Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Origen—Mafundisho Yake Yaliathirije Kanisa?

Origen—Mafundisho Yake Yaliathirije Kanisa?

Origen—Mafundisho Yake Yaliathirije Kanisa?

“Ndiye kiongozi wa Kanisa mwenye kuheshimiwa zaidi baada ya Mitume.” Ndivyo Jerome, mtafsiri wa Biblia ya Kilatini ya Vulgate alivyomsifu Origen, mwanatheolojia wa karne ya tatu. Lakini si kila mtu aliyemsifu Origen kadiri hiyo. Wengine walimwona kuwa mtu mwovu aliyetokeza uzushi. Katika maneno ya mwandishi wa karne ya 17, wapinzani wa Origen walisisitiza hivi: “Kwa ujumla, mafundisho yake ni ya kipuuzi na yenye kudhuru, ni sumu yenye kufisha kama ya Nyoka, ambayo amemwaga ulimwenguni.” Kwa kweli Origen alitangazwa rasmi kuwa mzushi, karibu karne tatu baada ya kufa.

KWA nini watu wengine walivutiwa na Origen ilhali wengine wakamchukia? Aliathirije ukuzi wa mafundisho ya kanisa?

Mwenye Bidii kwa Ajili ya Kanisa

Origen alizaliwa yapata mwaka wa 185 W.K. katika jiji la Misri la Alexandria. Alifundishwa kikamili fasihi ya Kigiriki, lakini baba yake, Leonides, alimlazimisha afanye jitihada hiyohiyo katika kujifunza Maandiko. Origen alipokuwa na umri wa miaka 17, maliki Mroma alitoa amri iliyofanya liwe jambo haramu mtu kubadili dini yake. Babake Origen alifungwa gerezani kwa sababu ya kuwa Mkristo. Akiwa na bidii ya ujana, Origen aliazimia kujiunga na babake gerezani na kufa kwa ajili ya imani yake. Alipoona hivyo, mamake Origen alificha nguo zake ili kumzuia asiondoke nyumbani. Origen alimsihi babake hivi kupitia barua: “Uwe mwangalifu usibadili msimamo wako kwa sababu yetu.” Leonides aliendelea kuwa imara na kuuawa, huku akiacha familia yake ikiwa fukara. Lakini tayari Origen alikuwa amesoma vya kutosha kuweza kumtegemeza mama yake na ndugu zake sita wadogo kwa kufundisha fasihi ya Kigiriki.

Maliki alikuwa na nia ya kuzuia Ukristo usienee. Kwa kuwa amri yake haingeathiri tu wanafunzi, bali pia walimu, wafunzi wote wa dini ya Kikristo walitoroka Alexandria. Watu wasio Wakristo walipotaka kufundishwa Maandiko na kumwomba Origen mchanga awasaidie, alikubali kazi hiyo kama utume kutoka kwa Mungu. Wengi wa wanafunzi wake walifia imani, wengine hata kabla ya kumaliza masomo yao. Kwa kujihatarisha sana, Origen aliwatia moyo waziwazi wanafunzi wake, iwe walikuwa mbele za hakimu, gerezani, au wakielekea kuuawa. Mwanahistoria wa karne ya nne Eusebius aripoti kwamba walipokuwa wakipelekwa kuuawa, “kwa ujasiri mwingi [Origen] aliwasalimu kwa busu.”

Watu wengi wasio Wakristo walikasirishwa sana na Origen kwa sababu waliona kuwa yeye ndiye aliyesababisha wengi wa marafiki wao wabadili imani na hivyo kuuawa. Mara nyingi aliponea chupuchupu kupigwa na umati na kuuawa kikatili. Ingawa alilazimika kuhama kutoka nyumba moja hadi nyingine ili kukwepa watu waliokuwa wakimsaka, Origen hakuacha kufundisha. Hali hiyo ya kutoogopa na ya kujitoa ilimvutia sana Demetrius, kasisi wa Alexandria. Kwa hiyo, Origen alipokuwa na umri wa miaka 18 tu, Demetrius alimteua kuwa kiongozi wa shule ya mafundisho ya kidini huko Alexandria.

