Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Yehova Unapowazoeza Watoto Wako

Mwige Yehova Unapowazoeza Watoto Wako

Mwige Yehova Unapowazoeza Watoto Wako

“Je, wazazi wote hawawasahihishi watoto wao?”—WAEBRANIA 12:7, Contemporary English Version.

1, 2. Kwa nini wazazi wana tatizo la kulea watoto wao leo?

UCHUNGUZI uliofanywa nchini Japani miaka michache iliyopita ulionyesha kwamba nusu ya watu wazima waliohojiwa huko waliona kwamba wazazi huwaendekeza sana watoto wao na hawawasiliani nao vya kutosha. Katika uchunguzi mwingine uliofanywa katika nchi hiyo, karibu robo ya watu waliohojiwa walikiri kwamba hawakujua jinsi ya kuwasiliana na watoto. Hali hiyo haipatikani tu katika nchi za Mashariki. “Wazazi wengi Wakanada walikiri kwamba hawana uhakika kuhusu jinsi ya kuwa wazazi wazuri,” likaripoti The Toronto Star. Kila mahali, wazazi wanaona ugumu wa kulea watoto wao.

2 Kwa nini wazazi wana tatizo la kulea watoto wao? Sababu kuu ni kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” na “nyakati zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Isitoshe, “mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake,” yasema Biblia. (Mwanzo 8:21) Nao vijana hasa wanakabili hatari ya kushambuliwa na Shetani, ambaye kama “simba anayenguruma” hushambulia wale wasio na uzoefu. (1 Petro 5:8) Bila shaka wazazi Wakristo hukabili magumu mengi wanapodhamiria kuwalea watoto wao “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto wao wakue na kuwa waabudu wa Yehova waliokomaa na wanaoweza kutofautisha “lililo sahihi na lililo kosa pia”?—Waebrania 5:14.

3. Kwa nini mazoezi na mwongozo kutoka kwa wazazi ni muhimu ili kufanikiwa kulea watoto?

3 Mfalme Solomoni mwenye hekima alisema, “ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto.” (Mithali 13:1; 22:15) Ili kuondoa ujinga huo katika mioyo yao, wazazi wanahitaji kuwasahihisha watoto wao kwa upendo. Hata hivyo, kwa kawaida vijana hawapendi kusahihishwa. Kwa kweli, mara nyingi wao huchukia shauri hata liwe limetolewa na nani. Kwa hiyo, wazazi wanapaswa kujifunza ‘kumlea mtoto katika njia impasayo.’ (Mithali 22:6) Watoto wanaweza kupata uhai kwa kukubali nidhamu hiyo. (Mithali 4:13) Ni muhimu kama nini wazazi wajue mambo yanayohusika katika kulea watoto wao!

Nidhamu Ni Nini?

4. Ni nini maana hasa ya neno “nidhamu” kama litumiwavyo katika Biblia?

4 Baadhi ya wazazi hushindwa kuwasahihisha watoto wao kwa sababu ya kuogopa kulaumiwa kwamba wanawadhulumu kimwili, kihisia-moyo au kwa maneno. Hatupaswi kuwa na hofu ya namna hiyo. Neno “nidhamu” kama litumiwavyo katika Biblia halidokezi dhuluma au ukatili wa namna yoyote. Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “nidhamu” lahusiana hasa na maagizo, elimu, kusahihisha na nyakati nyingine, karipio thabiti lakini lenye upendo.

5. Kwa nini inanufaisha kuchunguza jinsi Yehova ashughulikavyo na watu wake?

5 Yehova Mungu ameweka kielelezo bora kabisa katika kutoa nidhamu hiyo. Akimlinganisha Yehova na baba wa kibinadamu, mtume Paulo aliandika hivi: “Je, wazazi wote hawawasahihishi watoto wao? . . . Baba zetu wa kibinadamu hutusahihisha kwa muda mfupi, nao hufanya hivyo kwa njia wanayoona inafaa kabisa. Lakini Mungu hutusahihisha kwa ajili ya faida yetu, kwa sababu anataka tuwe watakatifu.” (Waebrania 12:7-10, Contemporary English Version) Naam, Yehova huwatia nidhamu watu wake ili wawe watakatifu, au safi. Bila shaka, tunaweza kujifunza mengi kuhusu kutia watoto nidhamu kwa kuchunguza jinsi ambavyo Yehova amewazoeza watu wake.—Kumbukumbu la Torati 32:4; Mathayo 7:11; Waefeso 5:1.

