Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kumsaidiaje Mtoto “Mpotevu”?

Unaweza Kumsaidiaje Mtoto “Mpotevu”?

Unaweza Kumsaidiaje Mtoto “Mpotevu”?

‘Shangilia kwa sababu alikuwa amepotea naye akapatikana.’—LUKA 15:32.

1, 2. (a) Watoto wengine wamechukuaje kweli ya Kikristo? (b) Huenda wazazi na watoto walio katika hali hiyo wakahisije?

“NINAACHA kweli!” Wazazi wanaomwogopa Mungu na ambao wamejitahidi sana kulea watoto wao katika njia ya Kikristo hushtuka kama nini wanaposikia maneno hayo kutoka kwa mtoto! Vijana wengine ‘hupeperuka tu mbali’ bila kusema wanalokusudia. (Waebrania 2:1) Wengi wao ni kama yule mwana mpotevu anayetajwa katika mfano wa Yesu, aliyeondoka nyumbani mwa baba yake na kufuja urithi wake katika nchi ya mbali.—Luka 15:11-16.

2 Ijapokuwa Mashahidi wengi wa Yehova hawana tatizo hilo la watoto wao kuacha kweli, wale walio nalo huhuzunika sana. Pia twapaswa kutambua kwamba huenda kijana mpotevu akapatwa na huzuni. Huenda akasumbuliwa na dhamiri. Katika mfano wa Yesu, mwana mpotevu hatimaye ‘alirudiwa na fahamu zake,’ jambo lililomfurahisha baba yake. Wazazi na wengine kutanikoni wanaweza kusaidiaje wale walioacha kweli ‘warudiwe na fahamu zao’?—Luka 15:17.

Sababu Zinazofanya Wengine Waache Kweli

3. Ni baadhi ya sababu zipi zinazofanya watoto waache kutaniko la Kikristo?

3 Kuna watoto wengi sana wanaofurahia kumtumikia Yehova katika kutaniko la Kikristo. Kwa nini basi watoto wengine huacha kweli? Huenda wakahisi kwamba wanakosa kitu fulani kinachopatikana katika ulimwengu. (2 Timotheo 4:10) Au huenda wakaona kwamba kuna vizuizi vingi katika zizi la kondoo la Yehova lenye ulinzi. Dhamiri mbaya, kuvutiwa sana na mtu wa jinsia tofauti, au tamaa ya kukubaliwa na marika yaweza pia kufanya mtoto apeperuke mbali kutoka kwenye kundi la Yehova. Huenda kijana akaacha kumtumikia Mungu kwa sababu ya mambo fulani anayoona kuwa ya kinafiki yanayofanywa na wazazi au baadhi ya Wakristo.

4. Mara nyingi ni nini hasa hufanya watoto wapotoke?

4 Kwa kawaida mtazamo na tabia ya mtoto ya kuasi ni dalili ya udhaifu wa kiroho, unaodhihirisha kilicho moyoni mwake. (Mithali 15:13; Mathayo 12:34) Bila kujali sababu inayomfanya kijana apotoke, mara nyingi kiini cha tatizo lake ni kukosa kuwa na “ujuzi sahihi juu ya kweli.” (2 Timotheo 3:7) Badala ya kumwabudu Yehova kama desturi tu, ni muhimu watoto wasitawishe uhusiano wa karibu na wa kibinafsi na Mungu. Ni nini kinachoweza kuwasaidia kufanya hivyo?

Mkaribie Mungu

5. Ni lazima kijana afanye nini ili asitawishe uhusiano wa kibinafsi na Mungu?

5 Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi, “mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Ili kufanya hivyo, lazima mtoto asaidiwe kulipenda sana Neno la Mungu. (Zaburi 34:8) Hapo mwanzoni atahitaji “maziwa,” yaani mafundisho ya msingi ya Biblia. Lakini kadiri anavyopendezwa na Neno la Mungu na kuanza kufurahia “chakula kigumu” yaani, habari ya kiroho yenye kina, ndivyo atakavyokomaa haraka kiroho. (Waebrania 5:11-14; Zaburi 1:2) Kijana mmoja aliyekiri kwamba alikuwa anafuata kabisa njia za kilimwengu alianza kuthamini kanuni za kiroho. Ni nini kilichomsaidia ageuke kabisa? Alipopewa pendekezo la kusoma Biblia nzima, alidumisha ratiba ya kawaida ya kusoma Biblia. Naam, kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida ni muhimu ili kusitawisha uhusiano wa karibu na Yehova.

