Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Kitu Gani Chenye Thamani ya Kweli?

Ni Kitu Gani Chenye Thamani ya Kweli?

Ni Kitu Gani Chenye Thamani ya Kweli?

Ni jambo lenye kusisimua kuwa na kitu chenye thamani ya kweli. Lakini kitu hicho chaweza kuwa nini? Je, ni pesa nyingi? Ni kito adimu, cha bei ya juu? Ni sifa na umashuhuri? Watu wengi huthamini sana vitu hivyo. Kuwa na vitu hivyo humwezesha mtu ajiruzuku, hufanya maisha yawe na kusudi zaidi, au hutosheleza uhitaji wa moyoni wa kutaka kukubaliwa na kufanikiwa. Je, tunajitahidi kupata vitu hivyo, tukitumaini kwamba vitatimiza miradi yetu ya wakati ujao?

KWA kawaida, watu huthamini kitu ikitegemea jinsi kinavyotimiza mahitaji yao au kutosheleza tamaa zao. Tunathamini sana vitu ambavyo hutupa furaha na tumaini la wakati ujao ulio salama. Tunathamini vitu ambavyo hutupa kitulizo, faraja, au staha ya papo hapo. Hata hivyo, si jambo la hekima kuona kitu fulani kuwa chenye thamani kwa kutegemea tu tamaa yetu inayobadilika-badilika. Kwa kweli, tunaamua kama kitu kina thamani halisi kwa kutegemea uhitaji wetu mkubwa zaidi.

Uhitaji wetu mkubwa zaidi ni upi? Bila uhai hakuna kitu kinachoweza kuwa na thamani yoyote. Bila uhai, hatuwezi kuendelea kuishi. Mfalme Solomoni wa Israeli la kale aliandika hivi: “Wafu hawajui neno lolote . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburi la ujumla la wanadamu] uendako wewe.” (Mhubiri 9:5, 10) Tunapokufa, tunalazimika kuacha mali zozote tulizo nazo. Kwa hiyo uhitaji wetu mkubwa zaidi, ni kupata kitu ambacho kitahifadhi uhai wetu. Ni nini kitakachohifadhi uhai wetu?

Ni Nini Kitakachohifadhi Uhai Wetu?

‘Fedha ni ulinzi,’ akasema Mfalme Solomoni. (Mhubiri 7:12) Tukiwa na pesa za kutosha, tunaweza kununua chakula na kuwa na nyumba nzuri. Tukiwa na pesa tunaweza kufurahia kusafiri sehemu za mbali. Pesa zinaweza kutusaidia kutimiza mahitaji yetu ya msingi wakati ambapo hatuwezi kufanya kazi tena kwa sababu ya uzee au ugonjwa. Kuna faida nyingi za kuwa na pesa. Hata hivyo, pesa haziwezi kuhifadhi uhai wetu. Mtume Paulo alimshauri Timotheo hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo uliopo wasiwe wenye kunia ya juu, na waweke tumaini lao, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu.” (1 Timotheo 6:17) Pesa zote ulimwenguni haziwezi kutupa uhai.

Fikiria jambo lililompata Hitoshi. Kwa kuwa alilelewa katika familia maskini, Hitoshi alitamani sana kuwa tajiri. Alitumaini pesa sana hivi kwamba alifikiri watu wanaweza kuwa waaminifu kwako ukiwapa pesa. Kisha mtu fulani akamtembelea Hitoshi nyumbani mwake na kumwuliza ikiwa anajua kwamba Yesu Kristo alikufa kwa ajili yake. Swali hilo lilimvutia Hitoshi kwa sababu alihisi kwamba hakuna mtu ambaye angeweza kufa kwa ajili yake. Alihudhuria hotuba ya watu wote inayotegemea Biblia na alishangaa kusikia shauri kuhusu ‘kuweka jicho likiwa sahili.’ Msemaji alieleza kwamba jicho “sahili” ni lile linalozingatia wakati ujao na linalokazia mambo ya kiroho. (Luka 11:34) Badala ya kujitahidi sana kupata pesa, Hitoshi alianza kutanguliza mambo ya kiroho maishani mwake.

