Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msife Moyo Katika Kufanya Lililo Bora

Msife Moyo Katika Kufanya Lililo Bora

Msife Moyo Katika Kufanya Lililo Bora

“Acheni tusife moyo katika kufanya lililo bora, kwa maana katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—WAGALATIA 6:9.

1, 2. (a) Kwa nini uvumilivu unahitajiwa ili kumtumikia Mungu? (b) Abrahamu alionyeshaje uvumilivu, na ni nini kilichomsaidia kufanya hivyo?

TUKIWA Mashahidi wa Yehova, tunafurahia kufanya mapenzi ya Mungu. Pia tunaburudika kuchukua “nira” ya uanafunzi. (Mathayo 11:29) Hata hivyo, si rahisi sikuzote kumtumikia Yehova na Kristo. Mtume Paulo alionyesha jambo hilo waziwazi alipowasihi Wakristo wenzake hivi: “Mna uhitaji wa uvumilivu, ili kwamba, baada ya nyinyi kuwa mmefanya mapenzi ya Mungu, mpate kupokea utimizo wa ahadi.” (Waebrania 10:36) Uvumilivu unahitajiwa kwa sababu linaweza kuwa jambo gumu kumtumikia Mungu.

2 Bila shaka, maisha ya Abrahamu yanathibitisha jambo hilo. Nyakati nyingi alikabiliwa na maamuzi magumu na hali zenye mkazo. Kuamuriwa aache maisha ya anasa huko Uru ulikuwa mwanzo tu. Baada ya muda mfupi, Abrahamu alikabiliwa na njaa, uadui wa majirani, chuki ya watu fulani wa jamaa yake, ukatili wa vita, na hata karibu ampoteze mke wake. Na bado angekabili majaribu makubwa zaidi. Lakini Abrahamu hakuacha kutenda yaliyo mema. Hilo ni jambo lenye kutokeza ukifikiria kwamba hakuwa na Biblia nzima, kama sisi leo. Hata hivyo, yaelekea alijua juu ya unabii wa kwanza, ambao Mungu alisema: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao [“mbegu,” NW] wako na uzao [“mbegu,” NW] wake.” (Mwanzo 3:15) Bila shaka, Abrahamu angechukiwa na Shetani kwa kuwa ni kupitia yeye Mbegu huyo angekuja. Yaelekea kufahamu jambo hilo kulimsaidia Abrahamu avumilie majaribu yake kwa furaha.

3. (a) Kwa nini watu wa Yehova leo watarajie kupatwa na dhiki? (b) Andiko la Wagalatia 6:9 linatupa kitia moyo gani?

3 Leo watu wa Yehova pia wanapaswa kutarajia kupatwa na dhiki. (1 Petro 1:6, 7) Kwani andiko la Ufunuo 12:17 latuonya kwamba Shetani ‘anafanya vita’ na mabaki watiwa-mafuta. “Kondoo wengine” pia hushambuliwa na Shetani kwa sababu ya ushirikiano wao wa karibu na watiwa-mafuta. (Yohana 10:16) Mbali na upinzani ambao Wakristo wanaweza kupata katika huduma yao ya hadharani, wanaweza pia kupatwa na majaribu yenye mkazo katika maisha yao ya kibinafsi. Paulo anatuhimiza hivi: “Acheni tusife moyo katika kufanya lililo bora, kwa maana katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.” (Wagalatia 6:9) Naam, ingawa Shetani ameazimia kuharibu imani yetu, lazima tumpinge tukiwa thabiti katika imani. (1 Petro 5:8, 9) Mwenendo wetu wa uaminifu waweza kuwa na matokeo gani? Andiko la Yakobo 1:2, 3 laeleza hivi: “Fikirieni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mkutanapo na majaribu ya namna mbalimbali, kama mjuavyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu hutokeza uvumilivu.”

