Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha Yenye Mambo Yasiyotazamiwa Katika Utumishi wa Yehova

Maisha Yenye Mambo Yasiyotazamiwa Katika Utumishi wa Yehova

Simulizi la Maisha

Maisha Yenye Mambo Yasiyotazamiwa Katika Utumishi wa Yehova

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ERIC NA HAZEL BEVERIDGE

“Sasa ninakuhukumu kifungo cha miezi sita gerezani.” Nikiwa bado nakumbuka maneno hayo, nilipelekwa kwenye Gereza la Strangeways huko Manchester, Uingereza. Ilikuwa Desemba 1950 na nilikuwa na umri wa miaka 19. Nilikuwa nimekabili jaribu lililo kali zaidi katika ujana wangu—nilikuwa nimekataa kujiunga na jeshi.—2 Wakorintho 10:3-5.

NIKIWA painia, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, ningeruhusiwa kutojiunga na jeshi, lakini sheria ya Uingereza haikutambua msimamo wetu kama wahudumu. Kwa hiyo nilijikuta katika seli nikiwa peke yangu. Nilimfikiria babangu. Kwa njia isiyo ya moja kwa moja, baba alifanya nifungwe gerezani.

Babangu alikuwa afisa wa gereza kutoka Yorkshire, aliyefuata kanuni na imani thabiti. Alichukia sana Ukatoliki kwa sababu ya mambo aliyoona akiwa jeshini na akiwa afisa wa magereza. Alionana na Mashahidi kwa mara ya kwanza mapema mwaka wa 1930 alipoenda kwenye mlango kuwafukuza—kisha akarudi na baadhi ya vitabu vyao! Baadaye aliandikisha gazeti Consolation (ambalo sasa ni Amkeni!). Mashahidi walikuwa wakimtembelea kila mwaka kumtia moyo aandikishe upya gazeti hilo. Nilipokuwa na umri wa miaka 15 hivi, Mashahidi walizungumza na baba kwa mara nyingine nami nikawaunga mkono. Nilianza kujifunza Biblia wakati huo.

Nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa mnamo Machi 1949. Baadaye mwaka huo nilikutana na John na Michael Charuk, waliokuwa wametoka tu kuhitimu kwenye shule ya mishonari ya Gileadi, nao walikuwa njiani kwenda Nigeria. Nilivutiwa sana na roho yao ya umishonari nao waliitia roho hiyo ndani ya moyo wangu labda bila hata wao kujua.

Nilipokuwa ninajifunza Biblia, hamu yangu ya kujiunga na chuo kikuu iliisha. Mwaka mmoja tu baada ya kuondoka nyumbani kwenda kufanya kazi kwenye ofisi ya Forodha na Ushuru huko London, niliona kwamba singeweza kutimiza wakfu wangu kwa Mungu nikiendelea na utumishi wa umma. Nilipoacha kazi hiyo, mfanyakazi mwenzangu aliyekuwa amefanya kazi ya ofisi kwa muda mrefu alinipongeza kwa kuacha kazi aliyoitaja kuwa ‘yenye kuathiri mtazamo wa mtu.’

Kabla ya kuacha kazi hiyo, nilikabili jaribu jingine—jinsi ya kumwambia babangu kwamba nilitaka kuacha kazi hiyo ya kudumu na kuwa mhudumu wa wakati wote. Jioni moja nilipokuwa likizoni nyumbani, nilimwambia Baba habari hiyo. Nilitazamia Baba anijibu kwa ukali. Lakini nilishangaa aliposema hivi: “Utavuna ukipandacho. Ukipatwa na shida usinikimbilie.” Mnamo Januari 1, 1950, niliandika maneno haya kwenye kitabu changu cha kumbukumbu za kila siku: “Nilimwambia Baba kuhusu kazi ya upainia. Nilishangazwa sana na jinsi alivyokuwa mwenye kiasi na mwenye kusaidia. Fadhili zake zilinifanya nilie.” Niliacha utumishi wa umma na kukubali mgawo wa kuwa painia wa wakati wote.

