Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una Roho Isiyoweza Kufa?

Je, Una Roho Isiyoweza Kufa?

Je, Una Roho Isiyoweza Kufa?

“ANDIKO lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu,” akaandika mtume Paulo. (2 Timotheo 3:16) Naam, Biblia ni kitabu cha kweli kutoka kwa Mungu wa kweli, Yehova.—Zaburi 83:18.

Kwa kuwa Yehova ndiye Muumba wa vitu vyote, kutia ndani wanadamu, yeye ajua vema kinachotupata tunapokufa. (Waebrania 3:4; Ufunuo 4:11) Na katika Neno lake lililopuliziwa, Biblia, ametupa majibu ya kweli na yenye kuridhisha ya maswali kuhusu yanayotupata baada ya kifo.

Roho Ni Nini?

Katika Biblia, maneno ya awali yanayotafsiriwa “roho” humaanisha “pumzi.” Lakini jambo hilo humaanisha mengi zaidi ya tendo la kupumua tu. Kwa mfano, mwandikaji wa Biblia Yakobo, aandika hivi: “Mwili bila roho umekufa.” (Yakobo 2:26) Hivyo, roho ni kani ambayo huutendesha mwili.

Kani hiyo yenye kutendesha haiwezi kuwa tu pumzi, au hewa, inayoingia kwenye mapafu. Kwa nini? Kwa sababu baada ya kuacha kupumua, uhai hubaki kwenye chembe za mwili kwa kipindi kifupi—“kwa dakika chache,” kulingana na The World Book Encyclopedia. Ndiyo sababu, jitihada za kumhuisha mtu wakati huo zaweza kufaulu. Lakini mara tu kani hiyo ya uhai iishapo katika chembe za mwili, jitihada zozote za kumhuisha mtu huwa za bure. Hata pumzi au hewa iwe nyingi kiasi gani, haiwezi kuhuisha hata chembe moja. Basi, roho ni kani ya uhai isiyoonekana—ndiyo huendeleza uhai katika chembe na kumfanya mtu aishi. Kani hiyo ya uhai inaendelezwa na kupumua.—Ayubu 34:14, 15.

Je, roho hiyo hutenda katika wanadamu tu? Biblia hutusaidia kufikia uamuzi sahihi juu ya jambo hili. Sulemani mfalme mwenye hekima alikiri kwamba wanadamu na wanyama “wote wanayo pumzi [“roho,” NW] moja,” na akauliza: “Ni nani ajuaye kama roho ya binadamu huenda juu, na kama roho ya mnyama huenda chini?” (Mhubiri 3:19-21) Kwa hiyo wanyama na vilevile watu wana roho ileile. Hiyo yawezekanaje?

Roho, au kani ya uhai, yaweza kulinganishwa na mkondo wa umeme unaosambaa katika mashine au kifaa fulani. Umeme usioonekana unaweza kufanya mambo mbalimbali, ikitegemea aina ya kifaa kinachoufanya utoe nguvu. Kwa mfano, jiko la umeme laweza kutoa moto, nayo kompyuta itokeze habari fulani, na televisheni itokeze picha na sauti. Lakini, mkondo wa umeme hauwi kamwe na umbo la kifaa unachotendesha. Huo hubaki kuwa kani tu. Vivyo hivyo, kani ya uhai haichukui umbo lolote la viumbe inavyofanya viwe hai. Haina utu wala uwezo wa kufikiri. Wanadamu na wanyama “wanayo pumzi [“roho,” NW] moja.” (Mhubiri 3:19) Kwa hiyo, mtu anapokufa, roho yake haiendelei kuishi mahali pengine ikiwa kiumbe wa roho.

Basi, vipi hali ya wafu? Na ni nini huipata roho mtu anapokufa?

“Utarudi Mavumbini”

Mwanamume wa kwanza Adamu, alipoasi amri ya Mungu kimakusudi, Mungu alimwambia: “Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Adamu alikuwa wapi kabla Yehova hajamuumba? Hakuwa mahali popote! Yaani, hakuwapo. Kwa hiyo, Yehova Mungu alipomwambia Adamu kwamba “angerudi mavumbini,” alimaanisha kwamba Adamu angekufa na kurudi mavumbini. Adamu hangeenda kwenye makao ya kimbingu. Akiwa mfu, Adamu angerudia tena hali ya kutokuwapo. Adhabu hiyo ilikuwa kifo—kukosa uhai—si kuhama kwenda katika makao mengine.—Waroma 6:23.

Vipi wengine waliokufa? Hali ya wafu imefafanuliwa wazi kwenye Mhubiri 9:5, 10, ambapo twasoma: “Wafu hawajui kitu . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima ndani ya kaburi.” (Zaire Swahili Bible) Kwa hiyo, kifo ni hali ya kutokuwapo. Mtunga-zaburi aliandika kwamba mtu anapokufa, “pumzi [“roho,” NW] yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:4.

