Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Baraka za Yehova Hututajirisha

Baraka za Yehova Hututajirisha

Baraka za Yehova Hututajirisha

“Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni “maumivu,” “NW”] nayo.”—MITHALI 10:22.

1, 2. Kwa nini furaha haihusiani na utajiri wa kimwili?

WATU wengi leo hufuatia sana vitu vya kimwili. Lakini je, vitu vya kimwili huwaletea furaha? “Watu wamehuzunishwa sana na maisha yao sasa kuliko wakati mwingine wowote,” lasema gazeti The Australian Women’s Weekly. Gazeti hilo laendelea kusema: “Hiyo ni hali iliyo kinyume cha matarajio. Tunaelezwa kwamba hali ya uchumi nchini Australia ni nzuri sana, kwamba maisha yamekuwa mazuri sana. . . . Licha ya hayo, watu nchini humo hawatarajii mema. Wanaume kwa wanawake wanatambua kwamba kuna kitu wanachokosa maishani mwao lakini hawajui ni kitu gani.” Maandiko yanasema kweli kama nini yanapotaja kwamba furaha na uhai hazitokani na vitu tulivyo navyo!—Mhubiri 5:10; Luka 12:15.

2 Biblia hufundisha kwamba furaha iliyo kuu zaidi hutokana na baraka ya Mungu. Kuhusiana na hilo, Mithali 10:22 husema: ‘Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi maumivu nayo.’ Mara nyingi maumivu hutokana na kujipatia utajiri wa kimwili kwa pupa. Kwa kufaa, mtume Paulo alionya: “Wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo. Kwa maana kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10.

3. Kwa nini watumishi wa Mungu hupatwa na majaribu?

3 Kwa upande mwingine, wale ambao ‘huendelea kusikiliza sauti ya Yehova’ hupata baraka zisizo na maumivu. (Kumbukumbu la Torati 28:2) Hata hivyo, huenda wengine wakauliza, ‘Ikiwa Yehova hachanganyi baraka yake na maumivu, kwa nini watumishi wengi wa Mungu huteseka?’ Biblia hufunua kwamba Mungu huruhusu majaribu yatupate lakini majaribu hayo hutokana na Shetani, mfumo wake mwovu, na utu wetu usiokamilika. (Mwanzo 6:5; Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Yohana 15:19; Yakobo 1:14, 15) Yehova ni chanzo cha “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17) Hivyo, baraka zake hazileti maumivu kamwe. Kwa hiyo, acheni tuchunguze baadhi ya upaji mkamilifu wa Mungu.

Neno la Mungu Ni Zawadi Yenye Thamani Kubwa

4. Watu wa Yehova wamepata baraka na zawadi gani yenye thamani kubwa ‘wakati huu wa mwisho’?

4 Kuhusu “wakati wa mwisho,” unabii wa Danieli wasema: “Maarifa yataongezeka.” Hata hivyo, unabii huo ulifafanuliwa kwa maneno haya: “Hataelewa mtu mbaya awaye yote; bali wao walio na hekima ndio watakaoelewa.” (Danieli 12:4, 10) Hebu fikiria jambo hilo! Neno la Mungu—hasa unabii—limeelezwa kwa hekima nyingi sana ya kimungu hivi kwamba wabaya hawawezi kulielewa, japo watu wa Yehova hulielewa. Mwana wa Mungu alisali hivi: “Nakusifu hadharani wewe, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umeficha mambo hayo kwa uangalifu kutoka kwa wenye hekima na walio na akili, nawe umeyafunua kwa vitoto.” (Luka 10:21) Ni baraka iliyoje kuwa na Biblia, Neno la Mungu lililoandikwa, ambayo ni zawadi yenye thamani kubwa, na kuwa miongoni mwa wale ambao Yehova amewapa ufahamu wa kiroho!—1 Wakorintho 1:21, 27, 28; 2:14, 15.