Shambulio la Moja kwa Moja

4. Shetani ametumiaje mashambulio ya moja kwa moja ili kujaribu kuvunja uaminifu-maadili wa watu wa Mungu?

4 Bila shaka maisha ya Abrahamu yanaonyesha “majaribu ya namna mbalimbali” ambayo Mkristo anaweza kukabili leo. Kwa mfano, ilimbidi kuchukua hatua dhidi ya wavamizi wa Shina. (Mwanzo 14:11-16) Si ajabu kwamba Shetani anaendelea kutushambulia moja kwa moja kupitia mnyanyaso. Tangu Vita ya Pili ya Ulimwengu imalizike, serikali za nchi nyingi zimepiga marufuku kazi ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova ya kuelimisha watu. Kitabu 2001 Yearbook of Jehovah’s Witnesses charipoti juu ya ujeuri ambao Wakristo huko Angola walitendewa na adui. Kwa kumtegemea Yehova, ndugu zetu katika nchi hizo wamekataa katakata kuacha kazi ya Kikristo! Badala ya kuchukua hatua ya ujeuri au ya uasi, ndugu hao wameendelea kwa busara na kazi yao ya kuhubiri.—Mathayo 24:14.

5. Huenda vijana wakanyanyaswaje shuleni?

5 Hata hivyo, si lazima mnyanyaso uhusishe ujeuri. Hatimaye, Abrahamu alibarikiwa kupata wana wawili—Ishmaeli na Isaka. Andiko la Mwanzo 21:8-12 latuambia kwamba katika pindi moja Ishmaeli alikuwa ‘anamfanyia Isaka dhihaka.’ Katika barua yake kwa Wagalatia, Paulo anaonyesha kwamba dhihaka hiyo haikuwa mchezo tu wa kitoto, kwa kuwa anaeleza kwamba Ishmaeli alikuwa anamnyanyasa Isaka! (Wagalatia 4:29) Kwa hiyo, dhihaka na matusi ya wanashule wenzetu yanaweza kwa usahihi kuitwa mnyanyaso. Mkristo kijana aitwaye Ryan anakumbuka jinsi alivyonyanyaswa na wanadarasa wenzake: “Dakika 15 nilizokuwa kwenye basi kwenda na kurudi kutoka shuleni zilionekana kama muda mrefu sana kwa sababu ya kutusiwa. Walinichoma kwa vibanio vya karatasi walivyokuwa wamepasha moto kwa kiberiti.” Kwa nini walimdhulumu hivyo? “Mazoezi niliyopata katika tengenezo la Mungu yalinifanya niwe tofauti na vijana wengine shuleni.” Hata hivyo, kwa utegemezo wa wazazi wake, Ryan aliweza kuvumilia kwa uaminifu. Enyi vijana, je, dhihaka za marika wenu zimefanya mvunjike moyo? Msikate tamaa! Kwa kuvumilia kwa uaminifu, mtaona utimizo wa maneno haya ya Yesu: “Wenye furaha ni nyinyi watu wawashutumupo na kuwanyanyasa nyinyi na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo ovu dhidi yenu kwa ajili yangu.”—Mathayo 5:11.

Mahangaiko ya Kila Siku

6. Ni mambo gani yawezayo kuharibu mahusiano miongoni mwa Wakristo wenzetu leo?

6 Mengi ya majaribu tunayokabiliana nayo leo yanahusisha mahangaiko ya kawaida ya kila siku. Ilimbidi Abrahamu akabili ugomvi ambao ulitokea kati ya wachungaji wake na wale wa mpwa wake Loti. (Mwanzo 13:5-7) Hali kadhalika leo, tofauti za nyutu na kuwa na wivu katika mambo madogo-madogo kunaweza kuharibu mahusiano na hata kuhatarisha amani ya kutaniko. “Kwa maana ambako kuna wivu na ugomvi, hapo ukosefu wa utaratibu na kila jambo ovu vipo.” (Yakobo 3:16) Ni muhimu kama nini kwetu kutokata tamaa bali, kama Abrahamu alivyofanya, kutanguliza amani badala ya kiburi na kutafuta masilahi ya wengine!—1 Wakorintho 13:5; Yakobo 3:17.

7. (a) Mtu apaswa kufanya nini iwapo ameumizwa na Mkristo mwenzake? (b) Abrahamu aliweka kielelezo gani kizuri katika kudumisha mahusiano mazuri na wengine?

