Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Bado Inawezekana Kuwa na Imani ya Kweli?

Je, Bado Inawezekana Kuwa na Imani ya Kweli?

Je, Bado Inawezekana Kuwa na Imani ya Kweli?

‘Imani ni kuwa na uhakika thabiti katika wema wa Mungu, ni uhakika ulio kamili hivi kwamba mwamini anaweza kuhatarisha uhai wake mara elfu.’—MARTIN LUTHER, 1522.

“Makusudio yetu yote tayari yanaonyesha kwamba sisi ni jamii isiyojali mambo ya kidini na isiyo na desturi na imani ya Kikristo.”—LUDOVIC KENNEDY, 1999.

MAONI kuhusu imani yanaweza kutofautiana sana. Hapo zamani, lilikuwa jambo la kawaida kuwa na imani katika Mungu. Siku hizi, katika ulimwengu wenye kutilia shaka na wenye mateso, imani ya kweli katika Mungu na katika Biblia inafifia upesi sana.

Imani ya Kweli

Kwa watu wengi neno “imani” linamaanisha kuamini jambo fulani la kidini au kufuata ibada ya namna fulani. Hata hivyo, katika Biblia neno “imani” kwa msingi lamaanisha tumaini kamili—kuwa na uhakika kamili katika Mungu na ahadi zake. Ni sifa inayomtambulisha mwanafunzi wa Yesu Kristo.

Pindi moja, Yesu Kristo alisema kuhusu uhitaji wa kusali na ‘kutokata tamaa.’ Kwa kusema hivyo, alizusha swali la kama kungekuweko imani ya kweli wakati wetu. Aliuliza hivi: “Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli ataipata hiyo imani duniani?” Kwa nini alizusha swali hilo?—Luka 18:1, 8.

Imani Iliyopotea

Watu wanaweza kupoteza imani waliyo nayo kwa sababu nyingi. Miongoni mwa sababu hizo ni mateso na majaribu ya kila siku. Kwa mfano, Profesa Michael Goulder, alikuwa kasisi wa parokia moja huko Manchester, Uingereza, wakati kulipotokea aksidenti ya ndege huko Munich mwaka wa 1958 ambapo wachezaji wengi wa timu ya soka ya Manchester United walikufa. Katika kipindi cha televisheni ya BBC, mtangazaji Joan Bakewell alieleza kwamba Goulder “alihisi akiwa hoi alipoona jinsi wanadamu wanavyoteseka.” Kwa sababu hiyo “alipoteza imani yake katika Mungu ambaye huingilia kati mambo yanayompata mwanadamu.” Goulder alisema kuwa anaamini kwamba “Biblia si . . . neno la Mungu lisilo na kosa” bali “ni neno la binadamu linaloweza kukosea, na labda ni sehemu fulani tu za Neno hilo ambazo zimepuliziwa na Mungu.”

Nyakati fulani imani hufifia tu. Ndivyo ilivyotukia kwa mwandishi na mtangazaji Ludovic Kennedy. Anasema kwamba tangu utotoni alipatwa na shaka [kuhusu Mungu] mara kwa mara, akazidi kupoteza imani. Yaonekana hakuna mtu ambaye angeweza kujibu maswali yake kwa njia yenye kuridhisha. Imani yake ambayo tayari ilikuwa imedhoofika ilipata pigo kubwa sana babake alipokufa baharini. Sala kwa Mungu “atuhifadhi tusipatwe na hatari za baharini na jeuri ya adui” hazikujibiwa wakati meli ya kijeshi iliyogeuzwa kuwa ya abiria, ambamo baba yake alikuwa akisafiria, iliposhambuliwa na kuharibiwa na meli za kivita za Ujerumani wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu.—All in the MindA Farewell to God.

Kupoteza imani ni jambo la kawaida. Mtume Paulo asema kwamba “imani si miliki ya watu wote.” (2 Wathesalonike 3:2) Unaonaje? Je, bado inawezekana kuwa na imani ya kweli katika Mungu na Neno lake kwenye ulimwengu huu unaozidi kuwa na shaka? Soma habari hiyo katika makala ifuatayo.