Napewa Mgawo Pamoja na Nyumba Ndogo

Kisha nikapata jaribu jingine kuhusiana na ujitoaji wangu kwa Mungu. Nilipewa mgawo wa kuwa painia na nilitarajiwa kukaa katika nyumba moja ndogo, huko Lancashire, pamoja na Lloyd Griffiths, Mkristo mwenzangu kutoka Wales. Nikiwa na matazamio makubwa kuhusu nyumba hiyo, niliwasili katika mji wenye mvua nyingi na usiovutia wa Bacup. Muda si muda, matazamio yangu yalivunjika nilipotambua kwamba nyumba hiyo ilikuwa tu chumba kilichokuwa chini ya ardhi! Kulikuwa na panya na mende waliotembea-tembea chumbani humo usiku. Nilikuwa karibu kurudi nyumbani. Lakini nikasali kupata nguvu za kukabiliana na jaribu hilo. Nilipata utulivu papo hapo, nikaanza kuona mambo kwa njia ifaayo. Nilipewa mgawo huu na tengenezo la Yehova, hivyo nilimtumaini Yehova anisaidie. Ninashukuru kama nini kwamba nilivumilia hali hiyo, kwa kuwa kama ningerudi nyumbani maisha yangu yangekuwa tofauti kabisa!—Isaya 26:3, 4.

Kabla ya kutupwa gerezani kwa kukataa kujiunga na jeshi, nilihubiri kwa miezi tisa katika Bonde la Rossendale, eneo ambalo hali yake ya kiuchumi ilikuwa mbaya. Baada ya kukaa majuma mawili katika Gereza la Strangeways, nilihamishiwa Gereza la Lewes, huko pwani ya kusini ya Uingereza. Hatimaye tukawa Mashahidi watano katika gereza hilo, na tukaadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo ndani ya seli moja.

Baba alikuja kunitembelea pindi moja. Haikuwa rahisi kwake kunitembelea gerezani kwa kuwa alikuwa afisa wa magereza aliyejulikana sana! Sitasahau kamwe ziara hiyo. Hatimaye niliachiliwa mnamo Aprili 1951.

Nilipoachiliwa kutoka Gereza la Lewes, nilipanda gari-moshi kwenda Cardiff, Wales, ambako babangu alikuwa anatumika akiwa afisa mkuu wa magereza. Mimi ndiye mtoto wa kwanza kati ya watoto wanne—wavulana watatu na msichana mmoja. Ilinibidi nitafute kazi ya muda ili niweze kujiruzuku na kuendelea na upainia. Nilipata kazi kwenye duka moja la nguo, lakini kusudi langu kuu maishani lilikuwa kufanya huduma ya Kikristo. Mama yetu alituacha yapata wakati huo. Hilo lilikuwa pigo kubwa kwa Baba na kwetu pia. Tulikuwa na umri wa kati ya miaka 8 hadi 19. Kwa kusikitisha, wazazi wetu walitalikiana.

Apataye Mke Mwema. . .

Kulikuwa na mapainia kadhaa kutanikoni. Miongoni mwao kulikuwa na dada aliyesafiri kila asubuhi kutoka Bonde la Rhondda lenye mgodi wa makaa, kuja kufanya kazi na kuhubiri. Aliitwa Hazel Green—painia mzuri sana. Hazel alijua kweli miaka mingi kabla yangu kwa kuwa wazazi wake walikuwa wakihudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia (ambao sasa wanaitwa Mashahidi wa Yehova) katika miaka ya 1920. Hebu asimulie mwenyewe.

“Sikuichukua Biblia kwa uzito hadi mwaka wa 1944 niliposoma kijitabu Dini Yavuna Tufani (Religion Reaps the Whirlwind). Mamangu alinitia moyo nihudhurie kusanyiko la mzunguko huko Cardiff. Japo nilikuwa na ujuzi kidogo sana wa Biblia, nilijikuta kwenye maduka nikitangaza hotuba ya watu wote kwa bango lililokuwa shingoni mwangu. Nilivumilia licha ya kunyanyaswa na makasisi na watu wengine. Nilibatizwa mwaka wa 1946 na kuanza kupainia mnamo Desemba mwaka huo. Kisha mwaka wa 1951, Eric, painia mchanga aliyekuwa ameachiliwa karibuni kutoka gerezani, akaja Cardiff.

