Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kufanikisha Ujana Wako

Jinsi ya Kufanikisha Ujana Wako

Jinsi ya Kufanikisha Ujana Wako

WAKAZI wa nchi moja barani Ulaya waliombwa wachague kati ya mambo matatu: urembo, utajiri, au ujana. Wengi walichagua ujana. Naam, watu wa kila rika huona miaka ya utineja na miaka ya mapema ya 20 kuwa wakati wa pekee maishani. Na kila mtu anataka vijana wafanikiwe wanapokuwa watu wazima. Lakini jinsi gani?

Je, Biblia inaweza kusaidia? Kwa wazi jibu ni ndiyo. Acheni tuchunguze sehemu mbili ambazo Neno la Mungu linaweza kutoa msaada wa pekee unaoweza kuwasaidia vijana hasa kuliko watu wa rika lolote.

Kupatana na Wengine

Ripoti inayoitwa Jugend 2000 ni uchunguzi unaofanywa kuhusu mtazamo, maadili, na tabia ya vijana zaidi ya 5,000 katika sehemu nyingi nchini Ujerumani. Uchunguzi huo unafunua kwamba vijana wanapojifurahisha—kama vile wanaposikiliza muziki, wanapocheza, au wanapotembea-tembea tu—karibu wakati wote wanakuwa na watu wengine. Labda vijana ndio hupenda sana kuwa pamoja na marika wao, kuliko watu wa rika lolote. Kwa sababu hiyo, ni wazi kwamba mojawapo ya siri za kufanikiwa ujanani ni kupatana na wengine.

Lakini si rahisi sikuzote kupatana na wengine. Kwa kweli, mara nyingi vijana wa kiume na wa kike hukiri kwamba wana tatizo la kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine. Biblia inaweza kusaidia sana kutatua tatizo hilo. Neno la Mungu lina mwongozo wa msingi kwa vijana ili kuwasaidia wawe na mahusiano yanayofaa. Biblia husemaje?

Mojawapo ya kanuni muhimu zaidi katika uhusiano wa kibinadamu ni ile inayoitwa Kanuni Bora: “Sikuzote watendeeni wengine kama mnavyotaka wawatendee.” Kuwatendea wengine kwa heshima, adhama, na fadhili huwatia moyo wakutendee kwa njia hiyohiyo. Tabia yenye fadhili yaweza kumaliza ugomvi na mkazo. Unapojulikana kuwa mtu anayewatendea wengine kwa fadhili, yaelekea watakuheshimu na utapata kibali chao. Je, wewe hufurahi kukubaliwa na wengine?—Mathayo 7:12, Revised English Bible.

Biblia hukushauri “umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” Unahitaji kujipenda mwenyewe katika maana ya kujistahi kwa kadiri fulani, si kujistahi kupita kiasi. Kwa nini inafaa kuwa na mtazamo huo? Ikiwa hujistahi, huenda ukawachambua wengine kupita kiasi, jambo ambalo hufanya usiwe na mahusiano mazuri na wengine. Lakini kujistahi kwa njia iliyosawazika ni msingi wa kuwa na urafiki thabiti.—Mathayo 22:39.

Urafiki unapositawi, unahitaji kuimarishwa na jitihada za watu wote wawili. Wapaswa kufurahi kutumia wakati kuimarisha urafiki, kwa kuwa “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” Njia moja ya kutoa ni kusamehe ambako kunatia ndani kupuuza makosa madogo-madogo na kutotarajia ukamilifu kutoka kwa wengine. Biblia hutuambia: “Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote.” Kwa kweli, “kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” Namna gani rafiki akikutajia udhaifu fulani ulio nao? Unatendaje? Fikiria shauri hili la busara kutoka kwenye Biblia: “Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako” kwa kuwa “jeraha utiwazo na rafiki ni amini.” Je, si kweli kwamba marafiki huathiri kufikiri kwako, usemi, na mwenendo wako? Kwa hiyo, Biblia huonya: “Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” Kwa upande mwingine, ‘anayeenenda pamoja na wenye hekima, atakuwa mwenye hekima.’—Matendo 20:35; Wafilipi 4:5; Waroma 12:17, 18; Mhubiri 7:9; Mithali 13:20; 27:6; 1 Wakorintho 15:33.

