Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ibilisi—Si Ushirikina Tu

Ibilisi—Si Ushirikina Tu

Ibilisi—Si Ushirikina Tu

‘Katika maandishi yote ya Agano Jipya kuna pambano kati ya nguvu za Mungu za wema, na nguvu za uovu zinazoongozwa na Shetani. Hilo si wazo la mwandishi mmoja au wawili tu, bali ni wazo linalokubaliwa na watu wengi. Basi Agano Jipya lina ushuhuda ulio wazi kwamba Shetani ni kiumbe halisi na mwovu, na sikuzote huonyesha uadui kwa Mungu na watu wake.’—“The New Bible Dictionary.”

HIVYO basi, kwa nini wengi wanaodai kuwa Wakristo—na wanaodai kuamini Biblia—hukataa wazo kwamba Ibilisi yuko? Kwa sababu, wao kwa kweli hawakubali Biblia kuwa Neno la Mungu. (Yeremia 8:9) Wanasema eti kwamba waandishi wa Biblia hawakuandika kweli kutoka kwa Mungu kwa usahihi, bali waliandika falsafa za mataifa yaliyowazunguka. Kwa mfano, mwanatheolojia Mkatoliki Hans Küng aandika: “Ngano kuhusu Shetani na makundi ya roho waovu . . . zilitokana na Wababiloni na kupenya katika dini ya mapema ya Wayahudi kisha zikapenya katika Agano Jipya.”—On Being a Christian.

Lakini Biblia si neno la wanadamu tu. Biblia kwa kweli ni Neno la Mungu lililopuliziwa. Kwa hiyo, ni hekima kuchukua kwa uzito yale Biblia isemayo kuhusu Ibilisi.—2 Timotheo 3:14-17; 2 Petro 1:20, 21.

Yesu Alikuwa na Maoni Gani?

Yesu Kristo aliamini kwamba Ibilisi alikuwa kiumbe halisi. Yesu hakushawishiwa na uovu fulani uliokuwa ndani yake. Alishambuliwa na kiumbe halisi ambaye baadaye alimwita “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30; Mathayo 4:1-11) Pia aliamini kwamba viumbe wengine wa roho walimwunga Shetani mkono katika njama zake mbovu. Aliwaponya watu ‘waliopagawa na roho waovu.’ (Mathayo 12:22-28) Hata kichapo A Rationalist Encyclopædia kilichoandikwa na watu wasioamini kuwepo kwa Mungu chaonyesha maana ya jambo hilo kinaposema: “Sikuzote wanatheolojia wameshindwa kuelewa ni kwa nini Yesu anayetajwa katika Injili aliamini kuweko kwa roho waovu.” Yesu aliposema kuhusu Ibilisi na roho wake waovu, hakuwa anarudia tu mambo ya ushirikina yaliyotokana na ngano za Wababiloni. Alijua kwa kweli kwamba walikuweko.

Tunajifunza mengi kuhusu Ibilisi tunapofikiria maneno ambayo Yesu aliwaambia walimu wa kidini wa wakati wake: “Nyinyi mwatoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mwataka kufanya tamaa za baba yenu. Huyo alikuwa muua-binadamu kikatili wakati alipoanza, naye hakusimama thabiti katika kweli, kwa sababu kweli haimo katika yeye. Wakati asemapo uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.”—Yohana 8:44.

Kulingana na andiko hilo, Ibilisi, jina linalomaanisha “mchongezi,” alikuwa “mwongo na ndiye baba ya uwongo.” Yeye ndiye aliyekuwa kiumbe wa kwanza kusema uwongo kumhusu Mungu, naye alifanya hivyo kwenye bustani ya Edeni. Yehova alikuwa amesema kwamba wazazi wetu wa kwanza ‘wangekufa hakika’ iwapo wangekula kutokana na mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Kupitia kinywa cha nyoka, Shetani alisema kwamba maneno hayo hayakuwa ya kweli. (Mwanzo 2:17; 3:4) Kwa kufaa, yeye anaitwa “nyoka wa awali, yeye aitwaye Ibilisi na Shetani.”—Ufunuo 12:9.

