Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Inamaanisha Nini Kuwa Mwaminifu-mshikamanifu?

Inamaanisha Nini Kuwa Mwaminifu-mshikamanifu?

Inamaanisha Nini Kuwa Mwaminifu-mshikamanifu?

WAYAHUDI wa madhehebu ya Hasidim wa karne ya pili K.W.K. walijiona kuwa watu waaminifu-washikamanifu sana. Jina lao Hasidim latokana na neno la Kiebrania cha·sidhʹ, ambalo kwa kawaida hutafsiriwa “-enye uaminifu-mshikamanifu.” Neno hilo limetokana na nomino cheʹsedh, ambayo mara nyingi hutafsiriwa “fadhili-upendo,” “upendo mwaminifu-mshikamanifu,” “fadhili,” “wema,” “rehema.” Kamusi Theological Dictionary of the Old Testament yasema kwamba nomino cheʹsedh ‘hutumiwa kuonyesha bidii, ushirikiano, na uvumilivu, na huonyesha pia mtazamo wa kibinadamu na tendo linalotokana na mtazamo huo, tendo ambalo hudumisha au kuendeleza uhai. Tendo hilo ni hatua inayochukuliwa kwa niaba ya mtu ambaye amepatwa na jambo baya au msiba nalo ni wonyesho wa urafiki.’

Ni wazi kwamba lugha nyingi hazina neno linalotoa maana kamili ya neno hilo la Kiebrania kama linavyotumiwa katika Biblia. Vyovyote vile, neno uaminifu-mshikamanifu kulingana na Biblia humaanisha mengi zaidi ya kutimiza wajibu mbalimbali kwa uaminifu. Linatia ndani wazo la kupenda wengine na pia kuchukua hatua madhubuti ili kuwasaidia. Ili kuelewa maana ya uaminifu-mshikamanifu wa kweli, ona jinsi Yehova alivyoonyesha sifa hiyo kwa Abrahamu, Musa, Daudi, taifa la Israeli, na wanadamu kwa ujumla.

Yehova Alionyesha Uaminifu-Mshikamanifu

Yehova alimwambia rafiki yake Abrahamu hivi: “Mimi ni ngao yako.” (Mwanzo 15:1; Isaya 41:8) Hayo hayakuwa maneno matupu tu. Yehova alimlinda na kumwokoa Abrahamu na jamaa yake kutoka kwa Farao na Abimeleki. Alimsaidia Abrahamu kumwokoa Loti kutoka kwa muungano wa wafalme wanne. Yehova alimwezesha Abrahamu aliyekuwa na umri wa miaka 100 na mkewe mwenye umri wa miaka 90 kuzaa mtoto ili Mbegu aliyeahidiwa aje kupitia kwao. Yehova alizungumza na Abrahamu kwa ukawaida kupitia maono, ndoto, na wajumbe wa kimalaika. Kwa kweli, Yehova alionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Abrahamu alipokuwa hai na pia muda mrefu baada ya yeye kufa. Kwa karne nyingi, Yehova alitimiza ahadi zake kwa wazao wa Abrahamu, taifa la Israeli, licha ya upotovu wao. Uhusiano wa Yehova na Abrahamu ulidhihirisha maana ya uaminifu-mshikamanifu wa kweli—upendo uliogeuzwa kuwa matendo.—Mwanzo, sura ya 12 hadi 25.

Ilisemekana kwamba ‘BWANA alisema na Musa uso kwa uso, kama vile mtu asemavyo na rafiki yake.’ (Kutoka 33:11) Naam, Musa alikuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova kuliko nabii mwingine yeyote aliyewahi kuishi kabla ya Yesu Kristo. Yehova alimwonyeshaje Musa uaminifu-mshikamanifu?

Alipokuwa na umri wa miaka 40, Musa, mwanamume mwenye nguvu na uwezo, alichukua kwa kimbelembele jukumu la kuwakomboa watu wake. Lakini wakati wa kufanya hivyo haukuwa umewadia. Alilazimika kutoroka ili asalimishe uhai wake. Alichunga kondoo huko Midiani kwa miaka 40. (Matendo 7:23-30) Hata hivyo, Yehova hakumwacha. Wakati ulipowadia, Musa alirudishwa Misri ili awaongoze Waisraeli watoke huko.