“Tulikuwa tukihubiri pamoja na tulipatana. Tulikuwa na miradi ileile maishani—kuendeleza masilahi ya Ufalme wa Mungu. Kwa hiyo tukaoana Desemba 1952. Ingawa sote tulitumikia wakati wote tukiwa mapainia na hatukuwa na mapato makubwa, hatukukosa kamwe mahitaji ya msingi. Mara kwa mara tulipokea zawadi kutoka kwa Shahidi ambaye alinunua jamu au sabuni nyingi kupita kiasi. Tulikuwa tukipokea zawadi hizo wakati tu tulipozihitaji! Tulishukuru sana kwa zawadi hizo. Lakini, bado tungepatwa na mambo yasiyotazamiwa.”

Jambo Lisilotazamiwa Lililobadili Maisha Yetu

Mnamo Novemba 1954, mimi na Hazel tulipokea kitu ambacho hatukutazamia—fomu kutoka ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko London iliyonitaka nitembelee kutaniko tofauti kila juma nikiwa mwangalizi asafiriye. Hatukuwa na shaka kwamba tuliletewa fomu hiyo kimakosa, kwa hiyo hatukuambia yeyote kutanikoni. Hata hivyo, nilijaza fomu hiyo, nikairudisha, na kungojea majibu kwa hamu kubwa. Siku kadhaa baadaye nilipata majibu: “Njoo London uzoezwe”!

Kwenye ofisi ya tawi ya London, singeweza kuamini kwamba mimi, nikiwa na umri wa miaka 23, nilikuwa huko na ndugu wenye sifa nzuri walioonekana kuwa wakomavu sana kiroho. Ndugu hao ni: Pryce Hughes, Emlyn Wynes, Ernie Beavor, Ernie Guiver, Bob Gough, Glynn Parr, Stan na Martin Woodburn, na wengine wengi, ambao wengi kati yao tayari wamekufa. Waliweka msingi thabiti wa bidii na uaminifu nchini Uingereza katika miaka ya 1940 na 1950.

Sikuchoshwa Kamwe na Kazi ya Kuzunguka Niliyofanya Uingereza

Tulianza kazi ya kusafiri katika miaka yenye baridi kali na theluji nyingi ya 1954/1955. Tulipelekwa Anglia Mashariki, eneo tambarare la Uingereza ambalo hupata pepo baridi kutoka Bahari ya Kaskazini. Kulikuwa na Mashahidi 31,000 tu nchini Uingereza wakati huo. Mzunguko wetu wa kwanza ulikuwa mgumu kwetu na kwa ndugu tuliotembelea. Niliwaudhi ndugu hao mara kwa mara kwa kuwa sikuwa na uzoefu na nilikuwa nikisema mambo waziwazi kulingana na asili ya watu wa Yorkshire. Kwa miaka ambayo imepita, imenibidi kujifunza kwamba kuwa na fadhili ni muhimu kuliko kuwa stadi, na kuwafikiria watu ni muhimu kuliko kufuata sana utaratibu fulani. Bado ninajitahidi kufuata kielelezo cha Yesu cha kuwaburudisha wengine, lakini sifanikiwi sikuzote.—Mathayo 11:28-30.

Baada ya kukaa Anglia Mashariki kwa miezi 18, tulipelekwa kutumika katika mzunguko fulani kaskazini-mashariki mwa Uingereza, Newcastle upon Tyne, na Northumberland. Niliwapenda watu wachangamfu wa eneo hilo lenye mandhari nzuri. Nilisaidiwa sana na Don Ward, mwangalizi wa wilaya aliyetutembelea kutoka Seattle, Washington, Marekani. Alikuwa amehitimu katika darasa la 20 la Gileadi. Nilikuwa nikitoa hotuba zangu kwa kasi sana. Alinifunza kuzungumza pole pole, kutua, na kufundisha.

