Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Utapata Baraka za Yehova?

Je, Utapata Baraka za Yehova?

Je, Utapata Baraka za Yehova?

“Na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo [“ukiendelea kusikiliza,” “NW”] sauti ya BWANA, Mungu wako.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 28:2

1. Ni nini ambacho kingeamua kama Waisraeli wangepata baraka au laana?

WALIPOKARIBIA kumaliza safari yao ya miaka 40 nyikani, Waisraeli walipiga kambi kwenye Nyanda za Moabu. Bara Lililoahidiwa lilikuwa mbele yao. Wakati huo Musa aliandika kitabu cha Kumbukumbu la Torati, ambacho kina orodha ya baraka na laana. Iwapo Waisraeli ‘wangeendelea kusikiliza sauti ya BWANA’ kwa kumtii, ‘wangepata’ baraka. Yehova aliwapenda kwa kuwa walikuwa ‘wametengwa wawe wake yeye’ na alitaka kuonyesha uwezo wake kwa niaba yao. Lakini kama hawangeendelea kumsikiliza, hapana shaka kwamba wangepatwa na laana.—Kumbukumbu la Torati 8:10-14; 26:18; 28:2, 15.

2. Ni nini maana ya vitenzi vya Kiebrania vinavyotafsiriwa ‘endelea kusikiliza’ na “-pata” kwenye Kumbukumbu la Torati 28:2?

2 Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa ‘endelea kusikiliza’ kwenye Kumbukumbu la Torati 28:2 chamaanisha kitendo chenye kuendelea. Watumishi wa Yehova wanapaswa kumsikiliza wakati wote wala si pindi kwa pindi tu. Watapata baraka za Yehova kwa kufanya hivyo. Kitenzi cha Kiebrania ambacho kimetafsiriwa “-pata” kimethibitishwa kuwa neno litumiwalo wakati wa kuwinda ambalo mara nyingi humaanisha “kufikia.”

3. Tunawezaje kuwa kama Yoshua, na kwa nini jambo hilo ni muhimu sana?

3 Yoshua kiongozi wa Waisraeli alipata baraka alipochagua kumsikiliza Yehova. Yoshua alisema: “Chagueni hivi leo mtakayemtumikia . . . mimi na nyumba yangu tutamtumikia BWANA.” Ndipo watu wakajibu: “Hasha! tusimwache BWANA, ili kuitumikia miungu mingine.” (Yoshua 24:15, 16) Kwa sababu ya mtazamo wake mzuri, Yoshua alikuwa miongoni mwa watu wachache wa kizazi chake waliopata pendeleo la kuingia Bara Lililoahidiwa. Leo, sisi tuko karibu sana kuingia katika Bara Lililoahidiwa ambalo ni bora sana—dunia paradiso ambamo wale walio na kibali cha Mungu watapata baraka nyingi kuliko baraka walizopata Waisraeli wakati wa Yoshua. Je, wewe utapata baraka hizo? Ndiyo, ikiwa utaendelea kumsikiliza Yehova. Ili kuimarisha azimio lako la kufanya hivyo, chunguza historia ya taifa la Israeli la kale na pia mifano ya watu mmoja-mmoja inayoweza kutufunza jambo fulani.—Waroma 15:4.

Baraka au Laana?

4. Mungu alijibu sala ya Solomoni kwa kumpa nini, nasi twapaswa kuzionaje baraka hizo?

4 Kwa kipindi kirefu cha utawala wa Mfalme Solomoni, Yehova aliwabariki Waisraeli kwa njia ya pekee. Walikuwa na usalama na walikuwa na vitu vingi vizuri. (1 Wafalme 4:25) Utajiri wa Solomoni ulikuwa maarufu, ingawa hakuwa amemwomba Mungu utajiri huo wa kimwili. Badala yake, alipokuwa bado mchanga na bila uzoefu, alisali awe na moyo mtiifu—ombi ambalo Yehova alijibu kwa kumpa hekima na ufahamu. Sifa hizo zilimsaidia Solomoni atawale watu ifaavyo, akipambanua mema na mabaya. Ingawa Mungu pia alimpa utajiri na utukufu, akiwa mwanamume kijana, Solomoni alithamini sana thamani bora ya utajiri wa kiroho. (1 Wafalme 3:9-13) Iwe sisi ni matajiri kimwili au la, tunaweza kuwa wenye shukrani kama nini iwapo tuna kibali cha Yehova na tu matajiri kiroho!