6, 7. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao wasitawishe tamaa ya Neno la Mungu?

6 Ni muhimu kama nini wazazi wawasaidie watoto wao kusitawisha tamaa ya Neno la Mungu! Licha ya kuwa na funzo la familia la kawaida, msichana mmoja tineja alishirikiana na wahuni. Asema hivi kuhusu funzo lao la familia: “Baba alipouliza maswali, nilisoma tu majibu, bila hata kumwangalia uso.” Badala ya kupitia kijuujuu tu habari wakati wa funzo la familia, wazazi wenye hekima hutumia ustadi wa kufundisha. (2 Timotheo 4:2) Ili kijana afurahie funzo, ni lazima ahusishwe kwenye funzo hilo. Kwa nini usiulize maswali ya maoni na kumwacha ajieleze? Mtie moyo mtoto aeleze jinsi yeye binafsi anavyoweza kutumia habari inayozungumziwa. *

7 Isitoshe, fanya mazungumzo ya Kimaandiko yawe yenye kuchangamsha. Inapofaa, waambie watoto waigize matukio na drama za Biblia. Mnapozungumzia matukio fulani, wasaidie watoto wapige picha akilini ya nchi ambako mambo hayo yalitukia na mandhari yake pia. Huenda ikasaidia kutumia ramani na chati. Naam, kwa kuwa mbunifu, funzo la familia laweza kufanywa kwa njia mbalimbali zenye kuchangamsha. Wazazi pia wanapaswa kuchunguza uhusiano wao na Yehova. Wanapokuwa na uhusiano wa karibu na Yehova, wanaweza kuwasaidia watoto wao wafanye hivyo.—Kumbukumbu la Torati 6:5-7.

8. Sala inasaidiaje mtu amkaribie Mungu?

8 Pia sala husaidia mtu amkaribie Mungu. Msichana mmoja aliyekuwa katika umri wa mapema wa utineja alishindwa kuamua kama atafuata njia ya Kikristo au atashirikiana na marafiki wake ambao walikuwa na imani tofauti na yake. (Yakobo 4:4) Alifanya nini? “Kwa mara ya kwanza kabisa, nilisali sana kwa Yehova kuhusu jinsi nilivyohisi,” akakiri. Alikata kauli kwamba sala yake ilijibiwa wakati alipopata rafiki mmoja mwenye kuaminika katika kutaniko la Kikristo. Alianza kusitawisha uhusiano wa kibinafsi na Mungu baada ya kuona kwamba Yehova alikuwa anamwongoza. Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao kwa kuboresha sala zao wenyewe. Wanaposali wakiwa familia, wazazi wanaweza kueleza waziwazi hisia na matatizo yao ili watoto wao waone uhusiano wa kibinafsi uliopo kati ya wazazi hao na Yehova.

Uwe Mwenye Saburi Lakini Thabiti

9, 10. Yehova aliweka kielelezo gani cha kuwastahimili Waisraeli waliopotoka?

9 Kijana anapoanza kupeperuka mbali, huenda akajaribu kujitenga na wengine na kukataa kuwa na mazungumzo yoyote ya kiroho pamoja na wazazi wake. Wazazi wanaweza kufanya nini chini ya hali hiyo ngumu? Fikiria jinsi Yehova alivyowatendea Waisraeli wa kale. Alivumilia Waisraeli “wenye shingo ngumu” kwa muda unaozidi miaka 900 kabla hajawaacha wafuate njia yao iliyopotoka. (Kutoka 34:9; 2 Mambo ya Nyakati 36:17-21; Waroma 10:21) Licha ya Waisraeli ‘kumjaribu’ Yehova mara kwa mara, yeye ‘alikuwa mwenye rehema’ kwao. ‘Mara nyingi aliipishia mbali ghadhabu yake, wala hakuiwasha hasira yake yote.’ (Zaburi 78:38-42) Mungu alishughulika nao kwa njia kamilifu. Wazazi wenye upendo humwiga Yehova nao huonyesha saburi mtoto anapokataa kuitikia mara moja jitihada zao za kumsaidia.