Jambo Jingine Lisilotazamiwa Lililobadili Maisha Yetu

Katika mwaka wa 1958 tulipokea barua iliyobadili maisha yetu. Tulialikwa kuhudhuria Shule ya Gileadi huko South Lansing, New York, Marekani. Tuliuza gari letu na kununua tiketi za meli kwenda New York. Kwanza tulihudhuria mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova huko New York City. Kutoka huko tulienda Peterborough, Ontario, kupainia kwa miezi sita kabla ya kuhudhuria Shule ya Gileadi.

Walimu wa shule hiyo walikuwa Albert Schroeder, ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, na vilevile Maxwell Friend na Jack Redford, ambao tayari wamekufa. Tulijengwa sana kwa kushirikiana na wanafunzi 82 kutoka nchi 14. Tulianza kuelewa kidogo-kidogo tamaduni zetu mbalimbali. Kuchangamana na wanafunzi wa nchi nyingine waliojitahidi kuzungumza Kiingereza kulitusaidia kuelewa matatizo ambayo tungepata wakati wa kujifunza lugha nyingine. Darasa letu lilimaliza mafunzo baada ya miezi mitano na kupewa mgawo wa kwenda kutumika katika nchi 27. Siku chache baada ya kuhitimu, tulikuwa New York City, tukingojea meli iitwayo Queen Elizabeth, ili turudi Ulaya.

Mgawo Wetu wa Kwanza Katika Nchi ya Kigeni

Tulipewa mgawo wa kwenda nchi gani? Ureno! Tulifika Lisbon Novemba 1959. Sasa tulikabili jaribu la kujifunza lugha mpya na kuzoeleana na utamaduni mpya. Katika mwaka wa 1959 kulikuwa na Mashahidi 643 nchini Ureno, ambayo ilikuwa na watu wapatao milioni 9. Lakini kazi yetu ya kuhubiri haikuwa imesajiliwa kisheria. Ingawa tulikuwa na Majumba ya Ufalme, hatukuweka vibao nje.

Baada ya kufunzwa Kireno na mishonari aitwaye Elsa Piccone, mimi na Hazel tulitembelea makutaniko na vikundi karibu na Lisbon, Faro, Evora, na Beja. Kisha mwaka wa 1961 mambo yakaanza kubadilika. Nilikuwa nikijifunza Biblia na kijana aitwaye João Gonçalves Mateus. Kijana huyo aliamua kuchukua msimamo wa Kikristo wa kutojiunga na jeshi. Muda mfupi baadaye, nikaombwa nifike kwenye makao makuu ya polisi ili kuhojiwa. Jambo jingine lisilotazamiwa likatokea! Siku chache baadaye, tuliarifiwa kwamba tulikuwa na siku 30 tu kuondoka nchini! Mishonari wenzetu Eric na Christina Britten na Domenick na Elsa Piccone waliamriwa kuondoka pia.

Niliomba tupewe nafasi ya kujieleza, kisha tukaruhusiwa kumwona mkuu wa kikosi cha polisi wa siri. Alituambia kinaganaga sababu iliyofanya tuamriwe kuondoka, kisha akataja jina la João Gonçalves Mateus, mwanafunzi wangu wa Biblia! Alisema kwamba nchi ya Ureno ni tofauti na Uingereza na haingeweza kuruhusu watu wasijiunge na jeshi kwa sababu tu za kidini. Kwa hiyo, ilitubidi tuondoke Ureno na sikuweza kuwasiliana na João tena. Baada ya miaka 26, ilikuwa furaha iliyoje kuonana na João, mkewe, na binti zao watatu wakati wa kuwekwa wakfu kwa Betheli ya Ureno! Huduma yetu nchini Ureno haikuwa ya bure!—1 Wakorintho 3:6-9.

Hatukujua tungepewa mgawo wa kwenda nchi gani nyingine, lakini tulishangaa kupelekwa nchi jirani ya Hispania. Hivyo, mnamo Februari 1962 tulipanda gari-moshi huko Lisbon kwenda Madrid huku tukilengwalengwa na machozi.