UpendoNguvu Yenye Kuchochea

6. Kwa nini huenda ikawa vigumu kwa wazazi kuiga upendo wa Yehova?

6 “Mungu ni upendo,” asema mtume Yohana. Kwa hiyo, basi, mazoezi ambayo Yehova hutoa, sikuzote huchochewa na upendo. (1 Yohana 4:8; Mithali 3:11, 12) Je, hilo lamaanisha kwamba itakuwa rahisi kwa wazazi wanaowapenda watoto wao kumwiga Yehova katika kutoa nidhamu? Sivyo. Upendo wa Mungu unaongozwa na kanuni. Msomi mmoja wa Kigiriki asema kwamba upendo huo unaoongozwa na kanuni “haupatani na upendezi wa kiasili sikuzote.” Mungu haongozwi tu na hisia. Sikuzote yeye hufikiria mambo yanayowafaa kabisa watu wake.—Isaya 30:20; 48:17.

7, 8. (a) Yehova ameweka kielelezo gani cha upendo wenye kuongozwa na kanuni katika kushughulika na watu wake? (b) Wazazi wanawezaje kumwiga Yehova katika kuwasaidia watoto wao wasitawishe uwezo wa kufuata kanuni za Biblia?

7 Fikiria upendo ambao Yehova alionyesha aliposhughulika na Waisraeli. Musa alitumia mfano wenye kugusa moyo kueleza upendo wa Yehova kwa taifa changa la Israeli. Twasoma hivi: “Mfano wa tai ataharikishaye kioto chake; na kupapatika juu ya makinda yake, alikunjua mbawa zake, akawatwaa, akawachukua juu ya mbawa zake; BWANA peke yake alimwongoza [Yakobo].” (Kumbukumbu la Torati 32:9, 11, 12) Tai hufunza kinda lake jinsi ya kupuruka kwa ‘kutaharikisha kioto chake,’ na kupigapiga mabawa yake ili kuyahimiza makinda yake yapuruke. Hatimaye kinda linaporuka kutoka kwenye kiota ambacho mara nyingi hujengwa juu ya mwamba, tai ‘hupapatika juu ya’ kinda hilo. Akiona kwamba kinda litaanguka, tai hupuruka chini yake, na kulichukua “juu ya mbawa zake.” Kwa njia hiyohiyo, Yehova alilitunza kwa upendo taifa changa la Israeli. Aliwapa watu hao Sheria ya Kimusa. (Zaburi 78:5-7) Kisha Mungu alililinda taifa lake kwa makini, na alikuwa tayari kuokoa watu wake walipopatwa na magumu.

8 Wazazi Wakristo wanawezaje kuiga upendo wa Yehova? Kwanza, wanapaswa kuwafundisha watoto wao kanuni na viwango vinavyopatikana katika Neno la Mungu. (Kumbukumbu la Torati 6:4-9) Lengo lapaswa kuwa kusaidia mtoto ajifunze kufanya maamuzi yanayopatana na kanuni za Biblia. Kwa kufanya hivyo, wazazi wenye upendo hupapatika juu ya watoto wao, kwa njia ya mfano, wakichunguza jinsi wanavyotumia kanuni walizojifunza. Watoto wao wanapozidi kukua na kupewa uhuru zaidi hatua kwa hatua, wazazi wanaojali huwa tayari ‘kupuruka chini’ na ‘kubeba watoto wao juu ya mbawa zao’ hatari inapotokea. Hatari ya aina gani?

9. Wazazi wanapaswa kuwa macho kuhusiana na hatari ipi hasa? Toa mfano.

9 Yehova Mungu aliwaonya Waisraeli juu ya matokeo ya mashirika mabaya. (Hesabu 25:1-18; Ezra 10:10-14) Leo pia ni hatari kuwa na mashirika mabaya. (1 Wakorintho 15:33) Wazazi Wakristo wanapaswa kumwiga Yehova kwa habari hii. Lisa, msichana mwenye umri wa miaka 15 alianza kupendezwa na mvulana fulani ambaye, tofauti na familia ya akina Lisa, hakuwa akifuata kanuni na maadili ya kiroho. “Mara moja wazazi wangu walitambua kwamba mtazamo wangu ulikuwa umebadilika na wakaanza kuwa na wasiwasi,” asema Lisa. “Nyakati nyingine walinisahihisha na nyakati nyingine walinitia moyo kwa upendo.” Waliketi pamoja na Lisa na kumsikiliza kwa makini, na hivyo kumsaidia kushughulika na kile walichong’amua kuwa chanzo cha tatizo lake—tamaa ya kutaka kukubaliwa na marika wake. *