Mali za kimwili pia zinaweza kutupa usalama na utulivu kwa kiasi fulani. Kuwa na vitu vingi kwaweza kufanya tusihangaikie sana mahitaji yetu ya kila siku. Tunaweza kuhisi kuwa tumefanikiwa tukiwa na nyumba nzuri katika mahali panapopendeza. Huenda wengine wakavutiwa nasi tunapokuwa na mavazi mazuri na gari zuri.

Ni baraka “kufurahia matunda ya kazi zetu.” (Mhubiri 3:13, Biblia Habari Njema) Na tunapokuwa na pesa za ziada, wapendwa wetu wanaweza ‘kustarehe, kula, kunywa, na kujifurahisha wenyewe.’ Hata hivyo, vitu vya kimwili vina thamani ya muda tu. Yesu alitoa onyo hili kuhusu tamaa aliposema: “Hata wakati mtu ana wingi uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15-21) Vitu vya kimwili, bila kujali thamani yake, au wingi wake, haviwezi kutupa uhai.

Kwa mfano, Liz aliolewa na mtu mwenye pesa nyingi. Asema hivi: “Tulikuwa na nyumba nzuri na magari mawili, na kwa kuwa tulikuwa na pesa za kutosha tungeweza kupata kitu chochote cha kimwili ambacho tungetaka . . . Lakini huenda ikashangaza kwamba bado nilikuwa na wasiwasi kuhusu pesa.” Aeleza hivi: “Tulikosa mambo mengi sana yenye thamani kubwa. Inaonekana kwamba kadiri unavyokuwa na pesa nyingi, ndivyo unavyokosa usalama.”

Wengi huthamini sana kuwa na sifa na umashuhuri kwa kuwa zinaweza kumfanya mtu aheshimiwe. Katika ulimwengu wa leo, ni jambo linalotamanika kuwa na kazi nzuri. Kusitawisha sifa au ustadi wa kipekee kwaweza kutusaidia tuwe na sifa nzuri. Huenda wengine wakatusifu, wakaheshimu sana maoni yetu na kutamani kupata kibali chetu. Mambo hayo yote yanaweza kuwa yenye kusisimua na kuridhisha. Hata hivyo, hatimaye mambo hayo huisha. Solomoni alikuwa na fahari na uwezo kuliko mfalme yeyote, lakini aliomboleza hivi: “Hakuna kumbukumbu la milele la mwenye hekima, wala la mpumbavu . . . Wote pia watakuwa wamekwisha kusahauliwa.” (Mhubiri 2:16) Sifa au umashuhuri hauwezi kumpa mtu uhai.

Mchongaji mmoja wa sanamu anayeitwa Celo alipata kuthamini kitu fulani chenye thamani kuliko umashuhuri. Kwa kuwa alikuwa na kipawa, alifaulu kwenda katika shule iliyomsaidia kuboresha ustadi wake. Punde si punde, vyombo vya habari na wachambuzi wakaanza kuisifu kazi yake. Sanamu nyingi alizochonga zilipelekwa kwenye maonyesho katika miji mikuu ya Ulaya. Celo asema: “Kwa kweli, kwa muda fulani sanaa ndiyo iliyokuwa jambo la maana zaidi maishani mwangu. Hata hivyo, nilipata kutambua kwamba kufuatia kazi kungekuwa sawa na kutumikia mabwana wawili. (Mathayo 6:24) Nilisadiki kwamba kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu ndilo jambo muhimu zaidi ambalo ningeweza kufanya. Kwa hiyo niliamua kuacha kazi yangu ya kuchonga sanamu.”

Ni Kitu Gani Chenye Thamani Kubwa Zaidi?

