Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Una Haki ya Kuamini Utakalo

Una Haki ya Kuamini Utakalo

Una Haki ya Kuamini Utakalo

Labda unathamini sana haki yako ya kuamini jambo lolote utakalo. Kila mtu pia huthamini haki ya kuamini jambo lolote atakalo. Kwa kutumia haki hiyo, wakazi bilioni sita duniani wameamini mambo mengi sana tofauti-tofauti. Kama vile tofauti iliyopo ya rangi, umbo, umbile, ladha, harufu, na sauti ambayo tunaona katika uumbaji, kuamini mambo tofauti-tofauti hufanya maisha yapendeze na yawe yenye kusisimua zaidi. Tofauti hizo zinaweza kuwa kama viungo vinavyotiwa katika chakula ili kiwe kitamu.—Zaburi 104:24.

LAKINI inafaa kuwa wenye tahadhari. Imani nyingine haziwi tofauti tu bali pia ni hatari. Kwa mfano, mapema katika karne ya 20, watu fulani waliamini kwamba Wayahudi na Freemasons (wanachama wa chama cha siri cha kusaidiana) walikuwa wamekula njama ya “kuvuruga ustaarabu wa Kikristo na kutawala ulimwengu wakiwa pamoja.” Imani hiyo ilichochewa na trakti fulani yenye kichwa Protocols of the Learned Elders of Zion iliyoendeleza chuki dhidi ya Wayahudi. Trakti hiyo ilidai kwamba njama hiyo ilitia ndani kutetea kodi ziongezwe, kuzidisha utengenezaji wa silaha, kampuni moja idhibiti biashara zote ili ‘mali za watu wasio Wayahudi ziharibiwe kwa ghafula.’ Madai hayo yalitia ndani pia kudhibiti mfumo wa elimu kwa njia ya hila ili ‘kufanya watu wasio Wayahudi wawe kama wanyama wasiofikiri,’ na hata kujenga reli za chini ya ardhi ili kuunganisha miji mikuu kusudi viongozi Wayahudi ‘waweze kuwashinda wapinzani wowote kwa kuwaangamiza.’

Bila shaka, huo ulikuwa uwongo uliokusudiwa kufanya watu wawachukie Wayahudi. ‘Trakti hiyo iliyoendeleza chuki dhidi ya Wayahudi,’ asema Mark Jones wa Jumba la Makumbusho la Uingereza, ‘ilienea katika nchi nyingine kutoka Urusi,’ ambako ilichapishwa mara ya kwanza kwenye makala ya gazeti moja mnamo mwaka wa 1903. Ilichapishwa katika gazeti The Times la London, Mei 8, 1920. Zaidi ya mwaka mmoja baadaye, gazeti The Times lilifichua kwamba trakti hiyo ilikuwa bandia. Hata hivyo, tayari ilikuwa imesababisha madhara. ‘Ni vigumu sana kukomesha uwongo kama huo,’ asema Jones. Mara tu watu wanapokubali uwongo huo, unatokeza imani zenye uhasama, zenye sumu na hatari na mara nyingi kunakuwa na matokeo mabaya, kama ilivyotukia katika karne ya 20.—Mithali 6:16-19.

Jinsi Imani Inavyotofautiana na Kweli

Bila shaka, imani isiyo ya kweli yaweza kutokea pasipo uwongo wa kukusudia. Nyakati nyingine tunaelewa mambo vibaya. Ni watu wengi kadiri gani ambao wamekufa bila kutazamia kwa kufanya jambo fulani waliloamini kuwa sawa? Pia, mara nyingi tunaamini jambo fulani kwa sababu tu tunataka kuliamini. Profesa mmoja asema kwamba hata wanasayansi “huthamini sana nadharia zao na mikataa yao.” Imani yao huwafanya washindwe kuchanganua mambo bila kupendelea upande wowote. Kisha wanaweza kutumia muda wote wa maisha yao wakijaribu kuunga mkono imani isiyo ya kweli.—Yeremia 17:9.

Mambo kama hayo yametokea kuhusiana na imani za kidini ambazo zinapingana sana. (1 Timotheo 4:1; 2 Timotheo 4:3, 4) Mtu fulani anaweza kuwa na imani yenye nguvu katika Mungu na mwingine aone imani hiyo kuwa ya upuuzi tu. Mtu fulani anasisitiza kwamba una nafsi isiyoweza kufa. Mwingine anaamini kwamba unapokufa, unakufa kabisa-kabisa, haundelei kuwa hai tena. Bila shaka, imani hizo zinazotofautiana haziwezi kuwa za kweli. Kwa hiyo, je, si jambo la hekima kuhakikisha kwamba jambo unaloamini ni la kweli na si kwa sababu tu unataka kuliamini? (Mithali 1:5) Unawezaje kufanya hivyo? Habari hiyo itachunguzwa katika makala ifuatayo.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Makala ya 1921 iliyofichua trakti yenye kichwa “Protocols of the Learned Elders of Zion”