Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Tafuteni Sana Amani na Kuifuatia’

‘Tafuteni Sana Amani na Kuifuatia’

Tafuteni Sana Amani na Kuifuatia’

“Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—WAROMA 12:18.

1, 2. Ni zipi baadhi ya sababu zinazofanya amani inayoletwa na wanadamu isidumu?

HEBU wazia nyumba yenye msingi dhaifu, nguzo zilizooza, na paa linalobonyea. Je, ungetaka kuhamia nyumba hiyo na kuifanya iwe makao yako? Labda hungetaka. Hata kuipaka rangi tena hakutaifanya iwe thabiti. Yaelekea nyumba hiyo itabomoka baadaye.

2 Amani yoyote inayotokana na ulimwengu huu ni kama nyumba hiyo. Inategemea msingi usio thabiti yaani, ahadi na mipango ya mwanadamu, “ambaye hakuna wokovu kwake.” (Zaburi 146:3) Rekodi ya matukio mengi ya zamani yaonyesha kwamba kumekuwa na vita kati ya mataifa, na kati ya makabila kwa muda mrefu. Ni kweli kwamba kumekuwa na vipindi vifupi vya amani, lakini ni amani ya aina gani? Ikiwa mataifa mawili yanapigana kisha amani inatangazwa kwa sababu taifa moja limeshindwa au kwa sababu mataifa yote mawili hayaoni haja ya kuendelea kupigana, hiyo ni amani ya aina gani? Mambo ambayo yalisababisha vita hiyo, ambayo ni chuki, shaka, na wivu bado yangalipo. Amani ya kinafiki tu, haidumu.—Ezekieli 13:10.

3. Kwa nini amani ya watu wa Mungu inatofautiana na amani inayoletwa na wanadamu?

3 Hata hivyo, kuna amani ya kweli katika ulimwengu huu uliokumbwa na vita. Wapi? Miongoni mwa wafuasi wa Yesu Kristo, Wakristo wa kweli wanaotii maneno ya Yesu na kujitahidi kuiga maisha yake. (1 Wakorintho 11:1; 1 Petro 2:21) Amani iliyopo kati ya Wakristo wa kweli wanaotoka katika jamii, vyeo na mataifa mbalimbali ni ya kweli kwa sababu inatokana na uhusiano wa amani walio nao pamoja na Mungu, unaotegemea imani yao katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Amani yao ni zawadi kutoka kwa Mungu, si amani inayoletwa na wanadamu. (Waroma 15:33; Waefeso 6:23, 24) Wanapata amani hiyo kwa sababu ya kujitiisha kwa “Mfalme wa Amani,” Yesu Kristo, na kumwabudu Yehova, “Mungu wa upendo na amani.”—Isaya 9:6; 2 Wakorintho 13:11.

4. Mkristo anaweza ‘kuifuatiaje’amani?

4 Wanadamu wasio wakamilifu hawawezi kupata amani bila jitihada yoyote. Kwa sababu hiyo, Petro alisema kila Mkristo apaswa ‘kuitafuta sana amani na kuifuatia.’ (1 Petro 3:11) Tunawezaje kufanya hivyo? Unabii mmoja wa zamani unatoa jibu. Yehova alisema hivi kupitia Isaya: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13; Wafilipi 4:9) Naam, wale wanaotii mafundisho ya Yehova hupata amani ya kweli. Isitoshe, amani, pamoja na “upendo, shangwe, . . . ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti,” ni matunda ya roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Mtu asiyeonyesha upendo, asiye na furaha, subira, fadhili, mwovu, asiye mwaminifu, mkali, au asiyejidhibiti hawezi kufurahia amani.

“Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”

5, 6. (a) Kuna tofauti gani kati ya kuwa mwenye amani na kuwa mwenye kufanya amani? (b) Wakristo hujitahidi kufanya amani na watu gani?