Hatimaye, Origen akawa msomi mashuhuri na mwandikaji mwenye matokeo sana. Watu wengine walisema kwamba aliandika vitabu 6,000, ingawa labda walitilia chumvi jambo hilo. Anajulikana sana kwa kichapo chake Hexapla, kitabu kikubwa sana chenye mabuku 50 ya Maandiko ya Kiebrania. Origen alipanga Hexapla katika safu sita zilizo sambamba zenye: (1) maandishi ya Kiebrania na Kiaramu, (2) utohozi wa maandiko hayo katika Kigiriki, (3) tafsiri ya Kigiriki ya Aquila, (4) tafsiri ya Kigiriki ya Symmachus, (5) Septuagint ya Kigiriki iliyosahihishwa na Origen ili ipatane kikamili zaidi na maandiko ya Kiebrania, na (6) tafsiri ya Kigiriki ya Theodotion. “Kwa kuyaweka maandiko hayo pamoja,” akaandika msomi wa Biblia John Hort, “Origen alitumaini kufafanua maana ya vifungu vingi ambavyo ama vingemtatanisha ama kumpotosha msomaji wa Kigiriki ikiwa angekuwa na Septuagint peke yake.”

‘Kupita Mambo Yaliyoandikwa’

Hata hivyo, hali yenye kutatanisha ya kidini katika karne ya tatu iliathiri sana njia ya Origen ya kufundisha Maandiko. Ingawa Jumuiya ya Wakristo ilikuwa ndiyo tu inaanza, tayari ilikuwa imechafuliwa na itikadi zisizo za Kimaandiko, na makanisa yake yaliyoenea kote yalikuwa yakifundisha mafundisho ya namna nyingi.

Origen alikubali baadhi ya mafundisho hayo yasiyo ya Kimaandiko na kuyaita mafundisho ya mitume. Hata hivyo, alijihisi huru kukisia-kisia majibu mengineyo. Wengi wa wanafunzi wake walikuwa wakipambana na masuala ya kifalsafa ya wakati wao. Katika jitihada ya kuwasaidia, Origen alichunguza kwa uangalifu wafuasi mbalimbali wa falsafa waliokuwa wakielekeza akili za wanafunzi wake wachanga. Alikusudia kujibu maswali ya kifalsafa ya wanafunzi wake kwa njia yenye kuridhisha.

Katika jitihada ya kupatanisha Biblia na falsafa, Origen alitumia sana njia ya kufasiri Maandiko kwa kuzingatia maana iliyositiriwa ya kiroho. Alikata kauli kwamba sikuzote Maandiko yana maana iliyositiriwa ya kiroho na si lazima yawe na maana halisi. Kama alivyosema msomi mmoja, jambo hilo lilimpa Origen “uwezo wa kuyapa maana ya Biblia mawazo yoyote yasiyo ya Biblia yaliyokubaliana na mfumo wake wa kitheolojia, huku akidai (na bila shaka akijiona mwenyewe kwa unyofu) kuwa mfasiri mwenye bidii na mwaminifu wa mawazo ya Biblia.”

Barua moja ambayo Origen alimwandikia mmoja wa wanafunzi wake yaeleza kwa kina kufikiri kwake. Origen alisema kwamba Waisraeli walitengeneza vyombo vya hekalu la Yehova kwa kutumia dhahabu ya Misri. Kwa kutumia mfano huo, yeye pia angeweza kutumia falsafa ya Kigiriki kufundisha Ukristo. Aliandika hivi: “Jinsi wana wa Israeli walivyofaidika kwa vitu walivyotoa Misri, ambavyo Wamisri hawakuvitumia ifaavyo, lakini Waebrania wakiongozwa na hekima ya Mungu, wakavitumia katika utumishi wa Mungu.” Kwa hiyo Origen aliwatia moyo wanafunzi wake ‘watwae habari zozote kutoka katika falsafa ya Kigiriki na kuzitumia kujitayarishia Ukristo.’

Njia hii isiyo na mipaka ya kufasiri Biblia, ilifanya iwe vigumu sana kutofautisha mafundisho ya Kikristo na falsafa ya Kigiriki. Kwa mfano, katika kitabu chake chenye kichwa On First Principles, Origen alimfafanua Yesu kuwa ‘Mwana mzaliwa-pekee, aliyezaliwa, lakini asiye na mwanzo.’ Aliongezea hivi: ‘Uzaliwa wake ni wa umilele. Hakuwa Mwana kwa sababu ya kupokea pumzi ya uhai, wala si kupitia tendo jinginelo, bali kwa asili ya Mungu mwenyewe.’

Origen hakupata wazo hilo katika Biblia, kwa kuwa Maandiko hufundisha kwamba Mwana pekee wa Yehova ni “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote” na “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Wakolosai 1:15; Ufunuo 3:14) Kulingana na mwanahistoria wa dini Augustus Neander, Origen alifikia uamuzi wa dhana ya “uzaliwa wa umilele” kupitia “elimu yake ya kifalsafa katika shule ya Plato.” Kwa hiyo, Origen alikiuka kanuni hii ya Kimaandiko iliyo ya msingi: “Msiyapite mambo ambayo yameandikwa.”—1 Wakorintho 4:6.