7 Inaweza kuwa vigumu kuwa wenye amani tunapohisi kwamba tumetendewa isivyofaa na mwamini mwenzetu. Andiko la Mithali 12:18 lasema: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.” Maneno yanenwayo bila kufikiri, hata yakinenwa bila ubaya wowote, yanaweza kuumiza sana. Maumivu hayo yanaweza kuwa makali hata zaidi tukihisi kwamba tumesingiziwa jambo au mtu amepiga porojo zenye kutudhuru. (Zaburi 6:6, 7) Lakini Mkristo hawezi kuruhusu maumivu ya kihisia-moyo yamkatishe tamaa! Iwapo hali yako iko hivyo, chukua hatua ya kurekebisha mambo kwa kuzungumza kwa fadhili na mtu aliyekukosea. (Mathayo 5:23, 24; Waefeso 4:26) Uwe na mwelekeo wa kumsamehe mtu huyo. (Wakolosai 3:13) Kwa kutoweka kinyongo, tunaweza kumaliza maumivu ya kihisia-moyo na kuwa na uhusiano mzuri na ndugu yetu. Abrahamu hakuweka kinyongo chochote ambacho huenda alihisi kuelekea Loti. Kwani, Abrahamu alichukua hatua mara moja kumwokoa Loti na familia yake!—Mwanzo 14:12-16.

Majaribu Tunayojiletea Wenyewe

8. (a) Wakristo wanawezaje ‘kujichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi’? (b) Kwa nini Abrahamu aliweza kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu vitu vya kimwili?

8 Ni kweli kwamba majaribu mengine tunajiletea wenyewe. Kwa mfano, Yesu aliwaamuru hivi wafuasi wake: “Komeni kujiwekea akiba ya hazina duniani, ambako nondo na kutu hula kabisa, na ambako wezi huvunja na kuiba.” (Mathayo 6:19) Hata hivyo, ndugu wengine ‘hujichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi’ kwa kutanguliza masilahi ya kimwili badala ya masilahi ya Ufalme. (1 Timotheo 6:9, 10) Abrahamu alikuwa tayari kuacha maisha ya anasa ili kumpendeza Mungu. “Kwa imani yeye alikaa kama mgeni asiye mzalia katika nchi ya ahadi kama katika nchi ya ugenini, na kukaa katika mahema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ileile. Kwa maana alikuwa akingojea jiji lililo na misingi halisi, ambalo mjenzi na mfanyi wa jiji hilo ni Mungu.” (Waebrania 11:9, 10) Imani ya Abrahamu katika “jiji” la wakati ujao, serikali ya Mungu, ilimsaidia asitegemee utajiri. Je, halingekuwa jambo la hekima kwetu kufanya vivyo hivyo?

9, 10. (a) Tamaa ya makuu inawezaje kutokeza jaribu? (b) Ndugu anawezaje leo kujiendesha kama ‘aliye mdogo zaidi’?

9 Fikiria pia jambo jingine. Biblia hutoa agizo hili thabiti: “Ikiwa yeyote afikiri yeye ni kitu wakati yeye si kitu, anadanganya akili yake mwenyewe.” (Wagalatia 6:3) Isitoshe, tunahimizwa ‘tusifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa majisifu ya bure, bali kwa hali ya akili ya kujishusha chini.’ (Wafilipi 2:3) Wengine hujiletea majaribu kwa kushindwa kutumia ushauri huo. Wakichochewa na tamaa ya makuu badala ya tamaa ya kufanya “kazi njema,” wanavunjika moyo na kutoridhika wanapokosa kupata mapendeleo kutanikoni.—1 Timotheo 3:1.

10 Abrahamu aliweka kielelezo kizuri kwa ‘kutojifikiria mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima.’ (Waroma 12:3) Alipokutana na Melkizedeki, Abrahamu hakutenda kana kwamba hali yake yenye kukubalika kwa Mungu ilimfanya awe mtu bora zaidi. Kinyume chake, alitambua cheo cha Melkizedeki akiwa kuhani kuwa bora kwa kumtolea sehemu ya kumi. (Waebrania 7:4-7) Vivyo hivyo, Wakristo leo wanapaswa kuwa tayari kujiendesha kama ‘walio wadogo zaidi’ bila kutaka kujionyesha mbele ya watu. (Luka 9:48) Iwapo wale wenye kuongoza kutanikoni wanaonekana kana kwamba wanakuzuia usipate mapendeleo fulani, jichunguze kwa unyofu na kuona jinsi uwezavyo kuboresha utu wako au njia yako ya kushughulikia mambo. Badala ya kuwa na uchungu kwa sababu ya mapendeleo ambayo huna, tumia kikamili pendeleo ulilo nalo—lile la kuwasaidia wengine wapate kumjua Yehova. Naam, “jinyenyekezeni chini ya mkono wa Mungu wenye uweza, ili apate kuwakweza nyinyi katika wakati upasao.”—1 Petro 5:6.