Ni wazi kwamba, wafu hawaishi. Hawawezi kujua chochote. Hawawezi kukuona, kukusikia, au kuongea nawe. Hawawezi kukusaidia wala kukuumiza. Kwa kweli hupaswi kuhofu wafu. Lakini inakuwaje kwamba roho “hutoka” mtu anapokufa?

Roho ‘Humrudia Mungu’

Biblia husema kwamba, mtu anapokufa ‘roho humrudia Mungu aliyeitoa.’ (Mhubiri 12:7) Je, hilo lamaanisha kwamba roho husafiri angani kihalisi na kwenda kwa Mungu? Sivyo, hasha! Namna ambavyo Biblia hutumia neno “kumrudia” ina maana kwamba roho haihitaji kuhama kihalisi kutoka mahali pamoja hadi pengine. Kwa mfano, Waisraeli wasio waaminifu waliambiwa hivi: “Nirudieni mimi nami nitawarudia ninyi, asema BWANA wa majeshi.” (Malaki 3:7) Ili Waisraeli ‘wamrudie’ Yehova walihitaji kutubu mwenendo wao mbaya na kujipatanisha na njia ya Mungu ya uadilifu. Naye Yehova ‘angewarudia’ Waisraeli kwa kuwakubali watu wake tena. Katika hali zote mbili “kurudia” kulimaanisha mtazamo wala si kuhama kutoka eneo moja kwenda jingine.

Vivyo hivyo, mtu anapokufa hahami kutoka duniani kwenda mbinguni roho yake ‘inapomrudia’ Mungu. Mara tu kani ya uhai imtokapo mtu huyo, ni Mungu peke yake aliye na uwezo wa kumrudishia. Kwa hiyo roho ‘humrudia Mungu’ katika maana ya kwamba tumaini lolote la kuishi wakati ujao la mtu huyo sasa lamtegemea Mungu pekee.

Kwa mfano, fikiria yale ambayo Maandiko husema juu ya kifo cha Yesu Kristo. Mwandikaji wa Injili Luka anasimulia hivi: “Yesu akaita kwa sauti kubwa na kusema: “Baba, ndani ya mikono yako naikabidhi roho yangu.” Alipokuwa amesema hilo, akaisha.” (Luka 23:46) Roho ya Yesu ilipomtoka, hakuwa akielekea mbinguni. Yesu hakufufuliwa mpaka siku ya tatu baada ya kufa na akapaa mbinguni siku 40 baadaye. (Matendo 1:3, 9) Hata hivyo, wakati wa kifo chake, Yesu aliacha roho yake mikononi mwa Baba yake, akitumaini kabisa uwezo wa Yehova wa kumfufua.

Naam, Mungu anaweza kumfufua mtu. (Zaburi 104:30) Hilo ni taraja kubwa kama nini kwetu!

Tumaini Hakika

Biblia husema: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake [Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Yesu Kristo aliahidi kwamba wote walio katika kumbukumbu la Yehova watafufuliwa, au kurudishiwa uhai. Miongoni mwao watakuwa wale ambao walifuatia mwenendo mwadilifu wakiwa watumishi wa Yehova. Lakini mamilioni ya watu wengine wamekufa bila kuonyesha kwamba wangeishi kupatana na viwango vya Mungu vya uadilifu. Labda hawakujua matakwa ya Yehova au walikosa wakati wa kutosha kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. Watu wa aina hiyo pia wako katika kumbukumbu la Mungu nao watafufuliwa, kwa kuwa Biblia husema: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.

Leo, dunia imejaa chuki na ugomvi, jeuri na umwagaji wa damu, uchafuzi na magonjwa. Wafu wakifufuliwa katika dunia kama hii, kwa kweli hawatakuwa na furaha ya kudumu. Lakini Muumba ameahidi kwamba hivi karibuni ataangamiza jamii ya ulimwengu wa sasa ambayo iko chini ya utawala wa Ibilisi. (Mithali 2:21, 22; Danieli 2:44; 1 Yohana 5:19) Jamii yenye uadilifu ya wanadamu—“dunia mpya”—itakuwako hakika.—2 Petro 3:13.

Wakati huo “hakuna mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Hata uchungu wa kifo hautakuwapo, kwa kuwa Mungu “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Kwa kweli hilo ni taraja bora kwa wale walio katika “makaburi ya ukumbusho”!

Yehova atakapoondoa uovu wote duniani, hataharibu waadilifu pamoja na waovu. (Zaburi 37:10, 11; 145:20) “Umati mkubwa” wa watu “kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” wataokoka ile “dhiki kubwa,” ambayo itaharibu ulimwengu mwovu wa sasa. (Ufunuo 7:9-14) Kwa hiyo, kutakuwako umati mkubwa wa kuwakaribisha wale wanaofufuliwa.

Je, watamani kuona wapendwa wako tena? Je, wataka kuishi milele katika Paradiso duniani? Basi lazima utwae ujuzi sahihi kuhusu mapenzi ya Mungu na makusudi yake. (Yohana 17:3) Ni mapenzi ya Yehova kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:3, 4.

[Picha katika ukurasa wa 4]

“U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Roho yaweza kulinganishwa na umeme

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ufufuo utaleta shangwe yenye kudumu