Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasiliana na Wasioweza Kufikiwa kwa Urahisi

Kuwasiliana na Wasioweza Kufikiwa kwa Urahisi

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

Kuwasiliana na Wasioweza Kufikiwa kwa Urahisi

MASHAHIDI WA YEHOVA hujitahidi wawezavyo kuwapelekea watu wote ujumbe wa Ufalme. Mara nyingine, jitihada ya pekee yahitajiwa ili kuwasiliana na wale ambao ni vigumu kuwapata nyumbani. (Marko 13:10) Kuhusiana na hilo, mhudumu aliye painia wa pekee katika nchi moja ya Amerika Kusini anasimulia jambo lililoonwa lifuatalo.

“Siku moja nilipata habari kwamba gavana wa jimbo angetembelea eneo ambalo mimi na mke wangu tumegawiwa kuhubiri. Kwa kuwa ilikuwa vigumu kumpata nyumbani, nilimwandikia barua na kuweka ndani vichapo kadhaa vya Biblia vilivyotia ndani broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? na vitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu na Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Nilieleza kusudi la kila kichapo katika barua hiyo.

“Nilimwomba tukutane kwa kuwa nilitaka kujua maoni yake kuhusu vichapo hivyo. Majuma kadhaa baadaye alikubali tukutane, nami nikabeba video Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name. Tulizungumza kwa muda wa saa mbili hivi. Baada ya kutazama video hiyo pamoja, nilimwuliza maoni yake kuihusu. Alijibu: ‘Hakuna tengenezo jingine duniani kama lenu. Ningetamani kuwa na watu kama nyinyi wa kunisaidia kukamilisha miradi niliyopewa na serikali!’ Kisha akaniuliza kama nimewahi kutembelea makao makuu ya tengenezo letu. Nilimwambia kwamba japo huo ulikuwa mradi wangu tangu nilipokuwa na umri wa miaka 14, sijawahi kutembelea makao yetu makuu yaliyo Brooklyn, New York. Hiyo ni baadhi ya miradi ambayo haikuwa rahisi kuifikia. Alinitazama kwa makini kwa muda fulani, kisha akaniambia kwamba angetaka nitembelee makao hayo. Alitusaidia kupata hati za kisheria za kusafiria na kutulipia nauli ya ndege kama zawadi!

“Sasa gavana huyo hupokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa ukawaida. Tunatumaini kwamba karibuni tutaanza kujifunza naye Biblia.”