Kuwa na Imani Katika Vitu Visivyoonekana

11, 12. (a) Kwa nini huenda wengine katika kutaniko wakaacha kuwa na uharaka? (b) Abrahamu aliweka kielelezo gani kizuri katika kutegemeza maisha yake juu ya imani yake katika ahadi za Mungu?

11 Huenda jaribu jingine likahusisha mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo ambao huenda ukaonekana kama unakawia sana. Kulingana na 2 Petro 3:12, Wakristo wanapaswa kuwa ‘wakingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’ Hata hivyo, wengi wamengoja “siku” hii kwa miaka mingi, wengine hata kwa miongo mingi. Kwa hiyo, huenda wengine wakavunjika moyo na kuacha kuwa na uharaka.

12 Hebu fikiria kielelezo cha Abrahamu tena. Alitegemeza maisha yake yote juu ya imani yake katika ahadi za Mungu, hata ingawa hakukuwa na uwezekano wowote kwamba zingetimizwa katika maisha yake. Ni kweli kwamba aliishi muda mrefu vya kutosha kuona mwanawe Isaka akikua na kuwa mtu mzima. Lakini karne nyingi zingepita kabla uzao wa Abrahamu kuweza kulinganishwa na “nyota za mbinguni” au “mchanga ulioko pwani.” (Mwanzo 22:17) Hata hivyo, Abrahamu hakuwa na uchungu wala hakuvunjika moyo. Hivyo, mtume Paulo alisema hivi kuhusu Abrahamu na wazee wengine wa ukoo: “Katika imani wote hao walikufa, ijapokuwa hawakupata utimizo wa ahadi, bali waliziona kwa mbali na kuzikaribisha na kutangaza hadharani kwamba wao walikuwa watu wasiojulikana na wakaaji wa muda katika nchi.”—Waebrania 11:13.

13. (a) Wakristo leo ni “wakaaji wa muda” jinsi gani? (b) Kwa nini Yehova atamaliza mfumo huu wa mambo?

13 Ikiwa Abrahamu angeweza kutegemeza maisha yake juu ya ahadi ambazo kutimizwa kwake kulikuwa ‘mbali,’ sisi tunapaswa kufanya hivyo kwa kadiri kubwa hata zaidi, kwa kuwa kutimizwa kwa ahadi hizo kumekaribia sana! Kama Abrahamu, twapaswa kujiona kuwa “wakaaji wa muda” katika mfumo wa Shetani na kukataa kujiingiza katika maisha ya anasa. Bila shaka tungependa “mwisho wa mambo yote” uje mara moja, si uwe karibu tu. (1 Petro 4:7) Labda tuna matatizo mabaya ya kiafya. Au huenda ikawa hali zetu za kiuchumi ni mbaya sana. Hata hivyo, inatupasa kukumbuka kwamba Yehova hataleta mwisho ili tu kutuokoa kutoka kwa hali mbaya, bali ili kulitakasa jina lake mwenyewe. (Ezekieli 36:23; Mathayo 6:9, 10) Si lazima mwisho uje wakati unaotufaa, bali wakati unaofaa kuhusiana na makusudi ya Yehova.

14. Subira ya Mungu huwanufaishaje Wakristo leo?

14 Kumbuka pia kwamba “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Ona kwamba Mungu ni “mwenye subira kwenu”—washiriki wa kutaniko la Kikristo. Yaelekea baadhi yetu twahitaji muda zaidi wa kufanya marekebisho ili ‘mwishowe tupatikane naye tukiwa bila doa na bila waa na katika amani.’ (2 Petro 3:14) Basi, je, haitupasi kushukuru kwamba Mungu ameonyesha subira hiyo?