5. Kulitokea nini wakati watu wa Israeli na Yuda waliposhindwa kuendelea kumsikiliza Yehova?

5 Waisraeli walishindwa kuonyesha shukrani kwa baraka za Yehova. Kwa sababu hawakuendelea kumsikiliza, walipatwa na laana zilizokuwa zimetabiriwa. Kwa sababu hiyo walishindwa na maadui wao na wakazi wa Israeli na Yuda wakapelekwa uhamishoni. (Kumbukumbu la Torati 28:36; 2 Wafalme 17:22, 23; 2 Mambo ya Nyakati 36:17-20) Je, watu wa Mungu walijifunza kutokana na mateso hayo kwamba Yehova huwabariki tu wale wanaoendelea kumsikiliza? Mabaki ya Wayahudi waliorudi kwenye nchi yao mwaka wa 537 K.W.K. walikuwa na fursa ya kuonyesha kama walikuwa wamejipatia “moyo wa hekima” na kuona uhitaji wa kuendelea kumsikiliza Mungu.—Zaburi 90:12.

6. (a) Kwa nini Yehova alimtuma Hagai na Zekaria kutolea watu wake unabii? (b) Ni kanuni gani iliyodhihirishwa na ujumbe wa Mungu kupitia Hagai?

6 Wayahudi waliorudishwa walijenga madhabahu na kuanza kujenga hekalu huko Yerusalemu. Lakini upinzani mkali ulipozuka, bidii yao ilianza kufifia, wakaacha kujenga. (Ezra 3:1-3, 10; 4:1-4, 23, 24) Pia walianza kutanguliza mambo ya anasa. Hivyo, Mungu akawatuma manabii Hagai na Zekaria kuchochea tena bidii ya watu wake kwa ajili ya ibada ya kweli. Yehova alisema hivi kupitia Hagai: “Je! huu ndio wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenye mapambo ya mbao, iwapo nyumba hii inakaa hali ya kuharibika? . . . Zitafakarini njia zenu. Mmepanda mbegu nyingi mkavuna kidogo; mnakula lakini hamshibi. . . . Na yeye apataye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka.” (Hagai 1:4-6) Kuachilia mambo ya kiroho ili kufuatia vitu vya kimwili hakuleti baraka za Yehova.—Luka 12:15-21.

7. Kwa nini Yehova aliwaambia Wayahudi ‘wazitafakari njia zao’?

7 Kwa kuhangaikia sana mambo yao ya kila siku, Wayahudi walikuwa wamesahau kwamba wangepata baraka za Mungu za mvua na misimu yenye mazao mengi kama wangeendelea kumtii, japo upinzani. (Hagai 1:9-11) Basi, himizo hili lafaa kama nini: “Zitafakarini njia zenu”! (Hagai 1:7) Kwa kweli, Yehova alikuwa akiwaambia hivi: ‘Fahamuni kwamba kwa sababu mmeacha ukiwa nyumba yangu ya ibada, kazi mnayofanya katika mashamba yenu itakuwa ya bure.’ Maneno ya Yehova yaliyopuliziwa ambayo alinena kupitia manabii wake, yaligusa mioyo ya watu waliosikiliza, kwa kuwa walianza kujenga hekalu tena na kulimaliza mwaka wa 515 K.W.K.

8. Yehova aliwahimiza Wayahudi wafanye nini katika siku za Malaki, na kwa nini?

8 Baadaye katika siku za nabii Malaki, Wayahudi walianza tena kuyumbayumba kiroho, na hata kumtolea Mungu dhabihu zisizokubalika. (Malaki 1:6-8) Hivyo, Yehova akawahimiza walete sehemu ya kumi ya mazao yao kwenye ghala na wamjaribu waone kama hatawafungulia milango ya mbinguni na kuwamwagia baraka, hata kusiwepo uhitaji tena. (Malaki 3:10) Lilikuwa jambo la upumbavu kama nini kwa Wayahudi kufanya kazi ya kuchosha wakitafuta vitu ambavyo Mungu angewapa kwa wingi kama wangeendelea kusikiliza sauti yake!—2 Mambo ya Nyakati 31:10.

9. Tutachunguza watu gani watatu ambao maisha yao yamesimuliwa katika Biblia?

9 Mbali na historia ya taifa la Israeli, Biblia pia inasimulia kuhusu maisha ya watu wengi waliopokea baraka au laana ya Mungu, ikitegemea kama waliendelea kumsikiliza Yehova au la. Acheni tuone tunachoweza kujifunza kutokana na watatu kati ya watu hao—Boazi, Nabali, na Hana. Huenda ukataka kusoma kuhusu watu hao katika kitabu cha Ruthu na pia cha 1 Samweli 1:1–2:21 na 1 Samweli 25:2-42.

