Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kung’aa Kama Wamulikaji Katika Jiji la Nuru

Kung’aa Kama Wamulikaji Katika Jiji la Nuru

Kung’aa Kama Wamulikaji Katika Jiji la Nuru

Shime ya jiji la Paris ni Fluctuat Nec Mergitur, au “Unapigwa na mawimbi lakini hauzami.”

KAMA vile meli inayokumbwa na mawimbi, jiji la Paris limekabili uvamizi mwingi wa wageni, na uasi wa wakazi wake kwa zaidi ya miaka 2,000 iliyopita. Sasa jiji la Paris ni mojawapo ya majiji yenye kuvutia zaidi ulimwenguni kwa sababu ya majengo yake makubwa, njia zake pana zenye miti pande zote, na majumba ya makumbusho yaliyo mashuhuri ulimwenguni. Wengine huliona kuwa jiji linalotembelewa sana na washairi, wachoraji, na wanafalsafa. Wengine hufurahia vyakula vya Paris vyenye kupendeza na huvutiwa na mafundi wake stadi wa nguo za wanawake.

Kulingana na historia, jiji la Paris limekuwa ngome ya Ukatoliki. Miaka zaidi ya mia mbili iliyopita, jiji la Paris liliitwa Jiji la Nuru kwa sababu ya fungu muhimu lililotimiza kuhusiana na harakati iliyoitwa Enlightenment (harakati ya wanafalsafa ya karne ya 18) ya wasomi wa Ulaya. Leo, wakazi wengi wa Paris wawe wanajua au hawajui wameathiriwa na falsafa ya wakati huo kuliko wanavyoathiriwa na dini.

Hata hivyo, hekima ya wanadamu haijaboresha maisha ya watu kama ilivyotarajiwa. Wengi leo wanatafuta nuru kutoka chanzo kingine. Kwa miaka ipatayo 90 sasa, Mashahidi wa Yehova wamekuwa ‘waking’aa wakiwa wamulikaji” jijini Paris. (Wafilipi 2:15) Kama vile mabaharia stadi, wamelazimika kufanya marekebisho daima kwa sababu ya mawimbi au matukio yanayobadilika-badilika ili kuleta “vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote.”—Hagai 2:7.

Ni Vigumu Kuhubiri Katika Jiji Hilo

Katika mwaka wa 1850, jiji la Paris lilikuwa na wakazi 600,000. Sasa idadi ya watu, kutia ndani wale wanaoishi kwenye vitongoji ni zaidi ya milioni tisa. Ongezeko hilo la watu limefanya Paris liwe jiji lenye watu wengi zaidi wa kutoka tamaduni mbalimbali kuliko jiji jinginelo nchini Ufaransa. Ni kituo cha elimu ya juu ulimwenguni, lina mojawapo ya vyuo vikuu vya kale zaidi ulimwenguni, na lina wanafunzi wapatao 250,000. Jambo fulani lisilopendeza kuhusu Paris, ni vitongoji vyake vyenye nyumba za orofa ndefu ambamo mna uhalifu na ukosefu wa kazi za kuajiriwa. Bila shaka, Mashahidi wa Yehova wanahitaji kuwa stadi na wenye kubadilikana na hali ili kuhubiri habari njema kwa njia inayovutia watu wa aina zote.—1 Timotheo 4:10.

Watalii zaidi ya milioni 20 huzuru jiji la Paris kila mwaka. Wanaweza kupanda mnara wa Eiffel Tower, watembee kandokando ya mto Seine, au kukaa kwenye mikahawa iliyo kandokando ya barabara, na kufurahia mandhari ya mikahawa hiyo. Hata hivyo, maisha ya wakazi wa Paris ni yenye hekaheka nyingi. “Watu huwa na haraka-haraka sikuzote,” aeleza Christian, mhudumu wa wakati wote. “Wanaporudi kutoka kazini, wanakuwa wamechoka kabisa.” Si rahisi kuzungumza na watu hao wenye shughuli nyingi.

Hata hivyo, tatizo kubwa ambalo Mashahidi wa Yehova hukabili jijini Paris, ni kuwapata watu nyumbani mwao. Nyumba fulani zina mfumo wa mawasiliano ya ndani. Hata hivyo, kwa kuwa uhalifu unazidi kuongezeka, mara nyingi nyumba za orofa zina mfumo wa usalama wa kielektroni ambao umewekwa kwenye kiingilio. Bila shaka jambo hilo laonyesha ni kwa nini katika sehemu fulani, kuna Shahidi mmoja kati ya watu 1,400. Kwa hiyo watu wengi wanazidi kutoa ushahidi kwa simu na kutoa ushahidi wa vivi hivi. Je, Mashahidi wa Yehova wamefaulu kuacha ‘nuru yao ing’ae’ katika njia nyinginezo?—Mathayo 5:16.