5 Amani imefasiriwa kuwa “hali ya utulivu au ushwari.” Ufafanuzi huo ungefaa hali nyingi hata hali ambapo hakuna vita. Kwani, hata mfu huwa katika hali hiyo! Hata hivyo, ili mtu afurahie amani ya kweli, anahitaji kuendeleza amani. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wenye kufanya amani, kwa kuwa wao wataitwa ‘wana wa Mungu.’” (Mathayo 5:9) Yesu alikuwa akizungumza na watu ambao baadaye wangekuwa na fursa ya kuwa wana wa Mungu wa kiroho na kupokea uhai usioweza kufa huko mbinguni. (Yohana 1:12; Waroma 8:14-17) Hatimaye, wanadamu wote waaminifu ambao hawana tumaini la kimbingu watafurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Ni watu wenye kufanya amani peke yao wanaoweza kuwa na tumaini hilo. Mara nyingi kuna tofauti kati ya kuwa mwenye amani—kuwa na amani—na kuwa mwenye kufanya amani. Kwa hiyo, kupatana na Maandiko, kufanya amani kwamaanisha kuendeleza amani kwa bidii, nyakati nyingine kufanya amani mahali ambapo haikuwepo hapo awali.

6 Tukiwa na hayo akilini, fikiria shauri la mtume Paulo kwa Waroma: “Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” (Waroma 12:18) Paulo hakuwa akiwaambia Waroma wawe watulivu tu, ijapokuwa hilo lingewasaidia. Alikuwa anawatia moyo wafanye amani. Na nani? Na “watu wote”—washiriki wa familia, Wakristo wenzao, hata na watu waliokuwa na imani tofauti na yao. Aliwatia moyo Waroma wafanye amani na wengine ‘kwa kadiri ilivyowategemea.’ La, hakutaka waridhiane imani yao kwa sababu tu ya amani. Badala ya kuwaudhi wengine isivyo lazima, walipaswa kuwafikia kwa amani. Wakristo walipaswa kufanya hivyo wawe walikuwa wakishughulika na watu walio ndani au nje ya kutaniko. (Wagalatia 6:10) Kupatana na hayo, Paulo aliandika hivi: “Sikuzote fuatieni lililo jema kuelekea mtu na mwenzake na kwa wengine wote.”—1 Wathesalonike 5:15.

7, 8. Kwa nini Wakristo wafanye amani na watu walio na imani tofauti na yao, na wanaweza kufanyaje hivyo?

7 Tunawezaje kufanya amani na watu ambao wana imani tofauti na yetu na ambao huenda hata wakapinga imani yetu? Njia moja ni kuepuka kujiona kuwa bora kuliko wengine. Kwa mfano, hatuwezi kufanya amani kwa kuzungumza kuhusu watu fulani kwa madharau. Yehova amefunua hukumu zake kuelekea mashirika na jamii mbalimbali, hata hivyo hatuna haki ya kuzungumza kuhusu mtu fulani kana kwamba ameshahukumiwa tayari. Kwa kweli, hatupaswi kuwahukumu wengine, hata wapinzani wetu. Baada ya kumwambia Tito awashauri Wakristo katika Krete kuhusu namna ya kushughulika na watu wenye mamlaka, Paulo alisema wakumbushwe “wasiseme kwa ubaya juu ya yeyote, wasiwe wataka-vita, wawe wenye kukubali sababu, wakionyesha wazi upole wote kuelekea watu wote.”—Tito 3:1, 2.

8 Kufanya amani na watu walio na imani tofauti na yetu hufanya iwe rahisi kwao kuikubali kweli. Bila shaka, hatusitawishi urafiki ‘unaoharibu mazoea yenye mafaa.’ (1 Wakorintho 15:33) Hata hivyo, tunapaswa kuwa na heshima, na twapaswa kuwatendea watu wote kwa staha na fadhili. Petro aliandika hivi: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.”—1 Petro 2:12.

Ni Wenye Kufanya Amani Katika Huduma

9, 10. Mtume Paulo aliweka kielelezo gani cha kushughulika kwa amani na watu ambao si waamini?

9 Wakristo wa karne ya kwanza walijulikana kwa ujasiri wao. Hawakupunguza uzito wa ujumbe wao, na walipokabiliwa na upinzani, waliazimia kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu. (Matendo 4:29; 5:29) Hata hivyo, walitofautisha ujasiri na ukatili. Fikiria mbinu aliyotumia Paulo alipotetea imani yake mbele ya Mfalme Herode Agrippa wa Pili. Herode Agrippa alikuwa na uhusiano wa kingono na dada yake, Bernike. Hata hivyo, Paulo hakuanza tu kumkemea Agrippa kuhusu maadili. Bali alikazia mambo waliyokubaliana, huku akimsifu Agrippa kwa ujuzi wake mwingi kuhusu desturi za Wayahudi na namna alivyowaamini manabii.—Matendo 26:2, 3, 27.