Kwa kuwa hakuna kitu chochote kilicho na thamani bila uhai, tunaweza kujipatia nini ili tuwe na hakika kwamba tutaendelea kuishi? Yehova Mungu ndiye chanzo cha uhai. (Zaburi 36:9) Kwa kweli, “kwa njia yake tuna uhai na twaenda na kuwako.” (Matendo 17:28) Anawapa wale anaowapenda zawadi ya uhai udumuo milele. (Waroma 6:23) Twapaswa kufanya nini ili tustahili kupewa zawadi hiyo?

Ili tupokee zawadi ya uhai udumuo milele twapaswa kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. Kwa hiyo, kibali chake ni chenye thamani kubwa kuliko kitu chochote tunachoweza kuwa nacho. Tukiwa na kibali chake, tuna taraja la kupata furaha ya kweli na inayodumu. Hata hivyo, tusipokuwa na kibali cha Mungu, tutaharibiwa milele. Basi, ni wazi kwamba jambo lolote linaloweza kutusaidia kuwa na uhusiano mzuri na Yehova ni lenye thamani kubwa.

Jambo Tunalopaswa Kufanya

Ili tufanikiwe, tunahitaji kujipatia ujuzi. Neno la Yehova, Biblia, ndiyo chanzo cha ujuzi sahihi. Biblia pekee ndiyo hutuambia jambo tunalopaswa kufanya ili kumpendeza Mungu. Kwa hiyo tunahitaji kujifunza Maandiko kwa uangalifu. Tukijifunza kwa bidii yote tuwezayo kuhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo tutapata ‘ujuzi unaomaanisha uhai udumuo milele.’ (Yohana 17:3) Ujuzi huo ni hazina tunayopaswa kuthamini sana!—Mithali 2:1-5.

Ujuzi tunaopata kutoka kwa Neno la Mungu hutusaidia tuchukue hatua inayofuata—kudhihirisha imani katika Yesu Kristo. Yehova ameagiza kwamba wote wanaokuja kwake lazima wafanye hivyo kupitia Yesu. (Yohana 14:6) Kwa kweli “hakuna wokovu katika mwingine yeyote.” (Matendo 4:12) Hatimaye, tutaokoka si kwa kutegemea ‘fedha au dhahabu . . . , bali kwa damu yenye bei ya Kristo.’ (1 Petro 1:18, 19) Lazima tudhihirishe imani yetu kwa kuamini mafundisho ya Yesu na kufuata kielelezo chake. (Waebrania 12:1-3; 1 Petro 2:21) Dhabihu yake ni yenye thamani kama nini! Uhai wa milele kwa ajili ya wanadamu wote unategemea kutumiwa kwa dhabihu hiyo. Itakapotumiwa kikamili kwa niaba yetu, tutapewa zawadi yenye thamani kwelikweli, uhai udumuo milele.—Yohana 3:16.

Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Kumpenda Yehova kwamaanisha kwamba “tushike amri zake.” (1 Yohana 5:3) Amri zake hutaka tujitenge na ulimwengu, tudumishe mwenendo mzuri na kuunga mkono Ufalme wake kwa uaminifu. Hivyo ndivyo ‘tunavyochagua uzima’ badala ya mauti. (Kumbukumbu la Torati 30:19) ‘Tukimkaribia Mungu, naye atatukaribia.’—Yakobo 4:8.

Kuwa na uhakika kwamba una kibali cha Mungu ni jambo lenye thamani zaidi ya hazina zote ulimwenguni. Wale ambao wana kibali cha Mungu ndio watu wenye furaha zaidi duniani! Kwa hiyo basi, acheni tujitahidi kupata kitu chenye thamani ya kweli—kibali cha Yehova. Kwa kweli, acheni tutii shauri hili la mtume Paulo: “Fuatia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole. Pigana pigano bora la imani, pata mshiko imara juu ya uhai udumuo milele.”—1 Timotheo 6:11, 12.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Ni nini unachothamini sana? Pesa, vitu vya kimwili, umashuhuri, au kitu kingine?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tunahitaji kujifunza Maandiko kwa uangalifu