Kuna fursa nyingi na pia pahali pengi pa kutoa ushahidi wa vivi hivi. Martine aliona mwanamke fulani aliyeonekana kuwa na huzuni akiwa amesimama kwenye kituo cha basi. Mwanamke huyo alikuwa amefiwa na binti yake wa pekee. Martine alimpa broshua yenye ujumbe wa Biblia unaofariji kuhusu tumaini la ufufuo. Kisha hawakukutana tena kwa miezi kadhaa. Martine alipomwona mwanamke huyo tena, aliweza kuanzisha funzo la Biblia pamoja naye. Licha ya upinzani kutoka kwa mume wake, mwanamke huyo akawa Shahidi.

Kutoa Ushahidi wa Vivi Hivi kwa Njia Yenye Matokeo

Mfumo wa usafiri wa umma wa jiji la Paris ni mojawapo ya mifumo bora zaidi ulimwenguni. Mfumo maarufu wa reli za chini ya ardhi, husafirisha abiria 5,000,000 kila siku. Kituo cha Paris cha Châtelet-Les-Halles, kilicho chini ya ardhi ndicho kikubwa zaidi na chenye shughuli nyingi zaidi ulimwenguni. Kuna fursa nyingi sana za kukutana na watu kwenye kituo hicho. Alexandra hutumia njia hiyo ya usafiri anapoenda kazini kila siku. Siku moja alizungumza na mwanamume fulani kijana aliyekuwa na ugonjwa usiotibika wa lukemia. Alexandra alimpa trakti inayozungumzia tumaini la Paradiso. Walikuwa na mazungumzo ya Biblia kwa muda wa majuma sita, na mazungumzo hayo yalifanywa mahali palepale na siku ileile. Kisha siku moja mtu huyo akaacha kuja. Muda mfupi baada ya hapo, mke wake alimpigia simu Alexandra na kumwambia aende hospitalini, kwa kuwa mume wake alikuwa mahututi. Kwa kusikitisha, Alexandra alifika na kukuta amekufa. Baada ya mumewe kufa, mwanamke huyo alihamia Bordeaux, kusini-magharibi mwa Ufaransa, ambapo alitembelewa na Mashahidi wa eneo hilo. Alexandra alifurahi kama nini alipopata habari mwaka mmoja baadaye kwamba mjane huyo alikuwa amebatizwa na kuwa Mkristo Shahidi wa Yehova, akiwa na tumaini la kuona mume wake atakapofufuliwa!—Yohana 5:28, 29.

Mwanamke mmoja Mkristo ambaye ni mzee-mzee alizungumza na Renata kwenye gari-moshi lililokuwa likisafiri kutoka Paris hadi Limoges, katikati ya Ufaransa. Akiwa katika nchi ya kwao huko Poland, Renata alikuwa amejifunza theolojia, Kiebrania, na Kigiriki kwa muda wa miaka mitano, lakini hakumwamini Mungu. Miezi mitatu kabla ya hapo, alikuwa amesali kwa Mungu. Ijapokuwa hakupendezwa hasa na mambo aliyokuwa akisema yule dada mzee-mzee na bila kufikiri kwamba dada huyo angewasiliana naye tena, Renata alimpa namba yake ya simu. Hata hivyo, dada huyo mwenye bidii alihakikisha kwamba Renata alitembelewa baada ya muda mfupi. Wenzi waliofunga ndoa ambao ni Mashahidi, walipomtembelea, Renata alijiuliza, ‘Watanifundisha nini?’ Licha ya elimu yake ya theolojia, Renata alivutiwa na kweli ya Biblia. “Nilielewa mara moja kwamba hii ni kweli,” aeleza. Sasa anafurahi kuwaeleza wengine ujumbe wa Biblia.

Michèle alikuwa akijifunza kuendesha gari. Wanafunzi wengine katika darasa lake wakaanza kuzungumza juu ya ngono kabla ya ndoa. Michèle akapinga jambo hilo. Juma moja baadaye, mfunzi wa kuendesha gari, Sylvie, akamwuliza: “Je, wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Sylvie alivutiwa na maoni ya Michèle’ yanayotegemea Biblia. Funzo la Biblia lilianzishwa, na mwaka mmoja baadaye Sylvie akabatizwa.

Mbuga na bustani nyingi za Paris ni mahali pazuri sana pa kuzungumza na watu. Josette alienda bustanini wakati wa mapumziko ambapo alikutana na Aline, mwanamke mmoja mzee-mzee, aliyekuwa akitembea-tembea huko. Josette alimweleza ahadi nzuri zinazopatikana katika Biblia. Walipanga kuanzisha funzo la Biblia, na baada ya muda mfupi Aline akafanya maendeleo na kubatizwa. Sasa, Aline, ambaye ana umri wa miaka 74 ni painia wa kawaida mwenye matokeo, ambaye hufurahi kuwaeleza wengine kweli ya Kikristo.

