Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Amani ya Kristo Inawezaje Kudhibiti Mioyoni Mwetu?

Amani ya Kristo Inawezaje Kudhibiti Mioyoni Mwetu?

Amani ya Kristo Inawezaje Kudhibiti Mioyoni Mwetu?

“Acheni amani ya Kristo idhibiti mioyoni mwenu, kwa maana nyinyi, kwa kweli, mliitiwa hiyo katika mwili mmoja.”—WAKOLOSAI 3:15.

1, 2. Ni katika njia gani “amani ya Kristo” inadhibiti moyoni mwa Mkristo?

NENO dhibiti linachukiwa na watu wengi, kwa kuwa linatufanya tufikiri juu ya kudhulumiwa na kutendewa vibaya. Kwa hiyo, huenda himizo la Paulo kwa Wakristo wenzake huko Kolosai, “Acheni amani ya Kristo idhibiti mioyoni mwenu,” likafanya watu wengine wafikiri kwamba yeye hakuwa mwenye kukubali sababu. (Wakolosai 3:15) Je, sisi si viumbe walio na uhuru wa kuchagua? Kwa nini turuhusu kitu chochote au mtu yeyote adhibiti mioyoni mwetu?

2 Paulo hakuwa akiwaambia Wakolosai wasitumie hiari yao. Neno la Kigiriki lililotafsiriwa ‘dhibiti’ kwenye Wakolosai 3:15 linahusiana na neno refa, mtu ambaye alikuwa akitoa nishani kwenye michezo ya wakati huo. Ingawa washindanaji walikuwa na kiasi fulani cha uhuru kuhusiana na sheria za michezo, mwishowe refa ndiye aliyeamua ni nani aliyefuata sheria na hivyo kupata ushindi. Vivyo hivyo, tuna uhuru wa kufanya maamuzi mengi maishani, lakini tufanyapo hivyo, amani ya Kristo sikuzote yapasa iwe “refa”—au kama asemavyo mtafsiri Edgar J. Goodspeed, “kani inayodhibiti” mioyoni mwetu.

3. “Amani ya Kristo” ni nini?

3 “Amani ya Kristo” ni nini? Ni utulivu, amani ya akili tunayopata baada ya kuwa wanafunzi wa Yesu na kufahamu kwamba tunapendwa na kukubaliwa na Yehova Mungu na Mwana wake. Yesu alipokaribia kuwaacha wanafunzi wake, aliwaambia hivi: “Mimi ninawaachia nyinyi amani. . . . Msiache mioyo yenu itaabishwe wala msiiache ikunyatike kwa sababu ya hofu.” (Yohana 14:27) Kwa muda upatao miaka 2,000, amani hiyo imefurahiwa na watiwa-mafuta waaminifu ambao ni washiriki wa mwili wa Kristo, na leo inafurahiwa na waandamani wao, “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Amani hiyo yapasa kudhibiti mioyoni mwetu. Tunapokabili jaribu kali, amani hiyo inaweza kutusaidia tusilemewe na hofu au kuwa na wasiwasi kupita kiasi. Acheni tuone jinsi jambo hili lilivyo kweli tunapokabili ukosefu wa haki, tunapokuwa na mahangaiko mengi, na tunapohisi hatufai.

Tunapokabili Ukosefu wa Haki

4. (a) Yesu alitendewaje isivyo haki? (b) Wakristo wameitikiaje wanapotendewa isivyo haki?

4 Mfalme Solomoni alisema: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989) Yesu alijua ukweli wa maneno hayo. Alipokuwa mbinguni, aliona ukosefu mkubwa sana wa haki miongoni mwa wanadamu. Alipokuwa duniani, Yesu alitendewa kwa njia isiyo ya haki kabisa aliposhtakiwa kwamba amekufuru na kuuawa licha ya kwamba alikuwa mwanadamu mkamilifu. (Mathayo 26:63-66; Marko 15:27) Leo, bado kuna ukosefu mwingi sana wa haki, na Wakristo wa kweli wameteseka sana, kwa vile wamekuwa “vitu vya kuchukiwa na mataifa yote.” (Mathayo 24:9) Hata hivyo, licha ya mambo yenye kutisha katika kambi za mateso za Nazi na kambi za kazi ngumu za Sovieti, na licha ya kutendewa jeuri na wafanya-ghasia, kushtakiwa isivyo haki, na kushambuliwa kwa uwongo, amani ya Kristo imewasaidia waendelee wakiwa imara. Wamemwiga Yesu ambaye tunasoma hivi kumhusu: “Alipokuwa akitukanwa, hakuwa akitukana kwa kurudisha. Alipokuwa akiteseka, hakutisha, lakini alifuliza kujikabidhi mwenyewe kwa yeye ambaye huhukumu kwa uadilifu.”—1 Petro 2:23.

