Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu Kinachopuuzwa na Vijana Wengi

Kitabu Kinachopuuzwa na Vijana Wengi

Kitabu Kinachopuuzwa na Vijana Wengi

“NINAWEZAJE kuwa na hakika kabisa kwamba Biblia ni Neno la Mungu? Kitabu hicho hakinipendezi,” akasema mwanamke mmoja kijana anayeitwa Beate.

Nchini Ujerumani, anamoishi Beate, vijana wengi wana maoni kama yake; kwa hiyo, hawaoni umuhimu wa kusoma Biblia. Uchunguzi uliofanywa huko hivi karibuni, ulifunua kwamba asilimia 1 hivi ya vijana husoma Biblia mara nyingi sana, asilimia 2 mara nyingi, asilimia 19 mara chache sana, na karibu asilimia 80 hawaisomi kamwe. Yaelekea kuna idadi kama hiyo katika nchi nyingine, labda hata katika nchi unamoishi. Ni wazi kwamba Biblia ni kitabu kinachopuuzwa na vijana wengi.

Basi, haishangazi kwamba vijana wengi wanafahamu mambo machache sana kuhusu Biblia! Mapema katika mwaka wa 2000, gazeti Lausitzer Rundschau liliripoti kuhusu uchunguzi fulani uliofunua idadi ya vijana wanaofahamu zile Amri Kumi na ambao huzitumia kama mwongozo maishani. Kati ya watu wenye umri wa miaka 60 na zaidi, asilimia 67 ndio waliozijua amri hizo na kuongozwa nazo; na watu wenye umri wa miaka inayopungua 30, idadi ilikuwa asilimia 28 tu. Naam, vijana wengi hawafahamu Neno la Mungu.

Wengine Wana Maoni Tofauti

Kwa upande mwingine, kuna mamilioni ya vijana ulimwenguni pote wanaoliona Neno la Mungu kuwa lenye thamani sana. Kwa mfano, Alexander mwenye umri wa mika 19 husoma Biblia kila asubuhi kabla hajaenda kazini. “Hiyo ndiyo njia bora zaidi ya kuanza siku,” asema. Sandra ana zoea la kusoma sehemu fulani ya Biblia kila jioni. “Kuisoma kumekuwa zoea langu la kila siku,” asema. Naye Julia, mwenye umri wa miaka 13, tayari ana zoea la kusoma angalau sura moja ya Biblia kabla hajaenda kulala. “Ninaifurahia kwelikweli, na ningependa kudumisha zoea hilo hata wakati ujao.”

Ni maoni gani yaliyo sahihi na ya hekima? Je, inafaa kusoma Biblia? Je, ni yenye thamani na muhimu kwa vijana? Unaonaje?