Nuru kwa Mataifa Yote

Mashahidi wanaoishi jijini Paris hawahitaji kusafiri hadi nchi za mbali ili kufurahia tamaduni za namna mbalimbali. Karibu asilimia 20 ya watu wanaoishi humo ni wageni. Kuna makutaniko na vikundi vya Kikristo katika lugha zipatazo 25.

Mara nyingi ustadi na ubunifu hutokeza matokeo mazuri katika mgawo huu wa pekee wa kueneza injili. Shahidi mmoja Mfilipino alibuni eneo lake la pekee. Amefaulu kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia kwa kuanzisha mazungumzo na Wafilipino wengine anapokuwa akinunua vitu madukani.

Ni jambo linalothawabisha kuwa na ujasiri wa kuhubiri. Mnamo Desemba 1996, Mashahidi katika kutaniko fulani linalozungumza lugha ya kigeni walipopata habari kwamba wanasarakasi mashuhuri ulimwenguni wangekuja katika mji huo, waliamua kuzungumza na wanasarakasi hao. Jioni moja baada ya maonyesho, walifaulu kuzungumza na wanasarakasi hao walipokuwa wakirudi kwenye hoteli walimokaa. Kwa sababu ya ujasiri huo waliwaachia watu Biblia 28, vitabu vya Kikristo 59, broshua 131, na magazeti 290. Baada ya kukaa huko kwa muda wa majuma matatu, mwanasarakasi mmoja aliuliza hivi: “Ninawezaje kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Mwingine alisema: “Nitahubiri katika nchi yetu!”

Kupata Hazina Zilizofichwa

Watazamapo mahali popote pale, wageni wanaotembea katika jiji la Paris huona majengo ambayo ni hazina zenye kupendeza za nyakati za kale. Hata hivyo, vitu vyenye thamani zaidi bado vitapatikana. Aniza alienda nchini Ufaransa pamoja na mjomba wake ambaye ni balozi. Yeye husoma Biblia kwa ukawaida akiwa nyumbani. Siku moja alipokuwa akitoka nyumbani mbiombio, painia mmoja alimpa trakti yenye kichwa Sababu Kwa Nini Wewe Unaweza Kuitumaini Biblia. Alipanga kukutana naye juma lililofuata, na funzo la Biblia likaanzishwa. Aniza alipingwa sana na watu wa familia yake lakini akaendelea kujifunza hadi akabatizwa. Anaonaje pendeleo lake la kuwaeleza wengine kweli? “Mwanzoni ilikuwa vigumu kuhubiri kwa sababu mimi ni mtu mwenye haya. Hata hivyo, mimi huchochewa ninapoisoma Biblia. Siwezi kupata amani ya akili nisipohubiri.” Mashahidi wengi jijini Paris wana mtazamo kama huo na wana “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”—1 Wakorintho 15:58.

Kweli ya Biblia pia inang’aa kwenye miradi ya ujenzi ya viunga vya Paris, na kufunua “vito” vingine. Bruce alienda kumtembelea rafiki yake ambaye alikuwa amepata tu kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, akitaka kumwomba kaseti za nyimbo. Bruce alipata rafiki yake akizungumza na baadhi ya marafiki wake kuhusu Biblia, naye akajiunga na mazungumzo hayo. Alikubali kujifunza Biblia, lakini akawa na matatizo fulani. “Nilikuwa nimejulikana sana katika eneo hilo. Kaka yangu alikuwa akipigana sikuzote, nami nilikuwa nikipanga karamu za dansi zenye kelele nyingi. Wengi wangetambuaje kwamba nilikuwa nataka kuwa Shahidi?” Licha ya kuombwa mara nyingi apange karamu hizo, Bruce alikataa. Alianza kuhubiri mwezi mmoja baadaye: “Kila mtu katika eneo hilo alitaka kujua ni nini kilichonifanya niwe Shahidi.” Muda mfupi baadaye akabatizwa. Baada ya muda, alipata pendeleo la kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma.