5. Inapoonekana kwamba mtu fulani ametendewa isivyo haki kutanikoni, twapaswa kufikiria nini kwanza?

5 Kwa kadiri fulani, huenda tukawa na maoni kwamba mtu fulani katika kutaniko la Kikristo ametendewa isivyo haki. Katika hali hiyo huenda tukahisi kama alivyohisi Paulo, aliyesema: “Ni nani amekwazika, nami siwaki hasira?” (2 Wakorintho 11:29) Tunaweza kufanya nini? Twapaswa kujiuliza, ‘Je, kweli ametendewa isivyo haki?’ Mara nyingi, huwa hatujui habari zote. Huenda tukawa tunatenda kwa hisia kali tu baada ya kumsikiliza mtu fulani anayedai kwamba anajua. Biblia ina sababu nzuri inaposema: “Mjinga huamini kila neno.” (Mithali 14:15) Kwa hiyo tunahitaji kuwa waangalifu.

6. Tunaweza kutendaje ikiwa tunahisi kwamba tumetendewa isivyo haki katika kutaniko?

6 Hata hivyo, namna gani ikiwa inaonekana kwamba sisi wenyewe tumetendewa isivyo haki? Mtu mwenye amani ya Kristo moyoni mwake angetendaje? Huenda tukaona inafaa kuzungumza na mtu tunayehisi kuwa ametukosea. Baada ya hapo, badala ya kuzungumza jambo hilo na mtu mwingine, kwa nini tusimweleze Yehova jambo hilo kupitia sala na kutumaini kwamba atahakikisha haki imetekelezwa? (Zaburi 9:10; Mithali 3:5) Huenda ikawa baada ya kufanya hivyo, tutaridhika kutatua jambo hilo mioyoni mwetu na “kunyamaza.” (Zaburi 4:4) Mara nyingi, shauri la Paulo litafaa: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia.”—Wakolosai 3:13.

7. Twapaswa kukumbuka nini sikuzote tunaposhughulika na ndugu zetu?

7 Hata hivyo, lolote tufanyalo, tunahitaji kukumbuka kwamba ingawa hatuwezi kudhibiti mambo yaliyotokea, tunaweza kudhibiti jinsi tunavyoitikia. Tukiitikia kwa njia isiyofaa tunapohisi kwamba tumetendewa isivyo haki, matokeo yanaweza kuharibu zaidi amani yetu kuliko tendo lenyewe. (Mithali 18:14) Tunaweza hata kukwazwa na kuacha kushirikiana na kutaniko hadi tutakapohisi kwamba haki imetekelezwa. Mtunga-zaburi aliandika kwamba wale wanaopenda sheria za Yehova “hawana la kuwakwaza.” (Zaburi 119:165) Ukweli ni kwamba, kila mtu hutendewa isivyo haki pindi kwa pindi. Usiruhusu kamwe mambo hayo yasiyofaa yavuruge utumishi unaomtolea Yehova. Badala yake, acha amani ya Kristo idhibiti moyoni mwako.

Tunapokuwa na Mahangaiko Mengi

8. Ni baadhi ya mambo gani yanayosababisha hangaiko, na hangaiko laweza kutokeza nini?

8 Hangaiko ni jambo halisi kabisa maishani katika “siku [hizi] za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Ni kweli kwamba Yesu alisema: “Komeni kuwa wenye kuhangaikia nafsi zenu kuhusu ni nini mtakachokula au juu ya miili yenu kuhusu ni nini mtakachovaa.” (Luka 12:22) Lakini si mahangaiko yote yanayosababishwa na kutafuta vitu vya kimwili. Loti ‘alitaabishwa sana’ na ukosefu wa adili wa Sodoma. (2 Petro 2:7) Paulo ‘alihangaikia sana makutaniko yote.’ (2 Wakorintho 11:28) Yesu alikuwa na maumivu makali sana usiku uliotangulia kifo chake hivi kwamba “jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka kwenye ardhi.” (Luka 22:44) Bila shaka, si mahangaiko yote yanayoonyesha kwamba mtu ana imani dhaifu. Hata hangaiko liwe linasababishwa na nini, likizidi na kuendelea kwa muda mrefu, linaweza kutukosesha amani. Wengine wamekuwa na mahangaiko mengi sana hivi kwamba wamehisi hawawezi kuendelea kutimiza majukumu yao ya kumtumikia Yehova. Biblia husema: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha.” (Mithali 12:25) Tunaweza kufanya nini basi, ikiwa tuna mahangaiko mengi sana?