10 Kuwa mstahimilivu au mwenye saburi kwamaanisha pia kutokata tamaa kabisa kuhusu kuboresha uhusiano ulioharibika. Yehova ameweka kielelezo cha kuwa mstahimilivu. Alichukua hatua ya kwanza kwa kutuma wajumbe wake kwa Waisraeli “mara kwa mara.” Yehova “alikuwa na huruma kwa watu wake,” hata ingawa “waliendelea kuwadhihaki wajumbe wa Mungu na kuyapuuza maneno yake.” (2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16, Biblia Habari Njema) Aliwasihi Waisraeli kwa kusema: “Rudini sasa, kila mtu na aiache njia yake mbaya.” (Yeremia 25:4, 5) Hata hivyo, Yehova hakulegeza kanuni zake za uadilifu. Waisraeli waliagizwa ‘wamrudie’ Mungu na viwango vyake.

11. Wazazi wanawezaje kuwa wastahimilivu lakini thabiti wanaposhughulika na mtoto anayepotoka?

11 Wazazi wanaweza kumwiga Yehova kwa kuwa wastahimilivu kwa kutokata tamaa mara moja mtoto anapopotoka. Pasipo kukata tamaa, wanaweza kuchukua hatua ya kwanza ya kudumisha mawasiliano mazuri au kuanzisha tena mawasiliano. Huku wakifuata kanuni za uadilifu, wanaweza “mara kwa mara” kumwomba mtoto arudie ile kweli.

Mtoto Anapotengwa na Ushirika

12. Wazazi wana daraka gani kuelekea mtoto anayeishi nao ambaye ameondoshwa katika kutaniko?

12 Namna gani mtoto anayeishi na wazazi wake akifanya dhambi nzito na kwa sababu ya kutotubu aondoshwa katika kutaniko? Kwa kuwa mtoto huyo anaishi na wazazi wake, bado wana daraka la kumfundisha na kumtia nidhamu kupatana na Neno la Mungu. Jambo hilo laweza kufanywaje?—Mithali 6:20-22; 29:17.

13. Wazazi wanawezaje kujaribu kufikia moyo wa mtoto aliyekosea?

13 Kwa kweli inawezekana na lingekuwa jambo bora kutoa mafundisho hayo na kutoa nidhamu hiyo unapojifunza Biblia na mtoto huyo faraghani. Mzazi hapaswi kumhukumu mtoto kwa sababu tu ya mtazamo wake sugu bali apaswa kujitahidi kufahamu kilicho moyoni mwake. Kwa ujumla, ugonjwa wake wa kiroho ni nini? (Mithali 20:5) Je, anaweza kuguswa moyo kwa sababu ya sifa fulani nzuri aliyo nayo? Ni maandiko gani yanayoweza kutumiwa kwa matokeo? Mtume Paulo atuhakikishia hivi: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na uloto wavyo, na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Naam, wazazi wanaweza kufanya mengi zaidi ya kumwonya tu mtoto wao asifanye dhambi tena. Wanaweza kujitahidi kuanzisha na kuchochea hali nzuri ya kiroho.

14. Kijana aliyekosea anaweza kuchukua hatua gani ya kwanza ili kurudisha uhusiano wake na Yehova, nao wazazi wanaweza kumsaidiaje achukue hatua hiyo?