Ibilisi alisema uwongo kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Alidai kwamba kile kizuizi cha kutokula kutokana na mti huo hakikufaa, naye aliyekiweka alitumia uwezo wake vibaya. Alisema kwamba Adamu na Hawa wangeweza ‘kuwa kama Mungu’ katika kujiamulia mema na mabaya. Shetani alidokeza kwamba wakiwa viumbe walio huru kujichagulia mambo, walipaswa kujitegemea kabisa. (Mwanzo 3:1-5) Shambulio hilo dhidi ya kufaa kwa njia ya Mungu ya kutawala lilizusha masuala muhimu. Hivyo Yehova ameruhusu wakati upite ili masuala hayo yajibiwe. Hilo linamaanisha kwamba Shetani ameruhusiwa kuendelea kuishi kwa muda mfupi ambao unakaribia sana kwisha. (Ufunuo 12:12) Na bado, yeye anaendelea kutenganisha wanadamu na Mungu kupitia udanganyifu, akitumia watu walio kama waandishi na Mafarisayo wa wakati wa Yesu ili kueneza mafundisho yake.—Mathayo 23:13, 15.

Yesu pia alisema kwamba Ibilisi alikuwa “muua-binadamu kikatili wakati alipoanza” na kwamba “hakusimama thabiti katika kweli.” Hiyo haimaanishi kwamba Yehova alimwumba Ibilisi akiwa “muua-binadamu kikatili.” Hakuumbwa akiwa jitu lenye umbo la kutisha linalosimamia mahali pa moto ambapo watu wote wenye kumpinga Mungu huteswa. Moto wa mateso unaotajwa katika Biblia si makao ya Shetani bali ni kaburi tu la kawaida la wanadamu.—Matendo 2:25-27; Ufunuo 20:13, 14.

Mwanzoni Ibilisi alikuwa “katika kweli.” Pindi moja alikuwa mshiriki wa familia ya mbinguni ya Yehova akiwa mwana-roho mkamilifu wa Mungu. Lakini “hakusimama thabiti katika kweli.” Alipendelea kufuata njia zake mwenyewe na kanuni zake za uwongo. ‘Alianza,’ wakati alipomwasi Yehova kimakusudi na kuwadanganya Adamu na Hawa, bali si wakati alipoumbwa akiwa mwana wa kimalaika wa Mungu. Ibilisi ni kama wale watu ambao walimwasi Yehova wakati wa Musa. Tunasoma hivi kuwahusu: “Wametenda mambo ya uharibifu, hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao.” (Kumbukumbu la Torati 32:5) Tunaweza kusema Shetani yuko hivyo. Alipata kuwa “muua-binadamu kikatili” alipoasi na kusababisha kifo cha Adamu na Hawa, naam, cha wanadamu wote.—Waroma 5:12.

Malaika Wasiotii

Kuna malaika wengine waliojiunga na Shetani katika uasi wake. (Luka 11:14, 15) Malaika hao ‘waliachilia mbali mahali pao wenyewe pa kukaa penye kufaa’ na kujivika miili ya kibinadamu ili kufurahia uhusiano wa kingono pamoja na “binti za wanadamu” wakati wa Noa. (Yuda 6; Mwanzo 6:1-4; 1 Petro 3:19, 20) “Theluthi moja ya nyota za mbinguni,” au idadi ndogo ya viumbe wa roho walikosa kutii pia.—Ufunuo 12:4.

Kitabu cha Ufunuo ambacho kina mifano mingi humwonyesha Ibilisi kuwa “joka kubwa la rangi-moto.” (Ufunuo 12:3) Kwa nini? Si kwa sababu Ibilisi ana umbo lenye kuogofya na lisilovutia. Ni kweli kwamba hatujui viumbe wa roho wana miili ya aina gani, lakini yaelekea Shetani si tofauti na viumbe wengine wa roho wa kimalaika. Hata hivyo, maneno “joka kubwa la rangi-moto” yanafafanua vizuri roho ya Shetani yenye pupa, yenye kuogofya, yenye nguvu, na yenye kuharibu.