9. Ni baadhi ya hatua gani madhubuti zinazoweza kuchukuliwa ili kupunguza hangaiko, lakini ni mambo gani yanayosababisha hangaiko ambayo hatuwezi kuyaondoa?

9 Katika hali fulani, huenda tukafaulu kuchukua hatua madhubuti. Ikiwa hangaiko letu linasababishwa na ugonjwa, litakuwa jambo la busara kulishughulikia, ingawa mtu binafsi ndiye anayepaswa kuamua mambo hayo. * (Mathayo 9:12) Ikiwa tumelemewa na majukumu mengi, tunaweza kuwakabidhi wengine baadhi ya majukumu hayo. (Kutoka 18:13-23) Hata hivyo, vipi juu ya watu kama vile wazazi ambao wana majukumu mazito wasiyoweza kuwakabidhi watu wengine? Namna gani Mkristo anayeishi na mwenzi mpinzani? Namna gani familia inayokabili hali ngumu sana za kiuchumi au inayoishi katika sehemu yenye vita? Bila shaka, hatuwezi kuondoa mambo yote yanayosababisha hangaiko katika mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, tunaweza kudumisha amani ya Kristo mioyoni mwetu. Jinsi gani?

10. Mkristo anaweza kupunguza hangaiko katika njia gani mbili?

10 Njia moja ni kutafuta faraja kutoka kwa Neno la Mungu. Mfalme Daudi aliandika hivi: “Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako zaifurahisha roho yangu.” (Zaburi 94:19) “Faraja” anayotoa Yehova inaweza kupatikana katika Biblia. Kusoma kwa ukawaida Kitabu hicho kilichopuliziwa kutatusaidia tudumishe amani ya Kristo mioyoni mwetu. Biblia husema: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Vivyo hivyo, Paulo aliandika hivi: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Kusali kwa bidii na kwa ukawaida kutatusaidia kudumisha amani yetu.

11. (a) Yesu alituwekea kielelezo gani kizuri kuhusu sala? (b) Tuoneje sala?

11 Yesu alikuwa kielelezo kizuri kuhusiana na habari hii. Katika pindi fulani, alizungumza kwa sala na Baba yake wa kimbingu kwa muda wa saa nyingi kwa wakati mmoja. (Mathayo 14:23; Luka 6:12) Sala ilimsaidia kuvumilia majaribu makali zaidi. Usiku uliotangulia kifo chake, maumivu yalizidi sana. Alifanyaje? Alisali “kwa bidii zaidi.” (Luka 22:44) Naam, Mwana mkamilifu wa Mungu alikuwa mtu wa sala. Basi wafuasi wake wasio wakamilifu wana uhitaji mkubwa hata zaidi wa kuwa na zoea la kusali. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake ‘wasali sikuzote wala wasikate tamaa.’ (Luka 18:1) Sala ni mawasiliano halisi na muhimu pamoja na Yule anayetujua vyema zaidi ya tunavyojijua wenyewe. (Zaburi 103:14) Ikiwa tutadumisha amani ya Kristo mioyoni mwetu, ‘tutasali bila kukoma.’—1 Wathesalonike 5:17.

Kushinda Udhaifu Wetu

12. Kwa nini huenda wengine wakahisi kwamba utumishi wao haufai?

12 Yehova huona kila mtumishi wake kuwa mwenye thamani. (Hagai 2:7, NW, kielezi-chini) Hata hivyo, wengi huona ugumu kukubali jambo hilo. Huenda wengine wakavunjika moyo kwa sababu ya kuzeeka, kuongezeka kwa madaraka ya familia, au kuzorota kwa afya. Huenda wengine wakahisi kuwa wamevunjika moyo kwa sababu ya mambo mabaya yaliyowapata utotoni. Na bado huenda wengine wakasumbuliwa na makosa waliyofanya zamani, wakitilia shaka kama Yehova anaweza kuwasamehe. (Zaburi 51:3) Mtu anaweza kufanya nini anapohisi hivyo?

13. Maandiko huwafariji jinsi gani wale wanaohisi kwamba hawafai?

13 Amani ya Kristo itatuhakikishia upendo wa Yehova. Tunaweza kupata tena amani hiyo mioyoni mwetu kwa kutafakari uhakika wa kwamba Yesu hakusema kuwa tunaweza kujua thamani yetu kwa kulinganisha mambo tunayofanya na yale yanayofanywa na wengine. (Mathayo 25:14, 15; Marko 12:41-44) Alikazia uaminifu-mshikamanifu. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:13) Yesu mwenyewe “alidharauliwa” na watu, hata hivyo alikuwa na uhakika kwamba Baba yake alimpenda. (Isaya 53:3; Yohana 10:17) Naye aliwaambia wanafunzi wake kwamba wao pia walipendwa. (Yohana 14:21) Ili kukazia jambo hilo, Yesu alisema hivi: “Je, shore wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka kwenye ardhi bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiwe na hofu: Nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” (Mathayo 10:29-31) Huo ni uhakikisho ulioje wa upendo wa Yehova!