Kupata Furaha Licha ya Vikwazo

15. Yesu aliwezaje kudumisha furaha yake licha ya majaribu aliyokabili, na Wakristo leo wananufaikaje kwa kumwiga?

15 Wakristo leo hujifunza mambo mengi sana kutokana na maisha ya Abrahamu. Mbali na imani, Abramu alionyesha subira, werevu, ujasiri, na upendo usio na ubinafsi. Aliiona ibada ya Yehova kuwa muhimu maishani mwake. Hata hivyo, ni lazima ikumbukwe kwamba Yesu Kristo ndiye kielezo bora zaidi kwetu kuiga. Yeye pia alikabili majaribu mengi, lakini alikuwa mwenye furaha licha ya majaribu hayo. Kwa nini? Kwa sababu alizingatia tumaini lililokuwa mbele. (Waebrania 12:2, 3) Hivyo Paulo alisali: “Sasa Mungu apaye uvumilivu na faraja na awaruhusu miongoni mwenu wenyewe mwe na mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu.” (Waroma 15:5) Tukiwa na mtazamo wa akili ufaao, tunaweza kupata furaha licha ya vikwazo ambavyo Shetani anaweza kutuwekea.

16. Tunaweza kufanya nini matatizo yanapoonekana kuwa yanatulemea?

16 Matatizo yanapoonekana kuwa yanakulemea, kumbuka kwamba Yehova anakupenda kama alivyompenda Abrahamu. Anataka ufanikiwe. (Wafilipi 1:6) Mtumaini Yehova kabisa, ukiwa na uhakika kwamba ‘yeye hatakuacha wewe ushawishwe kupita vile uwezavyo kuhimili, bali pamoja na hicho kishawishi ataifanya pia njia ya kutokea kusudi uweze kuvumilia hilo.’ (1 Wakorintho 10:13) Sitawisha mazoea ya kusoma Neno la Mungu kila siku. (Zaburi 1:2) Dumu katika sala, ukimwomba Yehova akusaidie kuvumilia. (Wafilipi 4:6) Yeye atawapa “roho takatifu wale wanaomwomba.” (Luka 11:13) Tumia kwa manufaa maandalizi ambayo Yehova ametoa ili kukutegemeza kiroho, kama vile vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia. Pia, tafuta msaada wa akina ndugu. (1 Petro 2:17) Hudhuria mikutano ya Kikristo kwa uaminifu, kwa kuwa kwenye mikutano hiyo utapata kitia moyo unachohitaji ili kuvumilia. (Waebrania 10:24, 25) Shangilia kwa kuwa na hakika kwamba uvumilivu wako huongoza kwenye hali yenye kukubalika machoni pa Mungu na kwamba imani yako hufanya moyo wake ufurahi!—Mithali 27:11; Waroma 5:3-5.

17. Kwa nini Wakristo hawakati tamaa?

17 Mungu alimpenda Abrahamu aliyekuwa “rafiki” yake. (Yakobo 2:23) Hata hivyo, Abrahamu alipatwa na dhiki na majaribu mengi yenye mkazo katika maisha yake. Kwa hiyo, Wakristo wanatarajia kupatwa na hali kama hizo katika ‘siku hizi za mwisho’ zenye uovu. Hata Biblia hutuonya kwamba “watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi.” (2 Timotheo 3:1, 13) Badala ya kukata tamaa, ng’amua kwamba mikazo tunayokabili huthibitisha kwamba mwisho wa mfumo mwovu wa Shetani umekaribia. Lakini Yesu anatukumbusha kwamba “yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:13) Kwa hiyo, ‘usife moyo katika kufanya lililo bora!’ Mwige Abrahamu, na uwe miongoni mwa wale ambao “kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Waebrania 6:12.

Je, Umefahamu?

• Kwa nini watu wa Yehova leo watazamie majaribu na dhiki?

• Ni katika njia zipi Shetani anaweza kutumia mashambulio ya moja kwa moja?

• Ugomvi kati ya Wakristo mmoja-mmoja unaweza kusuluhishwaje?

• Kiburi na majisifu yanawezaje kutokeza majaribu?

• Ni katika njia gani Abrahamu aliweka kielelezo kizuri kwa kungojea kutimizwa kwa ahadi za Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Vijana wengi Wakristo hunyanyaswa na marika wao kwa kudhihakiwa

[Picha katika ukurasa wa 29]

Katika siku za Abrahamu kutimizwa kwa ahadi za Mungu kulikuwa ‘mbali,’ hata hivyo, alitegemeza maisha yake juu ya ahadi hizo