Sasa Shetani na roho wake waovu wamewekewa vizuizi vikali. Hawawezi kujivika miili ya kibinadamu kama walivyofanya wakati mmoja. Punde baada ya Ufalme wa Mungu kuanza kutawala chini ya uongozi wa Kristo mwaka wa 1914, Shetani na roho waovu walitupwa chini kwenye ujirani wa dunia.—Ufunuo 12:7-9.

Ibilisi Ni Adui Mwenye Kuogopesha

Hata hivyo, Ibilisi ni adui mwenye kuogopesha. Yeye “hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8) Yeye si uovu tu ulio ndani ya mwili wetu usiokamilika. Ni kweli kwamba tunapambana kila siku na mielekeo yetu yenye dhambi. (Waroma 7:18-20) Lakini tunapambana hasa “dhidi ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”—Waefeso 6:12.

Uwezo wa Ibilisi umeenea kadiri gani? “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu,” asema mtume Yohana. (1 Yohana 5:19) Bila shaka, hatutaki tuogopeshwe na Ibilisi au turuhusu hofu ya kishirikina itufanye tuwe hoi. Hata hivyo, ni jambo la hekima kujihadhari na jitihada zake za kutupofusha tusione ile kweli na kuvunja uaminifu wetu kwa Mungu.—Ayubu 2:3-5; 2 Wakorintho 4:3, 4.

Ibilisi hatumii njia za kikatili sikuzote kushambulia wale wanaotaka kufanya mapenzi ya Mungu. Nyakati nyingine, yeye hujifanya kuwa “malaika wa nuru.” Mtume Paulo alionya Wakristo juu ya hatari hiyo alipoandika: “Naogopa kwamba kwa njia fulani, kama nyoka alivyomshawishi Hawa kwa ujanja wake, huenda akili zenu zikafisidiwa kutoka kwenye weupe wa moyo na usafi wa kiadili ambao wamstahili Kristo.”—2 Wakorintho 11:3, 14.

Kwa hiyo, tunahitaji ‘kutunza akili zetu, kuwa wenye kulinda, na kuchukua msimamo wetu dhidi yake, tukiwa thabiti katika imani.’ (1 Petro 5:8, 9; 2 Wakorintho 2:11) Na tusijiingize katika jambo lolote linalohusiana na mizungu na hivyo kufanya iwe rahisi kwa Shetani kutudanganya. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Na uwe mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu, ukikumbuka kwamba Yesu Kristo alirejezea Neno la Mungu tena na tena aliposhawishiwa na Ibilisi. (Mathayo 4:4, 7, 10) Sali ili upate roho ya Mungu. Matunda ya roho hiyo yanaweza kukusaidia uepuke kazi za mwili ambazo Shetani hufaulu sana kuzichochea. (Wagalatia 5:16-24) Pia sali kwa Yehova kwa bidii unapohisi kwamba Ibilisi na roho wake waovu wanakushinikiza kwa njia fulani.—Wafilipi 4:6, 7.

Hakuna haja ya kumwogopa Ibilisi. Yehova huahidi kutulinda na chochote ambacho Shetani anaweza kufanya. (Zaburi 91:1-4; Mithali 18:10; Yakobo 4:7, 8) “Endeleeni kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezaji wa nguvu yake,” asema mtume Paulo. Ndipo ‘mtakapoweza kusimama imara dhidi ya mbinu za Ibilisi.’—Waefeso 6:10, 11.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yesu alijua kwamba Ibilisi alikuwa mtu halisi

[Picha katika ukurasa wa 6]

“Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu”

[Hisani]

NASA photo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Chukueni msimamo wenu dhidi ya Ibilisi kwa kujifunza Neno la Mungu na kusali kwa ukawaida