Vivyo hivyo, Yehova alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Daudi, mfalme wa pili maarufu wa Israeli. Daudi alipokuwa kijana tu, Yehova alimwambia hivi nabii Samweli: “Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye.” Tangu wakati huo, Yehova alimlinda na kumwongoza Daudi hadi akakomaa na baadaye akawa mfalme wa Israeli yote. Yehova alimwokoa “na makucha ya simba, na makucha ya dubu” na kumwokoa mikononi mwa Goliathi, jitu la Wafilisti. Alimsaidia Daudi kushinda vita vingi dhidi ya maadui wa Israeli na kumwokoa na mkuki wa Sauli mwenye wivu na chuki.—1 Samweli 16:12; 17:37; 18:11; 19:10.

Bila shaka, Daudi hakuwa mkamilifu. Hata alifanya dhambi nzito. Lakini Yehova hakumwacha Daudi bali alimwonyesha upendo mwaminifu-mshikamanifu alipotubu kikweli. Katika maisha yote ya Daudi, mara nyingi Yehova alichukua hatua ya kudumisha na kuendeleza uhai wake. Alichukua hatua kwa niaba ya mtu aliyekuwa anateseka. Hizo zilikuwa fadhili-upendo zilizoje!—2 Samweli 11:1–12:25; 24:1-17.

Taifa la Israeli kwa jumla liliingia katika uhusiano wa pekee na ulio wakfu pamoja na Yehova walipokubali masharti ya agano la Sheria ya Kimusa kwenye Mlima Sinai. (Kutoka 19:3-8) Hivyo, Israeli linaonyeshwa kuwa na uhusiano wa ndoa pamoja na Yehova. Taifa la Israeli liliambiwa: “BWANA amekuita kama mke.” Naye Yehova akamwambia: “Kwa fadhili za milele nitakurehemu.” (Isaya 54:6, 8) Yehova alionyeshaje uaminifu-mshikamanifu katika uhusiano huu wa pekee?

Yehova alichukua hatua ya kwanza kutimiza mahitaji ya Waisraeli na kuimarisha uhusiano wake pamoja nao. Aliwakomboa kutoka Misri, akawapanga kuwa taifa, na kuwaingiza katika “nchi ijaayo maziwa na asali.” (Kutoka 3:8) Alitoa mafundisho ya kiroho kwa ukawaida kupitia makuhani, Walawi, wajumbe, na manabii aliowatuma kwa kufuatana. (2 Mambo ya Nyakati 17:7-9; Nehemia 8:7-9; Yeremia 7:25) Taifa hilo lilipoanza kuabudu miungu mingine, Yehova aliwasahihisha na kuwasamehe walipotubu. Ni kweli kwamba Waisraeli walikuwa “mke” aliye mgumu kushughulika naye. Lakini Yehova hakutaka kumwacha kwa haraka. Kwa sababu ya ahadi zake kwa Abrahamu, Yeye alishikamana na Waisraeli kwa uaminifu-mshikamanifu hadi kusudi lake kuhusiana nao lilipotimizwa. (Kumbukumbu la Torati 7:7-9) Hicho ni kielelezo bora kama nini kwa wenzi wa ndoa leo!

Yehova pia huonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa wanadamu kwa jumla kwa kuwaandalia mahitaji muhimu ya maisha, wawe waadilifu au wasio waadilifu. (Mathayo 5:45; Matendo 17:25) Isitoshe, ameandaa dhabihu ya fidia ya Mwana wake ili watu wote waweze kukombolewa kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo na kufurahia matazamio matukufu ya kupata uhai udumuo milele ulio mkamilifu katika Paradiso. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Zawadi ya fidia ndilo tendo kuu zaidi la kudumisha na kuendeleza uhai. Kwa kweli, kufanya hivyo kulikuwa “kuchukua hatua kwa niaba ya mtu ambaye amepatwa na jambo baya au msiba.”