14. Tuna uhakikisho gani kwamba Yehova huthamini kila mmoja wetu?

14 Pia Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Kwa kuwa Yehova ametuvuta tumfuate Yesu, Anataka tuokolewe. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Si jambo la kutamanika kwa Baba yangu aliye mbinguni kwa mmoja wa wadogo hawa kuangamia.” (Mathayo 18:14) Kwa hiyo, ikiwa unatumikia kwa moyo wote, unaweza kufurahia kazi nzuri unazofanya. (Wagalatia 6:4) Ikiwa unasumbuka kwa sababu ya makosa uliyofanya zamani, uwe na hakika kwamba Yehova atawasamehe ‘kabisa’ wale wanaotubu kikweli. (Isaya 43:25; 55:7) Ikiwa unahisi umevunjika moyo kwa sababu nyingine yoyote, kumbuka kwamba “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwasaidia.”—Zaburi 34:18.

15. (a) Shetani hujaribuje kutunyang’anya amani yetu? (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani katika Yehova?

15 Shetani angependa sana kukunyang’anya amani yako. Yeye ndiye aliyesababisha dhambi tuliyorithi ambayo sote tunapambana nayo. (Waroma 7:21-24) Bila shaka angependa uhisi kwamba Mungu hakubali utumishi wako kwa sababu ya hali yako ya kutokamilika. Usikubali kamwe kuvunjwa moyo na Ibilisi! Tambua mbinu zake na hivyo uazimie kuvumilia. (2 Wakorintho 2:11; Waefeso 6:11-13) Kumbuka, “Mungu ni mkubwa zaidi kuliko mioyo yetu na ajua mambo yote.” (1 Yohana 3:20) Yehova haoni tu udhaifu wetu. Yeye pia huona nia na makusudi yetu. Kwa hiyo, pata faraja kutokana na maneno ya mtunga-zaburi: “BWANA hatawatupa watu wake, wala hatauacha urithi wake.”—Zaburi 94:14.

Tuna Umoja Katika Amani ya Kristo

16. Ni katika njia gani hatuko peke yetu tunapofanya yote tuwezayo kuvumilia?

16 Paulo aliandika kwamba twapaswa kuruhusu amani ya Kristo idhibiti mioyoni mwetu kwa sababu ‘tuliitiwa hiyo katika mwili mmoja.’ Wakristo watiwa-mafuta ambao Paulo aliwaandikia waliitwa wawe washiriki wa mwili wa Kristo, sawa na mabaki ya watiwa-mafuta leo. Waandamani wao “kondoo wengine” wameungana nao wakiwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja,” Yesu Kristo. (Yohana 10:16) Wote pamoja, “kundi” la ulimwenguni pote lenye mamilioni ya watu, wanaruhusu amani ya Kristo idhibiti mioyoni mwao. Kufahamu kwamba hatuko peke yetu hutusaidia kuvumilia. Petro aliandika hivi: “Chukueni msimamo wenu dhidi yake [Shetani], mkiwa thabiti katika imani, mkijua kwamba mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu katika ulimwengu.”—1 Petro 5:9.

17. Ni nini kinachotuchochea turuhusu amani ya Kristo idhibiti mioyoni mwetu?

17 Acheni sote tuendelee kusitawisha amani, tunda muhimu la roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Wale ambao Yehova atawapata wakiwa bila doa wala waa, na katika amani hatimaye watabarikiwa kwa kupewa uhai udumuo milele katika paradiso duniani, ambamo uadilifu utakaa. (2 Petro 3:13, 14) Tuna kila sababu ya kuruhusu amani ya Kristo idhibiti mioyoni mwetu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Nyakati nyingine, hangaiko linaweza kusababishwa au kuzidishwa na ugonjwa, kama vile mshuko-moyo.

Je, Unakumbuka?

• Amani ya Kristo ni nini?

• Amani ya Kristo inawezaje kudhibiti mioyoni mwetu tunapokabili ukosefu wa haki?

• Amani ya Kristo hutusaidiaje kushughulika na hangaiko?

• Amani ya Kristo hutufariji namna gani tunapohisi kuwa hatufai?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yesu alijikabidhi kwa Yehova, mbele ya washtaki wake

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kama kumbatio changamfu kutoka kwa baba mwenye upendo, faraja anayotoa Yehova yaweza kutuliza hangaiko letu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Uvumilivu ni wenye thamani kubwa mbele za Mungu