14 Kijana aliyekosea anahitaji kurudisha uhusiano wake na Yehova. Hatua ya kwanza anayopaswa kuchukua ni ‘kutubu na kugeuka kabisa.’ (Matendo 3:19; Isaya 55:6, 7) Wanapomsaidia kijana aliye nyumbani mwao atubu, lazima wazazi ‘wafulize kujizuia wenyewe chini ya uovu, wakiagiza kwa upole’ mtoto asiye na mwelekeo ufaao. (2 Timotheo 2:24-26) Wanahitaji ‘kumkaripia’ kupatana na Biblia. Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “karipia” laweza pia kutafsiriwa “toa uthibitisho wenye kusadikisha.” (Ufunuo 3:19; Yohana 16:8) Kwa hiyo, kukaripia kunatia ndani kutoa uthibitisho wa kutosha ili kumsadikishia mtoto kwamba mwenendo wake ni wenye dhambi. Kwa kweli, si rahisi kufanya hivyo. Inapowezekana, wazazi wanaweza kuchochea moyo wake, wakitumia njia zote za Kimaandiko zinazofaa ili kumsadikisha. Wanapaswa kujitahidi kumsaidia aelewe uhitaji wa ‘kuchukia mabaya na kupenda mema.’ (Amosi 5:15) Huenda akarudiwa na ‘fahamu zake nzuri kutoka katika mtego wa Ibilisi.’

15. Sala husaidiaje mtu aliyekosea arudishe uhusiano wake na Yehova?

15 Sala ni ya lazima ili kurudisha uhusiano na Yehova. Bila shaka, hakuna mtu anayepaswa “kuomba” kuhusu dhambi iliyo wazi ambayo inafanywa tena na tena na mtu asiyetubu ambaye alikuwa anashirikiana na kutaniko la Kikristo hapo awali. (1 Yohana 5:16, 17; Yeremia 7:16-20; Waebrania 10:26, 27) Hata hivyo, wazazi wanaweza kumwomba Yehova awape hekima ya kushughulika na hali hiyo. (Yakobo 1:5) Ikiwa kijana aliyetengwa na ushirika anaonyesha toba lakini hana “uhuru wa usemi kuelekea Mungu,” wazazi wanaweza kumwomba Mungu amsamehe mtoto kosa hilo ikiwa anaona kuna msingi wa kufanya hivyo ili mapenzi Yake yatendeke. (1 Yohana 3:21) Kusikiliza sala hizo kwapaswa kumsaidia kijana amwone Yehova kuwa Mungu mwenye rehema. *Kutoka 34:6, 7; Yakobo 5:16.

16. Tunaweza kusaidiaje washiriki wa familia ambao watoto wao wametengwa na ushirika?

16 Ikiwa kijana aliyebatizwa ametengwa na ushirika, washiriki wa kutaniko wanapaswa ‘wakome kuchangamana katika ushirika pamoja’ naye. (1 Wakorintho 5:11; 2 Yohana 10, 11) Kufanya hivyo huenda hatimaye kukamsaidia ‘arudiwe na fahamu zake’ na kurudi kwenye kundi la Mungu lenye ulinzi. (Luka 15:17) Hata hivyo, kama atarudi ama la, washiriki wa kutaniko wanaweza kuitia moyo familia ya kijana aliyetengwa na ushirika. Sote tunaweza kutafuta fursa za kuonyesha “hisia-mwenzi” na kuwaonyesha “huruma kwa njia ya wororo.”—1 Petro 3:8, 9.

Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia

17. Washiriki wa kutaniko wanapaswa kukumbuka nini wanapojaribu kumsaidia mtoto aliyepotoka?

17 Namna gani kijana ambaye hajatengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo lakini amekuwa na imani dhaifu? Mtume Paulo aliandika kwamba “kiungo kimoja kikiteseka, viungo vingine vyote huteseka pamoja [naye].” (1 Wakorintho 12:26) Wengine wanaweza kudhihirisha upendezi wao kwa kijana huyo. Bila shaka, uangalifu wa kadiri fulani wahitajiwa kwa kuwa kijana aliye mgonjwa kiroho anaweza kuwa na uvutano usiofaa kwa vijana wengine. (Wagalatia 5:7-9) Katika kutaniko moja, watu fulani wazima waliokuwa na nia njema na ambao walitaka kusaidia baadhi ya vijana waliokuwa dhaifu kiroho, waliwaalika kwenye vikusanyiko ili kucheza pamoja muziki fulani uliopendwa. Ingawa vijana hao walikubali mara moja na kufurahia vikusanyiko hivyo, uvutano wao hatimaye ulifanya vijana wengine waache kushirikiana kabisa na kutaniko. (1 Wakorintho 15:33; Yuda 22, 23) Jambo linaloweza kumsaidia mtoto aliye mgonjwa kiroho apone si vikusanyiko vya kirafiki ambavyo havina mwelekezo wa kiroho, bali ni ushirika utakaomsaidia kusitawisha tamaa ya mambo ya kiroho. *