Boazi Alimsikiliza Mungu

10. Boazi na Nabali walifanana katika mambo gani?

10 Ingawa Boazi na Nabali hawakuishi wakati mmoja, kuna mambo fulani yanayofanana katika maisha yao. Kwa mfano, wanaume hao wawili waliishi katika nchi ya Yuda. Walikuwa wamilikaji-ardhi matajiri, na wote wawili walikuwa na fursa ya pekee ya kumwonyesha upendo-fadhili mtu fulani mwenye uhitaji. Lakini walifanana katika mambo hayo tu.

11. Boazi alionyeshaje kwamba aliendelea kumsikiliza Yehova?

11 Boazi aliishi katika kipindi cha waamuzi wa Israeli. Aliwatendea wengine kwa heshima, nao wavunaji wake walimstahi sana. (Ruthu 2:4) Alitii Sheria kwa kuhakikisha kwamba masazo ya mavuno yaliachwa shambani mwake kwa ajili ya wenye shida na maskini. (Mambo ya Walawi 19:9, 10) Boazi alifanya nini alipopata habari kuhusu Ruthu na Naomi na kuona bidii ya Ruthu ya kumruzuku mama-mkwe wake mzee? Alimjali sana Ruthu, akaamuru watumishi wake wamruhusu aokote masazo kwenye shamba lake. Kwa maneno na matendo yake ya upendo, Boazi alionyesha kwamba alikuwa mtu wa kiroho aliyemsikiliza Yehova. Kwa hiyo, alipata kibali na baraka za Mungu.—Mambo ya Walawi 19:18; Ruthu 2:5-16.

12, 13. (a) Boazi alionyeshaje staha kubwa kwa sheria ya Yehova ya ukombozi? (b) Boazi alipata baraka gani kutoka kwa Mungu?

12 Uthibitisho wenye kutokeza kwamba Boazi aliendelea kumsikiliza Yehova ni jinsi alivyofuata sheria ya Mungu ya ukombozi. Boazi alifanya yote awezayo kuhakikisha kwamba urithi wa mtu wa jamaa yake—Elimeleki, mume aliyekufa wa Naomi—ungebaki katika familia yake. Kupitia “mpango wa ndoa ya ndugu-mkwe,” mjane angepaswa kuolewa na mtu wa jamaa wa karibu ili mwana wanayezaa aweze kuhifadhi urithi. (Kumbukumbu la Torati 25:5-10, NW; Mambo ya Walawi 25:47-49) Ruthu alijitoa aolewe badala ya Naomi, ambaye alikuwa amepita umri wa kuzaa. Baada ya mtu wa jamaa ya karibu ya Elimeleki kukataa kumsaidia Naomi, Boazi alimwoa Ruthu. Mwana wao Obedi alionwa kuwa uzao wa Naomi na mrithi halali wa Elimeleki.—Ruthu 2:19, 20; 4:1, 6, 9, 13-16.

13 Boazi alipata baraka nyingi kwa sababu ya kufuata sheria ya Mungu bila ubinafsi. Kupitia mwana wao Obedi, Boazi na Ruthu walipata pendeleo la kuwa babu na nyanya wa Yesu Kristo. (Ruthu 2:12; 4:13, 21, 22; Mathayo 1:1, 5, 6) Kutokana na matendo ya Boazi yasiyokuwa na ubinafsi, tunajifunza kwamba wale wanaowapenda wengine na kufuata matakwa ya Mungu hupata baraka.

Nabali Hakusikiliza

14. Nabali alikuwa mtu wa aina gani?

14 Tofauti na Boazi, Nabali alishindwa kumsikiliza Yehova. Alivunja sheria hii ya Mungu: “Umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mambo ya Walawi 19:18) Nabali hakuwa mtu wa kiroho; alikuwa “hana adabu; tena mwovu katika matendo yake.” Hata watumishi wake walimwona kuwa “mtu asiyefaa kabisa.” Kwa kufaa, jina lake Nabali lamaanisha “asiye na akili,” au “mpumbavu.” (1 Samweli 25:3, 17, 25) Hivyo, Nabali alitendaje alipopata fursa ya kumwonyesha fadhili mtu mwenye uhitaji—Daudi, mtiwa-mafuta wa Yehova?—1 Samweli 16:13.