Marco awakilisha vijana wengi wa kiume na wa kike asemapo: “Kanuni za Biblia husaidia sana katika kupatana na wengine. Watu fulani ninaowajua hujifikiria wenyewe tu na jinsi wanavyoweza kunufaika maishani. Biblia hutufundisha tusijifikirie wenyewe tu, bali tuwafikirie wengine. Kama nionavyo, hii ndiyo njia bora zaidi ya kuwa na uhusiano mzuri na wengine.”

Mambo ambayo vijana kama Marco hujifunza kutoka kwa Biblia huwasaidia si wakati wa ujana wao tu bali pia katika miaka mingi baadaye. Na kuhusu wakati ujao, tunaona njia nyingine ambayo Biblia inaweza kutoa msaada wa pekee kwa vijana.

Kuhangaikia Wakati Ujao

Vijana wengi hupenda kuulizia-ulizia habari. Labda hakuna rika lolote ambalo hutaka kujua mambo yanayotokea na kwa nini kuliko vijana. Nayo Biblia, zaidi ya kitabu kingine chochote, hueleza sababu inayofanya mambo yawe kama yalivyo ulimwenguni na hutuambia ni nini tunachoweza kutarajia wakati ujao. Hayo ndiyo mambo ambayo vijana wanataka kujua. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba vijana wanataka kujua mambo hayo?

Ijapokuwa wengi wanaamini kwamba vijana huridhika na maisha ya sasa tu, uchunguzi fulani waonyesha hali iliyo tofauti kidogo na hiyo. Uchunguzi huo waonyesha kwamba mara nyingi vijana huangalia kwa makini mambo yanayoendelea, kisha wanafikia mkataa kuhusu jinsi maisha yanavyoweza kuwa wakati ujao. Uthibitisho wa jambo hilo ni kwamba vijana 3 kati ya 4 wa kiume na wa kike hufikiri “mara nyingi” au “mara nyingi sana” kuhusu wakati ujao. Ijapokuwa kwa ujumla vijana hutarajia mema, vijana wengi huhangaikia wakati ujao.

Kwa nini wahangaike? Tayari vijana wengi wanakabiliwa na matatizo ya jeuri, uhalifu, na matumizi mabaya ya dawa za kulevya. Vijana wana wasiwasi wa kama watapata kazi nzuri katika jamii yenye mashindano makali. Wanahisi kuwa wanasongwa kupata maksi nzuri shuleni au kufanikiwa kazini. Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 17 alilalamika hivi: “Tunaishi katika jamii yenye ukatili na ubinafsi. Kila mtu hufanya lile atakalo. Lazima sikuzote uthibitishe kile unachoweza kufanya, na jambo hilo huniudhi.” Kijana mwingine mwenye umri wa miaka 22, alisema: “Watu waliofanikiwa maishani wanaweza kuishi maisha ya kustarehesha. Watu ambao hali zao ni mbaya, ambao hawawezi kufanikiwa kama wenzao kwa sababu mbalimbali, hubaki nyuma.” Kwa nini kuna mashindano makali sana katika maisha? Je, maisha yatakuwa hivyo sikuzote?

Ufafanuzi wa Busara

Vijana wanapohangaishwa na yale wanayoona katika jamii, wanakubaliana na Biblia—iwe wanajua au hawajui. Neno la Mungu huonyesha kwamba jamii ya leo yenye ukatili na ubinafsi ni ishara ya nyakati. Mtume Paulo alimwandikia barua kijana aitwaye Timotheo kuhusu siku zetu za leo: “Nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa.” Kwa nini ni za hatari na kwa nini ni ngumu kushughulika nazo? Kwa sababu, kama vile Paulo alivyoendelea kuandika, watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, . . . wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, . . . wakali.” Je, huo si ufafanuzi sahihi wa jinsi watu wengi wanavyojiendesha leo?—2 Timotheo 3:1-3.

Biblia husema kwamba nyakati hizi za hatari zingetukia “katika siku za mwisho,” kabla jamii nzima ya kibinadamu haijashuhudia mabadiliko makubwa. Mabadiliko hayo yataathiri watu wote, wadogo kwa wakubwa. Ni mabadiliko ya aina gani? Hivi karibuni serikali ya kimbingu itachukua mahali pa utawala wa kibinadamu, na raia watafurahia “wingi wa amani” kila mahali. “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Hali ya kuhangaika na kuwa na wasiwasi haitakuwako tena.—Zaburi 37:11, 29.

