Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Watu Wanaweza Kuungana Kikweli?

Je, Watu Wanaweza Kuungana Kikweli?

Je, Watu Wanaweza Kuungana Kikweli?

HATA uwe unaamini nini, huenda ukakubali kwamba lazima kuwe na watu wanaopenda kweli katika karibu dini zote. Watu wanaothamini sana kweli na wanaotaka kuitafuta wanaweza kupatikana miongoni mwa Wahindu, Wakatoliki, Wayahudi, na wengineo. Hata hivyo, inaonekana dini inagawanya wanadamu. Wengine hata hutumia dini ili kutimiza makusudi maovu. Je, siku moja itawezekana watu wote wanyofu kutoka dini zote na ambao wanapenda mambo ya uadilifu na kweli waungane? Je, wanaweza kukusanywa pamoja ili watimize kusudi fulani kwa pamoja?

Ni jambo lenye kusikitisha kama nini kuona kwamba dini inazidi kusababisha migogoro! Fikiria baadhi ya vita ambavyo vimesababishwa na dini. Wahindu wanapigana na Wabudha nchini Sri Lanka. Waprotestanti, Wakatoliki na Wayahudi wamemwaga damu katika vita mbalimbali. “Wakristo” wanapigana na Waislamu huko Bosnia, Chechnya, Indonesia, na Kosovo. Pia katika Machi 2000, raia 300 wa Nigeria waliuawa katika vita vya kidini vya siku mbili. Kwa kweli, vita hivyo vimechochewa na chuki ya kidini.

Mara nyingi watu wanyofu wamehuzunishwa na maovu ya kidini. Kwa mfano, watu wengi wanaoenda makanisani wamechukizwa kuona makasisi wanaowatenda watoto vibaya kingono wakiruhusiwa na makanisa fulani waendelee kutumikia. Waamini wengine wanaaibika sana kuona migawanyiko iliyopo miongoni mwa yale yanayoitwa madhehebu ya Kikristo kuhusiana na masuala kama vile ngono kati ya watu wa jinsia moja na utoaji-mimba. Bila shaka, dini haijaunganisha wanadamu. Hata hivyo, katika dini nyingi kuna watu wanaopenda kweli, kama ionyeshwavyo na mambo yaliyoonwa yafuatayo.

Walitamani Kweli Sana

Fedelia alikuwa mwabudu mnyofu na mwaminifu katika Kanisa Katoliki la San Francisco huko La Paz, Bolivia. Aliinamia sanamu ya Maria na kuweka mishumaa bora kabisa mbele ya msalaba wenye sanamu ya Yesu. Kila juma, alichanga chakula kingi kwa kasisi ili awagawie maskini. Hata hivyo, watoto watano wa Fedelia walikufa kabla hawajabatizwa. Kasisi huyo alipomwambia kwamba watoto hao wote walikuwa wakiteseka katika giza la Ahera, Fidelia alijiuliza, ‘Ikiwa Mungu ni mwenye upendo na fadhili, anawezaje kufanya hivyo?’

Tara, ambaye ni daktari, alilelewa katika dini ya Hindu huko Kathmandu, Nepal. Kwa kufuata desturi za karne nyingi za wazazi wake wa kale, aliabudu miungu yake katika mahekalu ya Wahindu na alikuwa na sanamu nyumbani mwake. Lakini Tara alitatanishwa sana na maswali kama vile: Kwa nini watu wanateseka sana? Kwa nini watu hufa? Dini yake haikumpa majibu yoyote yenye kuridhisha.

Kwa upande mwingine, Panya alilelewa katika dini ya Buddha huko Bangkok, Thailand. Alifundishwa kwamba mateso husababishwa na matendo yaliyofanywa katika maisha ya awali na kwamba mtu anaweza kuepuka mateso kwa kutokuwa na tamaa yoyote. Kama Wabudha wengine wanyofu, alifundishwa kustahi sana hekima ya watawa wa kiume waliovalia majoho ya rangi ya manjano ambao walienda nyumbani mwake kila wakati wa mapambazuko ili kuchukua sadaka kwa ajili ya maskini. Alikuwa akitafakari na kukusanya sanamu za Buddha huku akiamini kwamba zingeweza kumlinda. Baada ya kupata aksidenti mbaya iliyomfanya apooze kuanzia kiunoni hadi miguuni, Panya alizuru makao ya watawa Wabudha, akitumaini kwa moyo wote kuponywa kimuujiza. Hakupata ponyo au nuru ya kiroho. Badala yake, alianza kujihusisha na mambo ya uwasiliani-roho.

Virgil alizaliwa Marekani na akajiunga na kikundi cha Waislamu Weusi alipokuwa chuoni. Aligawanya kwa bidii vichapo vyao vilivyofundisha kwamba mzungu ni Ibilisi. Walifikiri hiyo ndiyo sababu wazungu waliwatenda watu weusi ukatili mwingi kadiri hiyo. Ijapokuwa alishikilia imani hiyo kwa unyofu, Virgil alitatanishwa na maswali kama vile: Wazungu wote wanawezaje kuwa wabaya? Na kwa nini sehemu kubwa ya mahubiri ilihusisha pesa?

Ingawa Charo alikulia katika nchi yenye Wakatoliki wengi ya Amerika Kusini, alikuwa Mprotestanti mwenye moyo mnyofu. Alifurahi kwamba hakuhusika katika ibada ya sanamu iliyomzunguka. Charo alifurahia kwenda kanisani kila Jumapili ili kuhudhuria ibada yenye kuchochea hisia, ambapo alipayuka “Haleluya!” na kushiriki kuimba nyimbo za kidini na dansi zilizofuata. Charo aliamini kwa unyofu kwamba ameokolewa na kuzaliwa mara ya pili. Alitoa fungu la kumi la mapato yake kwa kanisa, na wakati mhubiri aliyempenda sana alipoomba michango kwenye televisheni, alimtumia pesa za kusaidia watoto wanaoishi Afrika. Hata hivyo, alipomwuliza pasta wake kwa nini Mungu mwenye upendo hutesa nafsi katika moto wa mateso, alitambua kwamba pasta huyo hakuwa na jibu lenye kuridhisha. Baadaye, aligundua kwamba michango yake haikutumiwa kusaidia watoto wanaoishi barani Afrika.

Ingawa watu hao watano walikuwa na malezi tofauti, wana jambo moja linalofanana. Walipenda kweli na kutafuta kwa unyofu majibu ya moja kwa moja ya maswali yao. Lakini je, kweli wangeweza kuungana katika ibada ya kweli? Makala ifuatayo itajibu swali hilo.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Je, inawezekana watu walio na malezi tofauti waungane kikweli?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

G.P.O., Jerusalem