15. Nabali alimtendeaje Daudi, naye Abigaili alikuwaje tofauti na mume wake kuhusiana na hilo?

15 Walipokuwa wamepiga kambi karibu na mifugo ya Nabali, Daudi na watumishi wake walilinda mifugo hiyo dhidi ya magenge ya wanyang’anyi bila kudai malipo yoyote. “Walikuwa boma kwetu usiku na mchana,” akasema mmoja wa wachungaji wa Nabali. Hata hivyo, wajumbe wa Daudi walipoomba wapewe chakula, Nabali “aliwatukana,” akawaacha waende zao mikono mitupu. (1 Samweli 25:2-16) Abigaili mke wa Nabali alimpelekea Daudi chakula mara moja. Daudi mwenye hasira kali alikuwa karibu kumwangamiza Nabali na watumishi wake. Hivyo, hatua aliyochukua Abigaili iliokoa maisha ya watu wengi na kumzuia Daudi asiwe na hatia ya damu. Lakini pupa na ukatili wa Nabali ulikuwa umepita kiasi. Siku kumi hivi baadaye, “BWANA alimpiga huyo Nabali, hata akafa.”—1 Samweli 25:18-38.

16. Tunawezaje kumwiga Boazi na kukataa njia za Nabali?

16 Boazi na Nabali walitofautiana kama nini! Acheni tuige fadhili na ukarimu wa Boazi na kukataa njia za ukatili na ubinafsi za Nabali. (Waebrania 13:16) Tunaweza kufanya hivyo kwa kutumia ushauri huu wa mtume Paulo: “Maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Leo “kondoo wengine” wa Yesu, ambao ni Wakristo walio na tumaini la kuishi duniani, wana pendeleo la kuwafanyia mema watiwa-mafuta wa Mungu, mabaki ya wale 144,000, ambao watapewa uhai usioweza kufa mbinguni. (Yohana 10:16; 1 Wakorintho 15:50-53; Ufunuo 14:1, 4) Yesu huona matendo hayo ya upendo kana kwamba anatendewa yeye binafsi, na kufanya mambo hayo huleta baraka nyingi za Yehova.—Mathayo 25:34-40; 1 Yohana 3:18.

Majaribu na Baraka Alizopata Hana

17. Hana alipatwa na majaribu gani, naye alionyesha mtazamo gani?

17 Yehova pia alimbariki Hana, mwanamke mcha Mungu. Hana na mume wake Elkana, aliyekuwa Mlawi, waliishi katika eneo lenye milima-milima la Efraimu. Elkana alikuwa na mke mwingine—Penina—jambo lililoruhusiwa na kufanywa chini ya Sheria. Hana alikuwa tasa, hali yenye kuaibisha kwa mwanamke Mwisraeli, ilhali Penina alikuwa na watoto kadhaa. (1 Samweli 1:1-3; 1 Mambo ya Nyakati 6:16, 33, 34) Hata hivyo, badala ya kumfariji Hana, Penina alikuwa akitenda kwa kukosa upendo, jambo lililomwudhi Hana, likamfanya alie na kukosa hamu ya chakula. Na jambo lililofanya hali iwe baya hata zaidi ni kwamba Penina alimtendea hivyo “mwaka kwa mwaka,” kila wakati ambapo familia hiyo ilienda kwenye nyumba ya Yehova huko Shilo. (1 Samweli 1:4-8) Penina alionyesha ukatili ulioje, naye Hana alipata jaribu la imani lililoje! Lakini Hana hakumlaumu Yehova kamwe; wala hakuachwa nyumbani wakati mume wake alipoenda Shilo. Kwa hiyo, hapana shaka kwamba hatimaye angepata baraka nyingi.

18. Hana aliweka kielelezo gani?

18 Hana aliweka kielelezo kizuri kwa watu wa Yehova leo, hasa wale ambao huenda wameumizwa na maneno yasiyo na huruma ya wengine. Katika hali hizo, suluhisho si kujitenga. (Mithali 18:1) Hana hakuruhusu majaribu yaliyompata yapunguze tamaa yake ya kuwa mahali ambapo Neno la Mungu lilifundishwa na ambapo watu wa Mungu walikutana ili kuabudu. Kwa hiyo, aliendelea kuwa thabiti kiroho. Sala yake iliyoandikwa kwenye 1 Samweli 2:1-10 inatuonyesha jinsi hali yake ya kiroho ilivyokuwa thabiti. *