Dhihirisha Uaminifu-Mshikamanifu Wako kwa Matendo Yafaayo

Neno uaminifu-mshikamanifu, lililo na maana sawa na fadhili-upendo, hudokeza hasa wazo la kutendeana jambo. Unapoonyeshwa fadhili-upendo, basi unatazamiwa ufanye vivyo hivyo. Mtu anayeonyesha wengine uaminifu-mshikamanifu huonyeshwa uaminifu-mshikamanifu pia. Maneno haya ya Daudi yanadhihirisha kwamba alifahamu maana ya neno cheʹsedh: “Nitasujudu nikilikabili hekalu lako takatifu, nitalishukuru jina lako.” Kwa nini? “Kwa ajili ya fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zako na uaminifu wako.” (Zaburi 138:2) Yehova alimwonyesha Daudi fadhili-upendo, jambo ambalo bila shaka lilimchochea amwabudu na kumsifu. Hivyo, tunapotafakari fadhili-upendo ambazo Yehova ametuonyesha, je, tunachochewa kutenda vivyo hivyo? Kwa mfano, jina la Yehova likishutumiwa, je, hangaiko lako kwa ajili ya sifa yake linakuchochea umtetee?

Mkristo mmoja aliyebatizwa hivi karibuni na mkewe walichochewa kufanya hivyo walipohudhuria mazishi ya mtu wa jamaa yao aliyekufa katika aksidenti ya pikipiki. Mazishi hayo hayakuwa ya kidini, nao waliohudhuria waliruhusiwa kusema jambo fulani kuhusu mtu aliyekufa. Msemaji mmoja alianza kumlaumu Mungu kwa kifo cha mapema cha mwanamume huyo kijana akisema, ‘Mungu alimtaka mbinguni, kwa hiyo alimchukua.’ Ndugu yetu Mkristo hakuweza kunyamaza. Alipanda kwenye jukwaa japo hakuwa na Biblia wala maandishi yoyote. Kisha akauliza, “Je, mnafikiri Mungu mweza yote, mwenye rehema, na huruma anapendezwa na hali kama hizi?” Ndipo akatoa hotuba ya papo hapo ya dakika kumi huku akitumia Maandiko kueleza ni kwa nini tunakufa, Mungu amefanya nini kuwaokoa wanadamu kutoka kwa kifo, na kueleza matazamio mazuri ya kufufuliwa kupata uhai udumuo milele katika dunia paradiso. Watu zaidi ya 100 waliokuwepo walipiga makofi kwa muda mrefu. Ndugu huyo alisema hivi baadaye: “Nilikuwa na furaha moyoni ambayo sijawahi kuwa nayo. Nilimshukuru Yehova kwa kunifundisha hekima yake na kunipa fursa hiyo ya kulitetea jina lake takatifu.”

Uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova hutia ndani kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Neno lake Biblia. Kwa nini? Kwa sababu Yehova hutumia Biblia kutufundisha jinsi ya kuishi. Sheria na kanuni za Biblia ni bora na hutunufaisha sana maishani. (Isaya 48:17) Usiache mikazo kutoka kwa wengine au udhaifu wako mwenyewe ukukengeushe uache kufuata sheria za Yehova. Uwe mwaminifu-mshikamanifu kwa Neno la Mungu.

Uaminifu-mshikamanifu kwa Mungu hutia ndani pia kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo lake. Katika miaka iliyopita kumekuwa na uhitaji wa kusahihisha na kurekebisha ufahamu wetu wa maandiko fulani. Ukweli ni kwamba hakuna watu wengine wanaolishwa vizuri kiroho kama sisi. (Mathayo 24:45-47) Hapana shaka kwamba Yehova analiunga mkono kwa uaminifu-mshikamanifu tengenezo lake la kisasa. Je, tunaweza kufanya vivyo hivyo? A. H. Macmillan alifanya hivyo. Alisema hivi muda mfupi kabla ya kifo chake: “Tangu nijiweke wakfu kwa Mungu mnamo Septemba 1900 nikiwa na umri wa miaka ishirini na mitatu, nimeliona tengenezo la Yehova likikua kutoka mwanzo mdogo, na kuwa jamii ya ulimwenguni pote ya watu wenye furaha wanaotangaza kweli zake kwa bidii. . . . Nikaribiapo mwisho wa utumishi wangu kwa Mungu duniani, nina hakika sasa kuliko wakati mwingine wowote kwamba Yehova amewaongoza watu wake na kuwapa kile tu wanachohitaji kwa wakati ufaao.” Ndugu Macmillan alitumikia kwa uaminifu-mshikamanifu kwa miaka 66 hivi, hadi alipokufa Agosti 26, 1966. Aliweka kielelezo kizuri cha kudhihirisha uaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo la Mungu lionekanalo.