5. Hekima ni nini na tunaweza kuipataje?

5 Hatungekuwa na ufahamu wowote wa kiroho kama hatungepata “hekima ya kutoka juu.” (Yakobo 3:17) Hekima ni uwezo wa kutumia ujuzi na ufahamu kutatua matatizo, kuepuka au kukinga hatari, kufikia miradi, au kutoa ushauri mzuri. Tunapataje hekima ya Mungu? Mithali 2:6 husema: “BWANA huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu.” Naam, Yehova atatupa hekima tukiendelea kusali ili tuipate, kama alivyompa Mfalme Solomoni “moyo wa hekima na wa akili.” (1 Wafalme 3:11, 12; Yakobo 1:5-8) Ili kupata hekima, ni lazima pia tuendelee kumsikiliza Yehova kwa kujifunza na kutumia Neno lake kwa ukawaida.

6. Kwa nini ni hekima kutumia sheria na kanuni za Mungu katika maisha yetu?

6 Tunaweza kupata mifano bora sana ya hekima ya Mungu katika sheria na kanuni za Biblia. Hizo hutunufaisha kwa kila njia—kimwili, kiakili, kihisia-moyo, na kiroho. Kwa kufaa mtunga-zaburi aliimba hivi: “Sheria ya BWANA ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya BWANA ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya BWANA ni safi, huyatia macho nuru. Kicho cha BWANA ni kitakatifu, kinadumu milele. Hukumu za BWANA ni kweli zina haki kabisa. Ni za kutamanika kuliko dhahabu, kuliko wingi wa dhahabu safi.”—Zaburi 19:7-10; 119:72.

7. Ni nini matokeo ya kupuuza viwango vya Mungu vya uadilifu?

7 Kwa upande mwingine, wale wanaopuuza viwango vya uadilifu vya Mungu hawapati furaha na uhuru wanaotafuta. Hatimaye, wao hutambua kwamba Mungu si wa kudhihakiwa, kwa kuwa mtu atavuna anachopanda. (Wagalatia 6:7) Watu wengi wanaopuuza kanuni za Biblia wanavuna matokeo yenye kuhuzunisha kama vile mimba zisizotakikana, maradhi mabaya, au uraibu wenye kudhoofisha mwili. Wasipotubu na kubadili maisha yao, hatimaye watakufa au labda waangamizwe na Mungu.—Mathayo 7:13, 14.

8. Kwa nini wanaopenda Neno la Mungu wana furaha?

8 Hata hivyo, wale wanaopenda Neno la Mungu na kulitumia watapata baraka nyingi sasa na wakati ujao. Wana sababu ya kuhisi kwamba sheria ya Mungu imewaweka huru, wana furaha ya kweli, na wanangojea kwa hamu wakati ambapo watawekwa huru na dhambi na matokeo yake yenye kuleta kifo. (Waroma 8:20, 21; Yakobo 1:25) Tumaini hilo ni hakika kwa sababu linategemea zawadi ya upendo mwingi ambayo Mungu aliwapa wanadamu—dhabihu ya fidia ya Mwana wake mzaliwa-pekee, Yesu Kristo. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; Waroma 6:23) Zawadi hiyo bora yathibitisha kina cha upendo wa Mungu kwa wanadamu na huwahakikishia wote wanaoendelea kumsikiliza Yehova, baraka zisizo na mwisho.—Waroma 8:32.

Tunashukuru kwa Zawadi ya Roho Takatifu

9, 10. Tunanufaikaje na zawadi ya Yehova ya roho takatifu? Toa mfano.

9 Twapaswa kushukuru kwa ajili ya roho takatifu ambayo ni zawadi nyingine ya upendo kutoka kwa Mungu. Katika siku ya Pentekoste 33 W.K., mtume Petro alisihi umati uliokuwa Yerusalemu hivi: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.” (Matendo 2:38) Leo, Yehova huwapa roho takatifu watumishi wake waliojiweka wakfu wanaosali ili kuipata na wanaotaka kufanya mapenzi yake. (Luka 11:9-13) Katika nyakati za kale, nguvu hii iliyo kuu kuliko zote ulimwenguni—roho takatifu ya Mungu, au kani ya utendaji—iliwatia nguvu wanaume na wanawake wenye imani, kutia ndani Wakristo wa mapema. (Zekaria 4:6; Matendo 4:31) Inaweza kututia nguvu pia, ingawa huenda tukakabili vikwazo vyenye kutisha au magumu tukiwa watu wa Yehova.—Yoeli 2:28, 29.