18. Tunaweza kumwigaje baba ya mwana mpotevu katika mfano wa Yesu?

18 Kijana aliyeacha kushirikiana na kutaniko anaporudi kwenye Jumba la Ufalme au kuhudhuria kusanyiko, ebu wazia jinsi anavyohisi. Je, hatupaswi kumkaribisha kama vile baba ya mwana mpotevu katika mfano wa Yesu? (Luka 15:18-20, 25-32) Tineja fulani aliyeacha kushirikiana na kutaniko la Kikristo na baadaye akahudhuria mkusanyiko wa wilaya alisema hivi: “Nilidhani kwamba kila mtu atanipuuza, lakini ndugu na dada walinifikia na kunikaribisha. Niliguswa moyo kwelikweli.” Alianza kujifunza Biblia tena na baadaye akabatizwa.

Usikate Tamaa

19, 20. Kwa nini tunapaswa kudumisha mtazamo ufaao kuhusu mwana mpotevu?

19 Kusaidia mtoto “mpotevu” ‘arudiwe na fahamu zake’ kwahitaji saburi na kwaweza kuwa jambo gumu kwa wazazi na wengineo. Lakini usikate tamaa. “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Maandiko yanatuhakikishia kwamba Yehova anataka watu watubu wakaishi. Kwa kweli, amechukua hatua ya kwanza ya kufanya mipango ya kuwapatanisha wanadamu naye. (2 Wakorintho 5:18, 19) Subira yake imewezesha mamilioni ya watu warudiwe na fahamu zao.—Isaya 2:2, 3.

20 Hivyo basi, je, wazazi hawapaswi kutumia njia zote za Kimaandiko kusaidia mtoto wao mpotevu arudiwe na fahamu zake? Kwa kumwiga Yehova, uwe mstahimilivu unapochukua hatua hususa kusaidia mtoto wako amrudie Yehova. Fuata kwa ukaribu kanuni za Biblia, na ujaribu kudhihirisha sifa za Yehova kama vile upendo, haki, na hekima huku ukisali akusaidie. Kama vile waasi wengi walio sugu walivyoitikia mwaliko wenye upendo wa Yehova wa kumrudia, mwana au binti yako mpotevu anaweza kurudia kundi la Mungu lenye ulinzi.—Luka 15:6, 7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ili kupata madokezo zaidi kuhusu jinsi ya kufundisha watoto kwa matokeo, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1999, ukurasa wa 13-17.

^ fu. 15 Sala hizo hazitatolewa kwenye mikutano ya kutaniko kwa niaba ya mtoto aliyetengwa na ushirika, kwa kuwa huenda wengine wasifahamu hali ya mtoto huyo aliyetengwa na ushirika.—Ona gazeti Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 1979, ukurasa wa 31 la Kiingereza.

^ fu. 17 Kwa madokezo hususa, ona gazeti Amkeni!, Juni 22, 1972, ukurasa wa 13-16 la Kiingereza; Septemba 22, 1996, ukurasa wa 21-23.

Je, Unakumbuka?

• Huenda kiini cha tatizo kikawa nini vijana wanapoacha kushirikiana na kutaniko?

• Vijana wanaweza kusaidiwaje wasitawishe uhusiano wa kibinafsi na Yehova?

• Kwa nini wazazi wanahitaji kuwa wastahimilivu lakini thabiti katika kusaidia mtoto mpotevu?

• Wale walio kutanikoni wanawezaje kusaidia kijana mpotevu arudi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ni muhimu kusoma Neno la Mungu ili kusitawisha uhusiano wa karibu na Yehova

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wazazi wanaposali kutoka moyoni wanaweza kusaidia watoto wao waone uhusiano wa kibinafsi uliopo kati yao na Yehova

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mkaribishe mtoto mpotevu ‘anaporudiwa na fahamu zake’

[Picha katika ukurasa wa 18]

Chukua hatua hususa kusaidia mtoto wako amrudie Yehova