Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni “pumziko” gani linalotajwa kwenye Waebrania 4:9-11, na mtu ‘anaingiaje ndani ya pumziko hilo’?

Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza: “Kumebaki pumziko la sabato kwa watu wa Mungu. Kwa maana mtu ambaye ameingia ndani ya pumziko la Mungu amepumzika pia mwenyewe kutokana na kazi zake mwenyewe, kama vile Mungu alivyofanya kutokana na zake mwenyewe. Kwa hiyo acheni sisi tufanye yote kabisa tuwezayo ili kuingia ndani ya pumziko hilo.”—Waebrania 4:9-11.

Paulo alipotaja kwamba Mungu amepumzika kutokana na kazi Zake, yaelekea alikuwa akirejezea maneno ya Mwanzo 2:2, ambapo twasoma: “Siku ya saba Mungu alimaliza kazi yake yote aliyoifanya; akastarehe [“akaanza kupumzika,” NW] siku ya saba, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoifanya.” Kwa nini Yehova alianza “kupumzika siku ya saba”? Si kwa sababu alikuwa amechoka kutokana na “kazi yake yote aliyoifanya.” Mstari unaofuata unadokeza sababu: ‘Mungu akaibariki siku ya saba, akaitakasa kwa sababu katika siku hiyo Mungu alipumzika, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya.’—Mwanzo 2:3; Isaya 40:26, 28.

“Siku ya saba” ilikuwa tofauti na siku sita zilizotangulia kwa kuwa Mungu aliibariki na kuitakasa, yaani, aliitenga au kuiweka wakfu kwa kusudi la pekee. Hilo lilikuwa kusudi gani? Awali Mungu alikuwa amefunua kusudi lake kuhusu wanadamu na dunia. Mungu alimwambia hivi yule mwanamume wa kwanza na mke wake: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” (Mwanzo 1:28) Ingawa Mungu alikuwa amewaandalia wanadamu na dunia mwanzo mkamilifu, ingechukua muda kwa dunia nzima kutiishwa na kufanywa kuwa paradiso iliyojaa wanadamu wakamilifu, kama Mungu alivyokusudia. Hivyo, Mungu alipumzika “siku ya saba,” au akaacha kazi ya kuumba vitu duniani ili avipe nafasi ya kusitawi kupatana na mapenzi yake. Mwishoni mwa “siku” hiyo, yote ambayo Mungu alikuwa amekusudia yangetimizwa. Pumziko hilo litakuwa na urefu gani?

Tukirejezea maneno ya Paulo kwa Waebrania, twaona alitaja kwamba “kumebaki pumziko la sabato kwa watu wa Mungu,” hivyo akawahimiza Wakristo wenzake wafanye yote wawezayo “ili kuingia ndani ya pumziko hilo.” Hilo laonyesha kwamba Paulo alipoandika maneno hayo, “siku ya saba” ya pumziko la Mungu, iliyokuwa imeanza miaka 4,000 hivi mapema, ilikuwa bado inaendelea. Siku hiyo haitaisha hadi kusudi la Mungu kwa wanadamu na dunia litimizwe kabisa mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo, ambaye ni “Bwana wa sabato.”—Mathayo 12:8; Ufunuo 20:1-6; 21:1-4.

Akiwa na matarajio hayo mazuri, Paulo alieleza jinsi mtu awezavyo kuingia katika pumziko la Mungu. Aliandika: “Mtu ambaye ameingia ndani ya pumziko la Mungu amepumzika pia mwenyewe kutokana na kazi zake mwenyewe.” Jambo hilo laonyesha kwamba ingawa mwanzo wa mwanadamu na dunia ulikuwa mkamilifu, wanadamu kwa jumla hawakuingia ndani ya pumziko la Mungu. Hiyo ni kwa sababu Adamu na Hawa hawakuzingatia kwa muda mrefu pumziko la Mungu katika “siku ya saba,” kwa kuwa walikataa mpango walioandaliwa na Mungu. Badala yake, waliasi, wakataka kuwa huru bila kumtegemea Mungu. Hata wakashirikiana na Shetani katika mbinu zake badala ya kukubali mwongozo wa Mungu wenye upendo. (Mwanzo 2:15-17) Kwa sababu hiyo walipoteza matazamio ya kuishi milele katika dunia paradiso. Tangu wakati huo, wanadamu wote wamekuwa watumwa wa dhambi na kifo.—Waroma 5:12, 14.

Uasi wa mwanadamu haukuzuia kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Siku yake ya kupumzika bado inaendelea. Hata hivyo, Yehova aliandaa mpango wenye upendo—fidia—kupitia Mwana wake, Yesu Kristo, ili wote wanaoukubali kwa msingi wa imani waweze kutazamia ukombozi na pumziko kutokana na mzigo wa dhambi na kifo. (Waroma 6:23) Ndiyo sababu Paulo aliwasihi Wakristo wenzake ‘wapumzike kutokana na kazi zao wenyewe.’ Walihitaji kukubali maandalizi ya Mungu kwa ajili ya wokovu na kutojaribu kujipangia maisha yao ya wakati ujao kama Adamu na Hawa walivyofanya. Pia walihitaji kuepuka kujitetea.

Inaburudisha kwelikweli kufanya mapenzi ya Mungu badala ya kufuatilia mambo ya ubinafsi au ya ulimwengu. Yesu alitoa mwaliko huu: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28-30.

Bila shaka, mazungumzo ya Paulo kuhusu pumziko la Mungu na jinsi mtu awezavyo kuingia katika pumziko hilo, yaliwatia moyo Wakristo Waebrania huko Yerusalemu, ambao walikuwa wamevumilia mnyanyaso na dhihaka nyingi kwa sababu ya imani yao. (Matendo 8:1; 12:1-5) Vivyo hivyo, maneno ya Paulo yanaweza kuwatia moyo Wakristo leo. Sisi pia tunapaswa kupumzika kutokana na kazi zetu wenyewe na kufanya yote tuwezayo kuingia ndani ya pumziko hilo. Tunafanya hivyo kwa kuwa tunatambua kwamba kutimizwa kwa ahadi ya Mungu ya kuleta dunia paradiso chini ya Ufalme wake wenye uadilifu kumekaribia sana.—Mathayo 6:10, 33; 2 Petro 3:13.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Ahadi ya Mungu ya dunia paradiso itatimizwa mwishoni mwa siku yake ya pumziko