Mbali na kuwa waaminifu-washikamanifu kwa tengenezo, je, tutakuwa waaminifu-washikamanifu kwa mmoja na mwenzake? Tunapokabili tisho la kunyanyaswa vikali, je, tunakuwa waaminifu-washikamanifu kwa ndugu na dada zetu? Wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, ndugu zetu huko Uholanzi waliweka kielelezo kizuri cha uaminifu-mshikamanifu. Klaas de Vries, mzee mmoja wa Kutaniko la Groningen, alihojiwa kwa njia ya ukatili na askari wa Nazi, akazuiliwa akiwa peke yake kwa siku 12 na kupewa mkate na maji tu, kisha akahojiwa tena. Huku wakimwelekezea bastola na kutisha kumwua, walimpa muda wa dakika mbili awaambie mahali walipokuwa ndugu wenye madaraka na pia awape habari nyingine muhimu. Klaas alisema hivi tu: “Sisemi zaidi. . . . Sitakuwa msaliti.” Walimtisha mara tatu kwa bastola. Hatimaye askari hao walichoka na kumpeleka Klaas katika gereza lingine. Hakuwasaliti kamwe ndugu zake.

Je, tutakuwa waaminifu-washikamanifu kwa wenzi wetu wa ndoa, ambao ndio watu wa jamaa wa karibu zaidi? Kama vile Yehova alivyokuwa mwaminifu katika uhusiano wake wa agano na taifa la Israeli, je, sisi tu waaminifu-washikamanifu kwa nadhiri zetu za ndoa? Tunapaswa kujitahidi kuwa na uhusiano thabiti na mwenzi wetu wa ndoa. Jitahidi kuimarisha ndoa yako. Tumieni wakati pamoja, zungumzeni kwa uhuru na waziwazi, tegemezaneni na kutiana moyo, msikilize mwenzako anapozungumza, chekeni pamoja, lieni pamoja, chezeni pamoja, jitahidini pamoja kufikia miradi yenu, pendezaneni, iweni marafiki. Iweni waangalifu sana msisitawishe hisia za kimapenzi kuelekea watu wengine. Ingawa hakuna ubaya wowote kusitawisha urafiki wa karibu na watu wengine, hisia za kimapenzi zapaswa kuonyeshwa mwenzi wako wa ndoa pekee. Usiruhusu yeyote awatenganishe.—Mithali 5:15-20.

Uwe mwaminifu-mshikamanifu kwa Mashahidi wenzako na familia yako. Usiwasahau kadiri miaka ipitavyo. Endelea kuwasiliana nao kwa kuwaandikia barua, kuwapigia simu, na kuwatembelea. Hata hali yako iweje, usiwavunje moyo. Acha wafurahie kusema kwamba wanakujua au ni watu wa jamaa yako. Uaminifu-mshikamanifu kwao utakufanya uazimie kufanya yaliyo mema na utatiwa moyo.—Esta 4:6-16.

Naam, uaminifu-mshikamanifu wa kweli hutia ndani kutenda ifaavyo ili kudumisha mahusiano yenye thamani. Fanya yote uwezayo ili kuonyesha uthamini kwa fadhili-upendo za Yehova. Iga uaminifu-mshikamanifu wa Yehova unaposhughulika na kutaniko la Kikristo, mwenzi wako wa ndoa, familia, na marafiki. Tangaza kwa uaminifu-mshikamanifu sifa za Yehova kwa majirani wako. Maneno haya ya mtunga-zaburi ni ya kweli: “Fadhili [“fadhili-upendo,” NW] za BWANA nitaziimba milele; kwa kinywa changu nitavijulisha vizazi vyote uaminifu wako.” (Zaburi 89:1) Je, hatuvutiwi na Mungu kama huyo? Bila shaka, “rehema [“fadhili-upendo,” NW] zake ni za milele.”—Zaburi 100:5.

[Picha katika ukurasa wa 23]

A. H. Macmillan