Ahukumiwa Kuwa Mzushi

Wakati wa miaka yake ya mapema akiwa mwalimu, Origen alinyang’anywa ukasisi na Sinodi ya Alexandria. Labda jambo hilo lilitukia kwa sababu Kasisi Demetrius alionea wivu umashuhuri wa Origen uliokuwa ukiongezeka. Origen alihamia Palestina ambako wengi waliendelea kumwona kuwa mtetezi mwaminifu wa fundisho la Kikristo, na kuendelea kutumikia akiwa kasisi huko. Kwa hakika, “uzushi” ulipozuka sehemu za Mashariki, watu walitafuta msaada wake ili kuwasadikisha makasisi waliokosea warudie imani ya Ukristo asilia. Origen alipokufa mwaka wa 254 W.K., jina lake liliharibiwa sifa sana. Kwa nini?

Ukristo wa jina tu ulipopata kuwa dini mashuhuri, mafundisho yaliyokubaliwa na kanisa yakaja kufafanuliwa kwa usahihi. Hivyo, vizazi vilivyofuata vya wanatheolojia vilikataa maoni mengi ya kifalsafa ya Origen yaliyokuwa ya kukisia na yasiyo sahihi. Kwa hiyo mafundisho yake yalianzisha ubishi mkali sana katika kanisa. Katika jitihada za kutatua mabishano hayo na kudumisha muungano, kanisa lilimhukumu rasmi Origen kuwa mzushi.

Kuna wengine pia waliokosea kama Origen. Kwa kweli, Biblia ilikuwa imetabiri kwamba kungekuwa na ukengeufu mkubwa kutoka kwa mafundisho safi ya Kristo. Uasi-imani huo ulianza kusitawi mwishoni mwa karne ya kwanza, baada ya mitume wa Yesu kufa. (2 Wathesalonike 2:6, 7) Hatimaye, watu fulani waliodai kuwa Wakristo walijitangaza wenyewe kuwa na “mafundisho yanayokubaliwa,” na kuwaona wengine wote kuwa “wazushi.” Lakini kwa kweli, Jumuiya ya Wakristo ilikengeuka kabisa kutoka kwa Ukristo wa kweli.

“Yenye Kuitwa ‘Ujuzi’ Isivyo Kweli”

Licha ya makisio mengi ya Origen, vitabu vyake vina mambo yenye kunufaisha. Kwa mfano, Hexapla ilihifadhi jina la Mungu jinsi lilivyoandikwa hapo awali kwa herufi nne za Kiebrania, zinazoitwa Tetragramatoni. Jambo hilo latoa uthibitisho muhimu kwamba Wakristo wa mapema walijua na kutumia jina la kibinafsi la Mungu—Yehova. Hata hivyo, wakati mmoja mwanzilishi fulani wa kanisa wa karne ya tano aitwaye Theophilus alitoa tahadhari hii: “Vitabu vya Origen ni kama konde lenye maua ya kila namna. Nikipata ua lolote zuri, ninalichuma; lakini nikiona ua lolote lenye miiba ninaliepuka kama vile ningeepuka kitu kinachodunga.”

Kwa kuchanganya mafundisho ya Biblia na falsafa ya Kigiriki, theolojia ya Origen ilijaa makosa, na matokeo yakawa mabaya sana kwa Jumuiya ya Wakristo. Kwa mfano, ijapokuwa makisio mengi ya ajabu-ajabu ya Origen yalikataliwa baadaye, maoni ya Origen juu ya “uzaliwa wa umilele” wa Kristo yalisaidia kuweka msingi wa fundisho lisilo la Biblia la Utatu. Kitabu The Church of the First Three Centuries chasema hivi: “Watu wangezidi kupendelea falsafa [iliyoanzishwa na Origen] kwa muda mrefu.” Kukiwa na matokeo gani? “Ule usahili wa imani ya Kikristo ulichafuliwa, na makosa mengi sana yakaingia katika Kanisa.”

Kwa upande wake, Origen angetii shauri la mtume Paulo na kuepuka kuchangia uasi-imani huo kwa “[ku]geuka mbali kutoka kwenye semi tupu ambazo huhalifu lililo takatifu na kutoka kwenye mapinganisho yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli.” Badala yake, kwa kutegemeza mengi ya mafundisho yake kwenye “ujuzi” huo, Origen “alikengeuka kutoka kwenye imani.”—1 Timotheo 6:20, 21; Wakolosai 2:8.

[Picha katika ukurasa wa 31]

“Hexapla” ya Origen inathibitisha kwamba jina la Mungu lilitumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo

[Hisani]

Published by permission of the Syndics of Cambridge University Library, T-S 12.182

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 29]

Culver Pictures