Kuzoea Utamaduni Mwingine

Huko Hispania ilitubidi tuzoee kuhubiri na kufanya mikutano kisiri. Kwa kawaida hatukuhubiri nyumba mbili zilizokaribiana. Baada ya kuhubiri kwenye nyumba moja, tungeenda mtaa mwingine, kwenye jengo jingine. Hiyo ilifanya iwe vigumu kwa polisi—au makasisi—kutukamata. Kumbuka kwamba tulikuwa tunaishi chini ya utawala wa kiimla wa Wafashisti na Wakatoliki, na kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku. Kwa kuwa tulikuwa wageni, tulijiita majina ya Kihispania ili tusitambuliwe. Nilijiita Pablo, naye Hazel akajiita Juana.

Baada ya kukaa miezi kadhaa huko Madrid, tulipewa mgawo wa kazi ya kuzunguka katika jiji la Barcelona. Tulitembelea makutaniko mbalimbali jijini humo, mara nyingi tukikaa majuma mawili au matatu kwenye kila kutaniko. Ziara hizo zilichukua muda mrefu hivyo kwa sababu ilitupasa kutembelea kila kikundi cha funzo la kitabu kama vile tungetembelea kutaniko, na kwa kawaida hiyo ilimaanisha kutembelea vikundi viwili kila juma.

Magumu Tusiyotarajia

Katika mwaka wa 1963 tulialikwa kuanza kazi ya mwangalizi wa wilaya huko Hispania. Ili kutumikia Mashahidi watendaji wapatao 3,000, ilitubidi kusafiri nchini mwote na kutembelea mizunguko tisa iliyokuwako wakati huo. Tulifanya makusanyiko ya kisiri tusiyoweza kusahau ndani ya msitu uliokuwa karibu na Seville, katika shamba lililokuwa karibu na Gijon, na pia kando-kando ya mito iliyo karibu na Madrid, Barcelona, na Logroño.

Nilipokuwa nikihubiri kutoka nyumba hadi nyumba nilichukua tahadhari kuchunguza mpangilio wa mitaa iliyokuwa karibu ili kujua njia ya kutorokea mambo yakienda mrama. Pindi moja mimi na Shahidi mwingine tulikuwa tunahubiri huko Madrid na tulikuwa kwenye orofa ya juu wakati tuliposikia kwa ghafula makelele kutoka chini. Tuliposhuka chini, tulikuta kikundi cha wasichana matineja, washiriki wa kikundi cha Kikatoliki kiitwacho Hijas de María (Binti za Maria). Walikuwa wanawaonya majirani kutuhusu. Hatungeweza kusababu nao, na nilijua kwamba ingetubidi tuondoke mara moja la sivyo tungekamatwa na polisi. Hivyo tulitoroka, tena kwa haraka sana!

Ilisisimua sana kukaa nchini Hispania miaka hiyo. Tulijitahidi kuwatia moyo ndugu na dada, na wahudumu mapainia wa pekee. Walikabiliwa na tisho la kufungwa gerezani na mara nyingi wakavumilia ufukara ili kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, kuanzisha makutaniko na kuyaimarisha.

Wakati huohuo tulipata pia habari mbaya. Hazel aeleza: “Katika mwaka wa 1964 mamangu, ambaye alikuwa Shahidi mwaminifu alikufa. Lilikuwa pigo kubwa kumpoteza bila hata kumuaga. Jambo hilo huwapata wamishonari wengi.”

Uhuru wa Ibada Hatimaye

Hatimaye, kazi yetu ilihalalishwa na serikali ya Franco mnamo Julai 1970 baada ya miaka mingi ya mnyanyaso. Mimi na Hazel tulisisimka sana kwenye ufunguzi wa Majumba ya Ufalme, la kwanza huko Madrid na la pili huko Lesseps, Barcelona. Majumba hayo yalikuwa na vibao vikubwa, ambavyo mara nyingi vilikuwa vimeangazwa. Tulitaka watu wajue kwamba kazi yetu sasa ilikuwa halali na tungeendelea kuweko Hispania! Katika mwaka wa 1972, kulikuwa na Mashahidi wapatao 17,000 nchini Hispania.

