Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Ni Mvumilivu Kweli?

Je, Wewe Ni Mvumilivu Kweli?

Je, Wewe Ni Mvumilivu Kweli?

JE, UMEWAHI kukasirishwa sana na mwenendo usiofaa wa mtu fulani? Je, wewe hutenda kwa haraka wakati marafiki wako wa karibu wanapoathiriwa sana na uvutano mbaya?

Nyakati nyingine hatua ya haraka na thabiti huhitajiwa ili kuzuia dhambi nzito isienee. Kwa mfano, katika karne ya 15 K.W.K., Waisraeli walipokuwa karibu kuchafuliwa na mtazamo wa kutenda kosa kwa ushupavu, mjukuu wa kiume wa Haruni, anayeitwa Finehasi alichukua hatua ya kukata maneno ili kuondoa uovu huo. Yehova Mungu alikubali hatua aliyochukua, kwa kusema hivi: “Finehasi . . . amezigeuza hasira zangu zisiwe juu ya wana wa Israeli, kwa kuwa hakuvumilia ushindani wowote kati yao kunielekea.”—Hesabu 25:1-11, NW.

Finehasi alichukua hatua iliyofaa, ili kuzuia dhambi hiyo isienee. Lakini vipi tukikasirika kwa sababu ya makosa ya wengine? Tukitenda kwa haraka au bila sababu inayofaa, hilo laweza kufanya tuwe watu wasio na uvumilivu—watu wasiochukuliana na udhaifu wa wengine—badala ya kuwa watetezi wa uadilifu. Ni nini kiwezacho kutusaidia kuepuka mtego huo?

‘Yehova Husamehe Maovu Yako Yote’

Yehova ni “Mungu mwenye wivu (bidii); Mungu asiyevumilia ushindani.” (Kutoka 20:5, NW, kielezi-chini) Akiwa Muumba, ana haki ya kutudai ujitoaji usiohusisha wengine. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, Yehova huvumilia udhaifu wa wanadamu. Kwa hiyo, mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi kumhusu: “BWANA amejaa huruma na neema, haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili. Yeye hatateta [“hatatafuta makosa,” NW] sikuzote . . . Hakututenda sawasawa na hatia zetu, wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu.” Naam, tukionyesha toba, Mungu ‘husamehe maovu yetu yote.’—Zaburi 103:3, 8-10.

Kwa sababu anaelewa asili yenye dhambi ya wanadamu, Yehova ‘hatafuti makosa’ ya watenda-dhambi waliotubu. (Zaburi 51:5; Waroma 5:12) Kwa hakika, anakusudia kuondoa dhambi na hali ya kutokamilika. Hadi wakati atakapotimiza kusudi hilo kikamili, badala ya kutulipa “kwa kadiri ya maovu yetu,” kwa neema Mungu hutusamehe kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Hakuna mmoja wetu ambaye angestahili kuokoka ikiwa Yehova hangemwonyesha rehema wakati unaofaa. (Zaburi 130:3) Twaweza kushukuru kama nini kwamba Baba yetu wa kimbingu, anayedai kwa haki ujitoaji usiohusisha wengine, ni Mungu mvumilivu!

Usawaziko Wahitajiwa

Kwa kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu huonyesha uvumilivu anaposhughulika na wanadamu wasio wakamilifu, je, hatupaswi kumwiga? Uvumilivu umefasiriwa kuwa “mwelekeo wa kuwa mwenye subira kuhusu maoni na mazoea ya wengine.” Je, sisi binafsi tuna mwelekeo wa namna hiyo—mwelekeo wa kuwa wenye subira na wavumilivu wakati wengine wanaposema au kufanya mambo ambayo si dhambi nzito lakini yasiyotupendeza?

Bila shaka, twahitaji kuepuka kuwa wavumilivu kupita kiasi. Kwa mfano, madhara makubwa hutokea wakati viongozi wa kidini wanapowavumilia makasisi wenye zoea la kuwasumbua kingono wavulana na wasichana. “Likichukua jambo hilo lililowapata watoto kuwa tukio tu la dhambi viongozi wa kanisa walimhamisha tu kasisi mwenye kosa [hadi sehemu nyingine],” akasema ripota mmoja nchini Ireland.

Je, kumhamisha tu mtu kama huyo ni kielelezo cha uvumilivu ufaao? Sivyo! Tuseme baraza la kitiba linamruhusu daktari-mpasuaji asiyejali aendelee kufanya upasuaji, huku likimhamisha kutoka hospitali moja hadi nyingine, ijapokuwa anaua au kulemaza wagonjwa wake. Wataalamu wa kitiba wanaweza kudumisha mapatano kati yao na hivyo kuwepo na “uvumilivu” wa namna hiyo. Lakini vipi juu ya watu ambao walikufa au wakaathiriwa vibaya kwa sababu ya kutojali au hata na vitendo vya uhalifu?

Kuna hatari pia ya kuonyesha uvumilivu kidogo sana. Yesu alipokuwa duniani, Wayahudi fulani walioitwa Wazeloti walijaribu kutumia mfano wa Finehasi katika jitihada za kutolea udhuru utendaji wao wa kupita kiasi. Tendo moja la kupita kiasi lililofanywa na Wazeloti fulani lilikuwa “kuchangamana na umati huko Yerusalemu wakati wa sherehe na kuwachoma kwa sime maadui wao wasio na habari.”

Tukiwa Wakristo, hatuwezi kufanya kama vile Wazeloti walivyofanya kwa kushambulia maadui wetu. Lakini je, kukosa uvumilivu kwa kiasi fulani hutufanya tushambulie katika njia nyinginezo wale tusiokubaliana nao—labda kwa kuzungumza isivyofaa kuwahusu? Ikiwa sisi ni wavumilivu kwelikweli, hatutasema mambo kama hayo yenye kuumiza.