Dumisha Mawasiliano Mazuri

10. Ni katika njia gani Yehova aliweka kielelezo kizuri cha kuwasiliana na Waisraeli?

10 Ili kufanikiwa kuwalea watoto, lazima wazazi wajitahidi kudumisha mawasiliano mazuri pamoja na watoto wao. Japo Yehova anajua kabisa mambo yaliyo katika mioyo yetu, yeye hututia moyo tuwasiliane naye. (2 Mambo ya Nyakati 28:9) Baada ya kuwapa Waisraeli Sheria, Yehova aliwapa Walawi mgawo wa kuwafundisha, na akatuma manabii wasababu nao na kuwasahihisha. Pia alikuwa tayari kusikiliza sala zao.—2 Mambo ya Nyakati 17:7-9; Zaburi 65:2; Isaya 1:1-3, 18-20; Yeremia 25:4; Wagalatia 3:22-24.

11. (a) Wazazi wanaweza kufanya nini ili wawe na mawasiliano mazuri na watoto wao? (b) Kwa nini ni jambo la maana wazazi wawe wasikilizaji wazuri wanapowasiliana na watoto wao?

11 Wazazi wanawezaje kumwiga Yehova wanapowasiliana na watoto wao? Jambo muhimu zaidi ni kwamba lazima wazazi watenge wakati kwa ajili ya watoto wao. Pia wazazi wanapaswa kujiepusha na maneno yenye dhihaka, kama vile, “Ni hayo tu? Nilifikiri ni jambo la maana”; “Huo ni upuuzi”; “Ungetarajia nini? Wewe ni mtoto tu.” (Mithali 12:18) Ili kuwatia moyo watoto wajieleze, wazazi wenye hekima hujitahidi kuwa wasikilizaji wazuri. Wazazi wanaopuuza watoto wao wanapokuwa wadogo, huenda wakapuuzwa na watoto hao wanapokuwa watu wazima. Sikuzote Yehova amekuwa tayari kuwasikiliza watu wake. Yeye husikiliza wale wanaomwomba kwa unyenyekevu.—Zaburi 91:15; Yeremia 29:12; Luka 11:9-13.

12. Wazazi wanaweza kusitawisha sifa zipi ili iwe rahisi kwa watoto wao kuwafikia?

12 Pia fikiria jinsi sifa fulani za Mungu zimefanya iwe rahisi kwa watu wake kumfikia kwa uhuru. Kwa mfano, Mfalme Daudi wa Israeli la kale alifanya dhambi nzito alipozini pamoja na Bath-sheba. Akiwa mwanadamu asiye mkamilifu, Daudi alitenda dhambi nyingine nzito maishani mwake. Hata hivyo, hakukosa kumfikia Yehova na kumwomba msamaha na karipio. Bila shaka, fadhili-upendo za Mungu na rehema yake ilifanya iwe rahisi kwa Daudi kumrudia Yehova. (Zaburi 103:8) Kwa kudhihirisha sifa hizo za Mungu kama vile huruma na rehema, wazazi wanaweza kudumisha mawasiliano mazuri hata wakati watoto wanapokosea.—Zaburi 103:13; Malaki 3:17.

Uwe Mwenye Kukubali Sababu

13. Kuwa mwenye kukubali sababu kwahusisha nini?

13 Wanapowasikiliza watoto wao, wazazi wanapaswa kuwa wenye kukubali sababu na kudhihirisha “hekima ya kutoka juu.” (Yakobo 3:17) “Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote,” akaandika mtume Paulo. (Wafilipi 4:5) Inamaanisha nini kuwa mwenye kukubali sababu? Ufafanuzi mmoja wa maneno ya Kigiriki yaliyotafsiriwa “-enye kukubali sababu” ni “kutofuatia sana mambo madogo-madogo ya sheria.” Wazazi wanawezaje kuwa wenye kukubali sababu huku wakidumisha kwa uthabiti viwango vya maadili na vya kiroho?

14. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu aliposhughulika na Loti?

14 Yehova ametuwekea kielelezo bora kabisa cha kuwa mwenye kukubali sababu. (Zaburi 10:17) Alipomhimiza Loti na familia yake watoke kwenye jiji lililohukumiwa maangamizi la Sodoma, Loti ‘alikawiakawia.’ Baadaye, wakati malaika wa Yehova alipomwomba akimbilie mlimani, Loti alisema: “Siwezi kukimbilia mlimani . . . Basi mji huu [Soari] u karibu, niukimbilie, nao ni mdogo, nijiponye sasa huko, sio mdogo huu?” Yehova aliitikiaje? Alisema: “Tazama nimekukubali hata kwa neno hili, kwamba sitauangamiza mji huo uliounena.” (Mwanzo 19:16-21, 30) Yehova alikuwa tayari kukubali ombi la Loti. Naam, wazazi wanahitaji kufuata viwango ambavyo Yehova Mungu ameweka katika Neno lake, Biblia. Hata hivyo, yawezekana kukubali ombi la watoto mradi halipingani na kanuni za Biblia.

15, 16. Wazazi wanaweza kujifunza somo gani kutokana na mfano unaopatikana katika andiko la Isaya 28:24, 25?

15 Kuwa mwenye kukubali sababu kwatia ndani kutayarisha mioyo ya watoto ili wawe tayari kukubali shauri. Kwa njia ya mfano, Isaya alimlinganisha Yehova na mkulima aliposema: “Je! mwenye kulima alima daima, ili apande? afunua daima madongoa ya nchi yake, na kuyavunja? Akiisha kuulainisha uso wa nchi yake, je! hamwagi huko na huko kunde, na kutupatupa jira, na kuitia ngano safu safu, na shayiri mahali pake palipochaguliwa, na kusemethi karibu na mipaka yake?”—Isaya 28:24, 25.

16 Yehova ‘hulima ili apande’ naye ‘hufunua madongoa ya nchi yake na kuyavunja.’ Kwa hiyo, yeye hutayarisha mioyo ya watu wake kabla ya kuwatia nidhamu. Wanapowasahihisha watoto wao, wazazi wanawezaje ‘kulima’ moyo wa mtoto wao? Baba mmoja alimwiga Yehova alipomsahihisha mvulana wake mwenye umri wa miaka minne. Mwana huyo alipompiga mvulana jirani, kwanza baba yake alisikiliza kwa makini udhuru wake. Kisha, kana kwamba ‘analima’ moyo wa mwanawe, baba alisimulia kisa cha mvulana mdogo aliyeteswa sana na mchokozi fulani. Baada ya kusikiliza kisa hicho, mvulana huyo alichochewa kusema kwamba lazima mchokozi huyo aadhibiwe. ‘Ulimaji’ huo ulitayarisha moyo wa mvulana huyo na kumfanya aone kwa urahisi kwamba kumpiga mvulana wa jirani ni uchokozi na ni kosa.—2 Samweli 12:1-14.

17. Andiko la Isaya 28:26-28 linatoa somo gani kwa wazazi kuhusu jinsi ya kusahihisha watoto?

17 Isaya aliendelea kulinganisha kusahihishwa na Yehova na hatua nyingine ya ukulima—upuraji. Mkulima hutumia vifaa mbalimbali vya upuraji kulingana na ugumu wa makapi ya nafaka. Fimbo hutumiwa kupura kunde na ufito kupura jira, lakini gurudumu la gari hutumiwa kwa nafaka zenye makapi magumu zaidi. Hata hivyo, mkulima hataziponda-ponda nafaka hizo ngumu. Vivyo hivyo, Yehova anapotaka kuondoa sifa fulani isiyofaa kutoka kwa watu wake, yeye hubadilikana kulingana na uhitaji na hali. Yeye hatumii kamwe uwezo wake kudhulumu au kuwa mkali na mwonezi. (Isaya 28:26-29) Watoto wengine hujirekebisha wanapotazamwa tu na wazazi wao, na hawahitaji kuchukuliwa hatua yoyote. Wengine huhitaji kukumbushwa mara kwa mara, ilhali huenda wengine wakahitaji kuhimizwa kwa bidii zaidi. Wazazi wenye kukubali sababu hutoa sahihisho kulingana na mahitaji ya kila mtoto.