10 Fikiria kielelezo cha Laurel, aliyeugua polio na ambaye aliishi ndani ya pafu la chuma (mashine iliyomsaidia kupumua) kwa miaka 37. * Licha ya hali zake ngumu sana, alimtumikia Mungu kwa bidii hadi kifo. Kwa miaka mingi, Yehova alimbariki sana Laurel. Kwa mfano, aliweza kusaidia watu 17 wapate ujuzi sahihi wa kweli ya Biblia, ingawa alilazimika kutumia mashine hiyo saa 24 kwa siku! Hali yake inatukumbusha maneno haya ya mtume Paulo: “Niwapo dhaifu, ndipo niwapo mwenye nguvu.” (2 Wakorintho 12:10) Naam, mafanikio yoyote tuwezayo kupata katika kuhubiri habari njema hayatokani na uwezo na nguvu zetu wenyewe bali hutokana na msaada wa Mungu kupitia roho takatifu, anayowapa wale wanaoendelea kusikiliza sauti yake.—Isaya 40:29-31.

11. Roho ya Mungu hutokeza sifa gani ndani ya wale wanaovaa “utu mpya”?

11 Tunapomsikiliza Mungu kwa utiifu, roho yake hutokeza ndani yetu sifa za upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujidhibiti. (Wagalatia 5:22, 23) ‘Matunda hayo ya roho’ ni sehemu ya “utu mpya” ambao Wakristo huvaa badala ya tamaa za kinyama walizokuwa nazo zamani. (Waefeso 4:20-24; Isaya 11:6-9) Tunda la upendo ambalo ni “kifungo kikamilifu cha muungano,” ni muhimu sana.—Wakolosai 3:14.

Upendo wa Kikristo—Zawadi ya Kuthaminiwa Sana

12. Tabitha na Wakristo wengine wa karne ya kwanza walidhihirishaje upendo?

12 Upendo wa Kikristo ni zawadi nyingine nzuri kutoka kwa Yehova—zawadi ambayo tuna sababu ya kuithamini sana. Upendo huo unaongozwa na kanuni, lakini una shauku nyingi sana hivi kwamba unawaunganisha zaidi waamini kuliko hata uhusiano wa kifamilia. (Yohana 15:12, 13; 1 Petro 1:22) Kwa mfano, fikiria Tabitha, mwanamke Mkristo mwenye sifa nzuri wa karne ya kwanza. “Yeye alizidi katika vitendo vyema na zawadi za rehema,” hasa kwa niaba ya wajane kutanikoni. (Matendo 9:36) Huenda wanawake hao walikuwa na watu wa jamaa, lakini Tabitha alitaka kufanya yote awezayo kuwasaidia na kuwatia moyo. (1 Yohana 3:18) Tabitha aliweka kielelezo kizuri kama nini! Upendo wa kidugu ulimchochea Priska na Akila ‘kuhatarisha shingo zao’ kwa ajili ya Paulo. Upendo pia ulimchochea Epafrasi, Luka, Onesiforo, na wengine wamsaidie mtume huyo alipokuwa kifungoni Roma. (Waroma 16:3, 4; 2 Timotheo 1:16; 4:11; Filemoni 23, 24) Naam, leo Wakristo kama hao ‘wana upendo miongoni mwao wenyewe,’ ambao ni zawadi nzuri kutoka kwa Mungu inayowatambulisha kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu.—Yohana 13:34, 35.

13. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini sana udugu wetu wa Kikristo?

13 Je, wewe unathamini sana upendo unaoonyeshwa katika kutaniko la Kikristo? Je, wewe unashukuru kwa udugu wetu wa kiroho wa ulimwenguni pote? Hizi pia ni zawadi nzuri na zenye kutajirisha kutoka kwa Yehova. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunazithamini sana? Kwa kumtolea Mungu utumishi mtakatifu, kwa kushiriki kwenye mikutano ya Kikristo, na kwa kuonyesha upendo na matunda mengine ya roho ya Mungu.—Wafilipi 1:9; Waebrania 10:24, 25.