10 Je, Paulo alikuwa akimrairai kinafiki mtu huyo ambaye angempa uhuru? La. Paulo alifuata tu dokezo alilokuwa ametoa yeye mwenyewe na akasema kweli. Mambo yote aliyomwambia Herode Agrippa yalikuwa ya kweli. (Waefeso 4:15) Lakini Paulo alikuwa mtu mwenye kufanya amani naye alijua jinsi ya kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.” (1 Wakorintho 9:22) Lengo lake lilikuwa kutetea haki yake ya kuhubiri juu ya Yesu. Kwa kuwa alikuwa mwalimu mwenye matokeo, Paulo alianza kwa kutaja jambo ambalo yeye na Agrippa wangeweza kukubaliana. Kwa hiyo Paulo alimsaidia mfalme huyo asiye na maadili aone Ukristo kwa njia inayofaa.—Matendo 26:28-31.

11. Tunawezaje kuwa watu wenye kufanya amani katika huduma yetu?

11 Tunawezaje kuwa watu wenye kufanya amani katika huduma yetu? Kama Paulo, twapaswa kuepuka mabishano. Ni kweli kwamba nyakati fulani tunahitaji “kulisema neno la Mungu bila hofu,” na kutetea imani yetu kwa ujasiri. (Wafilipi 1:14) Hata hivyo, mara nyingi lengo letu kuu huwa ni kuhubiri habari njema. (Mathayo 24:14) Mtu akifahamu kweli kuhusu makusudi ya Mungu, anaweza kuacha mawazo ya dini isiyo ya kweli na kujisafisha kutokana na mazoea yasiyo safi. Kwa hiyo, kwa kadiri tuwezavyo, yafaa tukazie mambo yatakayowavutia wasikilizaji wetu, tukianza na mambo tunayokubaliana nao. Hatutatimiza lolote kwa kumwudhi mtu ambaye angeweza kusikiliza ujumbe wetu iwapo angefikiwa kwa busara.—2 Wakorintho 6:3.

Watu Wenye Kufanya Amani Katika Familia

12. Ni katika njia gani tunaweza kuwa watu wenye kufanya amani katika familia?

12 Paulo alisema kwamba wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Watakuwa na magumu mbalimbali. Mojawapo ni kwamba wenzi fulani wa ndoa watakosa kuelewana mara kwa mara. Kutoelewana huko kwapaswa kutatuliwaje? Kwa njia ya amani. Mtu mwenye kufanya amani atajitahidi kuzuia kutoelewana kusizidi. Jinsi gani? Kwanza, kwa kuzuia ulimi wake. Ulimi unapotumiwa kwa kukejeli na kutukana wengine, kiungo hiki kidogo kwa kweli chaweza kuwa ‘kitu kisichotawalika, kimejaa sumu yenye kuleta kifo.’ (Yakobo 3:8) Mtu mwenye kufanya amani hutumia ulimi wake kujenga wengine bali si kuwabomoa.—Mithali 12:18.

13, 14. Tunawezaje kudumisha amani tunapokosea kwa kusema au tunapokasirika sana?

13 Kwa sababu ya kutokamilika, mara kwa mara sisi husema mambo ambayo hutufanya tujute baadaye. Jambo hilo linapotokea, fanya haraka kurekebisha hali hiyo—fanya amani. (Mithali 19:11; Wakolosai 3:13) Usijihusishe sana na “mashindano juu ya maneno” na “mabishano makali sana juu ya mambo madogo-madogo.” (1 Timotheo 6:4, 5) Usichukue mambo kijuujuu tu, jaribu kuona mambo kwa njia halisi na ujaribu kuelewa hisia za mwenzi wako. Ukirushiwa maneno makali, usilipize kisasi. Kumbuka kwamba “jawabu la upole hugeuza hasira.”—Mithali 15:1.