Jitihada nyingi inahitajiwa ili kutafuta hazina. Hata hivyo, kazi hiyo inaweza kufurahisha jinsi gani inapokuwa na matokeo mazuri! Jacky, Bruno na Damien walikuwa waokaji jijini Paris. “Haikuwa rahisi kutupata kwa sababu tulifanya kazi sikuzote na hatukuwa tukipatikana nyumbani kamwe,” aeleza Jacky. Patrick, ambaye ni painia wa kawaida, aliona kwamba kulikuwa na vyumba vidogo juu ya jengo fulani, na akaona kwamba angalau chumba kimoja kilikuwa na mtu. Jitihada yake yenye kuendelea ya kumfikia mwenye nyumba huyo ilikuwa na matokeo mazuri wakati ambapo hatimaye alasiri moja alimpata Jacky, aliyekuwa akiishi humo kwa muda mfupi. Matokeo yakawaje? Marafiki hao watatu wakawa Mashahidi na waliweza kupata kazi nyingine iliyowaruhusu kushiriki kikamili katika utendaji wa kitheokrasi.

Kukomesha Uvumi

Hivi karibuni, baadhi ya vyombo vya habari nchini Ufaransa vimeonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova ni madhehebu hatari. Mnamo mwaka wa 1996, Mashahidi walishiriki kwa moyo wote kugawanya zaidi ya nakala milioni tisa za trakti iliyokuwa na habari ya pekee yenye kichwa Unachopaswa Kujua Kuhusu Mashahidi wa Yehova (Jehovah’s Witnesses—What You Need to Know). Kulikuwa na matokeo mazuri sana.

Jitihada ya pekee ilifanywa ili kufikia kila mtu. Maafisa wengi waliwashukuru sana Mashahidi. Mshauri mmoja wa manispaa aliandika hivi: “Mashahidi wa Yehova wamefanya vizuri kugawanya trakti hii. Inasahihisha uwongo uliosemwa.” Daktari mmoja alisema: “Nimekuwa nikisubiri habari hii kwa muda mrefu!” Mtu mmoja kutoka ujirani wa jiji la Paris aliandika hivi: “Nilisoma trakti Jehovah’s Witnesses—What You Need to Know pasipo kutarajia. Ningependa kujua mengi zaidi na kunufaika na funzo la Biblia la nyumbani bila malipo.” Mwingine aliandika hivi: “Asanteni kwa kueleza mambo waziwazi.” Bibi mmoja Mkatoliki aliwaambia Mashahidi hivi: Aha! Hatimaye mmekanusha uwongo huo!”

Vijana wengi Mashahidi wanaoishi katika ujirani wa jiji la Paris walipata furaha ya pekee wakati wa kampeni ya kuhubiri iliyopangwa wakati wa sherehe ya Siku za Vijana Wakatoliki Ulimwenguni mwaka wa 1997. Ingawa halijoto ilizidi digrii 32 Selsiasi, vijana wapatao 2,500 walishiriki. Baada ya siku chache tu, waliwaachia vijana kutoka sehemu zote za ulimwengu nakala 18,000 za broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote. Mbali na kutoa ushahidi juu ya jina la Yehova na kupanda mbegu za kweli, kampeni hiyo iliwachangamsha Mashahidi hao wachanga. Dada mmoja mchanga, aliyefupisha likizo yake ili ashiriki kikamili kampeni hiyo ya pekee, aliandika hivi: “Yehova ana watu wenye furaha duniani wanaotumia nguvu zao kulisifu jina lake. Siku hizi mbili zenye kuthawabisha sana, kwa kweli ni bora kuliko likizo zote maishani! (Zaburi 84:10)”

Februari 28, 1998, iliashiria siku ya ukumbusho wa 65 tangu amri itolewe na Hitler ya kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani. Mashahidi nchini Ufaransa walikodisha majumba na kutumia tarehe hiyo kuonyesha umma video Jehovah’s Witnesses Stand Firm Against Nazi Assault ambayo huonyesha jinsi watu wa Yehova walivyonyanyaswa. Waligawanya vikaratasi vya mialiko zaidi ya milioni saba. Wanahistoria na watu fulani waliokuwa wamefungwa kwenye kambi hizo hapo zamani, walisimulia mambo yenye kuhuzunisha. Katika ujirani wa jiji la Paris, watu wapatao 5,000 walihudhuria, kutia ndani idadi kubwa ya watu ambao si Mashahidi.

Watu wengi katika jiji la Paris hufurahia nuru ya kiroho, na wanafurahi kwamba watangazaji wa Ufalme wanang’aa wakiwa wamulikaji. Ni kama alivyosema Yesu: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” (Mathayo 9:37) Azimio la Mashahidi wa Yehova la kukabiliana na magumu ya kuhubiri katika jiji hilo limefanya Paris kuwa Jiji la Nuru katika maana ya pekee, na hivyo kumletea Yehova sifa.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Makao Makuu ya Halmashauri ya Jiji

[Picha katika ukurasa wa 9]

Jumba la Makumbusho la Louvre

[Picha katika ukurasa wa 9]

Jumba la Opera la Garnier

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kuwaeleza watu wenye shughuli nyingi ujumbe wa Biblia mahali popote wanapopatikana