Fanya Mazungumzo ya Familia Yapendeze

18. Wazazi wanawezaje kutenga wakati kwa ajili ya funzo la Biblia la familia la kawaida?

18 Miongoni mwa njia bora zaidi za kufundisha watoto wako ni kuwa na funzo la Biblia la familia kwa ukawaida na kuzungumzia Andiko kila siku. Funzo la familia huwa na matokeo sana linapofanywa kwa ukawaida. Yaelekea halitakuwa la kawaida lisipopangiwa wakati hususa wa kufanywa. Kwa hiyo lazima wazazi ‘wanunue wakati’ kwa ajili ya funzo. (Waefeso 5:15-17) Laweza kuwa jambo gumu kuchagua wakati hususa utakaowafaa wote. Baba mmoja aliona kwamba kadiri watoto walivyokua, ratiba zao zilitofautiana na ikawa vigumu kukusanya familia yote pamoja. Hata hivyo, washiriki wote wa familia hiyo walikuwepo sikuzote za mikutano ya jioni. Kwa hiyo baba huyo alipanga kufanya funzo la familia katika mojawapo ya jioni hizo. Mpango huo ukawa na matokeo. Sasa watoto wote watatu ni watumishi wa Yehova waliobatizwa.

19. Wazazi wanawezaje kumwiga Yehova wanapoongoza funzo la familia?

19 Hata hivyo, haitoshi kusoma habari fulani za Kimaandiko kijuujuu tu wakati wa funzo. Waisraeli waliorudishwa walifundishwa na Yehova kupitia makuhani ambao ‘walieleza maana ya’ Sheria “hata wakayafahamu yaliyosomwa.” (Nehemia 8:8) Kabla ya funzo la familia baba mmoja aliyefanikiwa kusaidia watoto wake wote saba wampende Yehova, alikuwa akienda chumbani mwake na kutayarisha kimbele habari ambayo itafaa mahitaji ya kila mtoto. Alifanya funzo lipendeze watoto wake. “Tulifurahia funzo sikuzote,” asema mmoja wa wanawe ambaye sasa ni mtu mzima. “Iwapo tungeitwa tulipokuwa tukicheza mpira uwanjani ili tukafanye funzo la familia, tungeacha kucheza mara moja na kukimbia tukajifunze. Siku ya funzo ilikuwa mojawapo ya jioni zenye kufurahisha zaidi ya zote katika juma.”

20. Ni tatizo gani linaloweza kutokea wakati wa kulea watoto ambalo lapaswa kuzungumziwa?

20 Mtunga-zaburi alisema: “Tazama, wana ndio urithi wa BWANA, uzao wa tumbo ni thawabu.” (Zaburi 127:3) Tunahitaji wakati na jitihada ili kuwazoeza watoto wetu, lakini kufanya hivyo kwa njia inayofaa kwaweza kumaanisha uhai udumuo milele kwa watoto wetu. Hiyo yaweza kuwa thawabu iliyoje! Basi, na tumwige Yehova tunapowazoeza watoto wetu. Hata hivyo, ingawa wazazi wamepewa jukumu la “kuwalea [watoto] katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova,” hakuna uhakikisho kwamba watafanikiwa. (Waefeso 6:4) Hata mtoto atunzwe vizuri namna gani, anaweza kuasi na kuacha kumtumikia Yehova. Basi iweje? Habari hiyo itazungumziwa katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Mambo yaliyoonwa katika makala hii na makala inayofuata huenda yakatoka katika nchi zilizo na utamaduni tofauti na nchi yako. Jaribu kuelewa kanuni zinazohusika, na kuzitumia kupatana na utamaduni wenu.

Ungejibuje?

• Wazazi wanawezaje kuiga upendo wa Yehova unaoelezwa katika andiko la Kumbukumbu la Torati 32:11, 12?

• Umejifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyowasiliana na Waisraeli?

• Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyosikiliza ombi la Loti?

• Umejifunza somo gani kuhusu kusahihisha watoto kutokana na andiko la Isaya 28:24-29?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Musa alilinganisha jinsi ambavyo Yehova huwazoeza watu wake na namna tai hushughulika na makinda yake

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wazazi wanahitaji kutenga wakati kwa ajili ya watoto wao

[Picha katika ukurasa wa 12]

“Ilikuwa mojawapo ya jioni zenye kufurahisha zaidi ya zote katika juma”