Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shinda Vikwazo Vinavyokuzuia Usifanye Maendeleo!

Shinda Vikwazo Vinavyokuzuia Usifanye Maendeleo!

Shinda Vikwazo Vinavyokuzuia Usifanye Maendeleo!

HEBU wazia kwamba umeweka gari lako gia, na injini inanguruma, lakini gari linakataa kwenda. Je, lina tatizo la kiufundi? La, jiwe kubwa limewekwa mbele ya gurudumu moja. Unahitaji tu kulitoa ili gari liweze kwenda.

Kwa njia hiyohiyo, watu fulani wanaojifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova wana vikwazo vinavyoweza kuwazuia wasifanye maendeleo ya kiroho. Kwa mfano, Yesu alionya kwamba mambo kama “hangaiko la mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa mali” yanaweza ‘kulisonga neno’ la ile kweli na kuzuia ukuzi.—Mathayo 13:22.

Wengine hushindwa kufanya maendeleo kwa sababu ya udhaifu au mambo ambayo wamezoea sana kufanya. Mwanamume Mjapani aitwaye Yutaka alipenda ujumbe wa Biblia, lakini alikuwa na tatizo kubwa la kucheza kamari. Alijaribu mara nyingi kuacha zoea hilo baya lakini akashindwa. Zoea hilo lilimpotezea pesa nyingi, nyumba tatu, staha ya familia yake, na heshima yake mwenyewe. Je, angeweza kushinda kikwazo hicho na kuwa Mkristo?

Au fikiria mwanamke aitwaye Keiko. Biblia ilimsaidia kuacha mazoea mabaya kama vile kuabudu sanamu, mwenendo mchafu, na uaguzi. Hata hivyo, Keiko anakiri: “Kikwazo kilichokuwa kikubwa zaidi kwangu ni kuvuta tumbaku. Nilijaribu mara nyingi kuacha lakini sikuweza.”

Huenda ikawa unazuiwa kufanya maendeleo na kikwazo kinachoonekana kana kwamba hakiwezi kushindwa. Hata kizuizi hicho kiwe nini, uwe na hakika kwamba unaweza kukishinda kwa msaada wa Mungu.

Kumbuka ushauri wa Yesu kwa wanafunzi wake baada ya wanafunzi hao kushindwa kufukuza roho mwovu kutoka kwa mwanamume mwenye kifafa. Baada ya Yesu kumfukuza roho huyo mwovu, aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mkiwa na imani yenye ukubwa wa punje ya haradali, mtaambia mlima huu, ‘Hama kutoka hapa hadi pale,’ nao utahama, na hakuna jambo litakalokuwa haliwezekani kwenu.” (Mathayo 17:14-20; Marko 9:17-29) Naam, tatizo linaloonekana kwetu kama mlima mkubwa, ni dogo sana mbele ya Muumba wetu mwenye nguvu zote.—Mwanzo 18:14; Marko 10:27.

Kutambua Vikwazo Vinavyokuzuia Usifanye Maendeleo

Ili kuvishinda vikwazo hivyo, ni lazima uvitambue. Unawezaje kufanya hivyo? Nyakati nyingine mshiriki wa kutaniko, kama vile mzee au mtu unayesoma naye Biblia, atakukumbusha jambo fulani. Badala ya kuudhiwa na ushauri huo wenye upendo, yakupasa ‘kusikiliza mafundisho na kupata hekima.’ (Mithali 8:33) Mara nyingine unaweza kufahamu udhaifu wako kupitia funzo la Biblia. Naam, neno la Mungu “liko hai na hukazia nguvu.” (Waebrania 4:12) Kusoma Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia kunaweza kufichua mawazo yako ya ndani kabisa, hisia zako, na makusudi yako. Hukusaidia kujichanganua kupatana na viwango vya juu vya Yehova. Hufichua na kutaja mambo ambayo yanaweza kukuzuia usifanye maendeleo ya kiroho.—Yakobo 1:23-25.

Kwa mfano, tuseme mwanafunzi wa Biblia amekuwa na mazoea ya kuwazawaza mambo yasiyo ya kiadili. Huenda asione ubaya wowote wa kufanya hivyo, akidhani kwamba yeye kwa kweli hafanyi lolote baya. Anapojifunza, anaona maneno haya ya Yakobo 1:14, 15: “Kila mmoja hujaribiwa kwa kuvutwa na kutongozwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetungika mimba, huzaa dhambi; nayo, dhambi, wakati imetimilika, hutokeza kifo.” Sasa anaona jinsi kuendelea kufanya hivyo kunavyoweza kuathiri maendeleo yake! Anawezaje kushinda kikwazo hicho?—Marko 7:21-23.

Kushinda Vikwazo

Labda kwa msaada wa Mkristo aliyekomaa, mwanafunzi huyo anaweza kufanya utafiti zaidi wa Neno la Mungu, akitumia kichapo Watch Tower Publications Index. * Kwa mfano, kichwa “Mawazo” (“Thoughts”) humwelekeza msomaji kwenye makala kadhaa zilizochapishwa zinazozungumza juu ya jinsi mtu anavyoweza kushinda kuwazawaza kunakodhuru. Makala hizo hukazia maandiko ya Biblia yenye manufaa kama vile Wafilipi 4:8, ambalo lasema: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaikio zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yaliyo ya kusemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa likiwako, endeleeni kufikiria mambo haya.” Naam, yatupasa kuacha kuwaza mambo yasiyo ya kiadili na badala yake kuwaza mambo yenye kujenga!