Karibu na wakati huo, nilipata habari zenye kutia moyo sana kutoka Uingereza. Babangu alitutembelea huko Hispania mwaka wa 1969. Alivutiwa sana na jinsi Mashahidi Wahispania walivyomtendea hivi kwamba alianza kujifunza Biblia aliporudi Uingereza. Kisha mwaka wa 1971 nikapata habari kwamba Baba alibatizwa! Tuliguswa moyo sana tulipotembea nyumbani na babangu, akiwa ndugu yangu Mkristo, akatoa sala kwa ajili ya chakula. Nilikuwa nimengoja siku hiyo kwa muda wa miaka 20. Ndugu yangu Bob na mkewe, Iris, walipata kuwa Mashahidi mwaka wa 1958. Sasa mwana wao, Phillip, anatumika akiwa mwangalizi wa mzunguko huko Hispania pamoja na mkewe, Jean. Tunafurahi sana kuwaona wakitumikia katika nchi hiyo nzuri.

Jambo Lisilotazamiwa Lililotokea Karibuni Zaidi

Katika Februari 1980, mwangalizi wa eneo la dunia aliye mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitembelea Hispania. Nilishangaa kwamba alitaka twende kuhubiri pamoja. Sikujua kwamba alikuwa ananichunguza! Kisha mnamo Septemba tukaalikwa kuhamia makao makuu huko Brooklyn, New York! Tulishangaa sana. Tulikubali mwaliko huo, hata ingawa tulihuzunika sana kuwaacha ndugu zetu Wahispania. Wakati huo, kulikuwa na Mashahidi 48,000!

Tulipokuwa tunaondoka, ndugu mmoja alinipa zawadi ya saa ya mfukoni. Alikuwa ameandika maandiko mawili kwenye saa hiyo—“Lucas 16:10; Lucas 17:10.” Alisema kwamba hayo yalikuwa maandiko yangu makuu. Luka 16:10 hukazia kwamba twapaswa kuwa waaminifu katika mambo madogo, na Luka 17:10 husema kwamba sisi ni “watumwa wasiofaa kitu” na hivyo hatuna sababu ya kujivuna. Sikuzote nimetambua kwamba lolote tufanyalo katika utumishi wa Yehova ni jukumu letu tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu.

Tatizo la Kiafya Lisilotazamiwa

Katika mwaka wa 1990, nilianza kupata matatizo ya moyo. Hatimaye, ikabidi niwekwe kifaa cha kupanua mshipa wa damu uliokuwa umeziba. Wakati huu mgumu kiafya, Hazel alinitegemeza kwa njia nyingi, mara nyingi akibeba mikoba na masanduku ambayo sikuwa na nguvu ya kuyabeba. Kisha mnamo Mei 2000, nikawekwa kifaa cha kurekebisha mapigo ya moyo. Kifaa hicho kimenisaidia sana!

Katika miaka 50 iliyopita mimi na Hazel tumeona kwamba mkono wa Yehova haupunguki na kwamba makusudi yake yanatimizwa kwa wakati wake, wala si kwa wakati wetu. (Isaya 59:1; Habakuki 2:3) Katika maisha yetu, tumepatwa na mambo mengi yenye kufurahisha ambayo hatukutazamia na mengine yenye kuhuzunisha pia, lakini Yehova ametutegemeza katika hayo yote. Hapa katika makao makuu ya watu wa Yehova, tunafurahi kila siku kuchangamana na washiriki wa Baraza Linaloongoza. Mara kwa mara mimi hujiuliza, ‘Sisi kweli tupo hapa?’ Hizo ni fadhili zisizostahiliwa. (2 Wakorintho 12:9) Tunatumaini kwamba Yehova ataendelea kutulinda dhidi ya mbinu za Shetani na kutukinga ili tuweze kufurahia utawala wake mwadilifu duniani.—Waefeso 6:11-18; Ufunuo 21:1-4.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Gereza la Strangeways, huko Manchester, mahali nilipoanza kifungo changu

[Picha katika ukurasa wa 27]

Tukiwa kando ya gari letu katika kazi ya kuzunguka huko Uingereza

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kusanyiko tulilofanya kisiri huko Cercedilla, Madrid, Hispania, mwaka wa 1962

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kwenye meza tunayowekelea vichapo tunapohubiri huko Brooklyn