19. Tunaweza kuonyeshaje shukrani zetu kwa mambo ya kiroho?

19 Sisi watumishi wa Yehova leo hatuabudu kwenye tabenakulo. Hata hivyo, tunaweza kuonyesha shukrani kwa mambo ya kiroho kama Hana alivyofanya. Kwa mfano, tunaweza kuonyesha shukrani zetu nyingi kwa utajiri wa kiroho kwa kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo, makusanyiko, na mikusanyiko. Acheni tutumie pindi hizo kutiana moyo katika ibada ya kweli ya Yehova, ambaye ametupa “pendeleo la kumtolea utumishi mtakatifu bila hofu kwa uaminifu-mshikamanifu na uadilifu.”—Luka 1:74, 75; Waebrania 10:24, 25.

20, 21. Hana alithawabishwaje kwa sababu ya ujitoaji wake kwa Mungu?

20 Yehova aliona jinsi Hana alivyojitoa kwake naye akamthawabisha sana. Kwenye mojawapo ya safari za kila mwaka ambazo familia hiyo ilifanya huko Shilo, Hana mwenye majonzi alisali kwa Mungu kwa bidii na kuweka nadhiri hii: “Ee BWANA wa majeshi, ikiwa wewe utaliangalia teso la mjakazi wako, na kunikumbuka, wala usinisahau mimi mjakazi wako, na kunipa mimi mjakazi wako mtoto mume, ndipo mimi nitakapompa BWANA huyo mtoto siku zote za maisha yake.” (1 Samweli 1:9-11) Mungu alisikia ombi la Hana, akambariki kwa kumpa mwana ambaye alimwita Samweli. Alipomwachisha kunyonya, alimpeleka Shilo, akatumike kwenye tabenakulo.—1 Samweli 1:20, 24-28.

21 Hana alionyesha upendo wake kwa Mungu na kutimiza nadhiri yake kuhusiana na Samweli. Hebu fikiria baraka nyingi ambazo yeye na Elkana walipata kwa sababu mwana wao mpendwa alitumika kwenye tabenakulo! Vivyo hivyo, wazazi wengi Wakristo hupata shangwe na baraka kwa sababu wana na binti zao wanatumika wakiwa wahudumu mapainia wa wakati wote, wanabetheli, au katika njia nyingine zinazomletea Yehova utukufu.

Endelea Kumsikiliza Yehova!

22, 23. (a) Tunaweza kuwa na hakika ya jambo gani tukiendelea kusikiliza sauti ya Yehova? (b) Tutazungumzia nini katika makala ifuatayo?

22 Tunaweza kuwa na hakika ya jambo gani tukiendelea kumsikiliza Yehova? Tukimpenda Mungu kwa nafsi yote na kudhihirisha kwamba tumejitoa kwake, hali yetu ya kiroho itakuwa nzuri. Hata ikiwa kufanya hivyo kutamaanisha kwamba tutalazimika kuvumilia majaribu makali, hapana shaka kwamba Yehova atatubariki—mara nyingi kwa njia kubwa kuliko tunavyoweza kuwazia.—Zaburi 37:4; Waebrania 6:10.

23 Watu wa Mungu watapata baraka nyingi wakati ujao. Kwa sababu ya kumsikiliza Yehova kwa utiifu, “umati mkubwa” utaokoka “dhiki kubwa” na utapata shangwe ya kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Ufunuo 7:9-14; 2 Petro 3:13) Humo, Yehova atatimiza kikamili tamaa za uadilifu za watu wake wote. (Zaburi 145:16) Hata hivyo, kama makala ifuatayo itakavyoonyesha, hata sasa wale wanaoendelea kusikiliza sauti ya Yehova hupata ‘zawadi njema na upaji mkamilifu kutoka juu.’—Yakobo 1:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Maneno ya Hana yanafanana kwa kadiri fulani na yale ya msichana bikira Maria, aliyosema punde baada ya kujua kwamba angekuwa mama ya Mesiya.—Luka 1:46-55.

Je, Unakumbuka?

• Historia ya Waisraeli inaweza kutufunza nini kuhusu baraka za Mungu?

• Boazi na Nabali walitofautianaje?

• Tunaweza kumwigaje Hana?

• Kwa nini tuendelee kusikiliza sauti ya Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mfalme Solomoni alisali awe na moyo mtiifu, naye Yehova akampa hekima

[Picha katika ukurasa wa 12]

Boazi aliwatendea wengine kwa heshima na fadhili

[Picha katika ukurasa wa 15]

Hana alibarikiwa sana kwa kumtegemea Yehova