14 Nyakati nyingine, huenda ukahitaji kufikiria shauri la Mithali 17:14: “Acheni ugomvi kabla haujafurika.” Ondoka katika hali inayochochea hasira. Baadaye utakapotulia kihisia-moyo, labda utaweza kutatua tatizo kwa njia ya amani. Nyakati nyingine, huenda likawa jambo la hekima kumwita mwangalizi Mkristo aliyekomaa akusaidie. Wanaume hao wenye uzoefu na huruma wanaweza kukupa burudisho wakati amani ya ndoa inapotishwa.—Isaya 32:1, 2.

Watu Wenye Kufanya Amani Kutanikoni

15. Kulingana na Yakobo, ni mtazamo gani mbaya uliokuwa umesitawi miongoni mwa Wakristo fulani, na kwa nini mtazamo huo ni ‘wa kidunia,’ ‘wa kinyama,’ na ‘wa roho waovu’?

15 Kwa kusikitisha, Wakristo fulani wa karne ya kwanza walikuwa na wivu na ugomvi—mambo yaliyo kinyume kabisa cha amani. Yakobo alisema hivi: “Hii siyo hekima iteremkayo kutoka juu, bali ni ya kidunia, ya kinyama, ya roho waovu. Kwa maana ambako kuna wivu na ugomvi, hapo ukosefu wa utaratibu na kila jambo ovu vipo.” (Yakobo 3:14-16) Watu fulani wanasadiki kwamba neno la Kigiriki lililotafsiriwa “ugomvi” ladokeza tamaa ya ubinafsi, kung’ang’ania mamlaka. Kwa hiyo Yakobo ana sababu nzuri anaposema kwamba ugomvi ni ‘wa kidunia, wa kinyama, wa roho waovu.’ Katika muda wote ambao umepita, viongozi wa ulimwengu wamekuwa na ugomvi kama wanyama wa mwitu wanaopigana. Kwa kweli ugomvi ni ‘wa kidunia’ na ‘wa kinyama.’ Pia ni ‘wa roho waovu.’ Tabia hiyo yenye hila ilidhihirishwa mara ya kwanza na malaika aliyetamani sana kuwa na mamlaka, ambaye alimpinga Yehova Mungu na kuwa Shetani, mtawala wa roho waovu.

16. Wakristo fulani wa karne ya kwanza walionyeshaje mtazamo kama wa Shetani?

16 Yakobo aliwahimiza Wakristo wakinze mtazamo wa ugomvi, kwa kuwa hauleti amani. Aliandika hivi: “Vita vyatokana na chanzo gani na mapigano miongoni mwenu yatokana na chanzo gani? Je, si kutoka katika chanzo hiki, yaani, kutokana na tamaa zenu za kufurahisha hisi za mwili ambazo huendeleza pambano katika viungo vyenu?” (Yakobo 4:1) Hapa, ‘tamaa ya kufurahisha hisi za mwili’ yaweza kurejezea tamaa ya pupa ya vitu vya kimwili au kutamani umashuhuri au mamlaka. Kama Shetani, yaelekea wengine kutanikoni walitaka kuwa mashuhuri badala ya kuwa ‘wadogo zaidi’ kama Yesu alivyosema wafuasi wake walipaswa kuwa. (Luka 9:48) Mtazamo kama huo unaweza kuondoa amani kutanikoni.

17. Leo Wakristo wanawezaje kuwa watu wenye kufanya amani kutanikoni?

17 Leo, lazima tukinze maelekeo ya kufuatia vitu vya kimwili, wivu, au tamaa isiyofaa ya kutaka makuu. Ikiwa sisi ni wafanya-amani wa kweli, hatutakuwa na wasiwasi iwapo baadhi ya watu kutanikoni ni stadi kutushinda katika kufanya mambo fulani, wala hatutawaharibia sifa mbele ya wengine kwa kutilia shaka nia yao. Ikiwa tuna kipawa fulani chenye kutokeza, hatutakitumia ili tuonekane kuwa bora kuliko wengine, na hivyo kudokeza kwamba kutaniko haliwezi kusonga mbele bila uwezo na ujuzi wetu. Mtazamo kama huo unaweza kuleta mgawanyiko; hauwezi kuleta amani. Watu wenye kufanya amani hawajigambi mbele ya wengine kwa sababu ya vipawa vyao bali huvitumia kwa unyenyekevu kutumikia ndugu zao na kumletea Yehova heshima. Wanatambua kwamba hatimaye, upendo wala si uwezo ndio unaotambulisha Mkristo wa kweli.—Yohana 13:35; 1 Wakorintho 13:1-3.