Wakati wa utafiti wake, yaelekea mwanafunzi atajifunza kanuni nyinginezo za Biblia zitakazomsaidia aepuke kufanya tatizo lake liwe baya hata zaidi. Kwa mfano, Mithali 6:27 na Mathayo 5:28 hutuonya tusisome habari zenye kuchochea kingono. Mtunga-zaburi alisali hivi: “Unigeuze macho yangu nisitazame visivyofaa.” (Zaburi 119:37) Bila shaka haitoshi kusoma tu maandiko hayo ya Biblia. “Moyo wa mwenye haki hufikiri,” asema mtu mwenye hekima. (Mithali 15:28) Kwa kutafakari yale Mungu huamuru na pia kujua ni kwa nini yeye hufanya hivyo, mwanafunzi anaweza kufahamu zaidi hekima na busara ya njia za Yehova.

Mwishowe, yule anayejitahidi kushinda kikwazo kinachomzuia asifanye maendeleo apaswa kutafuta msaada wa Yehova bila kukawia. Inafaa afanye hivyo kwa sababu Mungu anajua jinsi tulivyo, kwamba sisi ni watu wasio wakamilifu, tuliofanywa kwa mavumbi. (Zaburi 103:14) Kusali kwa Mungu daima ili kupata msaada, pamoja na jitihada za kuepuka kuwazawaza mambo yasiyo ya kiadili, kutakuwa na matokeo mazuri sana hatimaye, yaani, dhamiri safi, isiyosumbua.—Waebrania 9:14.

Usife Moyo

Hata uwe unapambana na tatizo gani, jua kwamba huenda nyakati nyingine ukapata vipingamizi. Inapokuwa hivyo, ni jambo la kawaida kufa moyo na kukata tamaa. Hata hivyo, kumbuka maneno ya Wagalatia 6:9: “Acheni tusife moyo katika kufanya lililo bora, kwa maana katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.” Watumishi wa Mungu kama vile Daudi na Petro walifanya makosa yenye kuaibisha. Lakini hawakukata tamaa. Walikubali ushauri kwa unyenyekevu, wakafanya mabadiliko, na kuthibitisha kwamba walikuwa watumishi wa Mungu wenye kutokeza. (Mithali 24:16) Licha ya makosa ya Daudi, Yehova alimwita “mwanamume mwenye kukubalika kwa moyo wangu, atakayefanya mambo yote ambayo natamani.” (Matendo 13:22) Petro vilevile alishinda makosa yake na kuwa nguzo katika kutaniko la Kikristo.

Leo wengi wamefurahia mafanikio kama hayo katika kushinda vikwazo. Yutaka aliyetajwa hapo awali alikubali kujifunza Biblia. Yeye asema: “Baraka na utegemezo wa Yehova katika kila hatua niliyochukua zilinisaidia kushinda tatizo langu la kucheza kamari. Nina shangwe nyingi kuona ukweli wa maneno ya Yesu kwamba imani inaweza kuhamisha ‘milima.’” Baada ya muda, Yutaka akawa mtumishi wa huduma kutanikoni.

Vipi Keiko aliyekuwa na zoea la kuvuta tumbaku? Dada aliyekuwa anajifunza naye alipendekeza kwamba asome makala mbalimbali za Amkeni! kuhusu zoea hilo. Keiko hata aliweka maneno ya 2 Wakorintho 7:1 kwenye gari lake ili yawe yakimkumbusha kila siku kuwa safi machoni pa Yehova. Hata hivyo, hangeweza kuacha kuvuta tumbaku. “Jambo hilo liliniudhi sana,” Keiko akumbuka. “Ndipo nikaanza kujiuliza nilichotaka hasa—je, nilitaka kumtumikia Yehova au Shetani?” Alipoamua kwamba anataka kumtumikia Yehova, alisali kwa bidii apate msaada. “Nilishangaa kwamba niliweza kuacha kuvuta tumbaku bila shida. Ninajuta tu kwamba sikuacha mapema zaidi,” yeye anasema.

Wewe pia unaweza kufanikiwa kushinda vikwazo vinavyokuzuia usifanye maendeleo. Utajiheshimu na kuwa na uhakika ukiendelea kupatanisha mawazo, tamaa, maneno, na matendo yako kulingana na viwango vya Biblia. Ndugu zako na dada zako wa kiroho, na vilevile watu wa familia yako, watachochewa na kutiwa moyo wanaposhirikiana nawe. La muhimu hata zaidi ni kwamba uhusiano wako na Yehova Mungu utakuwa mzuri hata zaidi. Yeye aliahidi kwamba ‘ataondoa kila kikwazacho katika njia ya watu wake’ wanapomkimbia Shetani. (Isaya 57:14) Na unaweza kuwa na hakika kwamba ukijitahidi kuondoa na kushinda vikwazo vinavyokuzuia usifanye maendeleo ya kiroho, Yehova atakubariki sana.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Vimechapishwa katika lugha kadhaa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Yesu aliahidi kwamba mtu akiwa na imani anaweza kushinda vikwazo vilivyo kama mlima

[Picha katika ukurasa wa 30]

Kusoma Biblia huimarisha jitihada yetu ya kushinda udhaifu wa kiroho