya Yehova.—Wagalatia 5:22, 23.

Mradi Mzuri kwa Wavunaji

16, 17. (a) Tunakuwa na mradi gani tunapofanya ziara za kurudia? (b) Tunaweza kuwasaidiaje wale walio na maswali ya Biblia?

16 Tukiwa wavunaji tunafurahi kushiriki kukusanya watu kwa ajili ya uhai udumuo milele. Nasi hufurahi kama nini wakati mtu tunayehubiria anapoitikia ifaavyo na kutaka kujifunza mengi zaidi, na kuwa “rafiki wa amani”! Labda ana maswali mengi ya Biblia na tunaona kwamba haiwezekani kuyajibu yote katika ziara moja. Kwa kuwa huenda isifae kukaa sana wakati wa ziara ya kwanza, tunaweza kufanya nini? Tunaweza kuweka mradi kama ule uliopendekezwa miaka 60 iliyopita.

17 “Mashahidi wote wa Yehova wapaswa kuwa tayari kuongoza mafunzo ya kigezo ya Biblia.” Maneno hayo yalikuwa katika kijitabu cha tatu katika mfululizo wa vijitabu viitwavyo Funzo la Kigezo (Model Study) vilivyochapishwa kuanzia mwaka wa 1937 hadi 1941. Kijitabu hicho kiliendelea kusema: “Watangazaji wote [wa Ufalme] wapaswa kuwa na bidii kuwasaidia katika kila njia iwezekanayo watu wenye nia njema wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme. Wapaswa kuwarudia watu hao na kujibu maswali mbalimbali . . . , kisha kuanzisha funzo la kigezo . . . haraka iwezekanavyo.” Naam, tunafanya ziara za kurudia tukiwa na mradi wa kuanzisha funzo la Biblia nyumbani na kuliongoza kwa ukawaida. * Kuwa wenye urafiki na kumhangaikia kwa upendo mtu anayependezwa hutuchochea kutayarisha vema na kuongoza funzo kwa mafanikio.

18. Tunaweza kuwasaidiaje wapya wawe wanafunzi wa Yesu Kristo?

18 Kwa msaada wa kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele na broshua kama vile Mungu Anataka Tufanye Nini?, tunaweza kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye matokeo na hivyo kushiriki kuwasaidia waliopendezwa karibuni kuwa wanafunzi. Tunapojitahidi kumwiga Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo, yaelekea wanafunzi hao wa Biblia watajifunza pia kutokana na amani na furaha yetu, unyofu wetu, na heshima yetu kwa viwango na miongozo ya Yehova. Tunapowasaidia wapya kupata majibu ya maswali yao, acheni tufanye yote tuwezayo kuwafunza jinsi ya kujibu wale wanaowauliza maswali. (2 Timotheo 2:1, 2; 1 Petro 2:21) Tukiwa wavunaji wa mfano, hapana shaka tunaweza kuwa wenye furaha kwamba mwaka uliopita wa utumishi, wastani wa mafunzo ya Biblia ya nyumbani 4,766,631 yaliongozwa ulimwenguni pote. Tunafurahi hasa iwapo sisi binafsi tu miongoni mwa wavunaji wanaoshiriki kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani.

Endelea Kufurahia Kazi ya Kuvuna

19. Kwa nini kulikuwa na sababu nzuri za kufurahia kazi ya kuvuna wakati wa huduma ya Yesu na muda mfupi baadaye?

19 Kulikuwa na sababu nzuri za kufurahia kazi ya kuvuna wakati wa huduma ya Yesu na muda mfupi baadaye. Wakati huo wengi waliitikia ifaavyo habari njema. Walifurahi hata zaidi wakati wa Pentekoste 33 W.K., kwa kuwa watu wapatao 3,000 walikubali mwelekezo wa Petro, wakapokea roho takatifu ya Mungu, na kuwa sehemu ya taifa la Mungu la Israeli wa kiroho. Naam, idadi yao iliendelea kuongezeka, na furaha ikazidi kuwa nyingi kwa kuwa ‘Yehova aliendelea kuongeza kwao kila siku wale wenye kuokolewa.’—Matendo 2:37-41, 46, 47; Wagalatia 6:16; 1 Petro 2:9.

20. Ni nini ambacho hutuletea furaha nyingi katika kazi yetu ya kuvuna?

20 Wakati huo, unabii huu wa Isaya ulikuwa unatimia: “[Ewe Yehova] umeliongeza taifa, umezidisha furaha yao; wanafurahi mbele zako, kama furaha ya wakati wa mavuno, kama watu wafurahivyo wagawanyapo nyara.” (Isaya 9:3) Ingawa leo tunaona kwamba taifa hilo la watiwa-mafuta ‘limeongezwa’ na karibu limekamilika kabisa, tunafurahi sana tunapoona idadi ya wavunaji wengine ikiongezeka mwaka baada ya mwaka.—Zaburi 4:7; Zekaria 8:23; Yohana 10:16.

21. Tutazungumzia nini katika makala ifuatayo?

21 Bila shaka tuna sababu nzuri za kuendelea kufurahia kazi ya kuvuna. Ujumbe wetu wa tumaini, kutafuta wanaostahili, na mtazamo wetu wa kudumisha amani, hutuletea furaha tukiwa wavunaji. Hata hivyo, mambo hayo huwachochea wengi watende isivyofaa. Mtume Yohana alitendwa isivyofaa. Alifungwa kwenye kisiwa cha Patmosi “kwa ajili ya kusema juu ya Mungu na kutoa ushahidi kuhusu Yesu.” (Ufunuo 1:9) Basi, tunaweza kudumishaje furaha tunaponyanyaswa na kupingwa? Ni nini kitakachotusaidia kukabiliana na mtazamo wa wengi tunaohubiria sasa ambao unazidi kuwa mgumu? Makala yetu ifuatayo inatoa msaada wa Kimaandiko katika kujibu maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kwanza, mafunzo yalipangwa katika sehemu ambako vikundi vya watu wanaopendezwa wangeweza kukusanywa pamoja. Hata hivyo, muda si muda mafunzo pia yalifanywa na watu mmoja-mmoja au familia—Ona kichapo Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 574, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Unaweza Kujibuje?

• Kazi ya uvunaji wa mfano ni nini?

• Tunatangaza ujumbe wa aina gani?

• Kwa nini kazi yetu ya kutafuta wanafunzi inafanikiwa?

• Tunadumishaje amani katika kazi ya kuvuna?

• Kwa nini tunaendelea kufurahia kazi ya kuvuna?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Kuhubiri katika karne ya 1 na ya 20

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kama Paulo, wavunaji wa siku hizi hujitahidi kuwahubiria watu kila mahali

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tangaza habari njema kwa uchangamfu