“Zawadi Zikiwa Wanadamu”

14. Mkristo anapaswa kutimiza matakwa gani iwapo anataka kutumikia akiwa mzee au mtumishi wa huduma?

14 Wanaume Wakristo wanaotaka kuwatumikia waabudu wenzao wakiwa wazee au watumishi wa huduma wana mradi mzuri. (1 Timotheo 3:1, 8) Ili kustahili kupata mapendeleo hayo, ndugu anapaswa kuwa mtu wa kiroho, anayeelewa Maandiko vizuri na mwenye bidii katika huduma ya shambani. (Matendo 18:24; 1 Timotheo 4:15; 2 Timotheo 4:5) Anapaswa kuonyesha unyenyekevu, kiasi, na subira, kwa kuwa Mungu hawabariki watu wenye kimbelembele, kiburi, na tamaa ya makuu. (Mithali 11:2; Waebrania 6:15; 3 Yohana 9, 10) Iwapo ameoa, anapaswa kuwa kichwa cha familia mwenye upendo, anayeweza kusimamia vizuri familia yake yote. (1 Timotheo 3:4, 5, 12) Kwa kuwa anathamini sana utajiri wa kiroho, mtu kama huyo atapata baraka za Yehova.—Mathayo 6:19-21.

15, 16. Ni nani wanaothibitika kuwa “zawadi zikiwa wanadamu”? Toa mifano.

15 Wale wanaotumikia wakiwa wazee kutanikoni wanapojikakamua katika kueneza injili, uchungaji, na kufundisha, tunakuwa na sababu nzuri za kuthamini sana ‘zawadi hizo zikiwa wanadamu.’ (Waefeso 4:8, 11) Huenda wale wanaonufaika na utumishi huo wenye upendo wasionyeshe uthamini wao sikuzote, lakini Yehova huona yale ambayo wazee waaminifu hufanya. Hatasahau upendo ambao wao huonyesha kwa ajili ya jina lake kwa kuhudumia watu wake.—1 Timotheo 5:17; Waebrania 6:10.

16 Hebu fikiria kisa cha mzee mmoja mwenye bidii aliyemtembelea msichana mmoja Mkristo ambaye alikuwa karibu kufanyiwa upasuaji wa ubongo. “Alikuwa mwenye fadhili sana, mwenye kufariji, na kujali sana,” akaandika rafiki ya familia ya msichana huyo. “Aliomba ruhusa asali kwa Yehova pamoja nasi. Alipokuwa anasali, baba ya msichana huyo [ambaye si mmoja wa Mashahidi wa Yehova] alilia, na wote waliokuwa kwenye chumba hicho cha hospitali wakabubujikwa na machozi. Sala ya mzee huyo ilikuwa yenye kugusa hisia kama nini, naye Yehova alionyesha upendo ulioje kwa kumtuma wakati kama huo!” Mgonjwa mwingine Shahidi alisema hivi kuhusu wazee waliomtembelea: “Walipokaribia kitanda changu katika chumba cha wagonjwa mahututi, nilijua kwamba hata kutokee nini, ningeweza kuvumilia. Nilipata nguvu na utulivu.” Je, kuna yeyote awezaye kununua hangaiko hilo lenye upendo? La, hasha! Ni zawadi kutoka kwa Mungu, ipatikanayo kupitia kutaniko la Kikristo.—Isaya 32:1, 2.

Zawadi ya Huduma ya Shambani

17, 18. (a) Ni zawadi gani ya utumishi ambayo Yehova amewatolea watu wake wote? (b) Ni msaada gani ambao Mungu ametoa ili tuweze kutimiza huduma yetu?

17 Kumtumikia Yehova, Aliye Juu Sana ndilo pendeleo kuu zaidi ambalo mwanadamu yeyote anaweza kupata. (Isaya 43:10; 2 Wakorintho 4:7; 1 Petro 2:9) Hata hivyo, wote wanaotamani kikweli kumtumikia Mungu—wawe vijana au wazee, wanaume au wanawake—wanaweza kushiriki pendeleo la kuhubiria watu. Je, unatumia zawadi hii yenye thamani? Huenda wengine wakasitasita kuhubiri kwa sababu wanahisi kwamba hawafai, lakini kumbuka kwamba Yehova huwapa roho takatifu wale wanaomtumikia, nayo husawazisha upungufu wowote tunaoweza kuwa nao.—Yeremia 1:6-8; 20:11.