Ni Biblia pekee ambayo hutoa ufahamu wenye kina na unaotegemeka kuhusu wakati ujao. Kijana anapojua mambo anayoweza kutarajia katika miaka michache inayokuja, anaweza kujitayarisha kwa ajili ya matukio hayo na kuhisi akiwa salama na hivyo kudhibiti maisha yake. Hisia hiyo hupunguza mkazo na wasiwasi. Kwa hiyo Biblia inazungumzia uhitaji huo wa pekee wa vijana wa kutaka kuelewa jamii na kujua mambo yatakayotokea wakati ujao.

Kufanikiwa Ujanani

Ni jambo gani linaloamua kama mtu atapata mafanikio ujanani? Je, ni elimu ya juu, vitu vya kimwili, na marafiki wengi? Huenda wengi wakafikiri hivyo. Miaka ya utineja na miaka ya mapema ya 20 yapaswa kumtayarisha mtu kwa ajili ya maisha ya baadaye. Yaani, kufanikiwa ujanani kwaweza kuwa ishara ya mambo yatakayotukia baadaye.

Kama vile tumeona, Biblia yaweza kumsaidia kijana afanikiwe ujanani. Vijana wengi wameona ukweli wa jambo hilo katika maisha yao. Wao husoma Neno la Mungu kila siku na kutumia mambo wanayojifunza. (Ona “Dokezo Linalofaa Kutoka kwa Mtumishi Mchanga wa Yehova,” katika ukurasa wa 6.) Kwa kweli, Biblia ni kitabu kinachowafaa vijana leo kwa sababu kinaweza kuwasaidia wawe ‘walioandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.’—2 Timotheo 3:16, 17.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Mojawapo ya siri za kufanikiwa ujanani ni kupatana na wengine

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Labda hakuna rika lolote ambalo hutaka kujua mambo yanayotokea na kwa nini yanatokea kuliko vijana

[Sanduku katika ukurasa wa 6, 7]

Dokezo Linalofaa Kutoka kwa Mtumishi Mchanga wa Yehova

Alexander ana umri wa miaka 19. Alilelewa katika familia ya Mashahidi wa Yehova, naye hufurahia sana kudhihirisha imani yake kwa moyo wote. Lakini hakuwa akifanya hivyo mbeleni. Alexander aeleza hivi:

“Amini usiamini, nilishirikiana na Mashahidi wa Yehova nikiwa kijana asiyebatizwa kwa miaka zaidi ya saba. Wakati huo, ibada yangu haikuwa ya moyo wote, ilikuwa kama desturi tu. Nafikiri sikuwa na ujasiri wa kujichunguza kwa unyofu.”

Kisha Alexander akabadili mtazamo wake. Aendelea kusema:

“Wazazi na rafiki zangu katika kutaniko walizidi kunihimiza nisome Biblia kila siku, ili nimfahamu Yehova kibinafsi. Hatimaye, nikaamua kujaribu. Kwa hiyo nikaacha kutumia muda mwingi kutazama televisheni na nikawa na zoea la kusoma Biblia kila asubuhi. Hatimaye, nikaanza kuielewa Biblia. Nikafahamu jinsi inavyoweza kunisaidia mimi binafsi. Na jambo lililo la maana hata zaidi, nilifahamu kwamba Yehova anataka nimjue. Nilipotilia maanani jambo hilo, uhusiano wangu pamoja naye ulianza kukua, na urafiki wangu pamoja na wengine kutanikoni ukaboreka. Biblia imebadili maisha yangu kwa njia iliyoje! Ninapendekeza kwamba kila mtumishi mchanga wa Yehova aisome Biblia kila siku.”

Kuna mamilioni ya vijana ulimwenguni pote wanaoshirikiana na Mashahidi wa Yehova. Je, wewe ni mmoja wao? Je, ungependa kufaidika kwa kusoma Biblia kwa ukawaida? Kwa nini usifuate mfano wa Alexander? Punguza mambo yasiyo ya maana sana na uwe na zoea la kusoma Biblia kila siku. Bila shaka, utanufaika.