Kikundi kingine cha watu ambao hawakuwa wavumilivu ni Mafarisayo wa karne ya kwanza. Walilaumu wengine daima na hawakuchukuliana na udhaifu wa kibinadamu. Mafarisayo wenye kiburi waliwadharau watu wa kawaida, na wakawakashifu kuwa “watu waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kushutumu watu hao waliojiona kuwa waadilifu, kwa kusema hivi: “Ole wenu nyinyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa sababu nyinyi huitoa sehemu ya kumi ya mnanaa na dili na jira, lakini mmepuuza mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu. Ilikuwa lazima mambo haya kuyafanya, na bado kutopuuza yale mambo mengine.”—Mathayo 23:23.

Alipotoa taarifa hiyo, Yesu hakuwa akipuuza umuhimu wa kushika Sheria ya Kimusa. Alikuwa akionyesha tu kwamba mambo “yenye uzito zaidi” au ya maana zaidi, ya Sheria yalitaka itumiwe kwa kiasi na kwa rehema. Yesu na wanafunzi wake walikuwa tofauti kama nini na Mafarisayo na Wazeloti wasio wavumilivu!

Wala Yehova Mungu wala Yesu Kristo hawaruhusu tu uovu uendelee. Karibuni ‘kisasi kitakuja juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.’ (2 Wathesalonike 1:6-10) Hata hivyo, katika bidii yake kwa ajili ya uadilifu, Yesu hashindwi kamwe kumwiga Baba yake wa kimbingu katika kuwaonyesha saburi, rehema, na hangaiko lenye upendo wote wanaotaka kufanya lililo sawa. (Isaya 42:1-3; Mathayo 11:28-30; 12:18-21) Yesu alituwekea kielelezo kizuri kama nini!

Chukulianeni Mtu na Mwenzake kwa Saburi

Ingawa huenda tukawa na bidii nyingi kwa lililo sawa, acheni tutumie shauri hili la mtume Paulo: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia.” (Wakolosai 3:13; Mathayo 6:14, 15) Uvumilivu hutaka tuchukuliane na udhaifu na makosa ya wengine katika ulimwengu huu usio mkamilifu. Twahitaji kuwa wenye kiasi kwa mambo tunayotazamia kutoka kwa wengine.—Wafilipi 4:5.

Kuwa wavumilivu hakudokezi kwa njia yoyote ile kwamba tunaunga mkono ukosaji au hatuoni makosa. Huenda mwamini mwenzetu akafikiri au kutenda kwa njia fulani isiyopatana na viwango vya Yehova. Ingawa huenda kukengeuka huko kusiwe kwa kadiri kubwa kiasi cha kukataliwa na Mungu, kwaweza kuwa ishara ya kwamba rekebisho fulani lahitajiwa. (Mwanzo 4:6, 7) Ni jambo la upendo kama nini kwa wale walio na sifa za kustahili kiroho kujaribu kurekebisha mkosaji huyo kwa roho ya upole! (Wagalatia 6:1) Hata hivyo, ili kufanikiwa katika jitihada hiyo, ni muhimu kuchukua hatua kwa kuchochewa na kujali wengine badala ya kutaka kuwachambua.

“Kwa Tabia-Pole na Staha Yenye Kina Kirefu”

Lakini vipi kuonyesha saburi watu ambao maoni yao ya kidini ni tofauti na yetu? “Somo la Ujumla” katika Shule zote za Kitaifa zilizoanzishwa nchini Ireland mwaka wa 1831 lasema hivi: “Yesu Kristo hakukusudia watu walazimishwe kujiunga na dini yake kupitia jeuri. . . . Kugombana na majirani wetu na kuwatukana sio njia ya kuwasadikisha kwamba wamekosea na kwamba sisi tuko sawa. Yaelekea hatutawasadikisha kwamba tuna roho ya Kikristo.”

Yesu alifundisha na kutenda kwa njia iliyowavuta watu kwa Neno la Mungu, nasi twapaswa kufanya vivyo hivyo. (Marko 6:34; Luka 4:22, 32; 1 Petro 2:21) Akiwa mwanadamu mkamilifu mwenye ufahamu aliopewa na Mungu, angeweza kusoma mioyo. Kwa hiyo, ilipohitajika Yesu alishutumu vikali maadui wa Yehova. (Mathayo 23:13-33) Hakufanya hivyo kwa sababu ya kutokuwa mvumilivu.

Tofauti na Yesu hatuwezi kusoma mioyo. Kwa hiyo twapaswa kutii shauri la mtume Petro: “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwenu sababu ya tumaini lililo katika nyinyi, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:15) Tukiwa watumishi wa Yehova, twapaswa kutetea imani yetu kwa sababu inategemea kabisa Neno la Mungu. Lakini twahitaji kufanya hivyo kwa kuwaheshimu wengine na mambo wanayoamini kwa moyo mweupe. Paulo aliandika hivi: “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi, ili kujua jinsi mpaswavyo kumpa jibu kila mmoja.”—Wakolosai 4:6.

Katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” (Mathayo 7:12) Kwa hiyo, basi, acheni tuchukuliane kwa saburi na kuheshimu watu tunaohubiria habari njema. Kwa kusawazisha bidii yetu ya uadilifu na uvumilivu unaotegemea Biblia, tutampendeza Yehova na tutakuwa wavumilivu kwelikweli.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Epuka mtazamo wa Mafarisayo wa kutokuwa na uvumilivu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yesu alidhihirisha mtazamo wa Baba yake wa uvumilivu. Je, wewe hufanya hivyo?