“Wasimamizi Wako Wawe Amani”

18. Wazee huendelezaje amani miongoni mwao wenyewe?

18 Wazee wa kutaniko ndio wanaokuwa wa kwanza kufanya amani. Yehova alitabiri hivi kuhusu watu wake: “Nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.” (Isaya 60:17) Kupatana na maneno hayo ya kiunabii, wale wanaotumikia wakiwa wachungaji Wakristo hujitahidi kuendeleza amani miongoni mwao wenyewe na miongoni mwa kundi. Wazee wanaweza kudumisha amani miongoni mwao wenyewe kwa kudhihirisha “hekima ya kutoka juu” ambayo ni yenye kufanya amani na yenye kukubali sababu. (Yakobo 3:17) Kwa sababu ya malezi yao na vilevile mambo ambayo wamejionea maishani, nyakati nyingine wazee wa kutaniko watakuwa na maoni yanayotofautiana. Je, hilo lamaanisha kwamba hawana amani? Sivyo, ikiwa hali hiyo inashughulikiwa ifaavyo. Watu wenye kufanya amani hujieleza kwa unyenyekevu kisha huwasikiliza wengine kwa heshima. Badala ya kushikilia kauli zake, mtu mwenye kufanya amani atafikiria maoni ya ndugu yake kwa sala. Ikiwa hakuna kanuni yoyote ya Biblia ambayo imevunjwa, kuna uhuru wa kuwa na maoni mbalimbali. Wengine wasipokubaliana naye, mtu mwenye kufanya amani hatashikilia kauli yake, badala yake ataunga mkono uamuzi ambao umefanywa na wengi. Hivyo ataonyesha kwamba yeye ni mwenye kukubali sababu. (1 Timotheo 3:2, 3) Waangalizi wenye uzoefu wanajua kwamba kudumisha amani ni muhimu kuliko kushikilia kauli zao.

19. Wazee huwa watu wenye kufanya amani jinsi gani katika kutaniko?

19 Wazee huendeleza amani miongoni mwa washiriki wa kutaniko kwa kuwasaidia wala si kwa kuchambua jitihada zao isivyofaa. Ni kweli kwamba nyakati fulani huenda wengine wakahitaji kurekebishwa upya. (Wagalatia 6:1) Lakini kazi ya mwangalizi Mkristo si kutoa nidhamu tu. Mara nyingi yeye hutoa pongezi. Wazee wenye upendo hujitahidi kuona sifa nzuri za wengine. Waangalizi huthamini kazi ngumu inayofanywa na Wakristo wenzao na wana uhakika kwamba waamini wenzao wanafanya yote wawezayo.—2 Wakorintho 2:3, 4.

20. Kutaniko linanufaika katika njia gani iwapo wote ni wenye kufanya amani?

20 Kwa hiyo, katika familia, katika kutaniko, na tunaposhughulika na watu wenye imani tofauti na yetu, tunajitahidi kuwa watu wenye kufanya amani, wanaotafuta amani. Tukijitahidi kusitawisha amani, tutachangia furaha kutanikoni. Wakati huohuo, tutalindwa na kuimarishwa katika njia nyingi, kama tutakavyoona katika makala ifuatayo.

Je, Unakumbuka?

• Inamaanisha nini kuwa mtu mwenye kufanya amani?

• Tunawezaje kuwa watu wenye kufanya amani tunaposhughulika na watu ambao si Mashahidi?

• Tunaweza kusitawisha amani katika familia katika njia zipi?

• Wazee wanawezaje kuendeleza amani kutanikoni?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Watu wenye kufanya amani huepuka kujionyesha kuwa bora kuliko wengine

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakristo ni watu wenye kufanya amani katika huduma, nyumbani, na kutanikoni