18 Yehova amewapa watumishi wake wanyenyekevu kazi ya kuhubiri Ufalme, wala si watu wenye kiburi au wenye kutegemea uwezo wao wenyewe. (1 Wakorintho 1:20, 26-29) Watu wanyenyekevu na wenye kiasi hutambua udhaifu wao na hutegemea msaada wa Mungu wanapokuwa katika huduma ya shambani. Pia wanathamini msaada wa kiroho anaotoa kupitia “msimamizi-nyumba mwaminifu.”—Luka 12:42-44; Mithali 22:4.

Maisha ya Familia Yenye Furaha Ni Zawadi Nzuri

19. Ni mambo gani yanayofanya kulea watoto kufanikiwe?

19 Ndoa na maisha yenye furaha ya familia ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Ruthu 1:9; Waefeso 3:14, 15) Watoto pia ni ‘urithi wenye thamani kutoka kwa Yehova,’ nao huwaletea shangwe wazazi wanaofanikiwa kuwasaidia wasitawishe sifa zinazompendeza Mungu. (Zaburi 127:3) Ikiwa wewe ni mzazi, endelea kusikiliza sauti ya Yehova kwa kuwazoeza watoto wako kupatana na Neno lake. Wale wanaofanya hivyo wana hakika ya kutegemezwa na kubarikiwa sana na Yehova.—Mithali 3:5, 6; 22:6; Waefeso 6:1-4.

20. Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazazi ambao watoto wao wameacha ibada ya kweli?

20 Licha ya jitihada nyingi za wazazi wanaomcha Mungu, labda baadhi ya watoto wao huamua kuacha ibada ya kweli wanapokuwa watu wazima. (Mwanzo 26:34, 35) Jambo hilo linaweza kuwahuzunisha sana wazazi. (Mithali 17:21, 25) Hata hivyo, badala ya kukata tamaa kabisa, linaweza kuwa jambo lenye manufaa kwao kukumbuka mfano wa Yesu wa mwana mpotevu. Ingawa mwana huyo aliondoka nyumbani na kuishi maisha mapotovu, baadaye alirudi nyumbani kwa babake, aliyemkaribisha kwa shangwe na kwa upendo. (Luka 15:11-32) Hata kutokee nini, wazazi Wakristo waaminifu wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anawaelewa, anawahangaikia kwa upendo, na kuwategemeza daima.—Zaburi 145:14.

21. Tunapaswa kumsikiliza nani, na kwa nini?

21 Basi, acheni sote tuamue ni nini kilicho muhimu maishani mwetu. Je, tunafuatia kwa bidii utajiri wa kimwili ambao unaweza kutuletea sisi na familia zetu maumivu? Au tunafuatia ‘zawadi njema na upaji mkamilifu’ unaotoka kwa “Baba wa mianga ya kimbingu”? (Yakobo 1:17) Shetani “baba ya uwongo,” anataka tufanye kazi yenye kuchosha ili kupata utajiri wa kimwili na kupoteza furaha na uhai. (Yohana 8:44; Luka 12:15) Lakini Yehova anatujali sana na anatutakia mema. (Isaya 48:17, 18) Hivyo basi, acheni tuendelee kumsikiliza Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo na ‘kujifurahisha’ kwake sikuzote. (Zaburi 37:4) Tukifanya hivyo, Yehova atatutajirisha kwa baraka nyingi na zawadi zenye thamani kubwa, bila maumivu yoyote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona gazeti la Amkeni!, la Januari 22, 1993, ukurasa wa 18-21.

Je, Unakumbuka?

• Unaweza kupata wapi furaha iliyo kuu zaidi?

• Ni zipi baadhi ya zawadi ambazo Yehova huwapa watu wake?

• Kwa nini huduma ya shambani ni zawadi?

• Wazazi wanaweza kufanya nini ili kupata baraka za Mungu wanapolea watoto wao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Je, unaonyesha uthamini kwa zawadi ya Mungu ya Neno lake lililoandikwa?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Licha ya hali ngumu sana, Laurel Nisbet alimtumikia Mungu kwa bidii

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kama Tabitha, Wakristo wa leo wanajulikana sana kwa matendo yao ya upendo

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wazee Wakristo huwahangaikia kwa upendo waamini wenzao